• MADA YA 8 DHIMA YA LUGHA YA KISWAHILI KATIKA JAMII

    Uwezo mahususi katika mada hii: 
    Kuonyesha dhima ya lugha ya Kiswahili kwa jamii ya nchi zinazozungumza 
    lugha hii.
    Malengo ya ujifunzaji:
    • Kutoa maana na umuhimu wa lugha,
    • Kusoma na kuelewa kifungu kuhusu lugha kama chombo cha 
    mawasiliano,
    • Kusikiliza kwa makini na kusimulia kwa ufasaha kifungu cha habari 
    kinachohusika,
    • Kujadili namna ya kuitunza lugha na mwenendo unaofaa.
    Kidokezo
    1. Taja lugha zote zinazozungumzwa nchini Rwanda.

    2. Andika dhima nne za lugha ya Kiswahili.

    SOMO LA 29: TUONGEE KISWAHILI SANIFU

    cc

    Kazi ya 1:
    Tazama mchoro hapa juu na kujadili kazi mbalimbali zinazoendelea.
    29.1. Kusoma na ufahamu: Kiswahili nchini Rwanda
    Soma kifungu cha habari kifuatacho kisha ujibu maswali 
    yanayoambatana nacho: 

    Lugha ya Kiswahili ni mojawapo ya lugha nne zinazozungumzwa nchini 
    Rwanda. Hizi ni Kinyarwanda, Kiingereza, Kifaransa na Kiswahili vilevile. 
    Hapo mwanzo, lugha ya Kiswahili ilikuwa lugha ya kibiashara lakini polepole 
    mambo yalibadilika kutokana na ushirikiano wa Rwanda pamoja na nchi 
    jirani zake ambazo ni Kenya, Tanzania, Uganda, Jamhuri ya Kidemokrasia 
    ya Kongo na Burundi zinazotumia lugha ya Kiswahili katika shughuli 
    mbalimbali. 

    Lugha ya Kiswahili ambayo ni chombo cha mawasiliano kwa kupashana 
    habari, nchini Rwanda, imeshamiri na kupata nguvu nyingi baada ya Rwanda 
    kuwa mwanachama wa Jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki, Kiswahili 
    kikiwemo lugha rasmi.

    Lugha ya Kiswahili hufundishwa nchini katika shule za sekondari na vyuo 
    vikuu. Vituo vya utangazaji habari kama vile redio na vituo vya televisheni 
    pia hutumia Kiswahili katika baadhi ya matangazo vinavyorusha. 

    Aidha, lugha ya Kiswahili hutunza, hukuza, na huendelezautamaduniwajamii, 
    bila ya kusahau kwamba ni alama ya utambulisho wa jamii au taifa fulani.
    Kazi ya 2:
    Maswali ya ufahamu

    1. Ni lugha gani zinazozungumzwa nchini Rwanda ?
    2. Kwa sababu gani, nchini Rwanda, lugha ya Kiswahili imekua 
    sana siku hizi?
    3. Onyesha dhima mbili za Kiswahili.
    4. Taja shule zinazofundisha Kiswahili nchini Rwanda .
    5. Je, lugha ya Kiswahili ni lugha ya mawasiliano nchini? Eleza jibu 
    lako kwa kutumia mifano sahihi kutoka kifungu.

    29.2. Matumizi ya msamiati
    Kazi ya 3:
    Toa maana ya maneno yafuatayo:

    1. Dhima 
    2. Ushirikiano
    3. Kupashana 
    4. Maarifa
    5. Utamaduni 
    6. Jamii

    7. Mzawa

    29.3. Sarufi: Matumizi ya hali ya kuamuru

    dd

    Kazi ya 4:
     Tazama michoro hapo juu na kueleza kinachofanyika pale.
    Kazi ya 5:
    Tunga sentensi tano kwa kutumia hali ya kuamuru.
    Maelezo muhimu

    • Katika hali ya kuamuru au ya kushurutisha, vitenzi vya silabi zaidi 
    ya moja na vyenye kiambishi tamati -a, huondolewa tu kiambishi 
    cha kitenzi ku- katika umoja hali yakinishi. Katika wingi, vitenzi hivi 
    huondolewa kiambishi ku- pamoja na kiambishi tamati-a, halafu 
    vikachukua kiambishi -eni badala ya kiambishi -a cha mwishoni.
    Mfano:Kitenzi: kusimama
    Umoja: (Wewe) Simama!
    Wingi: (Nyinyi/ Ninyi) Simameni!
    Kazi ya 6:
    Zikamilishe sentensi zifuatazo kwa kutumia hali ya kushurutisha 
    kwa vitenzi ambavyo vimo katika mabano. 

