• MADA YA 6 UIGIZAJI WA MAZUNGUMZO

    Uwezo mahususi katika mada hii: Kuigiza mazungumzo mbalimbali kwa 
    kutumia Kiswahili sanifu.
    Malengo ya ujifunzaji:

    • Kuzungumza Kiswahili Sanifu kwa ufasaha;
    • Kujiamini katika mazungumzo ya hadharani au jukwaani;
    • Kukuza stadi za kusikiliza, kukariri na kuzungumza hadharani;
    • Kuendeleza weledi wa kubuni mazungumzo mbalimbali.
    Kidokezo
    1. Nini maana ya mazungumzo?
    2. Ni faida gani zinazopatikana kutoka mazungumzo?
    3. Mazungumzo hujadili mada gani?
    4. Katika mazungumzo, inawabidi wahusika kuwa na sifa gani? 

    5. Mazungumzo huweza kutokea wapi?

    SOMO LA 22: KUIGIZA MAZUNGUMZO

    vv

    Kazi ya 1:
    Unaona nini kwenye mchoro huu?
    22.1. Kusoma na ufahamu: Mazungumzo kati ya mwalimu 

    mkuu wa shule na mzazi


    cc
    Mwalimu mkuu wa shule: Karibu bibi! Habari za asubuhi?
    Bibi: Si nzuri hedimasta! Ahsante sana kwa kunikaribisha.
    Mwalimu mkuu wa shule: Shida gani bibi? Nikusaidieje?
    Bibi: Labda ni makosa ya mwanangu kutumwa mzazi.
    Mwalimu mkuu wa shule: Jina lake ni nani?
    Bibi: Gasagara Peter, mwanafunzi wa mwaka wa kwanza. 
    Mwalimu mkuu wa shule: Kwa nini umeitwa na shule?
    Bibi: Kwa sababu ya utovu wa nidhamu wa mtoto wangu. Sababu hii 
    niliisoma kwenye barua aliyopewa na shule ya kuniita mimi mzazi wake nije 
    hapa shuleni haraka.
    Mwalimu mkuu wa shule: Ndiyo! Mtoto huyo namkumbuka. Ni yapi 
    yaliyomsibu? Je, alikuelezea kilichotokea?
    Bibi: Alikuwa na makosa! Aliyakiri makosa matatu hivi: Kosa la kuchelewa 
    shuleni, kuja shuleni bila vifaa vya shule na kukosa usafi mwilini.
    Mwalimu mkuu wa shule: Ni kweli. Ilitubidi tumwite mzazi wake aje shuleni 
    kwa sababu ya mwenendo wa mtoto wako ulikuwa unaendelea kuzorota 
    sana. Bibi, unaweza kunielezea kwa nini mtoto wako hufanya kinyume na 
    wenzake?
    Bibi: Ushahidi ni kwamba sisi wazazi ndisi tuliokuwa chanzo cha matatizo 
    haya yote. Kulingana na shughuli za kimaisha, tulidharau fursa ya kumchunga 
    mwanetu na kuongea naye kila siku. Maana yake tulisahau jukumu letu 
    kama wazazi. Kwa hiyo, naomba msamaha. Toka leo nimeahidi kurekebisha 
    mienendo yetu na ya mtoto ili kuimarisha sura ya familia yetu.
    Mwalimu mkuu wa shule: Ahsante sana kwa uamuzi mzuri huu. Kwa 
    mujibu wa shule, tutashirikiana bega kwa bega kwa njia ya mawasiliano ya 
    kila siku. 
    Bibi: Asante sana kwa makubaliano haya. 
    Mwalimu mkuu wa shule: Kumbuka kuwa ahadi ni deni. 
    Bibi: Ndiyo, usijali yote yatatimizwa.
    Kazi ya 2:
    Jibu maswali ya ufahamu yafuatayo:
    1. Kifungu cha habari cha hapo juu kinazungumzia nini?
    2. Habari hii imetokea wapi?
    3. Kwa nini mzazi ameitwa shuleni?
    4. Ni makosa yapi yanayojitokeza katika kifungu cha habari?
    5. Ni makubaliano gani yaliyofikiwa kati ya wahusika wawili?
    6. “Harakati za maisha ya leo ni changamoto kubwa kwa elimu ya 
    watoto katika jamii.” Husisha maoni haya na kifungu cha habari.

