• Sura 1:Mazungumzo na majadiliano


    Mada ndogo: Msamiati na mawasiliano katika shughuli za kilimo na ufugaji


    A . Msamiati wa msingi kuhusu mazao na shughuli za kilimo na ufugaji nchini Rwanda.
    i) Msamiati wa mazao nchini Rwanda
    Tazama mazao yafuatayo na usome maneno chini yake.

    Bidhaa zilizopo kwenye michoro zinaitwa mazao. Mazao ni vitu tunavyovuna
    baada ya kupanda mbegu zake.Ni vitu vinavyozaliwa na mimea iliyopandwa. Hapa
    nchini Rwanda, udongo wetu ungali na rutuba ya kutoa mazao mema. Tunapanda
    mimea mbalimbali inayotupatia mazao.

    Tazama mifano zaidi ya mazao yanayopatikana hapa nchini Rwanda na
    usome vifungu kando yake.                                



                                 Kahawa ni zao la mkahawa au mbuni. Kahawa
                                hukaushwa na kusagwa ili kutoa ungaunga.
                                Ungaunga huo hutumiwa kwa kutengenezea
                                kinywaji cha kahawa. Kinywaji cha kahawa
                                kina ladha nzuri. Kahawa pia huuzwa katika
                                nchi za nje na kuletea nchi yetu pesa za kigeni.










                                                                                                                      
      Haya ni
      majani ya mchai. Majani ya mchai hukaushwa
      na kusagwa. Majani haya hutumiwa kutengenezea
      kinywaji cha chai. Nchi yetu huuza majani ya
      mchai katika nchi za kigeni. Majani ya mchai
      pia huletea nchi yetu pesa za kigeni.
                                                                                                   






             
      

                                                                                         
                                                                                                Hizi ni ndizi. Ndizi 
                                                                                                ni zao la mgomba.  
                                                                                                Ndizi humea kwenye      
                                                                                                mkungu. Ndizi
                                        inaweza kuivishwa na kuliwa moja kwa moja. Baadhi ya
                                       ndizi hupikwa na kuliwa.Ndizi pia huuzwa na kutuletea
                                       mapato.





                                                                     

    Haya ni maharagwe. Maharagwe ni zao la mharagwe.
    Nafaka hii ni muhimu sana kwa chakula chetu. Hii ni
    kwa kuwa virutubishi vyake vya protini huhitajika sana
    miilini mwetu. Wale ambao hawali nyama mara kwa mara
    huweza kupanda miharagwe na kupata protini zao kutoka
    kwayo.





             



    Huu ni mtama. Mtama huzaa punje ndogo ndogo. Punje  
    za mtama hukaushwa na kuchanganywa na mihogo au mahindi. Baadaye husagwa ili kupata unga. Unga huu hutengenezewa  uji au sima (ugali).




                                                                
                
    Haya ni mahindi.Mahindi ni mazao
    ya mhindi. Mahindi hukaushwa na
    kusagwa ili kutoa unga wa dona.
    Unga wa mahindi hutengenezewa
    sima au ugali.Mahindi pia yanaweza kupikwa pamoja na
    maharagwe kutengenezea pure au kande. Pure ni chakula kitamu kinachoshibisha vilivyo. Ama hindi linaweza kuchomwa au kuchemshwa na likawa chakula kwetu. Mafuta ya mahindi hutumiwa kutengenezea mafuta ya kupikia. Mbali na mahindi, njugu pia hutengenezewa mafuta ya kupaka kwenye mkate. Njugu ni zao la karanga. Njugu hukaangwa na kuliwa. Baadhi ya watu hutwanga njugu na kutengeneza borohoa ya kuungia kitoweo.


                
                              Haya ni mananasi. Nanasi ni zao la mnanasi.   
                              Nanasi huivishwa na kuliwa.
                              Nanasi hutoa maji matamu yanayomaliza kiu.
                              Maji hayo hutumiwa kutengenezea sharubati au soda.



                                                                                                         
                                   Hii ni mihogo. Muhogo ni mzizi wa muhogo.
                                   Muhogo huweza kuchemshwa au kukaangwa na kuliwa.
                                   Muhogo pia huweza kukaushwa, ukasagwa na kutengenezewa
                                   sima.


                                                                                       
                       

                                                                                                      Hizi ni mbatata. Mbatata  
                                                        ni viazi vya mviringo. Viazi hivi havina sukari. Mbatata
                                                        huweza kupikwa kama kiungo. Pia, huchemshwa na
                                                        kuliwa na vinywaji au vyakula vinginevyo. Mbatata pia
                                                        hukatwakatwa kwa vipande vyembamba na kutiwa ndani           
                                                        ya mafuta ili kutengenezea vibanzi au chipsi.




    Hivi ni viazi vitamu. Viazi hivi hupandwa katika matuta au sesa.
    Viazi vitamu huchemshwa na kunywewa kwa chai au kahawa.
    Viazi vitamu huwa na sukari kiasi cha haja.





    Zoezi

    1. Angalia maana ya maneno yaliyokolezwa kwa wino katika kamusi.
       Tunga sentensi sahihi kwa kila neno.
    2. Taja mazao zaidi yanayopatikana nchini Rwanda lakini hayajatajwa katika kifungu.
         Je, mazao hayo yana faida gani?
    3. Tunga sentensi sahihi ukitumia maneno yafuatayo:
        a) ndizi           b) mahindi           c) kahawa 
        d) mbatata     e) maharagwe     f ) chai
    4. Taja majina ya mazao haya na faida zake.

    Kazi ya wanafunzi wawili wawili
    Jiunge na mwanafunzi mwenzako. Jadilianeni kuhusu majina na faida ya mazao mbalimbali katika maeneo mnakoishi

    Kazi ya kikundi
    Katika vikundi, kila mwanafunzi ataje mazao yasiyopatikana katika eneo anamoishi.
    Jadilianeni kuhusu faida za mazao mliyoyataja.

    ii) Msamiati kuhusu shughuli za kilimo nchini Rwanda
    Jiunge na mwanafunzi mwenzako. Jadilianeni kuhusu shughuli mbalimbali za kilimo kwenye michoro.
    Mfano
                   

    Soma kifungu kilichopo hapa chini na ujibu maswali chini yake.
    HABIMANA:  Habari za asubuhi wenzangu?
    KAREKEZI
    na ITUZE:       Nzuri sana Habimana.
    HABIMANA:   Wenzangu, naomba mnieleze maana ya kilimo.
    KAREKEZI:    Kilimo au zaraa ni kazi ya kulima shamba na kukuza mimea hadi
                            kufikia kiwango cha kuvunwa.
    HABIMANA:   Wenzangu, naomba mnitajie shughuli hizi za kilimo.
    KAREKEZI:    Kwanza, kuna kufyeka. Sisi hufyeka shamba letu kwa kutumia
                            upanga na fyekeo. Baadaye, kuna kulima shamba ili kuandaa konde.
                            Katika kijiji chetu, tunatumia jembe la mkono kuandalia konde.
    HABIMANA:   Kwa nini mnatumia jembe la mkono?
    KAREKEZI:    Kwa sababu mashamba katika kijiji chetu ni madogomadogo.
                            Vilevile, wakulima katika kijiji chetu hawawezi kumudu mbinu
                            nyinginezo za kulima. Je, Ituze, wakulima katika eneo lenu
                            hutumia mbinu zipi kuandaa mashamba yao?
    ITUZE:            Wakulima katika eneo letu hutumia plau inayovutwa na ng’ombe au punda.
                            Wakulima katika eneo jirani nao hutumia plau inayovutwa na trekta. Wakulima
                            hao wanamiliki mashamba makubwa. Pia wanaweza kulipia gharama za trekta.
                            Karekezi, hebu tueleze namna nyingine ya ukulima katika eneo lenu.
    KAREKEZI:    Sisi hulima sesa. Tunapojiandaa kupanda mbegu, huchanganya mbolea ya samadi
                            na udongo. Udongo wetu hauna rutuba ya kutosha. Baada ya kuweka mbolea,
                            tunapanda mbegu za mahindi na maharagwe ndani ya udongo na kuzifukia.
                            Mbegu zinapoota, tunapalilia miche ili kuondoa magugu au kwekwe. Baadhi ya
                            wakulima huweza kupiga dawa za kuwaua wadudu waharibifu.Wakati wa kiangazi,
                            kuna kunyunyizia mimea maji. Baada ya mimea kukua na kukomaa, tunavuna. Viazi
                            na mihogo yetu ndiyo hutuletea pesa za matumizi nyumbani kwetu. Tunakula baadhi
                            ya mazao hayo na kuyauza mengine.
    HABIMANA:   Kumbe kazi hii ya kilimo ni nzuri mno! Nilisoma juzi kuwa nchi yetu hupata pesa
                            za kigeni kwa kuuza chai na kahawa katika nchi za kigeni.
    ITUZE:            Kweli kabisa. Uchumi wa Rwanda umeimarika kwa sababu ya kilimo.
                            Maisha ya wakulima wengi yameimarika pia. Watu wengi
                            wameajiriwa kutokana na kilimo.
    HABIMANA:   Hata mimi nitaanza kufanya shughuli hizi za kilimo. Tuna shamba
                            dogo lakini lina rutuba nyingi. Nitapanda mboga na njugu.
                            Asanteni kwa kunifunza kuhusu kilimo. Kushauriana katika kazi
                            ya kilimo ni jambo lililo muhimu mno.
    KAREKEZI:     Pia, tusome kwa bidii hadi chuo kikuu ndipo tuwe wakulima bora zaidi.
                            Tukisoma kwa bidii, tutajifunza na kutumia mbinu za kisasa za kilimo.
                            Mbinu hizi zitatusaidia na kusaidia jamii. Kilimo kitaimarika.
    ITUZE:            Taibu! Pia tukisoma, tutabuni mbinu mpya za kurahisisha kilimona kujiongezea mazao.
                            Ni lazima tufanye juu chini kupata elimu na kufanya utafiti zaidi. Asanteni wenzangu.