    Kwa mfano: Swali: Mwalimu aliwaambia wanafunzi: “…….madaftari 
    yenu”. (kuchukua)
     Jibu: Mwalimu aliwaambia wanafunzi: “Chukueni madaftari yenu.”
    1. “…………… kazi yako ya shule kuhusu dhima ya Kiswahili.” Mama 
    alimwamrisha mtoto wake. (fanya)
    2. Mwalimu alimwomba mwanafunzi akisema: “…………… ubao 
    tufanye mazoezi!”(Kufuta)
    3. Baada ya kujiunga na nchi nyingine za Afrika Mashariki viongozi 
    wa Rwanda walituambia: “……… Kiswahili!” (kuzungumza).
    4. Kwa kuwa wewe ni mkazi wa nchi ya Rwanda …………. vizuri 
    lugha ya Kinyarwanda! (ongea)
    5. Mwalimu ameniambia kuwa mtafanya jaribio la Kiswahili kesho; 
    kwa hiyo……… (kurudia) masomo yenu.
    6. Mwalimu aliwaambia wanafunzi: “…………..runinga kuna mchezo 
    wa kuigiza uhusuo uhifadhi wa mazingira!” (kutazama).

    7. Katibu aliombwa na mwenyekiti: “……………….mawazo yote 
    yatakayotolewa mkutanoni!” (kuandika).
    8. Kama unataka kukuza stadi zako za kuzungumza na kusikiliza 
    lugha ya Kiswahili, ……………..matangazo ya redioni na utazame 
    runinga! (kusikiliza)
    29.4. Matumizi ya Lugha: Maana na umuhimu wa lugha 
    katika jamii

    Kazi ya 7:
    Panga maneno yafuatayo kwa utaratibu unaofaa ili yaweze kuleta 
    maana kamili

    1. ni -ya -Kiswahili- Mashariki- muhimu -lugha -Jumuia -ya -Afrika 
    -katika -sana
    2. Kiswahili -mwanzoni -kama- lugha -ilikuwa -ya- hapo- biasharalugha-ikitumiwa -ya.
    3. Walifurahi- rasmi- Wanyarwanda- kusikia- sana- mojawapo- lugha 
    ya- nchini- Kiswahili- kwamba- ni- Rwanda- ya- lugha.
    Kazi ya 8:
    Tunga sentensi kwa kutumia maneno yafuatayo:

    1. Jumuiya
    2. Utamaduni
    3. Matangazo
    4. Jamii
    29.5. Kusikiliza na Kuzungumza: Umuhimu wa lugha ya 
    Kiswahili katika jamii
    Kazi ya 9:

    Jadili kuhusu dhima za lugha ya Kiswahili

    29.6 Kuandika: Utungaji wa kifungu cha habari 

    Kazi ya 10:
    Tunga kifungu kifupi (mistari kumi) ukionyesha faida ya Rwanda 
    kutumia lugha ya Kiswahili

    SOMO LA 30: MAWASILIANO YETU.

    vv


    Kazi ya 1:
    Eleza kinachofanyika kwenye mchoro wa hapo juu.
    30.1. Kusoma na ufahamu: Ziara ya mjini

    Soma kifungu cha habari hiki na kujibu maswali yanayokifuata:
    Siku moja Bwana Mugisha aliondoka zake kijijini Kirenge kuelekea mjini. 
    Alichukua mkoba wake mweusi na kuujaza kila kitu cha kumsadia njiani na 
    mjini vilevile. Alipofika mjini, aliwakuta jamaa wawili mmoja aitwaye Rukundo 
    na mwingine Ruhara.Walisalimiana kwa hamu kubwa kwani siku zilikuwa 
    nyingi bila ya kuonana. 

    Wakati huo huo wasichana watatu Ange, Lidia na Isimbi walipita karibu nao 
    wakiwa wametoka kabisa. Lugha waliyokuwa wanaongea ilimshangaza 
    Mugisha sana kwani ilikuwa mara yake ya kwanza kuisikia.  « Mbona watu 
    hawa siwaelewi hata kidogo, wametoka wapi  ?  » Alitamka haya akiwa 
    na mshangao mkubwa sana. Ruhara ambaye alizoea maisha ya mjini 

    alimwambia, ‘’hii ni lugha ya Kiswahili, lugha nzuri yenye asili ya upwa 
    wote wa Afrika Mashariki.’’ Aliendelea kumsimulia yaliyompata alipokwenda 
    sehemu za Arusha huko Tanzania. ‘’Miaka miwili iliyopita, nilikwenda mjini 
    Arusha katika mkutano wa waumini wa dini moja huko, nilipoingia mjini 
    lugha ilikuwa hiyo, mitaani na migahawani, misikitini na makanisani, kweli 
    sikuwa na tamko lolote isipokuwa kimya tu na kutumia ishara. Kwa bahati 
    nzuri, nilipata usaidizi kutoka kwa raia wa huko kwani baadhi yao walijua 
    lugha nyingi ikiwemo yangu. Baada ya wiki moja, tulirudi kwetu nikiwa na 
    fikra moja kichwani mwangu ya kujifunza Kiswahili na kukizungumza vizuri. 
    Leo nina hatua nzuri. ’’