    22.2. Matumizi ya msamiati
    Kazi ya 3:
    Kwa kutumia Kamusi ya Kiswahili Sanifu au njia nyingine tofauti, toa 
    maana ya msamiati ufuatao na kuutungia sentensi sahihi.
    a. Utovu wa nidhamu
    b. Kuja
    c. Kukiri 
    d. Kuzorota
    e. Chanzo
    f. Kuahidi
    g. Kurekebisha
    h. Kuimarisha
    i. Uamuzi
    j. Kushirikiana bega kwa bega

    Kazi ya 4:
    Jaza nafasi iliyoachwa wazi kwa kutumia msamiati unaofaa kutoka 
    kifungu cha habari

    i. ............. kosa ni njia ya kusamehewa.
    ii. Ukosefu wa mwenendo mzuri ni ..........................cha kushindwa 
    masomo shuleni.
    iii. Ni lazima kuepuka vita kwa sababu bila usalama amani na utulivu 
    ..................................
    iv. Tunaombwa .....................tabia mbaya ili tujenge jamii nzuri.
    v. Tumechukua ................huu shuleni kwa ajili ya kugombana dhidi 
    ya uvivu miongoni mwa wanafunzi

    Kazi ya 5:

    Toa kinyume cha msamiati ufuatao
    a. Kumkaribisha mtu
    b. Utovu wa nidhamu
    c. Kushirikiana bega kwa bega
    d. Kuzungumza
    e. Kuheshimu
    22.3. Sarufi: Matumizi ya “nini”, “nani” na “lini’ katika 
    kuuliza maswali

    Kazi ya 6:
    Soma sentensi zifuatazo na kuzungumzia matumizi ya maneno 
    yaliyopigiwa mstar
    i
    i. Jina lako ni nani?
    ii. Kifungu cha habari kinazungumzia nini?
    iii. Nchi yetu ilijinyakulia uhuru lini?
    Maelezo muhimu
    Maneno yaliyopigiwa mstari huitwa viulizi, yaani maneno yanayotumiwa 
    kuulizia swali. 
    Viulizi huweza kutumiwa mwanzoni mwa sentensi au mwishoni mwake.
    Kwa mfano:
    Nani amepiga hodi?
    • Umesema bwana huyo anaitwa nani?
    Matumizi maalum ya viulizi
    a. Nani
    Neno hili hutumiwa kuulizia mtu, Mwenyezi Mungu, mnyama, ndege au 
    wadudu.

    Mfano:

    • Nani amezungumziwa hapa?
    • Jina lake ni nani?
    • Nani aliyeumba binadamu?
    • Baadhi ya sungura na fisi, nani mjanja kuliko mwingine?
    b. Nini
    Hutumiwa kwa kuulizia kitu.
    Mfano: Mmejifunza nini leo?
    c. Lini
    Neno hili hutumiwa kuuliza majira, kipindi cha muda (tarehe au mwaka)
    Mfano: Ulizaliwa lini?
     Wageni wako waliwasili nyumbani lini?
    Kazi ya 7:
    Uliza swali linalofaa kwa kila sentensi kulingana na maneno 
    yaliyopigiwa mstari
    a. Shule yetu ilijengwa miaka thelathini iliyopita.
    b. Ukosefu wa usafi huweza kusababisha magonjwa.

    c. Mgeni amewasili nyumbani.

    22.4. Matumizi ya lugha: Mazungumzo na uigizaji wake
    Kazi ya 8:
    Kwa kuzingatia mfano wa mazungumzo hapo juu, eleza maana ya 
    neno ‘mazungumzo’ pamoja na aina zake.

