• MADA YA 7 UTUNGAJI WA INSHA

    Uwezo mahususi wa mada : Kutunga insha fupifupi kwa kuzingatia kanuni 
    za utungaji na masimulizi.
    Malengo ya ujifunzaji:
    • Kueleza maana ya insha,
    • Kutofautisha aina za insha,
    • Kujadili umuhimu wa insha,
    • Kutunga insha kwa kuzingatia kanuni za utungaji wa insha, 

    • Kutumia kwa usahihi alama za vituo husika.

    Kidokezo
    Zungumzia aina mbalimbali za maandishi au masimulizi unazozijua.
    SOMO LA 25: DHANA YA INSHA 

    25.1. Kusoma na ufahamu: Mchuano wa fainali

    cc

    Wiki iliyopita nilibahatika kutazama mchuano wa fainali ya kuwania kombe 
    la Agaciro kati ya shule ya wasichana ya Elimu Bora na Tusonge Mbele

    kwenye uwanja wa michezo Amahoro. 

    Nilipofika nyumbani, wazazi wangu waliniuliza kwa mapana na marefu 
    kuhusu mchezo huo kwa sababu mmoja kati ya wachezaji ni dada yangu, 
    jina lake Umutesi Marie Alice.
     

    Nilianza kuelezea wazazi kwanza historia ya timu hizo. Timu hizi mbili ni 
    wapinzani sugu tangu jadi na jadi. Elimu Bora inajivunia historia nzuri kwa 
    kushinda kombe hili mara kumi. Wao ndio mabingwa watetezi. Tusonge 
    Mbele imeshinda kombe hili mara tatu. Mwaka jana walitimuliwa katika nusu 
    fainali. Katika awamu hii, wana rekodi ya kutoshindwa katika mechi zote 
    hadi kufikia fainali.

    Timu zote mbili ziliingia uwanjani tayari kwa mapambano. Kwa ufupi, kila timu 
    ilikuwa na golikipa mmoja. Elimu Bora waliweka wachezaji watatu katika safu 
    ya ulinzi wao Wakati ambapo tusone mbele walichezesha wachezaji wanne 
    katika safu hiyo hiyo. Timu ya Elimu Bora walitia wachezaji watano katika 
    kiungo cha kati nao Tusonge Mbele waliwachezesha wachezaji watatu. 
    Elimu Bora walikuwa na washambulizi wawili nao wakati ambapo tusonge 
    mbere walikuwa na washambulizi watatu katika safu ya mashambulizi. 
    Timu zote mbili zilikuwa na wachezaji wa akiba watano. Refa mkuu alipuliza 
    kipenga nao wasaidizi wake wawili walikimbia pembeni mwa uwanja kuinua 
    kijibendera. Mmoja alikimbia kushoto naye mwingine alikimbia kulia. 

    Manahodha wa timu zote mbili walisimama katikati ya uwanja kurusha sarafu 
    ili kuamua timu inayoanzisha mpira. Mashabiki wa timu zote mbili walikuwa 
    wanaimba nyimbo za kushangilia timu zao. Makochi wao walikaa pembeni 
    mwa uwanja kushuhudia wasichana wao wakimenyana. 

    Naam, refa alipuliza kipenga. Mpira ulianzishwa pale na Ikirezi na Umutesi 
    Marie Alice wa timu ya Elimu Bora. Elimu Bora walianza mchuano huo 
    kwa kasi mno. Walitafuta bao la mapema. Tusonge Mbele nao walifanya 
    shambulizi la kujibu. Kipindi cha kwanza kilimalizika bila goli kwa timu zote. 

    Katika kipindi cha pili, kila timu ilicheza vizuri. Kwenye dakika ya sabini 
    kulikuwa hatari katika lango la Tusonge Mbele. Kayitesi alinawa mpira. 
    Naam, kipenga kilipulizwa. Refa aliwapa Elimu Bora penalti. Shangwe na 
    vifijo vikahanikiza huku na huko kutoka kwa mashabiki wa Elimu Bora. 
    Kayitesi alionyeshwa kadi ya manjano. Ikirezi alisimama nyuma ya mpira 
    ule tayari kufyatua mkwaju wa penalti. Kabatesi akaruka na kuupiga mpira 
    ule ukapitia juu ya mtambaapanya wa goli hadi nje. Ilikuwa konakiki.

    Konakiki hiyo ilipigwa na Umulisa. Uwamwiza alikimbilia mpira ule. Alipiga 
    kichwa! Hatimaye Elimu Bora walipata goli la kwanza. Mashabiki wote wa 
    Elimu Bora na makochi wao waliacha viti vyao huku wakijirusharusha kwa 

    nderemo kama kulungu. Mashabiki wa Tusonge Mbele waliviinamisha vichwa 

    vyao mithili ya kondoo. Wachezaji wa Tusonge Mbele walipandwa na mori 
    kwa goli walilofungwa. Walimzingira refa mkuu. Walidai kuwa Uwamwiza 
    alikuwa ameotea. Nahodha wao, Mutoni, ambaye ni beki wa kupanda na 
    kushuka alimiminia refa maneno makali. Refa alitia mkono katika mfuko wa 
    nyuma ya kaptula na kuchomoa kadi nyekundu. Mutoni alionyeshwa kadi 
    nyekundu kwa kukosa adabu. Alisindikizwa nje ya uwanja. Timu ya Tusonge 
    Mbele walibaki na wachezaji kumi pekee. 

    Mchezo ulimalizika ikiwa ni goli moja la Elimu Bora kwa bila. 

    Kazi ya 1:
    Maswali ya ufahamu
    1. Timu hizi mbili ni zipi?
    2. Timu hizo mbili zinagombania kombe gani?
    3. Timu hizo zilikuwa marafiki? Eleza.
    4. Historia ya timu hizo ilikuwa namna gani katika mchezo wa 
    kandanda?
    5. Mchezo ulimalizika vyema? Eleza. 
    6. Kwa sababu gani wazazi walitaka kusikiliza matokeo ya mchezo huo?
    7. Kwa sababu gani Mutoni alipewa kadi nyekundu?
    8. Kwa maoni yako, michezo ina umuhimu gani?
    9. Ni vizuri kwa wasichana kucheza mchezo wa kandanda?
    25.2. Matumizi ya msamiati kuhusu kifungu cha habari
    Kazi ya 2:
    Eleza maana ya maneno yafuatayo kutoka katika kifungu cha habari 
    ulichokisoma hapo juu kuhusu “Mchuano wa fainali”
    Kabumbu 
    Mchuano 
    Fainali
    Kuwania kombe 
    Wapinzani 
    Bingwa tetezi
    Nusu fainali
    Safu ya ulinzi 
    Kiungo cha kati 
    Washambulizi
    Kazi ya 3:
    Kamilisha sentensi kwa kutumia maneno yanayofaa kati ya haya 
    yafuatayo: kabumbu, mchuano, fainali, kuwania kombe, washambulizi, 
    kuinua kijibendela, mabingwa watetezi, refa, mashabiki, penalti. 
    1. Elimu Bora ndiyo …………… kwa sababu walishinda mara 
    nyingi.
    2. ………anachomoa kadi nyekundu na kumuonyesha Mutoni. 
    3. Kulikuwepo mashabiki wengi katika mchezo wa …………..la 
    Agaciro nchini Rwanda
    4. ………….. ndio wanaofungia timu yao magoli mengi.
    5. Mara nyingi …………husababisha goli.
    6. Wasaidizi wa refa wanamsaidia katika mchezo kwa………………..
    7. Timu ya Arsenal ina ……….. wengi nchini Rwanda.
    8. Siku hizi wachezaji wa ………….hulipwa hela nyingi.
    9. Nchini Rwanda, …………wa APR FC na Rayon Sport unatazamwa 
    na watu wengi sana.
    10. Katika mchezo wa ………….kila timu hutakiwa kuwa bingwa.
    25.3. Sarufi: Matumizi ya herufi kubwa
    Kazi ya 4:

    Tazama herufi zinazopigiwa mstari na kueleza sababu ya kutumia 
    herufi kubwa
    a. Mjini Kigali panajulikana kuwa na usalama pamoja na usafi.
    b. Shule ya Mtakatifu Yohana inawapokea wasichana na wavulana.
    c. Jina lako ni nani? Ninaitwa Peter. Jina jingine ?
    Maelezo ya matumizi ya herufi kubwa 
    a. Hutumiwa kuanzishia sentensi: Tazama mfano ufuatao:
    Nilikuona jana. 
    b. Herufi kubwa hutumiwa mwanzoni mwa majina au nomino pekee 
    kama vile: majina ya watu, mahali, milima, mito, maziwa, nchi, 
    mabara, siku za wiki, miezi ya kalenda, sikukuu, dini mbalimali, 
    barabara, majina ya vitabu, visiwa, n.k.
    c. Hutumiwa kuandikia anwani: 
    Mfano: 
    JINSI YA KUPANDA MITI
    Kazi ya 5:

    Chunguza makosa ya kisarufi katika sentensi zifuatazo na 
    kuyasahihisha.
    1. musanze ni mji mkubwa.
    2. kalisa na uwineza ni wanafunzi wenye bidii.
    3. miti hutupatia kivuli cha kupumzikia.
    4. mwalimu anafundisha.
    5. berwa anacheza mpira. 
    25.4. Matumizi ya Lugha: Dhana ya insha na utungaji wake
    Kazi ya 6:
     Jadili maswali yafuatayo:
    a. Insha ni nini?
    b. Toa umuhimu wa kujifunza insha.
    c. Insha nzuri inastahili kuwa na sifa gani?
    d. Kifungu hiki cha habari ni cha aina gani ya insha ?
    Maelezo muhimu kuhusu insha
    Maana ya insha:
    Insha ni mtungo wa kinathari unaozungumzia suala au kusimulia kisa 
    fulani. Utungo huu huwa na urefu wa wastani. Kisa hicho au suala hilo 
    ndilo mada ya utungo huo. Insha hutumiwa kueleza maoni ya mwandishi 
    kuhusu masuala au mambo tofauti. Utungaji ni neno linalotokana na kitenzi 
    “tunga”. Kitenzi hiki kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili Sanifu (2004: 414) 
    kinamaanisha “Kutoa mawazo kutoka ubongoni na kuyakusanya, kisha 
    kuyadhihirisha kwa maandishi, kwa kusimulia, kwa kuyaimba au kwa 
    muziki.»
    Kwa hiyo, tunaweza kusema kuwa utungaji ni utoaji wa mawazo binafsi 
    kutoka akilini mwa mtu kuhusiana na mambo mbalimbali katika jamii, kisha 
    kuyaweka wazi kwa njia ya mdomo au maandishi. 
    Sehemu kuu za insha: Insha hugawika katika sehemu kuu tatu ambazo ni 
    pamoja na: 
    • Utangulizi (mwanzo) 
    Katika sehemu hii inampasa mwandishi/ mtungaji atoe maelezo mafupimafupi 
    na maana ya habari aliyopewa. 
    • Kiini cha insha (Kati au mwili) 
    Inamlazimu mwandishi afafanue kwa mapana na marefu mada 
    anayoishughulikia huku akitoa mifano hai inayoendana na hali halisi ya 
    maisha ya mtu kijamii. Kwa kawaida sehemu hii hueleza kwa ukamilifu kila 
    hoja iliyodokezwa katika utangulizi. 
    • Hitimisho na mwisho 
    Inampasa mwandishi kutoa mapendekezo (maoni) ya msingi au kusisitiza 
    kwa ufupi yale aliyoyaeleza katika habari yenyewe. Mwisho wa insha 
    huonesha uhusiano uliopo kati ya utangulizi na maelezo yaliyomo katika 
    mwili. 
    25.5. Kusikiliza na kuzungumza 
    Kazi ya 7:
    Fikiria juu ya insha moja uliyoisikiliza au kusoma na kuisimulia 
    mbele ya darasa
    176
    25.6. Kuandika: Utungaji wa insha
     
    Kazi ya 8:
    Kutokana na mfano wa insha uliotolewa hapo juu, andika insha
    kuhusu mada ifuatayo:
    “Umoja wa Afrika ni Msingi Muhimu kwa Maendeleo ya Afrika”

    SOMO LA 26: AINA ZA INSHA

    vv

                          cc

    b

    Kazi ya 1:
    Jadili michoro hii kwa kuelekea kwenye insha

    26.1. Kusoma na ufahamu: Usafi wa mavazi yetu

    ff

    Vazi ni nguo ya aina yoyote inayovaliwa mwilini. Binadamu huhitaji mavazi 
    kujikinga dhidi ya hali ya hewa ya aina mbalimbali. Wakati wa joto huhitaji 
    vazi jepesi na wakati wa baridi huhitaji vazi linaloweza kumtilia joto mwilini. 
    Hii ndiyo sababu wakati wa baridi watu hujifunika mavazi kama migolole, 
    makoti, makabuti, kaniki, vikoi, na sweta . 

     Mavazi ni pambo kwa binadamu. Vazi humfanya mtu aonekane maridadi na 
    apendeze zaidi. Labda, hii ndiyo sababu ya kuwepo kwa aina mbalimbali za 
    mavazi na mitindo tofauti inayomfanya mtu avutie.

    Mavazi huonesha utamaduni wa watu. Kusema kwamba mtu akivaa nguo 
    ya mtindo fulani mara nyingi utamaduni wake au asili yake hutambulika 
    waziwazi. Hata mtu awe mweupe anayetoka Ulaya au Marekani, akivaa 
    mgolole, kanga, kitenge, atakuwa akiiga vazi la utamaduni wa Afrika kwa 
    ujumla. Hadi leo, kuna mavazi unayoweza kusema kuwa ni ya Kichina, 
    Kihindi, Kiarabu, Kizungu, Kinyarwanda, Kiganda, Kimasai na kadhalika. 

    Tena mtu anaweza kuvaa nguo kwa mtindo wa aina fulani akafikiriwa kuwa ni 
    Mkongomani, Mganda, Mmasai, raia kutoka Afrika Magharibi na kadhalika. 
    Mavazi ni ya aina nyingi na mitindo tofauti. Lakini mavazi hayo yote huweza 
    kupangwa katika aina kuu tatu: mavazi ya kike, ya kiume na mavazi mahususi.