    Maelezo ya msamiati
    kufyeka      – kusafisha shamba kwa kukata miti au majani
    kulima        – kutayarisha shamba kwa kutifua ardhi
    konde         – sehemu ya shamba iliyolimwa
    sesa           – ukulima usiokuwa wa matuta katika ardhi tambarare
    kuzifukia     – kuzificha mbegu ardhini
    zinaota        – zinachipuka kutoka ardhini
    kupalilia       – kulima kwa kuondoa magugu katikati ya mimea au miche
    kunyunyizia – kumwagilia maji au dawa ya maji
    kukua           – kuongezeka ukubwa au kimo
    kukomaa      – kuwa tayari kuvunwa/kutolewa shambani
    kuvuna         – kutoa mazao shambani

    Maswali
    1. Angalia maana ya maneno haya katika kamusi na uyatungie sentensi sahihi.
        a) upanga                    b) fyekeo                   c) plau                             d) trekta                                        e) mbolea    
        f ) samadi                     g) udongo                 h) rutuba                           i) kwekwe                                     j) mbegu
         k) mche                        l) pampu
    2. Andika manufaa ya kilimo yaliyotajwa kwenye kifungu. Ongezea manufaa matano zaidi.
    3. Karekezi na Ndoli hawapendi kilimo. Je, kauli hii ni kweli? Toa sababu zako.
    4. Je, masomo ya kilimo yana umuhimu gani?
    5. Tumia maneno uliyopewa kutaja shughuli kwenye michoro.
         (kufyeka, kulima, kupanda mbegu, kupalilia, kupiga dawa, kunyunyizia maji, kuvuna)
    6. a) Taja majina na matumizi ya vifaa vilivyopo hapa chini.
       
        b) Tunga sentensi sahihi kuhusu kilimo ukitumia jina la kila kifaa hapo juu.
    7. Andika maneno kumi ya shughuli na zana za kilimo kutoka kwenye mraba huu.
        Tunga sentensi sahihi ukitumia kila neno.
         
    Kazi ya wanafunzi wawili wawili
    Jiunge na mwanafunzi mwenzako. Jadilianeni kuhusu shughuli za kilimo katika nchi
    ya Rwanda na manufaa ya shughuli hizo.

    iii) Msamiati kuhusu shughuli za ufugaji nchini Rwanda
    Ufugaji hasa ni kazi ya kutunza wanyama, ndege na hata wadudu. Kazi hii ina faida
    kubwa sana kama kilivyo kilimo cha mimea. Mfugaji anaweza kufuga wanyama ama wadudu.

    Kazi ya wanafunzi wawili wawili
    Jiunge na mwanafunzi mwenzako. Kumbushaneni majina ya mifugo mbalimbali
    mliyosoma katika kidato cha kwanza na umuhimu wake.

    Tazama michoro iliyopo hapa chini na usome kifungu cha maneno kando yake.
     


    Huyu ni Ikirezi. Ikirezi ni mfugaji wa nyuki. Ikirezi
    anarina asali.Baada ya kurina, yeye husafisha
    asali yake na kuiuza. Asali hiyo hutumiwa kama
    chakula au hutengenezewa dawa.








                
    Huyu ni Gabiro. Gabiro anakata sufu. Sufu ya kondoo
    hutumiwa kutengenezea nyuzi za kufumia nguo.

                                                                   






    Huyu ni Ituze. Ituze anakama
    ng’ombe.Kabla ya kukama, aliosha chuchu kwa
    maji vuguvugu na kuzikausha kwa kitambaa safi.
    Anatumia mkebe safi kuwekea maziwa. Ituze
    huwapandisha mitamba kwa dume au mpira.













    Hili ni josho. Ng’ombe hawa wanaogeshwa kwa dawa ndani ya josho. Wafugaji huosha mifugo katika josho ili kuikinga dhidi ya kupe. Dawa huua viroboto wanaoishi kwenye ngozi za mifugo.






    Hawa ni Mudenge na Gatera.
    Mudenge anawalisha kuku kwa mahindi. Pia,
    huwapa kuku mtama, ugali, wadudu na vyakula
    vinavyopatikana kwa urahisi. Wakati mwingine,
    yeye huwapa kuku chakula maalumu
    kilichotengenezwa katika viwanda. Mudenge anawafuga
    kuku wa mayai na nyama. Yeye huuza baadhi ya mayai ili kujipatia riziki. Mudenge pia huwaatamisha baadhi ya kuku wake ili apate vifaranga wa kuuza na kufuga. Gatera naye anawalisha ng’ombe kwa nyasi. Gatera anawafuga ng’ombe wake ndani kwa ndani. Anawapa lishe, maji na dawa humohumo zizini. Gatera hukata pembe za ng’ombe wake. Ng’ombe hukatwa pembe ili kumzuia kumdhuru mtu au kuharibu vitu.





    Huyu ni Kaliza. Kaliza anapenda kuchunga punda. Anawachunga punda penye maji safi na nyasi nyingi. Kulisha mifugo ni shughuli muhimu ya ufugaji. Mifugo wanapolishwa vizuri hukua kwa haraka, huwa na afya nzuri na hutupatia mapato mazuri.









    Kaliza anafagia zizi la ng’ombe. Mkulima
    bora husafisha makao ya mifugo na vyombo
    vyao vya kulia na kulalia. Mifugo wanaolala
    katika mahali safi na kula katika vyombo safi
    huwa na afya njema.













    Daktari wa mifugo anamtibu kuku kwa kumdunga sindano. Kutibu mifugo ni muhimu kwa mkulima. Ni vizuri kutambua dalili ya ugonjwa ili watibiwe mapema.


    Msamiati
    kurina         – kufukuza nyuki kutoka kwenye mzinga na kukata masega ili kupakua asali.
    kukata sufu – kunyoa manyoya ya kondoo kutoka kwenye ngozi yake
    kukama       – kuminya chuchu za mnyama kama vile ng’ombe ili maziwa yatoke
    kupandisha mtamba                     – kumpa ng’ombe wa kike mbegu za kiume ili kuzalisha ndama
    kufuga ng’ombe ndani kwa ndani – kufuga ng’ombe ndani ya eneo au jengo fulani na
                                                             kuwapa mahitaji yote humo bila kuwatoa nje
    kuwapeleka ng’ombe katika josho – kuwapelekea ng’ombe katika dimbwi maalumu lililotiwa dawa ya kuulia kupe
    kuatamisha kuku – kumfanya kuku kulalia mayai
    kuchunga            – kuwapeleka wanyama malishoni na kuwalinda wasiibwe
    kukata pembe     – kutoa pembe kwa kutumia kisu au chuma moto
    kulisha   – kupea chakula na maji

    Maswali
    1. Andika majina yote ya mifugo waliotajwa katika ufahamu hapo juu.
        Taja umuhimu wao.
    2. Eleza faida za shughuli za ufugaji ulizosoma katika kifungu.
    3. Jaza mapengo haya kwa shughuli sahihi ya ufugaji.
       
     
     
    4. Tunga sentensi sahihi ukitumia maneno hapo chini.
        a) rina asali
        b) chunga
        c) kata pembe
        d) kama
        e) lisha
        f ) fagia zizi
        g) tibu ng’ombe
        h) pandisha mtamba
         i) atamisha

    Kazi ya wanafunzi wawili wawili
    Jiunge na mwanafunzi mwenzako na mfanyeni zoezi hili:
    1) Kwa pamoja, andikeni shughuli mbalimbali za ufugaji na mifugo nchini Rwanda katika karatasi.
    2) Kunjeni karatasi hizo na kuziweka pamoja.
    3) Kila mwanafunzi achukue karatasi moja kwa zamu, asome shughuli ya ufugaji
        au mifugo katika karatasi aliyochukua na atunge sentensi sahihi kwa kutumia
        neno katika karatasi yake. Atakayekosea asahihishwe.