    Maelezo muhimu ya kuzingatia
    Maana ya mazungumzo

    Mazungumzo au dayolojia ni utanzu mojawapo wa fasihi simulizi. Ni utaratibu 
    wa kuongea baina ya watu wawili au miongoni mwa watu zaidi ya mmoja au 
    pande mbili tofauti kuhusu mada mbalimbali zinazobadilikabadilika. 
    Baadhi ya vipera vya mazungumzo, vipera vitatu vifuatavyo ndivyo 
    vinavyojulikana na kutumiwa sana. 
    Malumbano ya utani: Ni mashindano ya kuongea jukwaani baina ya watu 
    wa makundi au jamii mbili ambayo hutumia kejeli na chuku kukejeli tabia 
    mbaya katika jamii au kundi fulani. Watu husimama jukwaani na kushindana 
    kwa maneno. Mazungumzo haya hutumia mzaha na vichekesho pamoja na 
    kejeli ili kuangazia ukweli fulani katika jamii.
    Ulumbi: Ni uwezo wa kipekee wa kuzungumza mbele ya hadhira. Mtu 
    mwenye uwezo huo wa kipekee wa kuzungumza jukwaani huitwa mlumbi. 
    Walumbi husifika sana kwa kuzungumzia mambo yanayoathiri jamii.
    Soga: Ni mazungumzo baina ya watu wawili au zaidi ambayo aghalabu huwa 
    hayana mada maalum. Aghalabu soga huwa na vichekesho vingi, mzaha 
    na kejeli. Nia yake huwa kuburudisha na kupitisha wakati. Soga huwa na 
    vichekesho na mzaha mwingi. Mada hubadilikabadilika kutoka wakati mmoja 
    hadi mwingine. Haihitaji taaluma yoyote ya kisanaa na inaweza kufanyika 
    pahali popote - njiani, sebuleni, katika vyumba vya burudani, n.k. 
    22.5. Kusikiliza na kuzungumza
    Kazi ya 9
    Sikiliza mazungumzo kutoka video zifuatazo na kusimulia mbele ya 
    darasa mambo yafuatayo:

    https=//
    https=//
    a. Dhamira kuu iliyozungumziwa
    b. Maudhui
    Kazi ya 10
    Kwa kushirikiana na wenzako, igiza mazungumzo kati ya mwalimu 
    mkuu wa shule na mzazi wa mwanafunzi

    22.6. Kuandika
    Kazi ya11:
    Buni mazungumzo (yenye ukurasa mmoja) kati ya mwalimu na mwanafunzi.

    Kazi ya12:

     Tunga sentensi sita kwa kuzingatia viulizi “nani” na “nini”.

    SOMO LA 23: UMUHIMU WA UIGIZAJI WA MAZUNGUMZO

    Kazi ya1:
    Unaona nini kwenye mchoro huu? 
    23.1. Kusoma na ufahamu: Tujivunie lugha yetu
    Kamana na Zaninka ni wanafunzi wanaosomea darasa moja kwenye Shule 
    ya Sekondari ya Tarubwenge. Wanazungumzia faida za kujizoeza uigizaji 
    wa mazungumzo kama mojawapo ya njia za kupata weledi na umahiri wa 
    lugha fulani.
    Kamana: Dada, unakumbuka jinsi tulivyokuwa miaka mitatu iliyopita?
    Zaninka: Unataka kumaanisha nini? Unadhani nilihifadhi matukio yote 
    katika miezi thelathini na sita yote?
    Kamana: Nimetaka kuzungumzia mchakato wa kukuza ujuzi wetu katika 
    stadi nne za lugha ya Kiswahili.

    Zaninka: Aa! Kuna mambo tele ya kuongea kuhusu mafanikio tuliyonayo

    Kamana: Kiwango cha matumizi ya Kiswahili leo ni cha juu mithili ya 
    Waswahili wenyewe.
    Zaninka: Acha! Haya ni majivuno! Nakubali tumepiga hatua kubwa lakini 
    hatujashindana na wale wakazi wa pwani.
    Kamana: Mimi nina ushahidi mkubwa sana. 

    Zaninka: Ushahidi wako unautoa wapi? 
    Kamana: Weledi wangu katika kuizungumza kwa ufasaha lugha ya Kiswahili 

    ulitokana na mazoezi darasani kwa kuigiza mazungumzo mbalimbali. 
    Zaninka: Si hayo tu. Kwa nini huzungumzii faida nyingine?
    Kamana: Kwa mfano?
    Zaninka: Kama kujiamini katika masimulizi hadharani.