    Kwa upande wa kwanza, mavazi ya kike ni mavazi ambayo kwa kawaida

    huvaliwa na watu wa jinsia ya kike. Kuna mavazi au nguo za ndani, ambazo 
    huvaliwa na wanawake na hazipaswi kuonekana ovyo. Na hizo ni kama 
    chupi, fulana, sidiria na shimizi. 
    Tena, kuna nguo za nje ambazo ndizo zionekanazo mara nyingi. Hizo ni 
    kama sketi, blauzi, shati, jaketi, gauni, kanga, kaniki, kitenge, kaptula, suruali 
    na kadhalika.
    Kwa upande mwingine, wanaume nao huwa na nguo za staha yaani nguo 
    za ndani kama chupi na fulana. Pia, wana nguo zinazoonekana nje kama 
    kaptula, suruali, shati, koti, tai, suti, kanzu na kadhalika. 
    Zaidi ya hayo, kuna mavazi mahususi ambayo ni mavazi rasmi kwa ajili ya 
    shughuli maalum au kazi maalum. Mfano wa mavazi haya ni kama mavazi 
    ya viongozi wa kidini, masista, makasisi, mapadri na mashehe. Kundi la 
    aina hii huwa na nguo zao maalum kwa ajili ya kazi zao na pia huwasaidia 
    kujitambulisha kwa urahisi kwa umma au jamii. Baadhi ya nguo hizo ni kama 
    kasiki, joho, kanzu, kilemba na nguo zinazofanana na hizo. 
    Mfano mwingine ni mavazi rasmi kama ya askari jeshi, askari polisi, askari 
    magereza, wafanyakazi wa forodha, walinda usalama wa mashirika ya 
    kujitegemea, waganga na wauguzi, wafanyakazi wa mashirika ya ndege, 
    wachezaji na hata wanafunzi. Hawa wote wana mavazi yao rasmi kwa ajili 
    ya shughuli zao. Mtu akivaa nguo ya aina fulani, hujitokeza kuwa yeye ni 
    mtu wa namna fulani au kazi fulani. 

    Mavazi yetu yote ni lazima yawe na usafi. Usafi wa mavazi yetu ni muhimu 
    sana kwa sababu jambo hili husaidia mambo mengi maishani mwetu. 
    Kwanza tunaposafisha nguo zetu, tunajiepusha na magonjwa yanayotokana 
    na wadudu wanaoweza kuishi katika nguo chafu. 
    Wadudu hawa ni kama chawa, viroboto na kadhalika. 
    Nguo chafu hasa zile za ndani huweza kusababisha madhara katika sehemu 
    za uzazi na kuleta magonjwa mbalimbali kutokana na vidudu ambavyo 
    vinaweza kusababishwa na uchafu.
    Pili, mtu akiwa na nguo chafu hutoa harufu mbaya ambayo husumbua 
    wenzake wanapomsogelea. 

    Kwa ujumla, mavazi yetu ni ya aina nyingi na mitindo tofauti. Mavazi 
    haya yana umuhimu sana katika maisha yetu. Ndiyo maana tunalazimika 
    kuyatunza vizuri na kuyasafisha ili tuwe na usafi wa kutosha. Usafi huu 
    lazima uende bega kwa bega na usafi wa miili yetu. 
    (Kifungu hiki msingi wake ni kutoka: Ndalu A. (1997) Mwangaza wa Kiswahili, 

    East African Educational Publishers Ltd, Nairobi, Kenya.

    Kazi ya 2:
    Maswali ya Ufahamu: 
    1. Vazi ni nini ? 
    2. Kwa sababu gani vazi ni kifaa muhimu sana kwa binadamu? 
    3. Taja aina kuu tatu za mavazi. 
    4. Ni kwa namna gani vazi linavyoweza kutambulisha utamaduni wa 
    anayevaa vazi hilo? Eleza kwa kutoa mifano ya kutosha. 
    5. Taja mifano mitatu ya nguo mahususi. 
    6. Veli linaweza kutambulika kama vazi la aina gani miongoni mwa 
    aina za mavazi tulizotaja hapo juu? 
    7. Eleza jinsi ambavyo mavazi hutegemea sana utamaduni wa jamii husika? 
    8. Taja majina ya wadudu wanaoishi ndani ya mavazi machafu. 
    9. Kwa sababu gani nguo zilizofuliwa ni lazima zipigwe pasi baada 
    ya kukaushwa na jua? 
    10. Ni ushauri gani unaoweza kutoa kulingana na kifungu hiki?
    26.2. Msamiati kuhusu kifungu cha hatari
    Kazi ya 3:
    Tazama kwa makini jedwali hili. Bainisha msamiati mbalimbali na 

    kueleza maana yake. 

    vv

    Kazi ya 4:

    Unganisha msamiati kutoka sehemu A na maana yake kutoka sehemu B.

    xx

    26.3. Sarufi: Matumizi ya alama za vituo
    a. Matumizi ya nukta ( . )

    Kazi ya 5:
    Tazama sentensi zifuatazo na kuzungumzia matumizi ya alama 
    yanayojitokeza.

    i. Usafi ni muhimu sana kwa maisha ya binadamu. 
    ii. Kalisa alienda sokoni. Alikutana na rafiki yake sokoni.
    iii. Tunasoma ili tupate elimu.
    Maelezo muhimu 
    Nukta

    a. Huwekwa mwishoni mwa sentensi sahili sahihi. Kwa mfano
    i. Tunakula mboga kwa ajili ya afya nzuri
    ii. Inatubidi kusafisha mahali tunapoishi. 
    b. .Hutumiwa kuonyesha ufupisho wa maneno. Kwa mfano:
    i. S.L.P. – Sanduku la Posta
    ii. Bi. – Bibi
    182
    c. Hutumika kubainisha saa na dakika au tarehe. Kwa mfano:
    i. 3.20 – saa tisa na dakika ishirini
    ii. 14.5.2016- tarehe kumi na nne, mwezi wa tano, mwaka wa mbili elfu 
    kumi na sita
    d. Hutumiwa kuonyesha vipashio vya pesa. Kwa mfano:
     sh.10.50- shilingi kumi na thumuni hamsini
    e. Zikitumiwa mara tatu mfululizo (…) huonyesha kutokamilika kwa 
    sehemu husika
    Kwa mfano: Nitakupa lakini ni sharti...
    Kazi ya 6:
    Chunguza sentensi hizi na kusahihisha makosa ya kisarufi. 
    1. mwalimu anaandika ubaoni
    2. mifano ya ndege ni kv kuku, mwewe na bata
    3. tulianza mitihani yetu tarehe 12122017
    4. bi mutoni anaendesha gari
    5. wanafunzi wanasoma darasani
    b. Matumizi ya koma / mkato ( , )
    Kazi ya 7:
    Tazama sentensi zifuatazo na kuzungumzia matumizi ya alama 
    yanayojitokeza.