    Kuyasikia hayo, Mugisha aliunga mkono Ruhara na kusema kuwa naye 
    angepata mwalimu angejifunza Kiswahili. Wote waliendelea na safari zao 
    kwa makubaliano ya kujua lugha zaidi ya moja, msingi wa maendeleo na 
    ushirikiano na wengine.
    Punde si punde mabinti wale Ange, Lidia na Isimbi walimwita Mugisha 
    ambaye alionekana kuwa mgeni mjini. Walisema ‘’ Mzee njoo hapa, tunahitaji 
    kuongea na wewe.’’ Mugisha bila kusita alianza mbio kinyumenyume 
    akihofia kuibiwa au usumbufu mwingine. Yeye aliona wasichana hao kama 
    wakware ambao wanataka awape pesa zake alizokuwa ameficha mkobani 
    chini ya nguo. Ange alimfuata kwa hatua ndefu na maneno ya upole, jambo 
    lililopunguza wasiwasi wake Mugisha na kusimama. 

    Mazungumzo yalianza katika lugha ya Kinyarwanda Ange na wenzake 
    wakimwonyesha umuhimu wa lugha kama chombo cha mawasiliano kati 
    ya jamii fulani. Bwana Mugisha aliwajulisha uamuzi wake ili mara ijayo 
    asije akakabiliana na shida hiyo tena. Walimfundisha maneno machache 
    na kumshauri aendelee kuvifuata vipindi vya redio na televisheni katika 
    Kiswahili. Mugisha aliwaomba namba zao za simu ili kila mara atakapopata 
    shida au atahitaji msaada awapigie simu. Wasichana walimnunulia chakula 
    na chai akala na kushiba. Baadaye, kundi la watatu lilimuaga Mugisha. Tangu 
    siku hiyo, Mugisha hawezi kuidharau lugha na umuhimu wa mawasiliano.

    Kazi ya 2:
    Maswali ya ufahamu
    1. Toa majina ya wahusika katika kifungu cha habari hiki.
    2. Mgeni huyu alishangazwa na nini alipofika mjini?
    3. Kwa sababu gani Ruhara alikuwa kimya na kutumia ishara tu 
    alipokuwa mjini Arusha ? Alisaidiwa na nini ?
    4. Je, mabinti waliokutana na Mugisha walizungumza lugha zaidi ya 
    moja ? Fafanua jibu lako.
    5. Kwa nini Mugisha alianza kukimbia alipoitwa na wasichana ?
    6. Nini kilimridhisha Mugisha katika ziara yake mjini ?
    7. Ingekuwa wewe ungefanya nini baada ya kupata shida ya 
    kimawasiliano ? Jadili.
    30.2. Matumizi ya msamiati kuhusu mawasiliano yetu
    Kazi ya 3:
    Toa kinyume cha maneno haya:
    1. Mzee
    2. Mji
    3. Haraka
    4. Lugha nzuri
    5. Karibu
    Kazi ya 4:
    Jaza sentensi hizi kwa kutumia msamiati unaofaa ulioko katika 
    kifungu

    1. Bwana Mugisha alisaidiwa na……………………….wawili 
    waliomnunulia ………….akala akashiba.
    2. Miaka miwili iliyopita ……………..alikwenda mjini……………..
    katika …….wa waumini.
    3. Ange na ……..waliongea lugha ya………….na lugha ya..... 
    4. Mugisha alidhani wasichana walikuwa ……………..na kukimbia.

    Kazi ya 5:
    Eleza maana ya maneno yanayofuata: 

    a. Mkoba
    b. Jamaa
    c. Mkutano
    d. Kutoka
    e. Fikra
    f. Binti
    g. Mbio
    h. Kuaga
    Kazi ya 6:
    Kamilisha sentensi zifuatazo ili zilete maana kamili kwa kutumia 
    msamiati huu:
    lugha, jumuia, televisheni, simu, ishara.
    1. Kiswahili ni................................ambayo inatumiwa katika 
    ………………….ya afrika Mashariki.
    2. Jamila hufuata vipindi vya………………………kila siku.
    3. Wasichana watapigiwa …………………….. na mzee Karinda.
    4. Mtu asiye na ujuzi wa lugha lazima atumie……..……………….

    30.3. Sarufi: Hali ya kuamuru
    Kazi ya 7:
    Soma mazungumzo yafuatayo na kubainisha vitenzi vilivyotumiwa 
    katika hali ya kuamuru
    Baba: Waambaje, Nikuze?
    Nikuze: Salama babangu. Naona umechoka leo! Tafadhali nenda bafuni.
    Baba: Ehee! Leo nimefanya kazi nyingi bila kupumuzika. Nenda ukaniletee 
    maji na sabuni ya kuogea.
    Nikuze: Ndiyo. Jitayarishe, uchukue taulo na kandambili halafu uende 
    bafuni.
    Baba: Asante sana binti yangu. Niandalie chakula haraka iwezekanavyo 
    nina njaa.
    Nikuze: Chakula kimeiva na ninakaribia kukiweka mezani. Nimekupikia 
    ugali na kitoweo kitamu sana bila shaka utakifurahia. Karibu ndani mama.
    Mama: Asante binti yangu. Habari za nyumbani?
    Nikuze: Nzuri mama. Baba amekuja akiwa amechoka na hivi sasa yumo 
    bafuni.
    Mama: Ni kweli kabisa. Leo amefanya kazi isiyo rahisi. 
    Nikuze : Namwona baba anatoka bafuni usisahau kumpa pole kwa 
    uchovu alio nao.
    Mama: Wewe mwekee chakula na kinywaji mezani, mengine ni yangu. 
    Fanya haraka binti yangu.