    Kazi ya kikundi
    Kama darasa zima, fanyeni mjadala kuhusu: Njia za kisasa za ufugaji zinaleta mapato
    makubwa zaidi kuliko njia za kienyeji.

    B . Majira ya mwaka nchini Rwanda
    Tazama michoro iliyopo hapa chini. Je, nini kinafanyika?
     

     Soma kifungu hiki na ujibu maswali yaliyoulizwa chini yake.
    Majira ni kipindi maalumu cha hali ya hewa. Majira haya ndiyo huelekeza upanzi
    wa mimea na uvunaji wa mazao hapa kwetu.
    Tupo na majira mbalimbali. Yapo majira ya mvua nyingi. Majira ya mvua nyingi ya
    mfululizo huitwa masika. Majira haya hutokea kuanzia mwezi wa Machi hadi Mei
    kila mwaka. Shughuli za kupanda mimea kama vile maharage, mtama, mbatata,
    mahindi,na kadhalika hutokea mwanzoni mwa majira ya masika. Mimea hiyo    
    huota na kupaliliwa katika majira haya ya masika.
    Vilevile, mimea mbalimbali kama vile mikahawa, mipareto, migomba, minanasi na
    kadhalika hustawishwa mnamo majira haya.
    Msimu huu wa masika hufuatwa na majira ya kiangazi au ukame. Huu ni wakati
    ambapo jua kali huwaka, mvua hukosa kunyesha na ardhi hukauka. Yapo majira
    mafupi ya kiangazi ambayo hutokea kuanzia Juni hadi Septemba. Mifugo na mimea
    hukosa chakula na maji ya kutosha na huanza kuwa na afya mbaya mnamo majira haya.
    Baadhi ya wakulima huanza kuvuna mazao yao katika majira ya kiangazi.
    Wengine hulima na kuandaa makonde yao mnamo majira haya kabla ya mvua
    kuanza kunyesha.
    Mbali na majira haya, yapo majira ya vuli. Huu ni wakati ambapo huwepo mvua
    ndogo ndogo tu. Majira haya hutokea kati ya mwezi wa Novemba na Februari.
    Wakati wa vuli, wakulima hupanda vyakula vinavyochukua muda mfupi kukua na kukomaa.
    Hata hivyo, shughuli nyingi za upanzi hazifanyiki kwa kuwa mvua inyeshayo huwa haitoshi
    kukuza baadhi ya mimea.
    Hali kadhalika, yapo majira ya kipupwe. Kipupwe ni majira ya baridi ambayo hutokea katika
    miezi ya Septemba na Novemba nchini Rwanda. Wakati huu wa mwaka huwepo baridi kali
    na hubidi watu kuvaa sweta, makoti na hata makabuti.
    Kwa ufupi, wakulima wengi nchini Rwanda huzingatia majira mbalimbali
    wanapofanya shughuli zao za kilimo. Wao hutegemea mvua na jua katika kukuza mimea.

    Msamiati
    masika               – majira ya mvua nyingi ya mfululizo
    kiangazi/ukame  – majira ya jua kali
    vuli                      – majira ya mvua ndogo ndogo
    kipupwe              – majira ya baridi kali

    Maswali
    1. Taja miezi na majira ambapo shughuli hizi za kilimo hufanywa hapa kwetu Rwanda.
        a) kulima shamba kavu
        b) kuandaa konde lenye unyevunyevu
        c) kupanda mimea mingi
        d) kupalilia
        e) kustawisha mimea
        f ) kuvuna
        g) kupanda mimea michache inayokua na kukomaa haraka
    2. Ipo tofauti gani kati ya vuli na kipupwe?3. Tazama mraba ufuatao na uandike maneno manne ya majira.
          

    Kazi ya wanafunzi wawili wawili
    Jiunge na mwenzako. Chunguzeni michoro ifuatayo na mjaze mapengo kando yake.
     
     

    C . Msamiati wa msingi kuhusu wanyama wa porini na umuhimu wake

    i) Msamiati wa wanyama wa porini nchini Rwanda
    Tazama wanyama hawa. Je, hawa ni wanyama gani? Wanyama hawa
    wanapatikani katika mbuga na sehemu ipi ya Rwanda?

    Kisome kifungu kifuatacho ili kujifunza msamiati wa wanyama wa porini.
    Mnyama wa porini ni mnyama anayeishi katika pori. Pori ni mahali penye miti na nyasi nyingi.
    Mnyama wa porini hafugwi na binadamu. Wanyama wengi wa porini hupatikana katika mbuga
    za wanyama. Mbuga za wanyama ni sehemu zilizotengwa na serikali kuwa ndio makazi ya
    wanyama hao wa porini. Je, unafahamu mbuga gani za wanyama nchini Rwanda?
                                                                                                                              

    Nchi ya Rwanda ina wanyama wengi wa porini.
    Nchi yetu ya Rwanda inasifika sana kutokana
    na masokwe. Sokwe ni mnyama mkubwa zaidi
    katika jamii ya nyani. Mnyama huyu hana
    mkia. Sokwe ana akili nzuri inayokaribiana
    na ile ya binadamu. Wana uwezo wa
    kumwiga binadamu. Nchi yetu inajulikana
    sana kutokana na masokwe. Masokwe hawa
    wanapatikana katika mbuga zetu za wanyama.
    Masokwe wengi wanapatikana katika Mbuga
    ya Wanyama ya Volcanoes (Volkano).









    Nyani ni mnyama wa jamii ya sokwe na tumbiri.
    Nyani ni mdogo kuliko sokwe lakini ana akili nyingi zaidi.
    Ana masikio makubwa nao mwili wake una rangi ya kaki ya
    kijivu na ngoko nyekundu makalioni. Nyani huishi katika
    vikundi vya majike na madume. Wana uwezo wa kuishi
    kwa miaka zaidi ya arubaini.
     







                                                                                                                   

               Pia kuna tumbiri porini. Tumbiri ni mnyama mdogo
               zaidi katika jamii ya nyani. Tumbiri hupenda sana
               kukaa mitini. Hula vyakula mbalimbali kama vile
               matunda, mazao ya mimea mbalimbali na kadhalika.







    Simba ni mnyama mkubwa wa jamii ya paka.
    Simba hula nyama. Anaitwa mfalme wa wanyama
    au nyika. Simba huishi kwenye vikundi. Vikundi
    hivyo huongozwa na simba dume.



         
                   


                                 Ndovu ndiye mnyama mkubwa zaidi wa porini.
                                 Ndovu ana mkonga pamoja na pembe mbili
                                 kubwa zenye thamani. Ndovu wana masikio
                                 makubwa na miguu mifupi minene. Ndovu hula
                                 nyasi, mizizi, matunda na mashina ya miti. Pia,
                                 huishi katika vikundi. Kila kikundi huongozwa na
                                 ndovu jike ambaye ana umri mkubwa zaidi kuliko
                                 wote. Uwindaji wa ndovu na kuuza pembe
                                  zake ni hatia. Sisi sote tunafaa kuwatunza ndovu na wanyama wote wa porini.


    Chui pia hupatikana katika mbuga zetu. Chui ni
    mnyama wa jamii ya paka lakini aliye mkubwa na
    mkali na mwenye madoadoa ya manjano na meusi.
    Chui hula wanyama wadogo wadogo wanaoishi porini.
    Baada ya kuwinda, wao huficha nyama kwenye matawi
    ya mti. Wao hupenda sana kutembea na kuwinda wakati
    wa usiku na kupumzika wakati wa mchana.



    Pundamilia pia ni mnyama wa porini wa jamii ya farasi.
    Ana milia myeusi na myeupe katika mwili mzima.
    Inaaminika kuwa milia hiyo huwawezesha kujificha
    nyikani ili wasionekana na wanyama wanaowawinda.
    Pundamilia hutembea na kula nyasi katika vikundi vikubwa.



                                                                                                                                                      

                          Twiga naye ana shingo ndefu, rangi ya kahawia na madoadoa meusi.
                          Twiga  ndiye mnyama mrefu zaidi. Yeye hula majani ya miti.




    Kifaru pia hupatikana katika mbuga zetu. Ni mnyama
     mkubwa afananaye na kiboko na mwenye kipusa usoni.






                                                                       
                                          
                                  
     Nyati pia ni mnyama mkubwa sana. Hufanana na ng’ombe. Pembe zake zimepinda kwa mbele. Nyati hula nyasi. Wao pia huishi katika vikundi kutegemea jinsia. Nyati pia huitwa mbogo.                                    
     






    Swara ni mnyama mdogo anayefanana na mbuzi.
    Swara anaweza kukimbia haraka. Yeye hula nyasi.