    Kamana: Huo ni ukweli mtupu. Wiki iliyopita niliingia katika mashindano ya 
    mdahalo pamoja na wanafunzi kutoka shule tofauti za mjini ambao nilikuwa 
    ninawaogopa kulingana na tajriba yao ya kuitumia lugha ya Kiswahili kwa 
    ufasaha.
    Zaninka: Matokeo ya mashindano yalikuwaje?
    Kamana:Bila shaka nilijinyakulia ushindi na kutunukiwa kombe la almasi!
    Zaninka: Mimi nimeishafanya maajabu kijijini kwetu! Wakati wa sherehe 
    mbalimbali watu hunialika kwa ajili ya kuwaburudisha kupitia uigizaji wa 
    mazungumzo. Mwishowe hunipatia zawadi ya pesa zaidi ya elfu kumi. 

    Kamana: Hatuwezi kuorodhesha faida zote, ndiyo sababu tunapaswa 

    kujivunia lugha yetu tukufu.

    Kazi ya 2:
    Jibu maswali ya ufahamu yafuatayo:
    1. Kifungu cha habari kinazungumzia nini?
    2. Ni wahusika gani wanaozungumziwa kifunguni?
    3. Mafanikio ya wanafunzi hawa yalisababishwa na nini?
    4. Je, majivuno ya wanafunzi hawa yana sababu ya kuwepo? Eleza.

    23.2. Matumizi ya msamiati

    Kazi ya3:
    Kwa kutumia kamusi ya Kiswahili sanifu au njia nyingine uzipendazo, 
    toa maana ya msamiati ufuatao:
    a. Kujivunia
    b. Mchakato
    c. Tele 
    d. Mafanikio
    e. Kujiamini
    Kazi ya4:
    Jaza nafasi iliyoachwa wazi kwa kutumia msamiati huu: majivuno, pwani, ushahidi, tajriba, kujinyakulia
    i. Zaninka na Kamana wametoa..............................kwamba uigizaji 
    wa mazungumzo ulikuwa chanzo cha mafanikio yao.
    ii. Inahakikishwa kuwa asili ya Kiswali ni sehemu za................... au 
    mwambao wote wa Afrika Mashariki.
    iii. .......................ni tabia ya kujisikia bora kuliko wengine; maringo.
    iv. Baada ya kuishambulia timu B, timu A iliweza .........................ushindi wa mabao mawili kwa nunge.
    23.3. Sarufi: Matumizi ya “nini”, “wapi” na “kwa nini’ katika kuuliza maswali
    Kazi ya 5:
    Soma sentensi zifuatazo na kuzungumzia matumizi ya maneno yaliyopigiwa mstari
    i. Je, miti itapandwa wapi?
    ii. Kwa nini vijana hawajaelewa hasara ya kutumia dawa za kulevya?

     Maelezo muhimu

    a. Wapi
    Tunatumia neno hili kuulizia mahali au sehemu fulani
    Mfano: Unaishi wapi? ; Umesema uliniona juzi. Je, uliniona wapi?
    Tanbihi: Matumizi ya neno ‘pahali’, kiulizi ‘wapi’ hugeuka ‘papi’
    Mfano: Pahali papi panapotembelewa sana nchini humu?
    b. Kwa nini/ mbona
    Kiulizi hiki hutumiwa kuulizia sababu.
    Mfano: Kwa nini/ mbona mmechelewa kufika shuleni?
    c. Namna gani
    Neno hili hutumiwa kuulizia namna au jinsi jambo lilivyotendeka
    Kwa mfano:
    Mlifanya kazi hii namna gani?
    Kazi ya 6:
    Toa swali sahihi kutegemea maneno au kundi la maneno yaliyopigiwa mstari
    i. Sokwe mtu hupatikana katika mbuga ya wanyama iliyoko kaskazini 
    mwa Rwanda.
    ii. Taka zote hutupwa jalalani.
    iii. Hali ya hewa ilikuwa nzuri mwaka huu kwani raia walipanda miti 
    pahali pengi.
    iv. Mauaji ya kimbari dhidi ya Watutsi yaliwezekana nchini Rwanda 
    kwa sababu ya itikadi ya ubaguzi wa kikabila iliyofundishwa miaka mingi.