    Nikuze: Barabara kabisa.

    Kazi ya 8:
    Tunga sentensi tatu kwa kutumia hali ya kuamuru tungo yakinishi.

    Kazi ya 9:
    Tunga sentensi tatu zenye vitenzi vilivyoko katika hali ya kuamuru 
    tungo kanushi.

    Maelezo muhimu kuhusu hali ya kuamuru / hali ya amri
    Hali ya kuamuru ni ya vitenzi ambavyo vimo katika hali shurutishi au ya 
    kulazimisha yaani mtendaji wa tendo halitendi kwa hiari yake bali ni kwa 
    sharti ya mtu mwingine.
    Huonyesha kuwa mtu analazimishwa kufanya jambo fulani. Hutumiwa kwa 
    nafsi ya pili tu (umoja na wingi).
    Tunafuata kanuni zifuatazo :
    • Vitenzi vyenye silabi nyingi, hupoteza ku- ya kitenzi. Kwa wingi, kitenzi 
    huongezwa «-ni» mwishoni, katika hali yakinishi.
    Mfano: Nyamaza! (Umoja)
     Nyamazeni! (Wingi)
     shukuru! (umoja)
     shukuruni! (wingi)
    • Katika hali kanushi, vitenzi huishia na «-e» isipokuwa vitenzi vya asili 
    ya kigeni.
    Mfano: Usinyamaze! (Umoja)
     msinyamaze! (Wingi)
    • Usirudi! (umoja)
    • Msirudi! (wingi)
    • Vitenzi vyenye silabi moja hubaki na «ku-» ya kitenzi (katika hali 
    yakinishi) na huongezwa «-ni», kwa wingi.
    Mfano: - Kunywa! (umoja)
    • Usinywe!
    • Kunyweni! (wingi)
    • Msinywe!
    • Vitenzi: kuja, kwenda (kuenda) na kuleta, havifuati kanuni hizi.
    Mifano:
    a. Kuja:
    Njoo! (umoja hali yakinishi)
     Usije! (hali yakinishi)
    Njooni! (wingi hali yakinishi)
    Msije! (wingi hali kanushi)
    b. Kwenda/kuenda :
    Nenda! (Umoja hali yakinishi)
     Usiende! (Umujo hali kanushi)
    Nendeni! (Wingi hali yakinishi)
    Msiende! (Wingi hali kanushi)
    c. Kuleta:
    Lete! (Umoja hali yakinishi)
    Usilete! (Umoja hali kamushi)
    Leteni! (Wingi hali yakinishi)
    Msilete! (Wingi hali kanushi)
    d. Kupa:
    Nipe! (Umoja hali yakinishi)
    usinipe! (Umoja hali kanushi)
    Nipeni! (Wingi hali yakinishi)
    Msinipe! (Wingi hari kanushi)
    Kazi ya 10:
    Badilisha sentensi zifuatazo ziwe katika hali ya kuamuru katika wingi. 

    1. Njoo hapa utusalimu!
    2. Kimbia ili usichelewe shuleni!
    30.4. Matumizi ya lugha: Mawasiliano yetu
    Kazi ya 11:
    Jadili maswali yafuatayo: 
    Mawasiliano ni nini?
    Je,ndege na wanyama huwasiliana kwa njia gani?
    Mawasiliano yana umuhimu gani ?

    Maelezo muhimu
    Mawasiliano ni mchakato wa kuhawilisha taarifa kwa njia ya ubadilishanaji wa 
    mawazo, hisia, malengo, tabia, matarajio, mitazamo kupitia mazungumzo, 
    ishara na maandishi. Ni ubadilishanaji wa taarifa unaoleta maana baina ya 
    pande mbili au zaidi ambazo zinaweza kuwa viumbe hai au kinyume chake. 

    Lugha ni chombo cha mawasiliano ambacho amejaliwa binadamu tu na 
    kwamba hakuna kiumbe mwingine ambaye si binadamu mwenye uwezo 
    wa kuzungumza na kutumia lugha. Hii ina maana kuwa kuna sifa fulani za 
    lugha za binadamu ambazo hazipatikani kwa kiumbe mwingine yeyote yule 
    isipokuwa mwanadamu.

    Ingawa ndege, mbwa, nyuki, tumbili wanaweza kuwasiliana, mawasiliano 
    yao huwa ni ya sauti au ishara ambazo kimsingi siyo lugha, pia huwa 
    yanadhibitiwa na hisia tu kama hofu, njaa, na ishara za kutoa taarifa. 