    1. Nimemkuta mzee, nikamwuliza shida zake, nikamsaidia kupata 
    gari la kumpeleka nyumbani.
    2. Tumekuja kwa ajili ya akili, si kwa ajili ya pesa.
    3. Baadhi ya maadili na thamani Mnyarwanda anatakiwa kuwa na zo 
    ni kama vile utu, unyarwanda, ushirikiano na ushujaa.
    Maelezo muhimu
     Mkato / koma
    a. Hutumiwa kuonyesha pa kutua kwa muda mfupi katika sentensi. 
    Kwa mfano: 
    ii. Nilipowasili nyumbani, nilienda kuteka maji kisimani. 
    iii. Kwa kuwa tulijiandaa vilivyo kwa mtihani wa kitaifa, tulipita. 
    b. Hutumiwa kutenga maneno yaliyo katika orodha: 
    i. Nenda sokoni ununue mboga, nyama, mafuta, na unga. 
    ii. Mwanafunzi huyu ni mtiifu, mwerevu, mtanashati, na mwenye bidii. 
    c. Hutumiwa kubainisha sehemu mbili za sentensi zilizo kinyume: 
    i. Umoja ni nguvu, utengano ni udhaifu. 
    ii. Aliniambia atakuja, hakuja. 
    d. Hutumiwa kabla ya alama za mtajo. 
    Kwa mfano:
    Mama akasema, “Niletee chumvi.” 
    e. Hutumiwa wakati sentensi inapoanza kwa kiunganishi. 
    Kwa mfano: 
    Kweli, alikuwa mtu mwovu. 
    f. Hutumiwa unapoita mtu ili kupata usikivu wake kabla hujamwambia 
    chochote. Kwa mfano: 
    Nkusi, niletee kalamu. 
    g.Hutumiwa unapokubali au unapokataa kitu. Mfano: 
    i. Ndiyo, nitakuja. 

    ii. Hapana, sitakulipa.

    Kazi ya 8:
    Sahihisha makosa ya kisarufi katika sentensi zifuatazo
    1. Baba alinunua daftari kalamu rula na kifutio
    2. Mama alipofika sokoni alinunua nanasi mkate chungwa na 
    parachichi
    3. Familia yetu ina watoto wafuatao: Kabanda Kabalisa na Mukandoli
    4. Mwalimu wetu anatufundisha masomo ya Kiswahili Kiingereza na 
    Historia
    5. Katika lugha ya Kiswahili kuna alama za uandishi kama vile: nukta 
    mkato alama ya kuuliza ….
     26.4. Matumizi ya lugha: Ainaza insha
    Kazi ya 9:
    Jibu maswali yafuatayo: 
    1. Kifungu “ Usafi wa mavazi” ni aina gani ya insha?
    2. Kifungu “Mchuano wa fainali” ni aina gani ya insha?
    Maelezo muhimu kuhusu aina za insha 
    Insha ni za aina nyingi kulingana na namna zilivyoandikwa au kufuatana na 
    kusudi lake. Katika utungaji wa insha kuna :
    1. Insha za wasifu 
    Insha za wasifu ni aina ya utungaji ambao huchora picha ya kitu 
    kinachozungumziwa. Huonyesha waziwazi hisia za msanii. Aghalabu, kuna 
    vitu vingi ambavyo tunaviona kila siku kama vya kawaida lakini mtungaji 
    anaweza akavitungia insha za wasifu na tukaviona katika mtazamo tofauti 
    kabisa. Katika insha za wasifu kuna usanii wa kueleza sifa za mtu, mahali 
    au kitu fulani. 
    2. Insha ya mjadala au ya mdahalo 
    Inalenga mara nyingi kulieleza jambo na vile vile kuhimiza mtazamo fulani. 
    Hata hivyo, jambo lililo muhimu zaidi si kueleza bali ni kujibidiisha kushawishi. 
    Katika mdahalo shawishi, mwandishi hulenga katika kuathiri hisia na maoni 
    ya msomaji kwa njia ya kumfanya achukue hatua. Insha hii huhusisha mada 
    ambayo mwanafunzi anapaswa kuitetea au kuipinga katika kisa chake. Hoja 
    nyingi na nzito hutolewa kwenye upande anaounga mkono. 

    3. Insha fafanuzi 
    Katika aina hii ya insha, mwandishi hutumia mifano kufafanua au kutilia 
    mkazo hoja yake. Anaweza kutumia mfano mmoja wenye uzito au mifano 
    mingi yenye kuhusiana. 
    Mfano: Rushwa imepigwa marufuku nchini Rwanda. 
    4. Insha ya methali 
    Insha ya methali ni utungo unaoandikwa kwa kuzingatia methali. Kisa au 
    maelezo yatolewayo huwa yanaongozwa na maana iliyomo katika methali 
    husika. Kabla ya kuanza kuandika insha, ni bora kwanza kuielewa vyema 
    maana ya methali au maudhui yake. Mbali na kufahamu maana ya kijuujuu 
    ya methali, inambidi mtunzi wa insha kuelewa mazingira (miktadha mingine 
    ambapo methali husika inaweza kutumiwa). Kwa mfano: Akili ni nywele kila 
    mtu ana zake. Hapa, anayetunga insha hii lazima aeleze maana ya juu na 
    ya ndani ya methali. Pia, msamiati uliotumiwa hufafanuliwa.
    5. Insha ya mdokezo 
    Insha ya mdokezo ni aina ya utungo ambao huandikwa kwa kuongozwa 
    na maneno aliyopewa mtunzi wake. Maneno hayo yaliyotolewa ndiyo 
    mwongozo wa kumwelekeza mwandishi kuhusu maudhui atakayoandika. 
    Lililo muhimu ni kuhakikisha kuwa mtungo utakaoandikwa unaoana vizuri na 
    maneno yaliyotolewa kama mwongozo. 
    Mfano: Nilipofika katika eneo la tukio hilo, sikuamini niliyoyaona ………………
    Hapa, unaweza kuendeleza kidokezi hiki kwa kukitungia kisa mwafaka. 
    6. Insha za picha 
    Insha za picha ni zile ambazo msingi wake wa kuzitunga ni picha ambazo 
    huwa zimechorwa na ambazo humwongoza mwandishi kubuni hadithi au 
    kisa kinachooana na picha hizo. Kimsingi, huhitaji ufasiri wa picha zilizo 
    kwenye ukurasa na kuibuni hadithi kuzihusu. 
    Hivyo basi huwa ni insha za kusimulia. 
    7. Insha ya mawazo au ya kubuni 
    Insha hizi zinahusu jambo la kufikiriwa. Jambo linalojadiliwa katika aina hii ya 
    insha huwa halitokani na hali au tukio halisi katika maisha. Vipengele vyote 
    vinavyoijenga hubuniwa na mtunzi wake. Maudhui, wahusika, mandhari vya 
    mtungo wa aina hii vyote hubuniwa katika fikra ya mtunzi. 