    23.4. Matumizi ya lugha: Mazungumzo na uigizaji wake
    Kazi ya 7:

     Jadili maswali yafuatayo:
    a. Nini maana ya uigizaji wa mazungumzo?
    b. Uigizaji wa mazungumzo una umuhimu gani?
    Maelezo muhimu
    a. Kuigiza mazungumzo ni nini?
    Ni kuyakariri mazungumzo yaliyosimuliwa na mtu mwingine na kuyarudia 
    kwa kumwiga mtu huyo kimatendo kwa njia au namna ya mchezo; yaani 
    kuvaa uhalisia wa mtu huyo. Ni karibu na maigizo au michezo ya kuigiza.

    b. Umuhimu wa kuigiza mazungumzo
    • Huunganisha watu katika jamii
    • Hutumiwa kama chombo cha kuburudisha katika jamii.
    • Vilevile huelimisha kuhusu mambo fulani
    • Pia huleta umoja na utangamano
    • Hutumiwa kuonya dhidi ya matendo mabaya.
    • Hutumiwa kupitisha wakati.
    • Hukuza stadi za kuzungumza lugha kwa ufasaha
    23.5. Kusikiliza na kuzungumza
    Kazi ya 8:
    Kwa ushirikiano na wenzako, igiza mazungumzo kati ya Zaninka na 
    Kamana.
    23.6. Kuandika
    Kazi ya 9:
    Buni kifungu cha habari kwa kutilia mkazo juu ya umuhimu wa 
    uigizaji wa mazungumzo
    Kazi ya 10:
     Tunga sentensi nne kwa kutumia viulizi ‘’wapi’’ na ‘’kwa nini’’.

    SOMO LA 24: VIFAA KATIKA UIGIZAJI WA MAZUNGUMZO

    vv

    Kazi ya 1:
    Unaona nini kwenye mchoro huu? 
    24.1. Kusoma na ufahamu: Majukumu yetu katika uigizaji wa mazungumzo
    Egide na Liliane ni wanafunzi wanaosomea kidato kimoja kwenye Shule 
    ya Sekondari ya Mazungumzo. Wanazungumzia vifaa vinavyowasaidia 

    katika uigizaji wa mazungumzo pamoja na sifa za mwigizaji bora

    Egide: Liliane, unayakumbuka mashindano tutakayoshuhudia wiki ijayo?
    Liliane: Bila shaka nayakumbuka na nilazima tuanze maandalizi yake
    Egide: Hayo ni kweli. Je, ni vifaa gani tutakavyohitaji ili tuliambulie kombe?
    Liliane: Baadhi ya vifaa muhimu ni lazima kuwepo na simu ya mkononi, 
    kofia, aina tofauti za pesa, chupa, tarumbeta, n.k.
    Egide: Usisahau aina za mavazi mbalimbali kama suti, kimono, tarubushi 
    pamoja na bombo.
    Liliane: Aa! Hatukutaja vuvuzela, barakoa za ucheshi, mkongojo pamoja na 
    miwani.
    Egide: Asante sana kwa nyongeza. Sasa ni wakati wa kuzungumzia sifa 
    zinazofaa kwa kila mwigizaji wa mazungumzo.
    Liliane: Hizo ni mboga! Kwanza, mwigizaji bora ni lazima ajiamini katika 
    mazungumzo yake.
     Pili, anapaswa kutumia lugha ya ishara kama vile kusugua mikono, kutikisa 
    kichwa, kugusa pua, kupiga vidole, kuinua nyushi, n.k. 
    Tatu, kuwa na ucheshi wa kutosha
    Nne, kutumia vihisishi ili kufanya mazungumzo yawe ya kusisimua.
    Egide: Si hayo tu, sifa zifuatazo sharti zizingatiwe pia:
                    Kutumia matamshi au lafudhi bora
                    Kuzungumza kwa ufasaha Kuonyesha moyo wenye huruma
                   Kuwa na mazungumzo ya mkato na yasiyozidiana sana kati ya 
                   wahusika. Mhusika mmoja asitawale mazungumzo kupita wengine.
    Liliane: Naam! Egide, tujipigie makofi kabisa! Ushindi ni wetu bila shaka.
    Egide: Lakini kumbuka lililosemwa na wahenga kwamba chelewa chelewa utamkuta mtoto si wako.
    Liliane: Usijali kaka yangu! Nimekupata wazi, ni lazima maandalizi yaanze leo bila kungoja kesho. 
    Egide: Naam, liwezekanalo leo lisingoje kesho.