    Binadamu ana uwezo wa kujifunza lugha mbalimbali na kuzitumia katika 
    mazingira yake na kitu ambacho wanyama hawawezi. Kwa mfano, 
    ukimchukua paka wa Uchina na kumleta Rwanda atatoa sauti ile ile sawa 
    na paka wa Rwanda kwa kueleza shida ile ile au kutoa ishara ile ile. 

    Ulishawahi kujiuliza kwamba mawasiliano yangekuwaje pasipokuwepo 
    lugha? Mwalimu angekuwa anatumia mtindo gani kukufundisha darasani au 
    wewe ungemwombaje kalamu rafiki yako? (Unasema ungewasiliana kama 
    wanavyowasiliana watu wasiosikia au kuzungumza?) Hao pia wanawasiliana 
    hivyo kwa sababu wana maarifa ya lugha. Watu wasiosikia au kuzungumza 
    wanawasiliana kwa lugha ya ishara, lugha ambayo inafundishwa katika 
    baadhi ya shule za sekondari na vyuo vikuu nchini Rwanda. 

    Ufumbuzi wa kisayansi na kiteknolojia usingewezekana pasipo kuitumia 
    lugha, usingeweza kusogoa na marafiki zako kwenye fesibuku, usingeweza 
    kumwandikia ujumbe rafiki yako kupitia simu yako na kadhalika. Kiswahili 
    kinatarajiwa kutumika kama chombo cha mawasiliano katika taaluma 
    mbalimbali kama vile utawala na taasisi mbalimbali kama vile bungeni, 
    mahakamani na penginepo.
    Kazi ya 12:
    Jibu maswali yafuatayo:

    1. watu wasiosikia au kuzungumza huwasiliana kwa njia ipi?
    2. Ni tofauti gani kati ya mawasiliano ya binadamu na yale ya viumbe 
    wengine?
    3. Andika njia nne ambamo Kiswahili kinaweza kutumiwa na 
    kurahisisha mawasiliano.
    Kazi ya 13:
    Pamoja na picha hizi, sema ikiwa kuna mawasiliano ya lugha, ya 

    ishara au ya sauti na kujaza jedwali hapo chini:

    vv

    cc

    30.5. Kusikiliza na Kuzungumza: Majadiliano
    Kazi ya 14:
    ”Mawasiliano ya lugha ni bora kuliko mawasiliano ya ishara na 
    sauti.” jadili kauli hii. 
    30.6. Kuandika: Utangaji wa insha
    Kazi ya 15:
    Tunga insha fupifupi ukionyesha umuhimu wa lugha ya Kiswahili 
    nchini Rwanda.
    Kazi ya 16:

    Andika aya mbili kuhusu “umuhimu wa mawasiliano.”

    SOMO LA 31: UMUHIMU WA LUGHA

    cc

    Kazi ya 1:
    Eleza yale unayoyaona kwenye mchoro huu. 
    31.1. Kusoma na ufahamu: Umuhimu wa lugha
    Soma kifungu kifuatacho kuhusu “Umuhimu wa lugha” kisha, jibu 

    maswali uliyopewa hapo chini. 

    Familia ya mzee Yakobo inaishi katika kijiji cha Nyamugari. Kila mara Mzee 
    Yakobo huwahimiza watoto wake Maria na Maria kujifunza lugha mbalimbali 
    kwa madhumuni ya maisha yao ya usoni. Yeye anajua kwamba lugha, kama 
    mfumo wa ishara au sauti nasibu zinazowezesha jamii kuwasiliana, ina 

    umuhimu sana katika maisha ya kila siku. Tangu Maria alipoyasikia maneno 
    ya baba yake aliyazingatia sana mawaidha aliyopewa na kujifunza vizuri 
    lugha zote zilizopatikana kwenye ratiba yake ya masomo. Kwa sasa, yeye ni 
    mkuu wa kitengo cha utalii katika taasisi inayoshughulikia masuala ya utalii na 
    mazingira. Petro ni tofauti na ndugu yake Petro aliyeonyesha mtazamo hasi 
    kuhusu ujifunzaji wa lugha. Yeye alipenda kusema: « Siwezi kupoteza muda 
    wangu kujifunza lugha za watu wengine, lugha ninayozungumza inanitosha». 
    Kwa kweli, alikuwa mtoto mtukutu asiyejali maonyo na mawaidha ya wazazi 
    wake. Kwake, kujisomea hata sentensi fupi za Kiswahili lilikuwa jambo la 
    ajabu! Alikuwa amesitisha masomo yake alipomaliza darasa la pili katika 
    shule ya Sekondari ya Nyamugari ingawa baba yake hakuacha kumuonya 
    kuhusu umuhimu wa elimu na nafasi ya lugha katika maisha ya binadamu. 