    8. Insha ya kitawasifu (Insha elezi/ ya maelezo) 
    Insha hii huwasilisha sifa za vitu, watu, hali, matendo, mahali au hata 
    sherehe uliyohudhuria. Inalenga kutoa picha ya kitu katika akili zetu jinsi 
    ambavyo kinamdhihirikia anayekiona. Ili kuandika insha ya maelezo, 
    mwandishi wake anahitaji kwanza kabisa kukusanya habari za kina kuhusu 
    jambo analoliandikia. Hategemei tu yale ambayo yanaonekana kwa macho 
    bali pia aina nyingine za hisi kama vile kugusa, kuonja, kunusa, kusikia na 
    kadhalika. Hali hii humwezesha msomaji kupata taswira kamilifu kuhusu 
    jambo linaloelezewa kupitia viungo vya kuona, kuonja, kugusa na kusikia. 
    9. Insha ya masimulizi 
    Insha ya masimulizi ni insha yenye kuhadhiria tukio au hali fulani. Ni utungo 
    ambao husimulia au kueleza kisa. Dhima yake ni kuburudisha au kuteka 
    umakini wa msomaji. Kwa kuwa inalenga hadhira ni muhimu kufahamu na 
    kuitambua hadhira yako kabla ya kuandika utungo wako
    26.5. Kusikiliza na kuzungumza 
    Kazi ya 10:
    Jadili mada zifuatazo
    1. Mavazi ya kigeni yana athari kubwa katika utamaduni wa 
    Wanyarwanda
    2. Matumizi ya mtumba (mavazi) huleta hasara kwa Wanyarwanda.
    26.6. Kuandika
    Kazi ya 11:
    Tunga insha ya wasifu unayotaka yenye ukurasa mmoja.

    SOMO LA 27: INSHA YA MASIMULIZI

    cc

    Kazi ya 1:
    Unaona nini kwenye mchoro hapa juu?
    27.1. Kusoma na ufahamu: Mafanikio ya kudumu 

    Ilikuwa tafrija ya kijiji kizima, tuliposherehekea siku ya kupata tuzo kwa kijana 
    hodari ambaye aliyamudu maisha yake kiasi cha kuigwa na vijana wengine. 
    Kabatesi, kijana aliyezaliwa mwanapekee katika familia yake hakubahatika 
    kulelewa na wazazi wake kwani walifariki angali mdogo akachukuliwa na 
    kulelewa na shangazi yake. 

    Alipomaliza masomo yake katika shule za sekondari, Kabatesi alipata cheti 
    cha kuhitimu masomo ya sekondari huku akiwa na alama nzuri. Jambo hili 
    liliwafurahisha watu wengi: walimu na majirani zake. Alikuwa mwanafunzi 
    mwenye bidii tangu shule za chekechea hadi kiwango alichofikia. Muda mfupi 
    baadaye, alijiunga na vijana wenzake kufuata masomo ya muda mfupi yaliyokuwa 
    yakitolewa kijijini mwake. Masomo hayo ni kuandaa miradi midogo midogo ya 
    kujiendeleza na jinsi ya kuifanikisha. 

    Alipokubaliwa kufuata mafunzo pamoja na vijana wengine alielewa kwamba hiyo 
    ilikuwa njia nzuri ya kupata suluhisho na ufumbuzi wa tatizo lililokuwa likimkera 
    kwa muda mrefu. Mafunzo yalifanyika kwa muda wa mwaka mzima, akapewa 
    cheti katika fani ya maandalizi na utekelezaji wa miradi ya kimaendeleo.

    Mwezi mmoja uliofuata, Bodi ya Maendeleo Rwanda ilihitaji kuajiri vijana 
    waliokuwa wamemaliza masomo yao katika mkondo wa lugha ili wasaidie katika 
    kazi za ukalimani na uongozaji wa watalii kwenye vivutio vya utalii. 
    Kabatesi alipeleka ombi lake na baada ya muda mfupi akaitwa kwa mtihani. Hili 
    lilikuwa jambo jepesi kwake kwani aliufaulu vizuri mtihani na hivyo akaajiriwa na 
    bodi hiyo. Alifanya kazi yake kwa bidii kiasi kwamba watalii wengi walifurahia 
    huduma yake, wakampenda kwa uwezo wake wa kuzungumza lugha nyingi 
    tofauti na bidii aliyoonesha kazini. 

    Kabatesi alifungua akaunti kwenye benki moja na kuanza kuhifadhi sehemu 
    ya mshahara wake. Kwa kweli, alikuwa msichana asiyekata tamaa na kila 
    aliposhikilia jambo alilifuatilia mpaka lilipokamilika. Kwa hivyo, alipoona akaunti 
    yake imeshakua na pesa za kutosha, aliamua kuomba mkopo ili aweze 
    kutekeleza mengi aliyokuwa amejifunza katika maandalizi na utekelezaji wa 
    miradi ya kimaendeleo. Mawazo yake yalikuwa kwenye shamba lake kubwa 
    aliloachiwa na wazazi ambalo mpaka wakati huo lilikuwa halijatumiwa vizuri. 
    Aliandaa vizuri mradi wa kilimo na ufugaji, akajenga vibanda vya mifugo yake, 
    akawaajiri baadhi ya vijana waliokuwa pamoja katika mafunzo ya muda ule 
    mfupi, kila mmoja akapewa jukumu lake. 

    Pamoja na kazi yake ya ukalimani, Kabatesi alifuata vizuri mradi wake 
    akanunua vifaa vilivyohitajika. Ninakumbuka kuwa mwaka jana, serikali yetu 
    ilipotoa tuzo kwa watu waliochangia kubadilisha maisha ya watu wengine, 
    Kabatesi alikuwa miongoni mwa watu waliochangia kuyaboresha maisha ya 
    majirani zake. Kwa sasa ameanza kuendelea na masomo yake katika Chuo 
    kikuu cha Rwanda. 

    Kabatesi amekuwa mfano mzuri kwa vijana wengine wengi ambao 
    wanayakumbuka maisha yake, huyaamini yaliyosemwa na wahenga 
    kwamba” Mchumia juani hulia kivulini” na “mvumilivu hula mbivu”. 

     Wema kwa kila mtu, utulivu na upendo ni baadhi ya sifa zinazomtambulisha 
    kijana huyu ambaye amewashangaza wengi wanaofahamu alipotoka.

    Kazi ya 2:
    Maswali ya ufahamu 

    1. Eleza hali ya maisha ya Kabatesi alipokuwa mtoto mdogo. 
    2. Kwa nini Kabatesi alipewa zawadi nyingi baada ya kumaliza 
    masomo yake ya shule za Sekondari? 
    3. Masomo ya muda mfupi aliyoyafuata yalikuwa yanahusu nini? 
    4. Eleza jinsi ambavyo Kabatesi aliweza kufaidika kutokana na 
    masomo ya muda mfupi. 
    5. Eleza jinsi ambavyo Kabatesi aliweza kufaidika kutokana na 
    masomo yake ya Sekondari. 
    6. Ni mambo gani yanayokudhihirishia kwamba Kabatesi alikuwa 
    kijana asiyekata tamaa? 
    7. Eleza jinsi ambavyo Kabatesi aliweza kuboresha maisha ya watu 
    wengine. 
    8. Kwa nini Kabatesi alipewa tuzo? 
    9. Kwa kifupi, eleza tabia na mienendo ya Kabatesi. 
    10. Kwa nini Kabatesi anachukuliwa kuwa mfano kwa vijana wengine? 
    11. Umepata funzo gani kutokana na kifungu hiki? 
    12. .Kulingana na kifungu hiki, eleza maana ya methali hizi: 
    a. Mvumilivu hula mbivu.
    b. Mchumia juani hulia kivulini.
    27.2. Matumizi ya msamiati kuhusu kifungu
    Kazi ya 3:
    Tunga sentensi kwa kutumia maneno yafuatayo: 
    1. Kuandaa
    2. Karo
    3. Tafrija
    4. Ajira 
    5. Hodari
    6. Kukata tamaa 
    7. Akaunti
    8. Tuzo
    9. Mradi