    Maswali ya ufahamu

    Kazi ya 2:
    Jibu maswali ya ufahamu yafuatayo:
    1. Kifungu cha habari kinazungumzia nini?
    2. Ni wahusika gani wanaozungumza?
    3. Ni vifaa gani vilivyotajwa?
    4. Onyesha angalau sifa tatu muhimu anazostahili mwigizaji bora.
    5. Bila shaka wanafunzi hawa watajinyakulia ushindi. Tetea ukweli 
    huu kulingana na ushahidi kutoka mazungumzo.
    24.2. Matumizi ya msamiati
    Kazi ya 3:

    Kwa kutumia Kamusi ya Kiswahili Sanifu au njia nyingine tofauti, toa 
    maana ya msamiati ufuatao na kuutungia sentensi sahihi.
    a. Kombe
    b. Kujali
    c. Maandalizi
    d. Mkongojo
    e. Ucheshi
    f. Kimono
    g. Tarubushi
    h. Bombo
    i. Barakoa

    Kazi ya 4:
    Oanisha michoro hii na majina yake, kisha eleza umuhimu wa kila 
    aina: tarumbeta, vuvuzela, suti, miwani, barakoa.
    vv

    cc


    24.3. Sarufi: Matumizi ya “gani” na “-ngapi’ katika kuuliza maswali
    Kazi ya 5:
    Soma sentensi zifuatazo na kuzungumzia matumizi ya maneno yaliyopigiwa mstari 
    i. Swali gani ambalo halikutolewa jibu?
    ii. Miti mingapi mliyoipanda nyumbani kwenu?
    Maelezo muhimu
    a. Gani
    Neno hili hutumiwa kuulizia aina ya mtu au vitu.
    Mfano: Tatizo gani linalojitokeza hapa?
    Tanbihi: 
    1. Kiulizi gani huweza kuwakilishwa na kiwakilishi -pi
    Mfano: 
    • Tatizo lipi ambalo halijatatuliwa?
    • Vitambulisho vipi vinavyotakiwa kwa kila mwanafunzi?
    • Darasani mpi mnapatikana uchafu?
    2. Viulizi mbalimbali huweza kuchukua nafasi ya viwakilishi viulizi.
    Mfano:
    Zipi zimenunuliwa?
    Papi pamesafishwa?
    • Mpi mmesafishwa?
    b. -ngapi
    Hiki ni kiulizi cha kuulizia idadi ya watu au vitu.
    Kwa mfano:
    • Ng’ombe wangapi walitolewa kwa raia kwa ajili ya kujitegemea? 
    • Ni wanafunzi wangapi wanaoomba mahitaji maalum ya ujifunzaji?
    Tanbihi: Kiulizi hiki huweza kuchukua nafasi ya viwakilishi viulizi.

    Mfano: Vingapi vinahitajika?

    Kazi ya 6:
    Toa swali sahihi kulingana na maneno au kundi la maneno 
    linalopigiwa mstari
    i. Tumetumia vifaa vya aina nyingi katika maigizo yetu
    ii. Sabuni kadhaa zimewekwa nje ya choo kwa ajili ya usafi.
    iii. Wanafunzi kumi wamezawadiwa kwa sababu ya kuimarisha amani 
    na umoja darasani mwao.

    iv. Mwigizaji bora anapaswa kuwa na sifa kama vile kujiamini, 
    kuzungumza kwa ufasaha, kuzungumza kwa kutoa sauti, n.k.
    24.4. Matumizi ya lugha
    Kazi ya 7:
    Jadili mada zifuatazo:
    a. Umuhimu wa uigizaji wa mazungumzo
    b. Wahusika wanaoshiriki katika uigizaji wa mazungumzo
    c. Maigizo na aina zake
    Maelezo muhimu
    a. Kuigiza mazungumzo ni nini?