    Siku moja, Mzee Yakobo aliamua kwenda kumtembelea binti yake aliyeishi 
    katika nchi jirani. Petro alimsihi waende pamoja kuwasalimia binamu zake 
    ambao ni Kamugisha na Kana. Mzee Yakobo aliposikia maneno ya mtoto 
    wake, hakusita kukubali wazo lake. Alifikiria kwamba mtoto wake angekutana 
    na binamu zake wangemuuliza mengi kuhusiana na masomo yake. Kwa 
    hivyo, Mzee Yakobo alimwomba mtoto wake Petro ajiandae kwa safari. 
    Gari lao lilitoka Nyabugogo saa kumi na moja alfajiri. Walipofika njiani, Petro 
    alishindwa kuvumilia njaa iliyokuwa ikimuuma kutokana na safari ndefu. Kwa 
    bahati nzuri, walipofika katika mji mmoja, dereva aliamua kusimamisha gari 
    ili wasafiri waweze kwenda haja na wengine waweze kujinunulia chakula na 
    kinywaji kabla hawajaendelea na safari yao. Baba yake Yakobo alimwonea 
    huruma mtoto wake na kumpa shilingi mia mbili ili aweze kwenda kujinunulia 
    chakula. Petro alifurahi sana. Alikuwa na hamu ya kula mkate na kunywa 
    juisi ya matunda iliyotengenezewa katika nchi jirani. Alienda haraka na 
    kuingia dukani. Dukani alimkuta Bi Hassani aliyemkaribisha na kumuuliza 
    alichotaka kununua dukani humo. 

    Lo ! Petro alikosa neno. Alisimama akimkodolea macho kama aliyejiingiza 
    baharini bila kujua kuogelea. Kweli alishindwa kuulizia kile kilichomleta 
    pale. Alijitahidi kutumia ishara kumwonyesha sehemu palipowekwa mikate 
    na vyakula vingine lakini mfanyabiashara hakuelewa alichokuwa anahitaji 
    miongoni mwa vyakula vilivyokuwemo dukani. Petro aliposhindwa kusema 
    alichukua shilingi zote alizokuwa nazo na kumkabidhi Bi. Hassani. Hapo 
    ndipo alipewa mkate na maji. Petro alipokea kwa shingo upande alichopewa 
    na mwenye duka na kurudi haraka na kuziacha shilingi mia moja zilizobaki 
    kwenye jumla ya bei ya mkate na maji. Kama angekwenda shuleni 
    asingefanyiwa hayo. 

    Mara moja, dereva alianza kugeuza gari ili waendelee na safari. Petro 
    alikuwa ameketi kwenye kiti chake karibu na baba yake. “Salaalaa!” Yakobo 
    alishikwa na bumbuazi alipoona mtoto wake ameleta chakula kilichokuwa 
    kimepitisha tarehe ya kukila mwaka uliopita. “Wewe hujui kusoma wala 
    kuhesabu! Tazama tarehe iliyoandikwa hapa! Huoni kuwa chakula hiki 
    kingepaswa kuliwa kabla ya mwezi uliopita?” Kwa kweli, alianza kujiuliza 
    mengi kuhusu maisha ya mtoto wake. Alisikitika sana na kumwomba 
    asithubutu kula chakula hicho kwani kingeweza kuharibu afya yake. Petro 
    alikunywa maji tu aliyoleta na kuvumilia njaa iliyokuwa ikimbana wakati huo. 
    Alianza kujuta kwa kutofuata mawaidha aliyopewa na wazazi wake. Alifikiri, 
    “Nisingepuuza mawaidha ya baba yangu, nisingekutana na matatizo haya”. 

    Walipofika Dar-es-salaam, walifurahi kuonana na shangazi na binamu zake. 
    Walipokelewa vizuri na kupata muda wa kutembelea mazingira mazuri ya jiji 
    hilo. Tangu alipofika, Petro alifuatana na binamu zake kila wakati walipotoka 
    kununua vitu ili asikilize walivyoweza kuwasiliana na watu wengine katika 
    lugha ya Kiswahili. Hapo, aliweza kuelewa umuhimu wa kujifunza lugha na 
    aliamua kwamba angeanza kujifunza kwa bidii mara wakirudi nyumbani. Kwa 
    sasa, Petro amemaliza kidato cha tatu katika shule ya Sekondari ya Museta 
    ambapo walimu wake wanampenda kwa uwezo wake wa kuzungumza lugha 
    ya Kiswahili na lugha nyingine anazojifunza. 
    Kazi ya 2:
    Maswali ya Ufahamu
    1. Taja majina ya watu wanaozungumziwa katika kifungu hiki.
    2. Ni mawaidha gani mzee Yakobo aliyokuwa anawapa watoto 
    wake ?
    3. Maria amefaidika vipi kutokana na ujuzi wake wa lugha 
    mbalimbali ?
    4. Safari ya mzee Yakobo ilikuwa na lengo gani ?
    5. Ni hasara gani aliyoipata Petro aliposhindwa kuwasiliana na 
    mfanyabiashara ?
    6. Eleza tabia za mfanyabiashara Bi Hassani mbele ya mteja wake. 
    7. Ni jambo lipi lingetokea ikiwa mzee Yakobo hakumkataza mtoto 
    wake Petro kula chakula alichokinunua ? 
    8. Petro alikuwa na majuto gani? Kwa nini alijuta?
    9. Aliporudi nyumbani alifanya nini?
    10. Unajifunza nini kutokana na kifungu hiki cha habari?
    31.2. Msamiati kuhusu umuhimu wa lugha
    Kazi ya 3:
    Tunga sentensi sahihi kwa kutumia maneno yafuatayo huku ukizingatia 
    matumizi yake katika kifungu cha habari ulichosoma hapo juu.