    Kazi ya 4:
    Husisha maneno kutoka sehemu A na maana yake kwenye sehemu B.
     

    cc

    ff

    Kazi ya 5:
    Kamilisha sentensi kwa kutumia maneno unayoona yanafaa kati ya 
    yafuatayo:
    Bidii, inawapongeza, utulivu, majukumu, vibanda, shule za 
    chekechea, ukalimani 
    1. Nchini Rwanda watoto wengi wanaanzia masomo yao katika……
    2. Wanafunzi wanalazimishwa kusoma kwa ............ ili waweze 
    kufaulu mtihani wa taifa.
    3. Kuna uhusiano wa karibu wa kazi ya ………. na tafsiri. 
    4. Wanafunzi wenye tabia ya …….. wanapata alama nzuri katika 
    masomo yao. 
    5. Serikali ya Rwanda ………. na kuwahimiza wasichana wanaosoma 
    sayansi na teknolojia. 
    6. Wazazi wana ……. ya kuwalisha na kulipa karo za watoto wao. 
    7. Mjomba wangu alijenga ……… vitatu vya kuku wake
    27.3. Sarufi: Matumizi ya alama za vituo
     a. Matumizi ya alama ya kuuliza/ ulizo ( ? )
    Kazi ya 6:
    Tazama sentensi zifuatazo na kuzungumzia matumizi ya alama 
    inayojitokeza.

    i. Unasema nini?
    ii. Mnafanya nini hapa ?
    iii. Je, jina lako nani ?
    iv. Kwa sababu gani wototo wanapaswa kuheshimu wazazi wao ?
    Maelezo muhimu
    Alama ya kuuliza au ulizo hutumiwa mwishoni mwa sentensi kuonyesha 
    kuwa sentensi hiyo ni swali. 
    Kwa mfano: Unaitwa nani?
    Kazi ya 7:
    Sahihisha sentensi zifuatazo:

    1. Unasoma kitabu kipi
    2. Mwalimu wako wa Kiswahili anaitwa nani
    3. Je, unakunywa chai
    4. Kwa nini unapiga kelele darasani
    5. Unachora nini
    b. Matumizi ya alama ya mshangao ( ! )
    Kazi ya 8:
    Tazama sentensi zifuatazo na kuzungumzia matumizi ya alama 
    inayojitokeza.

    i. O lalala! Baba yako amekufa!
    ii. Gooooo ! Amefunga goli!
    Maelezo muhimu
    Alama ya mshangao hutumiwa kuashiria mahangaiko ya moyo kama vile 
    hasira, hofu, mshangao na kadhalika. 
    i. Lo! Mwanafunzi ameangusha kitabu cha mwalimu matopeni. 
    ii. Wamefungwa mabao kumi kwa nunge!
    Kazi ya 9:
     Chunguza sentensi zifuatazo na kuzisahihisha

    1. Ala umebeba mzigo huo pekee yako
    2. Hoyee wanariadha wametunzwa medali
    3. Pesa zangu zimeibiwa
    4. Nimepita mtihani wangu wa kitaifa
    5. Lo Akimana ameanguka chini
    27.4. Matumizi ya lugha: Sifa za inshe ya masimulizi
    Kazi ya 10:
    Je, kifungu “Mafanikio ya kudumu” ni aina gani ya insha? Toa maelezo.
    Maelezo muhimu
    Sifa kuu za aina hii ya insha:

    • Matamshi na lafudhi ni lazima yawe sahihi. 
    • Ni lazima mazungumzo haya yagawanyike katika sehemu kuu tatu: 
    mwanzo, kati, na mwisho. 
    • Utungaji wa masimulizi ni lazima uzungumzie ukweli wa jambo 
    linalozungumziwa. 
    • Uwasilishaji wa hali, matukio, na mazingira yanayodhihirika waziwazi. 
    • Mtiririko wa mawazo wenye mshikamano. 
    • Msimuliaji ni lazima azungumze kwa nidhamu na kwa lugha sanifu 
    inayoeleweka kwa watu wote. 
    Mfululizo wa matukio ya haraka haraka. 
    • Masimulizi yawe ya kupendeza sana, pengine ya kuchekesha na yenye 
    kuteka hisia kwa maelezo ya kushangaza au yenye kujaa taharuki. 
    • Kutoa funzo maalumu kutokana na hadithi yenyewe, yaani maadili 
    fulani kuhusu maisha kwa ujumla. 
    27.5. Kusikiliza na kuzungumza: Majadiliano 
    Kazi ya 11:
    Serikali ya Rwanda inawahimiza wananchi kujitafutia ajira kutokana 
    na uhaba wa kazi. Jadili kuhusu namna ya kujitafutia kazi. 

    27.6. Kuandika: Utangazaji wa insha ya masimulizi 
    Kazi ya 12:
    Baada ya kusoma kifungu kuhusu insha za masimulizi “Mafanikio 
    ya kudumu,” tunga insha ya masimulizi kuhusu tukio fulani, kisa au 
    tukio la kweli au la kubuni kwa kuheshimu vipengele muhimu vya 
    insha ya msimulizi na taratibu zake.


    SOMO LA 28: MWONGOZO WA KUTUNGA INSHA

    xx

    Kazi ya 1:
    Unaona nini kwenye mchoro hapa juu?
    28.1. Kusoma na kufahamu: Siku yangu ya kwanza katika 

    shule za mabweni

    cc

    Mwanzo wa masomo yetu ulipokaribia kufika, wazazi wote walianza 
    kujiandaa kwa kutimiza wajibu wao wa kuwanunulia watoto wao mahitaji 
    kwa ajili ya masomo yao katika shule za sekondari. Wazazi wangu nao 
    waliwajibika kuninunulia mahitaji yote muhimu yaliyohitajika.

    Ulikuwa wakati wa mwanzo wa mwaka, shule za msingi na za sekondari 
    zilifungua tayari kwa kuanza masomo. Mimi niliamka asubuhi na mapema 
    nikatoka nyumbani saa kumi na mbili kamili. Baba, mama, dada na kaka 
    zangu wawili walinisindikiza umbali wa takribani kilomita mbili toka nyumbani 
    kabla ya wengine kurudi nyumbani isipokuwa baba. Baba yangu alichukua 
    begi langu lililokuwa zito nami nikachukua ndoo na godoro langu tukaendelea 
    mpaka kituo cha basi. 

    Tulipofika njiani, baba yangu aliniambia kwa sauti ya upole akisema: 
    “Mwanangu, nenda ukasome kwa bidii. Wakati ni mali, kamwe usiuatili. 
    Kumbuka kuwa tumewauza mbuzi wetu wawili ili tuweze kukutafutia vifaa 
    vyote unavyohitaji. Huko shuleni utakutana na vijana wengi wenye tabia 
    tofauti. Tafadhali, usishabihiane na wanafunzi wabaya ambao hawazingatii 
    maonyo na mawaidha ya wazazi wao na walimu”. Nami nilifikiria kidogo ili 
    niweze kumpa baba yangu jibu kutokana na yale aliyoniambia. Hatimaye 
    nilipata cha kumuambia baba. “Baba! Sitakusaliti kamwe! Malezi uliyonipa 
    tangu utotoni mwangu nitayatilia maanani; nitajifunza kwa bidii kama 
    unavyonitakia. Sitalandana na vijana hao wasio na maadlili mema.” Baada 
    ya kusikia hayo, baba yangu alitikisa kichwa kuonyesha kukubaliana nami 
    kuhusu mwelekeo wangu wa maisha katika mazingira niliyokuwa natarajia 
    kuingia. 
    Tuliendelea na safari mpaka tulipofika kwenye kituo cha basi. Huo ulikuwa 
    mwendo wa saa moja tu kwa miguu. 