    Wanyama hawa wa porini hupatikana katika mbuga zetu kama vile Akagera,
    Nyungwe na Volcanoes. Wanyama hawa ni vivutio vikubwa vya watalii wanaotoka
    ndani na nje ya nchi yetu.

    Maswali
    1. Andika orodha ya majina ya wanyama wa porini wanaokula:
        a) nyama
        b) nyasi
    2. Eleza tofauti zilizopo kati ya sokwe na nyani.
    3. Jaza kila pengo kwa jina sahihi la mnyama wa porini.
         a) Mwenye tamaa kama______________.
         b) _________ ana mkonga na pembe mbili.
         c) _______ haoni kundule.
         d) Ndovu pia huitwa_____________.
         e) Nimemwona mnyama mwenye milia myeusi na myeupe mwilini.
             Nimemwona__________.
    4. Tunga sentensi sahihi ukitumia majina haya ya wanyama wa porini.
         a) pundamilia             b) simba               c) tumbir
        id) swara                     e) nyati                  f ) ndovu
    5. Taja majina ya wanyama hawa:


    6. Jiunge na mwanafunzi mwenzako. Fanyeni utafiti kuhusu majina na sifa
        za wanyama wa porini wanaopatikana ndani na nje ya Rwanda na ambao
        hawajatajwa katika ufahamu.

    ii) Umuhimu wa wanyama wa porini nchini Rwanda
    Kufikia sasa, umesoma mengi kuhusu wanyama wa porini. Wanyama hao wana
    umuhimu mbalimbali.
    Tazama mchoro huu na usome kifungu chini yake.
                                                  
    KANYANA:  Karibuni katika mbuga yetu ya Volcanoes.
    UWASE
    na HIRWA:   Asante.
    KANYANA: Hapa, mtaona wanyama wengi wa porini.
    UWASE:      Wanyama hao wana umuhimu gani?
    NGABO:     Wanyama hao wana umuhimu mkubwa sana kwa nchi hii yetu ya
                        Rwanda. Wanyama hao kama vile masokwe ni vitega uchumi. Kila
                        mwaka, watalii kutoka nchi za mbali huja hapa kwetu kuwaona
                        wanyama. Wajapo hivyo, huja na pesa za kigeni ambazo huinua sana
                        uchumi wetu.
    KANYANA: Nyinyi pia ni watalii wetu hapa. Pesa mnazolipa mkiingia hujenga
                        uchumi wetu. Pesa hizo pia hutumiwa kutulipia mshahara. Mimi na
                        wenzangu tumeajiriwa kwa sababu ya wanyama wa porini.
    HIRWA:       Je, nchi yetu hunufaika na pesa za kiingilio peke yake?
    NGABO:      Hapana. Wageni wanapokuja, wanaleta manufaa mengi zaidi. Wao
                         hulipia huduma mbalimbali. Kwanza kuna malazi yao. Sisi
                         huwakaribisha katika hoteli kubwa kubwa na nzuri nzuri. Hoteli
                         hizo zimepanuka na kuwaajiri watu wengi kwa sababu ya wageni
                         hao wanaokuja kuangalia wanyama wa porini. Wageni hao pia
                         hulipia usafiri wao uwe ni wa ndege au gari. Usafiri huo huwapeleka
                         huko wanakopenda kwenda kuwaona wanyama.
    KANYANA: Mbali na hayo, zipo bidhaa nyingi sana za hapa ambazo watalii hao
                        hununua kuwa ni ushahidi kwao kwamba kweli walikuwa hapa. Kwa
                        njia hiyo pia nchi hufaidika kiuchumi.
    UWASE:      Mbali na faida hizo za kifedha, zipo faida gani tena za wanyama hawa?
    NGABO:      Wanyama hawa hukuza elimu yetu. Wanafunzi, na hata watu wazima
                         huzuru mbuga zetu za wanyama ili kuwaona na kujifunza mengi
                         kuwahusu.
    KANYANA:  Isitoshe, wanyama wa porini ni hazina kwa vizazi vyetu vya baadaye.
                         Sisi sote tumewaona wanyama hawa. Vivyo hivyo, litakuwa jambo
                         zuri sana ikiwa wanetu, wajukuu, watukuu, vilembwe na hata
                         vilembwekeza wetu kuwaona wanyama wa porini pia. Hii ndiyo
                          sababu ya serikali yetu kuwatunza na kuwalinda wanyama wa porini.
    UWASE
    na HIRWA:  Asanteni kwa maelezo yenu.

    Maswali
    1. Taja faida za wanyama wa porini.
    2. Taja njia mbili ambazo serikali hutumia kuhifadhia wanyama wa porini.

    Kazi ya kikundi
    Jiunge na wanafunzi wenzako. Jadilianeni kuhusu umuhimu wa wanyama wa porini nchini Rwanda.

    D . Matini ya Kiswahili kuhusu kilimo na ufugaji pamoja na vipengele vya kisarufi
    Nomino
    Je, unakumbuka maana na aina za nomino ulizosoma katika kidato cha kwanza?
    Zitaje.
    Nomino ni neno linalotaja mtu, kitu, hali au jambo. Zipo aina mbalimbali za nomino.
    Zifuatazo ni baadhi ya nomino hizo.

    a) Nomino za pekee
    Nomino za pekee hutaja vitu au watu wenye sifa za kipekee. Zinapoandikwa katika
    sentensi, lazima zianze kwa herufi kubwa hata zikiwa katikati au mwishoni mwa
    sentensi. Kumbuka hapa ya kuwa majina haya hayachukui hali ya wingi.
      Mifano ya nomino za pekee katika sentensi.
    i) Rwanda ni nchi yenye wanyama wengi wa porini.
    ii) Mukangango ananyoa sufu ya kondoo.
    iii) Mwenyezi Mungu atujalie mvua nyingi ili tulime.
    iv) Kigali ni jiji linalopendeza.


    Zoezi

    a) Andika sentensi sahihi ukitumia nomino hizi za pekee:
        i) Munyana        ii) Kamana          iii) Mola
      iv) Mei                 v) Mto Kivu          vi) Msitu wa Nyungwe
    b) Tambua makosa katika sentensi hizi na uyarekebishe.
        i) Mimi na kayitesi tunapenda somo la kilimo.
        ii) Nitavuna mihogo yangu mwezi wa februari.
        iii) Ng’ombe anaitwaje kwa kinyarwanda?

    b) Nomino za kawaida
    Nomino za kawaida hutaja vitu vya kawaida vinavyoweza kuchukua umoja na
    wingi kama jina lolote lile. Nomino hizo zinapoandikwa, huchukua herufi ndogo
    isipokuwa pale zinapojitokeza mwanzoni mwa sentensi.

    Mifano ya nomino za kawaida:
    i) Nomino za viumbe wenye uhai:
      
    ii) Nomino zinazomtambulisha mtu na kazi yake:
         

    iii) Nomino za vitu vya kawaida
       
    iv) Nomino za mahali: shambani, uwanjani, mbugani, zizini, porini
    Kumbuka hapa kuwa nomino hizi za mahali huundwa kwa kuongeza ‘ni’ mwishoni
    mwa nomino husika.

    Mifano ya matumizi ya nomino za kawaida katika sentensi.
    i) Mavuno ya mwaka huu ni mazuri.
    ii) Niletee jembe hilo.
    iii) Sufu za kondoo hutumiwa kutengenezea sweta.
    iv) Mkulima hodari hupata mazao mengi.
    v) Ndovu ni mnyama mkubwa wa porini.

    Zoezi

    Tunga sentensi kumi sahihi ukitumia nomino za kawaida.

    c) Nomino za jamii
    Nomino za jamii pia huitwa nomino za makundi. Hizi ni nomino ambazo hutaja
    jumla ya vitu vingi au vitu katika makundi.

    Mifano ya nomino za jamii:


    Mifano katika sentensi
    i) Makole ya ndizi yamevunwa.
    ii) Matuta yamepigwa shambani.
    iii) Matita ya kuni yatatumika kuchomea nyama.
    iv) Mitumba ya aina hii haifai wakulima.
    v) Bunge letu limetenga pesa nyingi kwa wizara ya kilimo.
    vi) Baraza la wafuga farasi limevunjwa.
    vii) Hili ni robota la pamba.