    1. Kuhimiza
    2. Madhumuni
    3. Mawaidha
    4. Mtazamo
    5. Mtukutu
    6. Utalii 
    7. Kwenda haja
    8. Kwa shingo upande
    9. Bidii

    10. Bumbuazi

    Kazi ya 4:

    Oanisha maneno katika sehemu A na maana zake zilizopo katika sehemu B.

    cc

    Kazi ya 5:
    Jaza nafasi kwa kutumia maneno mwafaka yafuatayo: bidii, 
    madhumuni, kupuuza, maarufu, mawaidha, mtazamo, bumbuazi, 
    ratiba, kwenda haja, shingo upande.

    1. Nilianzisha mradi huu kwa ...................................ya kuhifadhi 
    mazingira yetu.
    2. Kila mwanafunzi analazimishwa kuwa na .........................ya 
    masomo yake ya kila siku.
    3. Usipojifunza kwa............................. basi hutafaulu mitihani yako. 
    4. Aliposikia habari hiyo alipigwa na ............................... na kukosa 
    la kufanya.
    5. Anaanza kujuta kwa kutofuata ....................................ya baba 
    yake.
    6. Baada ya kufanya safari ndefu, wasafiri wamesimamisha dereva 
    ili waweze ....................
    7. Sikubaliani na ...............................wako kuhusu uhifadhi mwafaka 
    wa mazingira.
    8. Alipokea zawadi hiyo kwa.................................................
    9. Amekuwa mchezaji.....................................kutokana na ustadi 
    wake wa kusakata mpira.
    10. Si vizuri ...............................fikra za mwenzako kabla hujamsikiliza.
     31.3. Sarufi: Matumizi ya hali ya kuamuru
    Kazi ya 6:
    Soma kifungu cha habari kifuatacho na kubainisha vitenzi 
    vilivyotumiwa katika hali ya kuamrisha

    Ona kwenye gazeti hili viongozi wa mataifa mbalimbali wamekusanyika 
    mjini Kigali. Lengo lao ni maendeleo ya lugha yetu. Soma habari yote 
    uelewe vizuri yanayoendelea pale na usiendelee kusimama kwenye 
    barabara. Kimbia nyumbani uwashe runinga yako ili uweze kuwaona 
    na uandike matangazo hayo kwa ufupi. Lakini jaribu kujifunza Kiswahili 
    kitakuwezesha kushirikiana na jamii, nchi zote za kanda hii hasa hasa 
    Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki kwani Kiswahili ni lugha rasmi.

    Kazi ya 7:
    Tunga sentensi tano zenye vitenzi mbalimbali katika hali ya kuamuru.
    Kazi ya 8:

    Tazama picha hizi kisha utunge sentensi katika hali ya kuamuru 

    kulingana na vitendo vinavyoendelea kwenye picha hizi:

    cc

    Kazi ya 9:
    Andika vitenzi vilivyopigiwa msitari katika hali ya kuamuru tungo 
    yakinishi na kanushi:
    Nchi yetu ni nzuri sana,ina milima na mabonde,viongozi bora na sehemu 
    mbalimbali za utalii. Mutesi hutembelea maziwa mengi naye Bugingo 
    husafisha kwake akipanda maua na miti ili kuhifadhi mazingira. Yeye 
    huwazuru wenzake akiwashawishi watende mema kila siku. Benita 
    aliamua kujenga nchi yake kwa kufanya kazi za umuganda, vilevile 

    akiwajengea wasiojiweza na kutengeneza barabara.

    Kazi ya 10:
    Weka sentensi zifuatazo katika hali ya kuamuru katika umoja na 
    kuzingatia mabadiliko ya kisintaksia katika sentensi. 

    a. Sauti ya pili,ingieni tuimbie Bwana.
    b. Teteeni maendeleo ya lugha ya kiswahili.
    c. Kuleni nyama yote pia osheni vyombo.
    d. Lieni kwa sauti ndogo majambazi yasituvamie.
    31.4. Matumizi ya lugha: Umuhimu wa lugha
    Kazi ya 11:
    Soma maelezo yafuatayo, kisha ujibu maswali hapo chini.
    Maelezo muhimu: Umuhimu wa lugha
    Lugha ni mojawapo ya vipengele vya utamaduni wa jamii na tena ni chombo 
    cha utamaduni. Hili ni kwa sababu chombo hiki hutumiwa kuwasilisha amali, 
    mila na desturi zote za jamii. Lugha ndio uti wa mgongo wa utamaduni. 
    Lengo kuu la lugha katika jamii ni pamoja na kuwafanya watu wawasiliane 
    kwa kupashana habari. Kujua lugha fulani kunamwezesha mtu kujipatia 
    marafiki, kukuza ujuzi kwa kusoma maandishi mbalimbali au kwa kufuata 
    vipindi mbalimbali kwenye redio, runinga na tovuti