    Kwenye kituo cha basi, kulikuwa na wanafunzi wengi lakini mabasi yalikuwa 
    machache. Baada ya dakika thelathini, basi lilikuja tukaingia sote. Mimi 
    nilikaa upande wa dirisha na baba alikaa karibu nami.Tuliendelea na safari 
    yetu mpaka shuleni. Kufika hapo, tulielekea kwenye ofisi ya mwalimu mkuu 
    wa shule ili tujitambulishe na kujisajilisha. Hapo nje palikuwa na umati wa 
    wanafunzi waliokuwa wakielekezwa kwenye mabweni yao na wengine 
    wakifanya shughuli za usafi. Labda hao walikuwa wenyeji wa shule hiyo 
    kwani walikuwa wakizungumza na kucheka kwa furaha kubwa pasipo 
    wasiwasi wowote

    Tulipiga hodi ofisini tukapokelewa vyema. Hedimasta alituuliza habari kamili, 
    tukamwelezea yote halafu nilielekezwa kwa katibu ambaye alinisajili baada 
    ya kuonyesha stakabadhi ya malipo ya karo ya shule. Mfanyakazi huyu 
    alimwita afisa wa nidhamu ili anipeleke bwenini na kunionyesha kitanda 
    changu. Hapo hapo nilimuaga baba yangu, naye akarudi nyumbani baada 
    ya kunitakia kila heri na fanaka katika masomo yangu. 

    Nilipofika bwenini nilishangaa sana kuona vitanda vingi katika ukumbi 
    mkubwa ambapo kila kitanda kilikuwa na sehemu mbili za kulala, moja chini 
    na nyingine juu yake. Nilitandika godoro langu kwenye sehemu ya chini ya 
    kitanda. Hata hivyo, nilikuwa na hofu kubwa moyoni kuwa yule atakayelala 
    juu yangu siku moja anaweza kuniangukia. Lakini nilijikaza kiume nikafikiria 
    kwamba hayo yalikuwa mazoea yao na kwamba shule haingekubali 
    kuendeleza hali hiyo kama kungetokea tatizo kama hilo. 
    Baadaye, kengele ililia kuwaita wanafunzi wote kuingia bwaloni kupata 
    chakula cha jioni. Chakula kilikuwa kizuri. Siku hiyo tulikula wali, maharagwe, 
    mboga na matunda.

    Tulipomaliza kula tuliambiwa kuingia madarasani mwetu kwa masomo ya 
    kibinafsi. Sisi sote tuliingia darasani, kila mwanafunzi alichukua daftari fulani 
    alilotaka na kuanza kujikumbusha yale tuliyokuwa tumesoma hapo awali. 
    Mimi nilichukua daftari langu la somo la Kiswahili nikaanza kupitia masomo 
    yote tuliyojifunza katika kidato cha tatu. Shughuli hii iliendelea mpaka saa 
    tatu za jioni ambapo kengele ililia tena kuashiria kuenda mabwenini kulala. 
    Mumo humo, tulilala kwa utulivu mpaka asubuhi tulipoamka kuanza masomo 
    yetu. 

    Kwa hakika, siku hiyo ya kwanza ya masomo yangu katika shule za mabweni 
    ilikuwa siku ya furaha na ugunduzi wa mambo mengi yanayohusu mazingira 
    ya shule hizo ambayo sikuyajua. Nilifurahia maonyo niliyopewa na wazazi 
    wangu na jinsi nilivyopokelewa na kuelekezwa na kila mmoja niliyemkuta 

    katika shule yangu.

    Kazi ya 2:
    Maswali ya Ufahamu 
    1. Eleza shughuli za wazazi kila wanapokaribia mwanzo wa masomo 
    ya watoto wao. 
    2. Mwanafunzi anayezungumziwa katika kifungu hiki anakwenda 
    kujifunza katika aina gani ya shule? 
    3. Nani ambaye alimsindikiza mwanafunzi hadi shuleni? 
    4. Ni mawaidha gani aliyompatia baba yake walipokuwa njiani?
    5. Eleza sifa za mwanafunzi anayezungumziwa katika kifungu hiki. 
    6. Ni nini kinachokuonyesha kwamba mwanafunzi huyu alipokelewa 
    vizuri mara tu alipofika shuleni? 
    7. Kwa nini alishangaa alipofika bwenini? 
    8. Wanafunzi walipewa chakula gani wakati wa jioni? 
    9. Walipoingia darasani mwanafunzi huyu alifanya nini? 
    10. Wanafunzi walitakiwa kulala saa ngapi? 
    28.2. Matumizi ya msamiati 
    Kazi ya 3:
    Tunga sentensi fupi kwa kutumia maneno yafuatayo kama 
    yalivyotumiwa katika kifungu ulichokisoma hapo juu.

    1. kujiandaa                                                       6. maadili 
    2. kusaliti                                                            7. heri na fanaka 
    3. kuuza                                                               8. ukumbi 
    4. bidii                                                                  9. kusajili 

    5. tabia                                                                10. kuashiria

    Kazi ya 4:

    Tumia mshale kwa kuonyesha maana ya maneno yafuatayo:

    c

    28.3. Sarufi: matumizi ya alama za vituo
    a. Nuktambili / koloni ( : )
    Kazi ya 5:
    Tazama sentensi zifuatazo na kuzungumzia matumizi ya alama 
    nuktambili inayojitokeza.

    i. Tunaenda sokoni kununua vitu vifuatavyo: nyanya, mahindi,… 
    ii. Katika familia yetu kuna watoto kama: Karangwa, Mukamurenzi…
    iii. Jimbo la kusini kuna wilaya kama: Ruhango, Kamonyi, Huye

    Maelezo muhimu

    Nukta mbili 
    a. Hutumiwa kutanguliza maneno yaliyo katika orodha. 
    Kwa mfano: 
    i. Nenda ukaniletee: kalamu, karatasi na kifutio. 
    ii. Amenunua: machungwa, sukari, na ndizi. 
    b. Hutumiwa kuashiria maneno ya msemaji badala ya alama za mtajo 
    hasa katika uandishi wa mazungumzo au tamthilia. 
    i. Mama: Lazima uniambie ulikokuwa tangu jana. 
    ii. Mwalimu alisema: Ingieni darasani. 
    c. Hutenganisha nambari za saa (saa na dakika). 
    Kwa mfano: 
    4: 10 – saa kumi na dakika kumi
    Kazi ya 6:
    Sahihisha sentensi zifuatazo
    1. Mifano ya ndege wanaofugwa ni kuku, bata, na njiwa
    2. Baba yangu hutengeneza meza, kiti, kitanda na kabati.
    3. Familia huwa na baba, mama, nyanya, babu na watoto
    4. Mimi huamka saa 2: 00 asubuhi kila siku
    5. Mchezo wa kandanda ulianza saa10: 00 jioni
    b. Nuktamkato / nukta na kituo / semikoloni ( ; )
    Kazi ya 7:
    Tazama sentensi zifuatazo na kuzungumzia matumizi ya alama 
    nuktamkato inayojitokeza.
    a. Sikwenda Kayonza; nilienda Kirehe.
    b. Usiwe na wasiwasi; nitakuwa pamoja nawe siku zote.
    c. Harusi hiyo ilihudhuriwa na watu wengi: wanawake kwa wanaume; 
    wadogo kwa wakubwa; wazee kwa vijana. 
     