    Ni kuyakariri mazungumzo yaliyosimuliwa na mtu mwingine na kuyarudia 
    kwa kumwiga mtu huyo kimatendo kwa njia au namna ya mchezo; yaani, 
    kuvaa uhalisia wa mtu huyo. Ni karibu sawa na maigizo au michezo ya 
    kuigiza
    b. Wahusika katika uigizaji wa mazungumzo

    Kwa kawaida wahusika huwa ni binadamu. Wahusika ndio wanaozungumza 
    katika sehemu zao mbalimbali. Kulingana na aina ya mazungumzo, wahusika 
    wanaweza kuwa wawili au zaidi. Katika uigizaji wa mazungumzo, majukumu 
    ya watu wa marika au viwango mbalimbali huigizwa kama vile wazee, rais, 
    waziri, askari jeshi, mbunge, mwalimu, mfanyabiashara, mfalme, daktari, 
    hakimu, n.k.
    Maigizo ni sanaa katika fasihi simulizi ambayo watendaji huwa ndio wahusika. 
    Maigizo hayasimuliwi kama mbinu nyingine za fasihi. Wahusika ndio 
    huzungumza katika sehemu zao mbalimbali. Ifuatayo ni mifano ya maigizo.
    1. Michezo ya kuigiza ( agh. huletwa jukwaani): Haya ni maigizo ya 
    jukwaani ambapo watendaji huiga maneno na matendo ya wahusika 
    mbele ya hadhira.
    2. Miviga: Sherehe mbalimbali katika jamii fulani. Watu hujumuika na 
    sherehe hizi kulingana na tamaduni zao
    3. Ngomezi: Ni sanaa ya ngoma. Midundo mbalimbali ya ngoma 
    hutumika kuwasilisha jumbe mbalimbali.
    4. Malumbano ya utani: Mashindano ya kuongea jukwaani baina ya 
    watu wa makundi au jamii mbili ambayo hutumia kejeli na chuku 
    kukejeli tabia mbaya katika jamii au kundi fulani
    5. Ulumbi: Uwezo wa kipekee wa kuzungumza mbele ya hadhira. Mtu 
    mwenye uwezo huo wa kipekee wa kuzungumza jukwaani huitwa 
    mlumbi.
    6. Soga : Mazungumzo baina ya watu wawili au zaidi ambayo aghalabu 
    huwa hayana mada maalum.
    7. Vichekesho: Aina ya sanaa ya fasihi simulizi ambayo watu hutoa 
    vihadithi vifupi au sentensi zenye uwezo wa kuwafanya wasikilizaji 
    wacheke.
    8. Maonyesho ya sanaa: Maonyesho huhusisha watu wa jamii au kundi 
    fulani wanaoonesha taaluma, ujuzi au sanaa yao kwa watazamaji.
    24.5. Kusikiliza na kuzungumza
    Kazi ya 8:
    Kwa ushirikiano na wenzako, igiza mazungumzo kati ya Egide na Liliane.
    24.6. Kuandika
    Kazi ya 9:
    Buni kifungu cha habari ambapo vifaa tofauti pamoja na sifa 
    mbalimbali zimeonekana kwa wahusika wanaoigiza mazungumzo.
    Kazi ya 10:
    Tunga sentensi nne kwa kutumia viulizi “gani” na “-ngapi”.
    Tathmini ya mada
    1. Taja aina tatu za mazungumzo na kuzieleza
    2. Nini umuhimu wa uigizaji wa mazungumzo?
    3. Mwigizaji wa mazunguzo anastahili kuwa na sifa gani? Toa angalau tano
    4. Kwa kutegemea mifano mitatu, onyesha mandhari au pahali panapoweza kuigiziwa mazungumzo.
    5. Toa maswali sahihi kwa sentensi zifuatazo:
    i. Barabara hii ilijengwa kabla ya Wazungu kufika nchini humu.
    ii. Mtoto wangu hakuweza kufika shuleni jana kwani alikuwa mgonjwa.
    iii. Tunakuja shuleni kwa miguu.
    iv. Maswali kumi yametolewa na washiriki.
    v. Wazazi pamoja na walimu ndio watu muhimu katika jitihada za kuimarisha elimu bora.
    vi. Mgeni amepiga hodi.












    MADA YA 5 KISWAHILI KATIKA SHUGHULI ZA KIBIASHARAMADA YA 7 UTUNGAJI WA INSHA