    Zoezi

    Fanya utafiti kupata nomino kumi zaidi za jamii. Tunga sentensi ukitumia kila
    nomino hizo katika umoja na wingi.

    d) Nomino za dhahania
    Katika kikundi hiki hupatikana nomino ambazo ni za kufikirika tu na wala
    haziwezi kuguswa. Chukua nomino kama urafiki. Urafiki ni neno la kufikirika au
    kudhaniwa tu na wala haliwezi kuonekana wala kushikika. Nomino hizi haziwezi
    pia kuhesabika.
    Mifano katika sentensi
    i) Upanzi hufanywa mvua inapoanza kunyesha.
    ii) Kilimo kinasaidia kumaliza umaskini nchini Rwanda.
    iii) Ushirikiano wao katika kupalilia unawafaidi.
    iv) Fikira za wafugaji hao ni za hekima.
    v) Tutafanya uvunaji mwezi ujao.

    Zoezi

    Tunga sentensi zozote kumi kuhusu kilimo na ufugaji ukitumia nomino za jamii.

    e) Nomino za wingi
    Hizi nazo ni nomino za vitu ambavyo daima hupatikana kwa wingi pekee au umoja
    pekee. Vitu vinavyotajwa na nomino hizi haviwezi kugawika.

    Mifano ya nomino za wingi:
    maziwa, sukari, chumvi, uji, chai, manukato, mvua na kadhalika.

    Mifano katika sentensi:
    i) Sukari ni zao la miwa.
    ii) Maua yale hutumiwa kutengenezea manukato.
    iii) Chai hii ni tamu.
    iv) Maji yanyunyiziwayo hapa ni ya mto huo.

    Zoezi

    Soma kifungu kilichopo hapa chini. Tambua na uanishe nomino mbalimbali kifunguni.
    Hapa nchini Rwanda, Mwenyezi Mungu ametujalia mazingira mazuri yenye
    kufanikisha ufugaji. Ufugaji ni kazi ya kutunza wanyama, ndege na hata wadudu.
    Mfugaji anaweza kufuga wanyama ama wadudu. Ikiwa ni wanyama, anaweza
    kutunza ng’ombe, mbuzi, kondoo, farasi, nguruwe, na kadhalika. Ikiwa nia yake ni
    kufuga ndege, anaweza kuwatunza kuku, bata na kadhalika. Hata hivyo, akichagua
    wadudu huweza kuwafuga nyuki.
    Ufugaji una kazi nyingi sana. Kwa mfano, mfugaji wa ng’ombe anapotaka matokeo
    ya kuridhisha, itambidi atumie njia za kisasa katika ufugaji wake. Kwanza kabisa, ni
    lazima awatafute ng’ombe bora wa maziwa. Ng’ombe hawa huleta mapato ya juu.
    Mbali na hayo ni sharti ahakikishe kwamba wanyama wake wana lishe ya kutosha
    hasa kwa ng’ombe wanaokaa ndani kwa ndani. Ng’ombe hawa, hasa ng’ombe jike,
    wa kukaa ndani kwa ndani hulishiwa zizini na kulala humo humo zizini. Hata hivyo,
    ni lazima zizi hilo liwe safi na ng’ombe huyo alale pahali safi. Kukosa kufanya hivyo
    ni kukaribisha magonjwa ya namna kwa namna.
    Iwapo mfugaji atawalisha wanyama wake vizuri, atafaidika pakubwa. Ataweza
    kupata maziwa ya kutosha. Atauza maziwa hayo na kujinunulia bidhaa nyinginezo
    kama vile chumvi, sukari, chane za ndizi na kadhalika. Umaskini pia utaisha.

    Vivumishi
    Je, unakumbuka vivumishi mbalimbali mlivyosoma katika kidato cha kwanza?
    Kwa kawaida, kivumishi ni neno linaloongezea nomino maana. Zipo aina mbalimbali za
    vivumishi. Baadhi ya vivumishi hivyo ni:

    a) Vivumishi vya sifa
    Haya ni maneno yatajayo tabia au sifa za kitu, mtu ama jambo.
    Zipo aina mbili za vivumishi vya sifa: vivumishi vya sifa vinavyochukua viambishi na
    vivumishi vya sifa visivyochukua viambishi.

    Mifano ya vivumishi vya sifa vinavyochukua viambishi:
    -aminifu         -zuri
    -pana             -kubwa
    -pya               -dogo
    -bovu             -fupi

    Kumbuka kuwa kiambishi au viambishi vinavyochukuliwa na vivumishi hivi hutegemea ngeli.
    Mifano katika sentensi:

    ii) Vivumishi vya sifa visivyochukua viambishi
    Hivi ni vivumishi ambavyo havibadiliki katika umoja na wingi au kutoka ngeli moja
    hadi nyingine; hubakia jinsi vilivyo.
    Mifano: bora, safi, hodari, bandia, haba, duni, laini na kadhalika.

    Mfano katika sentensi.
     


    Zoezi

    a) Tunga sentensi sahihi kuhusu kilimo na ufugaji katika umoja na wingi ukitumia vivumishi hivi vya sifa.
        i) -baya          ii) -fupi           iii) -dogo
       iv) -ingi           v) -chache
    b) Tunga sentensi sahihi ukitumia vivumishi hivi katika umoja na wingi.
       i) bora           ii) dhalimu       iii) duni
      iv) tele            v) laini
    c) Andika sentensi hizi katika umoja au wingi.
       i) Nipe ndizi chache.
      ii) Mhindi mrefu unafaa.
     iii) Farasi wakubwa watatubeba.
     iv) Zizi safi halileti magonjwa.
      v) Upanzi bora ni huu.
     vi) Mkulima nadhifu anapita.
    d) Tunga sentensi zozote kumi kuhusu wanyama wa porini na kilimo zenye
         vivumishi vya sifa katika umoja na wingi.

    b) Vivumishi vya pekee
    Vivumishi vya pekee hutoa habari kuhusu nomino au kiwakilishi chake kwa njia ya
    kipekee. Vivumishi vya peke ni sita katika Kiswahili kama ifuatavyo:

    i) -enye
    Huonyesha hali ya ‘kuwa na’ au ‘kumiliki’. Ni sharti kivumishi hiki kifuatwe na nomino wala si kitenzi.

    ii) -enyewe
    a) Hutumika mwanzoni mwa sentensi kuonyesha jambo au kitu kinachotarajiwa.

    b) Hutumika mwishoni mwa sentensi kuonyesha kuwa jambo limetokea bila
        kusababishwa na yeyote au chochote.
      
    iii) -ote
    Huleta maana mbili:
    a) Kuonyesha kila sehemu ya kitu hasa katika umoja.
     
    b) Kuonyesha kila kitu; bila kubakisha lolote hasa katika wingi.

    Zoezi

    Eleza maana ya sentensi ikiwa ni ‘kila sehemu’ au ‘kila kitu’.
    i) Zizi lote limefagiliwa.
    ii) Mazao yote yamevunwa.
    iii) Paka amekunywa maziwa yote.
    iv) Ndizi yote imeiva.
    v) Simba wote wamepita.

    iv) -o-ote
    Huonyesha mojawapo ya vitu au baadhi ya vitu bila kubagua.

    Zoezi

    Tumia ‘-ote’ au ‘-o-ote’ pamoja na viambishi sahihi vya ngeli kujazia pengo katika sentensi zifuatazo.
    1. Nitatumia jembe _____ nitakalopewa.
    2. Miharagwe _________ imemea.
    3. Kuku ______ wamepewa chakula.
    4. Sitachukua nanasi ____________.
    5. Fyeka nyasi____________.

    v) -ingine
    Kivumishi hiki cha pekee huweza kuwa na maana tatu:
    a) Kuonyesha kitu tofauti na kile kilichotajwa au kilichopo.
     

    b) Kuonyesha kitu zaidi/nyongeza


    c) Kuonyesha ‘baadhi ya’


    vi) -ingineo
    Kivumishi hiki hutumika kuleta maana mbili:
    a) 'zaidi ya'

    b) Kuonyesha hitimisho ya orodha ambayo haikukamilika.
      

    Zoezi

    a) Tumia ‘-ingine’ au ‘-ingineo’ pamoja na viambishi sahihi vya ngeli kujazia mapengo.
        i. Amevuna mananasi ____________.
        ii. Sitaki panga hili, nipe panga _____________.
       iii. Mama amepanda mbegu za maharagwe, mtama, mahindi na _____________.
       iv. Usiwakame ng’ombe __________. Maziwa haya yametosha.
       v. Mpe migomba hiyo na ______________.
    b) Tunga sentensi tano sahihi kuhusu kilimo na ufugaji katika umoja na wingi
         ukitumia nomino zozote na kivumishi cha ‘-ingine’.
    c) Tunga sentensi tano sahihi kuhusu wanyama wa porini na mifugo katika
         umoja na wingi ukitumia nomino zozote na kivumishi cha ‘-ingineo’.

    c) Vivumishi vionyeshi
    Vivumishi vionyeshi au viashiria ni maneno ya kuonyesha alipo mtu au kitu, yaani
    ujirani. Kuonyesha huko kunaweza kuwa kwa ujirani wa karibu – hapa, ujirani wa
    mbali kidogo – hapo, na ujirani wa mbali – pale.