    Maelezo muhimu
    Nukta na kituo 
    a. Hutumiwa kuunganisha vishazi vikuu bila kutumia kiunganishi.
     Kwa mfano: 
    • Tuliwasili darasani tukiwa tumechelewa; mwalimu alitukaribisha kwa 
    kutuuliza tulipokuwepo. 
    b. Hutumiwa kumpumzisha msomaji katika sentensi iliyo ndefu ili 
    apumzike zaidi kuliko pale inapotumiwa koma. 
    Kwa mfano: 
    Alipofikiri sana, alitanabahi kuwa hakikuwepo cha kutorokwa; yeye angeweza 
    kuondoka nyumbani au kumwacha mumewe, aende popote kufanya lolote.
    c. Kuorodhesha vitu hasa vinapokuwa na zaidi ya neno moja
    Mfano:
    Wakati wa likizo tulitembelea sehemu kadhaa: Mombasa, Kenya; Dodoma, 
    Tanzania; Kampala, Uganda na tukamalizia hapa Nairobi, Kenya.
    Kazi ya 8:
     Sahihisha sentensi zifuatazo: 
    1. Kabla ya kupata chakula ni lazima kunawa mikono hii ni tabia nzuri
    2. Akili ni mali kila mtu ana zake.
    28.4. Matumizi ya lugha: Taratibu za kutunga insha
    Kazi ya 9:
    Jibu maswali yafuatayo:
    1. Kwa sababu gani utangulizi mzuri ni muhimu katika insha? 
    2. Jadili sehemu kuu za insha. 
    3. Jadili mambo ya kuzingatia katika uandishi wa insha.
    Maelezo muhimu: Taratibu za kutunga insha: 
    • Soma kwa makini mada/ kichwa/ anwani uliyopewa zaidi ya mara moja, 
    ili uielewe vizuri. 

    • Ifikirie mada/ kichwa/ anwani kwa muda. 
    • Yaandike mambo muhimu yatakayokuongoza katika kuiandika insha .
    • Maelezo yote yatolewe kwa undani na kwa njia ya kuvutia. 
    • Kutumia vizuri alama za uakifishaji. 
    • Kupanga mawazo katika mtiririko wenye mantiki. 
    • Kutumia msamiati mwafaka kwa kutegemea mada. 
    • Lugha iwe ya adabu na isiyo ya matusi. 
    • Andika methali, misemo na nahau ambazo unadhania zinaweza 
    kukufaa katika utungaji. 
    Mambo ya kuzingatia katika uandishi wa insha 
    Bila kujali ni aina gani ya insha mtu anayoiandika, yapo mambo kadhaa ya 
    kuzingatia wakati wa uandishi wa insha. Mambo hayo ni pamoja na: 
    1. Kubaini ni mada gani ya kuandikia insha na kuielewa vyema, 
    2. Kupanga mawazo katika mtiririko wenye mantiki, 
    3. Kutumia mtindo unaoendana na kusudi la insha. 
    Kwa mfano: Mtindo wa masimulizi unafaa kwa hadithi au insha nyingine za 
    kisanaa.
    4. Kutumia lugha fasaha na inayoeleweka,
    5. Kufuata kanuni za uandishi. 
    Kwa mfano:
    Matumizi ya alama za uandishi, aya, herufi kubwa na herufi ndogo. 
    Kupanga insha katika muundo wake, yaani kichwa, utangulizi, kiini na 
    hitimisho. 
    1. Kichwa cha habari 
    Kichwa cha habari cha insha ni maneno machache, takribani matano, 
    ambayo ndiyo jina la insha. Kichwa cha habari huandikwa juu, katikati 
    kwenye ukurasa wa kwanza wa insha. Mara nyingi, huandikwa kwa herufi 
    kubwa na hubeba wazo kuu la insha. 
    2. Utangulizi wa insha 
    Utangulizi wa insha ni sehemu ya mwanzo yenye urefu usiozidi aya moja. 
    Utangulizi hudondoa kwa ufupi kabisa kile kinachoelezwa kwenye insha. 

    3. Kiini cha insha / mwili 
    Hii ni sehemu tunayoweza kusema ndiyo insha yenyewe. Kwenye kiini ndipo 
    ufafanuzi wote hutolewa. Ufafanuzi huu hupangwa katika aya moja au zaidi. 
    Hapa ndipo mwandishi hubainisha mawazo yake, huthibitisha, hushawishi, 
    huhimiza na hufafanua kiundani kabisa. 
    4. Hitimisho la insha 
    Hii ni sehemu ya mwisho ya insha ambayo nayo haizidi aya moja. 
    Katika sehemu hii, mwandishi anaweza kurejelea kwa ufupi sana yale 
    aliyozungumzia kwenye insha yake, anaweza kuonyesha msimamo wake, 
    anaweza kutoa mapendekezo, au kuwahimiza walengwa wake kuchukua 
    hatua fulani.
    28.5. Kusikiliza na kuzungumza
    Kazi ya 10:
    Chagua mada moja kati ya hizi, kisha uizungumzie kwa mapana na 
    marefu na kuiwasilisha mbele ya darasa.

    1. Harusi uliyoihudhuria
    2. Mchezo uliohudhuria
    28.6. Kuandika: Utungaji wa insha
    Kazi ya 11:
    Andika insha ya ukurasa mmoja kuhusu “Siku yangu ya kwanza shuleni.” 

    Tathmini ya mada
    A. Sahihisha makosa ya kimaandishi katika mazungumzo hapa chini
    Mgonjwa: hujambo daktari 
    Daktari: sijambo Karibu uketi. 
    Mgonjwa: asante daktari 
    Daktari: nikusaidie vipi 
    Mgonjwa: Jina langu ni kayitesi ninaumwa na tumbo sana. 
    Daktari: pole sana kayitesi tumbo lilianza kukuuma lini 
    Mgonjwa: Tangu jana usiku hata sijalala ninaendesha na kutapika sana
    Daktari: pole sana Ulikula nini jana usiku 
    Mgonjwa: Nilikula wali kwa kitoweo cha samaki
    Daktari Mmmmhh!Wewe hunywa maji yaliyochemshwa
    Mgonjwa Si kila siku daktari Mimi hunywa maji yoyote bora yanaonekana 
    kuwa safi.
    B. Andika insha ya masimulizi kuhusu mada zifuatazo: 
    i. Siku ya kuadhimisha mwaka mpya. 
    ii. Safari yangu mjini Kigali. 
    iii. Utoto wangu. 
    iv. Likizo iliyopita.



    

    MADA YA 6 UIGIZAJI WA MAZUNGUMZOMADA YA 8 DHIMA YA LUGHA YA KISWAHILI KATIKA JAMII