    Kutumia lugha moja katika jamii kunaweza kuwa na faida pamoja na 
    hasara mbalimbali kutokana na mazingira ya jamii. Rwanda kama nchi 
    inayozungukwa na nchi zinazotumia Kiswahili, itanufaika kwa kutumia 
    lugha ya Kiswahili. Vilevile, lugha ya Kiswahili ina umuhimu mkubwa sana 
    katika Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kuwa lugha hii ndiyo lugha rasmi 
    inayotumiwa katika Jumuiya hii.
    Maswali:
    1. “Lugha ndio uti wa mgongo wa utamaduni.” Eleza.
    2. Lipi ni lengo kuu la kuijua lugha?
    3. Jadili: “Kutumia lugha moja katika jamii kunaweza kuwa na faida 
    pamoja na hasara mbalimbali”.

    31.5. Kusikiliza na Kuzungumza: Majadiliano
    Kazi ya 12:

    Jadili kuhusu mambo yafuatayo: 
    1. Matatizo yawezayo kujitokeza baina ya watu wawili wanaposhindwa 
    kusikilizana kimawasiliano
    2. Umuhimu wa lugha katika jamii 
    3. Mambo mbalimbali yanayoweza kukwamisha mawasiliano yenye 
    kutumia lugha
    31.6. Kuandika: Utungaji wa kifungu cha habari
    Kazi ya 13:
    Kwa kutoa hoja zenye mifano, tunga kifungu chako kwa kutumia 
    mada ifuatayo: 

    “Lugha inapotumiwa vizuri hujenga jamii na ikitumiwa vibaya huangamiza 
    jamii”.
    Kazi ya 14:
    Chagua mada moja kati ya hizi zifuatazo na kuzitungia insha 
    isiyopungua maneno 100.

    • Lugha ni kitambulisho cha jamii
    • Lugha hurahisisha mawasiliano katika jamii
    • Lugha hukuza utamaduni
    • Lugha huburudisha

    Tathmini ya mada
    Jibu maswali yote.

    1. Je, ushirikiano wa Rwanda pamoja na nchi nyingine za kikanda 
    ulisaidia nini Kiswahili?
    2. Toa lugha rasmi nchini Rwanda.
    3. Ni vituo gani vya utangazaji habari vinavyotumia Kiswahili katika 
    baadhi ya matangazo vinavyorusha?
    4. Fafanua maneno haya: - Malighafi, chatu, mawaidha.
    5. Jaza sentensi zifuatazo kwa kutumia neno lililo mabanoni:
    i. “…………… kazi yako ya shule kuhusu dhima ya kiswahili!”. 
    Mama alimuamrisha mtoto wake (kurekebisha).
    ii. Mwalimu alimwomba mwanafunzi akisema: “…………… kurasa 
    mbili za kifungu!”(Kuandika).
    iii. Baada ya kujiunga na nchi nyingine za Afrika Mashariki viongozi 
    wa Rwanda walituambia: “……… Kiswahili!” (jifunza)

    6. Onyesha umuhimu wa lugha ya Kiswahili katika jamii.

    MAREJEO
    1. Ntawiyanga, S. na Wenzake (2016). Kiswahili kwa Shule za Rwanda, 
    Kidato cha Kwanza. Longhorn Publishers (K) Ltd.
    2. Ndalu, A. E. (2016). Masomo ya Kiswahili Sanifu, Kidato cha 2. Moran 
    (E.A.) Publishers Ltd.
    3. Rwanda Education Board (2019). Kiswahili kwa Shule za Rwanda, 
    Mchepuo wa Lugha, Kidato cha 4. Rwanda Education Board.
    4. Rwanda Education Board (2019). Kiswahili kwa Shule za Rwanda, 
    Michepuo Mingine, Kidato cha 6. Rwanda Education Board.
    5. TUKI (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu, Toleo la Pili. Oxford University 
    Press.
    6. NKWERA, F.M.V. (1979). Sarufi na Fasihi, Sekondari na Vyuo. Tanzania 
    Publishing House Dar-es-salaam, Tanzania.
    7. https://sw.wikipedia.org/wiki/Kito_(madini)
    8. ;
    9. ;
    10. http://swa.gafkosoft.com/maigizo

    11. https://www.facebook.com/1416762588414463/posts/hali-yakuamuru-hali-hii-ilichambuliwa-kwenye-tawi-la-mutanga-jumapili-hiikidat/1823486384408746

    MADA YA 7 UTUNGAJI WA INSHATopic 9