    Mifano ya vivumishi hivi ni hii ifuatayo:

    Mfano katika sentensi:
    i) Kijijini humu mna mfugaji hodari.
    ii) Hizi juhudi zenu za kulima zitamaliza umaskini.
    iii) Ng’ombe wale wanakunywa maji.
    iv) Fyekeo hilo halikati majani.
    v) Shambani pale pamepaliliwa.

    i) Vivumishi vionyeshi radidi
    Vivumishi hivi hutokana na kurudia vivumishi vionyeshi. Huleta maana ya kutilia mkazo.

    ii) Vivumishi vionyeshi visisitizi
    Hutumiwa kusisitiza jambo.

    Zoezi

    a) Jaza kila pengo kwa vivumishi sahihi vilivyowekwa katika mabano.
        i. Mazao __________ yatajaza guni. (vionyeshi visisitizi vya karibu)
        ii. Mkulima _________ analima. (vionyeshi vya mbali)
       iii. Twiga __________ ni wengi. (vionyeshi viradidi vya mbali kidogo)
       iv. Nyama __________ ni tamu. (vionyeshi vya karibu)
       v. Wafugaji _________ wana bidii. (vionyeshi vya mbali kidogo)
    b) Tunga sentensi tano tano kuhusu kilimo na ufugaji katika umoja na wingi
         ukitumia vivumishi vionyeshi, vivumishi vionyeshi rejeshi na vivumishi
         vionyeshi visisitizi.

    d) Vivumishi vya idadi
    Vivumishi vya idadi ni maneno yanayoonyesha idadi ya watu ama vitu.
    Vipo vivumishi vya idadi kamili, vivumishi vya idadi ya jumla na vivumishi
    vya idadi ya matokeo.

    i) Vivumishi vya idadi kamili
    Pia huitwa vivumishi vya idadi halisi au bainifu. Huonyesha hesabu halisi ya nomino
    husika.Baadhi ya vivumishi hivi huchukua viambishi vya ngeli kutegemea nomino
    inayohesabiwa.
    Mfano: -moja, -wili, -tatu, -nne, -tano na -nane.

    Baadhi ya vivumishi vya idadi kamili havichukui viambishi vyovyote vya ngeli.
    Yaani hutumika jinsi vilivyo bila kubadilika.
    Mfano: sita, saba, tisa na kumi, makumi, mia na kadhalika

    ii) Vivumishi vya idadi ya jumla/isiyo kamili
    Huonyesha idadi ambayo ujumla wake haujulikani. Baadhi ya vivumishi hivi
    huchukua viambishi vya ngeli ya nomino.

    Mfano: -chache na –ingi

    Mfano katika sentensi:
    1. Kuku hawa wametaga mayai machache.
    2. Mwaka huu tumepanda mbegu nyingi.
    3. Wakulima wengi wamevuna.
    4. Wao huuza maziwa mengi sana.
    Baadhi ya vivumishi vya idadi ya jumla havichukui viambishi vya ngeli.
    Yaani hubakia vivyo hivyo.
    Mfano: kadhaa, tele, kiasi, kidogo na haba.


    iii) Vivumishi vya idadi ya matokeo
    Pia huitwa vivumishi vya nafasi katika orodha. Vivumishi hivi huonyesha nafasi ya
    nomino katika orodha.

    Zoezi

    a) Jaza kila pengo kwa kivumishi sahihi katika mabano.
       i. Sungura ________ wanakimbia. (chache)
      ii. Masokwe __________ wanacheza. (sita)
     iii. Mkulima __________ atapewa mbolea. (moja)
     iv. Amenunua maembe_________. (ingi)
      v. Tumelima mashamba___________. (nane)
    b) Tunga sentensi kumi sahihi kuhusu kilimo na ufugaji ukitumia vivumishi vya
         idadi jumla na isiyo jumla.

    e) Vivumishi viulizi
    Hili ni kundi la vivumishi ambalo lina maneno yatumiwayo kuulizia maswali.
    Baadhi ya mifano ya vivumishi viulizi ni:

    i) Kiulizi -pi?

    ii) Kiulizi -ngapi?

    iii) Kiulizi gani?
    Kiulizi hiki hakichukui kiambishi chochote cha ngeli.

    Tanbihi
    Kivumishi kiulizi kinastahili kuandamana na nomino au kiwakilishi cha nomino.
    Viulizi ambavyo havitumiwi pamoja na nomino au viwakilishi vya nomino haviwezi
    kuitwa vivumishi bali ni viulizi.
    Mfano: lini, nani, nini, vipi. Hivi si vivumishi viulizi kwa sababu havitumiwi pamoja
    na nomino au kiwakilishi cha nomino.

    Zoezi

    a) Tumia kiulizi ‘-pi’ kwa usahihi kujazia kila pengo.
       i. Mashirika _________ yanasaidia wakulima?
      ii. Mkahawa __________ unakatwa?
     iii. Dawa _________ zinanyunyiziwa mimea?
     iv. Niwaite wafugaji ________?
     v. Kufyeka _______ kunafaa?
    b) Tumia kivumishi kiulizi ‘-ngapi’ kwa usahihi kujazia kila pengo.
     i. Tukupe magunia __________?
    ii. Pembe _________ zimekatwa?
    iii. Mbwa _________ wamechanjwa?
    iv. Mipera ___________ inapandwa?
    v. Vibuyu _________ vina maziwa?

    f) Vivumishi vimilikishi
    Maneno katika kundi hili la vivumishi hujibu swali mtu, kitu au jambo ni la nani au
    lina nini? Vivumishi hivi huwa sita pekee katika Kiswahili.
    -angu            -etu
    -ako              -enu
    -ake              -ao

    Kutokana na haya, unapata maneno kama vile:
    wangu               wetu
    chako                chenu
    kwake                kwao

    Unaweza kutunga sentensi hizi ukitumia vivumishi vimilikishi:
    1. Jibini hii ni yangu.
    2. Mawele yako yameliwa na fukusi.
    3. Mbatata zenu zinauzwa Zambia.
    4. Njugu za kwao ni tamu mno.
    5. Huwezi kusema kuwa huu ni mchicha wako!

    Zoezi

    Jaza kila pengo kwa kivumishi kiwakilishi sahihi.
    1. Nyinyi mna mihogo. Mihogo ni ___________.
    2. Sisi tuna maembe. Maembe ni _____________.
    3. Wao wana sufu. Sufu ni _____________.
    4. Mimi nina sukari. Sukari ni ____________.
    5. Yeye ana kole la ndizi. Kole ni __________.
    6. Wewe una muhogo. Muhogo ni _____________.

    Kazi ya wanafunzi wawili wawili
    Jiunge na mwanafunzi mwenzako. Someni kifungu kifuatacho huku mkitambua jinsi
    vivumishi vilivyotumiwa.
    Mimi ni mwanafunzi mwenye bidii. Nia yangu kuu maishani mwangu ni kuridhika
    na shughuli za kilimo cha kisasa kama mojawapo ya njia nzuri za kupigana dhidi
    ya umaskini. Lengo langu kuu la kwenda shuleni hasa ni kupata maarifa mema ya
    kuniwezesha kuishi maisha ya kitajiri. Maarifa hayo yataniwezesha kuwa mkulima
    bora.
    Nitaendelea na masomo hadi chuo kikuu. Nitafanya somo la Kilimo katika chuo
    kikuu. Hata hivyo, hilo pekee halitatosha. Nitafanya kazi ndogo ndogo kwa muda
    ili kutafuta pesa za kuanzisha kilimo. Kufikia hapo, nitakuwa nimepiga hatua lakini
    bado sitakuwa nimefikia lengo langu.
    Kuanzisha kilimo cha kisasa kutakuwa ni hatua kubwa lakini bado kutakuwa
    na kazi kubwa ya kufanywa. Ni sharti niupige vita vikali umaskini kupitia kilimo
    hicho. Umaskini ni adui mbaya ambaye lazima niangamize. Njia moja ya kumaliza
    umaskini ni kuweka uvivu kando.
    Mbali na kulima, nitafuga mifugo wengi. Nitahakikisha ya kuwa nina vifaa vyote
    vinavyohitajika kwa kufanyia kazi hizo mbili. Kutakuwa na trekta kubwa kubwa
    na mashine za kukamua. Nitanunua magari mazuri ya kusafirisha mazao mengi
    nitakayovuna. Nitawapa vijana wenzangu kazi ili nao wawe na kipato kizuri. Kwa
    jumla, nitahakikisha kuwa vitu vyote anavyohitaji mkulima wa kisasa vipo.
    Mwisho, nitatafuta masoko mazuri na ya kuaminika. Nia yangu hapa ni kuuza
    bidhaa zangu katika masoko yaya haya ya hapa kwetu. Baadaye nitaziuza katika
    masoko, nje ya nchi yetu. Hizi zote zitakuwa ni juhudi za kuendeleza vita vikali dhidi
    ya umaskini au uchochole.

    Zoezi

    1. Orodhesheni vivumishi vyote vilivyomo kifunguni humu kwa kuzingatia aina
        ya kila kivumishi husika.
    2. Tunga sentensi fupi fupi na sahihi ukitumia vivumishi mlivyoorodhesha hapo juu.

    Viwakilishi
    Viwakilishi ama vibadala ni maneno ama viambata (sehemu za maneno)
    vinavyosimama badala ya majina. Kundi hili la maneno huweza kugawika katika
    sehemu mbalimbali ifuatavyo.

    a) Viwakilishi nafsi
    Husimamia nafsi za nomino inayozungumziwa katika umoja au wingi. Kuna aina
    mbili kuu za viwakilishi vya nafsi:

    i) Viwakilishi nafsi huru
    Huwakilisha nafsi iliyo huru, yaani isiyounganishwa na kitenzi katika umoja na
    wingi kwenye sentensi.
    Mfano: nafsi ya kwanza (mimi, sisi), nafsi ya pili (wewe, nyinyi), nafsi ya tatu (yeye, wao).

    Zoezi

    Umoja                                                    Wingi
    1. Mimi ninalima.                                   Sisi tunalima.
    2. Wewe unavuna.                               Nyinyi mnavuna.
    3. Yeye anafyeka.                                Wao wanafyeka.

    ii) Viwakilishi nafsi viambata
    Viwakilishi hivi huambatanishwa na vitenzi.
    Mfano: nafsi ya kwanza (ni-, tu-), nafsi ya pili (u-, m-) nafsi ya tatu (a-, wa-)
    ii) Pia, vipo viwakilishi ambata vya ngeli. Navyo ni:
    b) Viwakilishi vitokanavyo na vivumishi
    Je, unakumbuka vivumishi ulivyosoma hapo juu? Endapo kivumishi husika
    kimetumika badala ya nomino, kivumishi hicho kinakuwa kiwakilishi. Nacho
    kiwakilishi hicho huchukua jina la kivumishi hicho. Mfano:
    i) Viwakilishi vionyeshi
    Hutokana na vivumishi vionyeshi. Tazama vivumishi vionyeshi. Unapoondoa
    nomino katika vivumishi hivyo, unapata viwakilisihi vionyeshi.
    Kumbuka kwamba hufai kutumia nomino na kiwakilishi katika sentensi moja.

    ii) Viwakilishi viulizi
    Viwakilishi hivi vinatokana na vivumishi viulizi.
    iii) Viwakilishi vimilikishi
    Viwakilishi hivi hutokana na vivumishi vimilikishi. Tazama mifano hapa chini.

    Zoezi A

    Tunga sentensi ukitumia viwakilishi mbalimbali.

    Zoezi A

    Soma kifungu kifungu kifuatacho huku ukitambua jinsi viwakilishi vilivyotumiwa.
    Zama hizo, fisi alikuwa jirani ya binadamu aliyependa kulima. Binadamu alimiliki
    shamba kubwa la mihogo. Naye Fisi alikuwa mvivu aliyependa kumtembelea
    binadamu kwake. Alidhani kuwa huyo binadamu naye alimpendana sana. Hata
    hivyo, binadamu hakumpenda sana fisi. Fisi hakupenda kulima bali alipenda sana
    kula.    
                                       
    Siku moja jioni, fisi alimuaga binadamu na kusema,    “Kesho nitaamkia huku kwako ili uniandalie kiamshakinywa! ”Kwa roho ya ndani, mwanadamu alijisemea, ‘Huyu hapendi kufanya kazi, anapenda tu kula. Kwa nini haoni kuwa simpendi?’Akamwambia fisi, “Labda utanipata, labda utanikosa.”
    Fisi kuona kuwa anaweza kukosa mlo alisema, “Basi nitajaribu nije hata mapema zaidi. Kwa namna hiyo tunaweza kula halafu wewe uende shambani. Napenda sana namna unavyopika nyama.” Bila kungoja jawabu, alitoka na kujiendea zake.
    Keshoye, mwendo wa saa kumi na moja asubuhi, fisi alibisha hodi kwa mwanadamu. Naye mwanadamu hakusita kumfungulia mlango. Mwanadamu aliazimia kumfunza fisi adabu.
    “Karibu, karibu kwangu rafiki yangu,” mwanadamu alijibu.
    Naye fisi kwa kusukumwa na njaa yake ya asubuhi pamoja na ulafi wake, alimpita
    tu na kuingia ndani. Harufu ya nyama mle ndani ilimfanya fisi ameze mafunda ya mate.
    “Karibu, karibu kaa,” mwanadamu alimlaki fisi. “Nipe dakika chache tu na chakula
    kitamu na kingi kitakuwa mezani hapa.”
    “Basi fanya haraka. Ninakufa kwa njaa,” fisi alisema.
    Baada ya muda usiokuwa mrefu vile, mwanadamu alikuwa ameandika meza
    kwa kila namna ya nyama ya mifupa. Ohoo! Fisi kuona hivyo, nusura kuirukia
    lakini mwanadamu akamzuia kwa kusema, “Bwana fisi, ili leo ushibe vya kutosha,
    tumbukiza kila sahani mdomoni mwako na umeze tu bila kutafuna.
    ”Hata kabla ya mwanadamu kumaliza usemi wake, fisi alikuwa ametumbukiza
    sahani mbili kinywani mwake!
    “Mbona hiki cha leo ni kikali jinsi hii? Lo! Kinawasha sana! Loooooooooo!”
     Fisi alilalamika.
    Kumbe mwanadamu alijaza pilipili kwenye nyama. Tangu siku hiyo, fisi hakurudi
    tena kwa mwanadamu.

    Maswali
    1. Je, fisi alikuwa mnyama wa aina gani?
    2. Ni kwa nini mwanadamu hakumpenda fisi?
    3. Mwanadamu aliikomeshaje tabia mbaya ya fisi?
    4. Unadhani ni yapi yaliyompata fisi?
    5. Jiunge na mwanafunzi mwenzako. Bainisheni viwakilishi vyote vilivyomo
        katika kifungu mlichosoma hapo juu. Tungeni sentensi sahihi mkitumia
        vivumishi hivyo.

    Vielezi
    Vielezi pia huitwa viarifa. Ni maneno yafafanuayo vitenzi, vivumishi au vielezi
    vingine. Mathalan, ukisema Anatembea haraka, neno 'haraka' linaeleza jinsi
    anavyotembea mhusika. Kwa hivyo, neno hilo linalokuarifu mengi kuhusu
    kutembea ni kielezi.
    Maneno haya hujigawa katika vikundi mbalimbali kama ifuatavyo:

    a) Vielezi vya namna au jinsi
    Haya ni maneno ambayo huarifu jinsi ya kutendeka mambo.
    Mfano: sana, bure, kitoto, vizuri, upesi, kwa miguu, kwa bidii, bwe!
    b) Vielezi vya wakati
    Nayo haya ni maneno yanayofafanua ama kueleza wakati wa kutokea tendo.
    Mathalan, ukisema Mgeni alifika jioni neno jioni ni kielezi cha wakati.
    Vipo vielezi vya wakati vya aina mbili:

    i) Vielezi vya wakati maalumu.
    Mfano: Januari, Disemba, Jumamosi, saa tatu, kesho, leo, mtondo na kadhalika.
    ii) Vielezi vinavyotaja wakati kwa jumla
    Mfano: baadaye, zamani, daima, milele, awali, punde, karibuni, zama hizo.

    c) Vielezi vya kiasi/idadi
    Vielezi vya kiasi ni namna ya maneno ambayo hufafanua vitenzi kwa kujulisha
    limetokea mara ngapi tendo linalotajwa.

    d) Vielezi vya mahali
    Haya nayo ni maneno ama mafungu ya maneno yanayofafanua panapotokea kitendo.
    Mara nyingi, maneno haya huwa ni majina ya mahali.

    Zoezi

    Jiunge na wenzako watatu na mworodheshe vielezi vyote vilivyomo kifunguni humu
    huku mkivitungia sentensi fupi na sahihi.
    Gakwerere alikuwa mfugaji mwenye bidii nyingi sana tangu zamani. Mwanzoni,
    Gakwerere alikuwa akifuga ng’ombe wa kienyeji. Aliwalisha ng’ombe hao uwanjani
    na pembeni mwa mashamba. Hata hivyo, ng’ombe hao hawakuwa wakimpa kiasi
    cha maziwa alichotarajia. Angewakamua mara moja tu kwa siku. Alikata shauri
    kuanzisha ufugaji wa ng’ombe bora wa maziwa.
    Mfugaji huyu aliwapeleka ng’ombe wake wa kienyeji sokoni na kuwauza mnamo
    Novemba. Baada ya kuwauza, aliamka alfajiri na kufunga safari ya kuzuru shamba
    la kisasa la Nyinawumuntu. Bi. Nyinawumuntu alikuwa mfugaji na mkulima
    mashuhuri sana katika eneo hilo alilokaa Gakwerere. Alipofika huko, alimpata
    bibiye yupo na wakaanza kupiga bei. Baada ya kukubaliana bei, alinunua mitamba
    wawili kwa bei nafuu. Alilipa papo hapo kwa sababu hakutaka kuwa na deni.
    Kumaliza hivi tu, yule bibi alimpa Gakwerere gari lake ili alitumie kuwasafirisha
    ng’ombe wake. Gakwere alimshukuru kwa wema wake na akawasafirisha hao
    mitamba wake hadi kwake.
    Alipofika nyumbani kwake, mfugaji huyo alianza kuwalisha ng’ombe wake kwa njia
    za kisasa. Kwa kuwa walikuwa wakilishwa kwa lishe bora ya ng’ombe, haukuchukua
    muda mrefu kuwapandisha. Muda ulipowadia, walizaa ndama wawili wenye afya
    nzuri.
    Baada ya muda usio mrefu, Gakwerere alianza kuvuna matokeo ya jasho lake la kila
    siku. Hakuamini kiasi cha maziwa alichokuwa akikama kila asubuhi na jioni.
    Aliweka akiba kwa muda. Hatimaye, mfugaji huyu alinunua gari. Alitumia gari hilo
    kuwatafutia na kuwabebea chakula ng’ombe hao wake wa gredi.

    E . Matumizi ya wakati uliopo na uliopita na vitenzi vya silabi moja
    i) Matumizi ya wakati uliopo (-na-) na vitenzi vya silabi moja
    Wakati uliopo -na-unaweza kuwa katika hali mbili: Hali hizo ni hali yakinishi na hali
    kanushi. Hali yakinishi ni ya ukubali na hali kanushi ni ya ukatavu.
    Soma sentensi hizi.

    Hali yakinishi
    Hali yakinishi ni hali ya kukubali. Tazama tena mifano iliyopo hapo juu. Vitenzi
    unakufa, anakula, anakunywa, anakuja, anampa na inanyesha vimo katika hali
    yakinishi, yaani hali ya kukubali.
    Hali kanushi
    Nayo hali kanushi ni hali ya kukataa. Itazame tena mifano hapo juu. Vitenzi haufi,
    hali, hanywi, haji, hampi na hainyeshi vipo katika hali kanushi, yaani hali ya kukataa.

    Unaweza kutunga sentensi zaidi za namna hii kama ifuatavyo:

    Kazi ya wanafunzi wawili wawili
    Jiunge na mwenzako. Tafuteni vitenzi zaidi vyenye silabi moja katika kamusi huku
    mkijadiliana mabadilko ambayo hutokea vitenzi hivyo vinapotumiwa katika hali
    kanushi na yakinishi.

    ii) Matumizi ya wakati uliopita -li- na vitenzi vya silabi moja
    Wakati uliopita huonyesha kuwa kitendo kilifanyika muda mrefu uliopita. Wakati
    huu huwakilishwa na -li-. Vitendo husika vinaweza kuwa katika hali yakinishi au
    kanushi. Kama ujuavyo, hali yakinishi ni ya kukubali na hali kanushi ni kukataa.

    Tazama mifano ifuatayo:

    Vitenzi hivyo vipo katika wakati uliopo. Tunaweza kuvigeuza viwe katika wakati
    uliopita kwa kuweka ‘-li-‘ mahali pa ‘-na-‘. Tunapofanya hivyo, tunamaanisha kuwa
    vitendo hivyo vilifanyika muda au wakati uliopita. Tazama jedwali hili.

    Tazama mifano ifuatayo:


    Katika jedwali lililopo hapo juu, vitenzi ulikufa, alikula, alikunywa, alikuja, alimpa,
    na ilimnyeshea vimo katika hali yakinishi au kukubali kwa wakati uliopita. Navyo
    vitenzi haukufa, hakula, hakunywa, hakumpa, haikumnyeshea vimo katika hali ya
    kukataa yaani hali kanushi.

    Mazoezi ya ziada

    Zoezi A

    Jiunge na mwanafunzi mwenzako na mworodheshe vitenzi vinane vya silabi moja
    huku mkivitungia sentensi sahihi katika wakati uliopita. Sentensi zenu zihusiane na
    kilimo na ufugaji. Someaneni vitenzi na sentensi huku mkisahihishiana.

    Zoezi B

    Jiunge na wanafunzi wenzako katika kikundi. Msomeane tungo au hadithi
    mbalimbali zilizopo katika kitabu hiki na vitabu vingine. Mbainishe na kuainisha aina
    za maneno katika tungo hizo (vivumishi, viwakilishi na vielezi) kama vinavyotokea
    katika umoja na wingi pamoja na matumizi ya wakati uliopo na wakati uliopita.
     
                              Maswali ya marudio
    li kujikumbusha mengi ya yale uliyojifunza katika sehemu hii, yajibu vilivyo maswali
    haya yafuatayo yote.
    1. Bila ya kuangalia popote, taja maneno kumi yanayohusu mazao na kumi
        yanayohusu ufugaji huku ukiyaeleza.
    2. Ipo misimu mingapi hapa Rwanda? Ieleze huku ukirejelea upanzi na uvunaji
        wa mimea.
    3. Tazama picha zifuatazo. Eleza misimu kulingana na kila mchoro.

    4. Tunga sentensi sahihi ukitumia msamiati ufuatao:
        a) mahindi
        b) ndizi
        c) kahawa
        d) viazi mviringo
        e) maharagwe
        f ) njugu
    5. a) Jaza kila pengo kwa jina sahihi la kifaa cha kilimo.
         i) Ndoli anafyeka shamba kwa ______________.
        ii) Mkulima yule anatumia _________ la mkono kulimia shamba lake.
       iii) Shamba kubwa hulimwa kwa _______________.
       iv) __________ hutumiwa kukata matawi ya miti shambani.
    6. Tunga sentensi tano fupi ukitumia vifaa mbalimbali vya kilimo ambavyo vinatumiwa katika eneo utokako.
    7. Eleza jinsi unavyopanga kupiga vita uchochole kwa kilimo cha kisasa.
    8. Taja majina kumi ya mifugo nchini Rwanda na uyatungie sentensi sahihi.
    9. Taja chuo cha kilimo hapa nchini ambacho ungependa kukiingia baada ya
         masomo yako huku ukieleza ni kwa nini unakistahi chuo hicho.
    10. Eleza umuhimu wa ufugaji katika jamii unapotoka.
    11. Zipo tamaduni zozote za kikwenu zihusuzo kilimo na ufugaji? Zitaje
         huku ukieleza huo uhusiano.
    12. Taja wanyama kumi wa porini wanaopatikana nchini Rwanda.
    13. Andika majina na sifa za wanyama wafuatao wa porini:

    14. Eleza faida za wanyama wanaoishi porini.
    15. Pendekeza njia zinazoweza kutumiwa kuwavutia watalii wanaozuru mbuga
          zetu za wanyama wa porini.
    16. Eleza maana ya:
         a) nomino
         b) vivumishi
         c) vielezi
         d) viwakilishi
    17. Huku ukitoa mifano, eleza aina nne nne za:
        a) nomino
        b) vivumishi
        c) vielezi
    18. a) Je, vitenzi vya silabi moja ni maneno ya aina gani?
          b) Andika mifano minne ya maneno yenye silabi moja na uyatungie sentensi sahihi.
    19. a) Huku ukitoa mifano, eleza tofauti zilizopo kati ya:
           i) wakati uliopo na wakati uliopita
          ii) hali kanushi na yakinishi
    b) Andika sentensi zifuatazo katika hali yakinishi au kanushi.
        i) Baba anakula mahindi.
       ii) Mahindi hayafi wakati wa kiangazi.
      iii) Ng’ombe hakunywa maji jana.
      iv) Mkulima alimpa ndizi nyingi.
    c) Andika sentensi zifuatazo katika wakati uliopo au uliopita.
       i) Ndoli anakula mihogo.
      ii) Mimi sinywi maziwa.
     iii) Mama alinipa jembe.
     iv) Kuku hao hawakufa.
    20. Kwa ufupi, elezea mambo muhimu uliyojifunza katika sura hii na useme jinsi
          yatakavyokufaidi na jamii.
Sura 2: Utungaji