• MADA YA 3 MSAMIATI KATIKA MAZINGIRA YA HOSPITALI

    Uwezo mahususi katika mada hii: 
    Kuzungumza na kuandika kwa ufasaha matini fupifupi kwa kutumia msamiati 
    unaofaa katika mazingira ya hospitalini.
    Malengo ya Ujifunzaji:
    • Kutumia kwa ufasaha msamiati maalum wa mazingira ya hospitali katika mawasiliano;
    • Kueleza vifaa vya hospitalini na umuhimu wake,
    • Kubainisha wafanyakazi wa hospitalini na majukumu yao,
    • Kusikiliza kwa makini na kusoma kwa ufasaha kifungu cha habari kinachohusika,

    • Kunyambua vitenzi kwa kuzingatia kauli mbalimbali.

    Kidokezo
    1. Hospitali ni nini?
    2. Orodhesha angalau hospitali tatu muhimu zinazojulikana nchini Rwanda.
    3. Taja vifaa vitano vinavyotumiwa hospitalini na kueleza umuhimu wake.
    4. Bainisha wafanyakazi angalau wanne wapatikanao hospitalini na kuainisha kazi au majukumu yao.

    SOMO LA 10: SEHEMU ZA HOSPITALI

    vvv

    Tazama kwa makini mchoro hapa juu. Zungumzia vitu muhimu 
    unavyoona vyenye uhusiano na hospitali.

    10.1. Kusoma na ufahamu: Ziara yetu hospitalini

    vv

    Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Maadili wamefanya ziara kwenye hospitali 
    moja wilayani Huye. Shabaha yao ni kuielewa vyema hospitali. Wamekaribishwa 

    na mpokezi wageni ambaye amewaongoza kwa Daktari Mkuu.

    Daktari: Hamjambo vijana!
    Vijana: Hatujambo Daktari! 

    Aminata: Jina langu ni Aminata na mimi ndimi kiranja wa darasa letu. Hawa 
    ni wanafunzi wenzangu.
    Tumefurahia fursa hii ya kuitembelea hospitali yenu kwa ajili ya kuyaelewa 
    vyema mazingira ya hospitali. 

    Daktari: Asante sana kwa nia yenu. Kwa hiyo, karibuni nyote! 
    Mimi ni Birashoboka, Daktari Mkuu wa hospitali hii. Na huyu ni muuguzi 
    wetu, jina lake Veneranda. 
    Nifuateni sasa niwatembeze sehemu mbalimbali za hospitali.

    Muuguzi: Tuanzie kwenye sehemu ambapo mmekaribishiwa na kupata kiti. 
    Sehemu hiyo huitwa pambajio. Ni sehemu ya kuwapokelea wagonjwa. 
    Pascal: Samahani Daktari! Sisi siyo wagonjwa, msije mkatudunga sindano!

    Daktari: Hahaaaa! Usiwe na wasiwasi kijana! Tafadhali tuendelee. Sehemu 
    hii ni chumba cha matibabu ya dharura, yaani chumba cha kuwatibia 
    wagonjwa wanaohitaji matibabu ya haraka sana kama vile majeruhi wa ajali. 

    Muuguzi: Samahani Daktari! Ni vizuri kuelewa kwamba chumba cha 
    dharura ni tofauti na wodi kwani wodi ni chumba cha kushughulikia maradhi 
    ambayo si ya kawaida kama vile maradhi ambayo yamezuka ghafla na bado 
    hayaeleweki vizuri. 

    Daktari: Asante sana Muuguzi! Kama nyongeza, kuna wodi nyingine 
    ambayo ni sehemu ya kuwalaza wagonjwa wanaoendelea na matibabu.

    Samilla: Samahani Daktari! Kwenye mlango ule nimesoma neno maabara. 
    Je, nini maana ya neno hili?

    Daktari: Vizuri sana! Maabara ni chumba cha kufanyia uchunguzi wa 
    magonjwa. Kwa kuwa hatuna muda wa kutosha wa kuizunguka hospitali 
    yote, inafaa kusimamia hapa na kumwomba Muuguzi awaelezee sehemu 
    nyingine za hospitali.

    Muuguzi: Asante sana Daktari! Kuna chumba cha kuhifadhia dawa; 
    kuna kungawi, yaani chumba cha kujifungulia kwa kina mama wajawazito; 
    chumba cha upasuaji; chumba cha uangalizi maalum ambacho ni chumba 
    cha matibabu ya kiwango cha juu sana. Hususan chumba hiki hutumiwa 

    kwa wagonjwa walio katika hali mahututi. 

    Daktari: Chumba hiki huwa na mitambo na mashine za hali ya juu sana za kumsaidia mgonjwa. 
    Muuguzi: Chumba cha mwisho ni ufuoni au makafani ambacho hutumiwa kuhifadhia maiti. 
    Jado: Asante sana kwa maelezo haya. Ningependa sasa mtuelezee kuhusu vifaa muhimu vinavyotumiwa humu.

    Kazi ya 2:
    Maswali ya ufahamu
    a. Soma kifungu cha habari hapa juu na kujibu maswali ya ufahamu yafuatayo:
    1. Habari hii imetokea wapi?
    2. Ni lengo gani la wanafunzi kuitembelea hospitali?
    3. Ni watu gani wanaozungumziwa katika kifungu cha habari hiki?
    4. Ni sehemu zipi za hospitali zilizotajwa?
    5. Aminata alikuwa na wajibu gani?
    b. Chagua jibu lililo sahihi kuliko mengine 
    1. Kifungu hiki cha habari kinazungumzia:
    a. Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Maadili na Daktari.
    b. Vifaa na wafanyakazi wa hospitali wilayani Huye.
    c. Ziara ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Maadili kwenye hospitali moja wilayani Huye.
    d. Mazungumzo kati ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Maadili kuhusu uchaguzi wa mchepuo wa udaktari.

    2. Walipofika hospitalini, wanafunzi walikaribishwa na

    a. Muuguzi.
    b. daktari mkuu.
    c. nesi.
    d. mpokeaji.
    3. wanafunzi walitembezwa sehemu za hospitali na
    a. daktari mkuu.
    b. muuguzi pamoja na daktari mkuu.
    c. mpokezi.
    d. majibu yote ni sahihi.
    4. Wanafunzi walielezewa vyumba vingapi ?
    a. vyumba tisa.
    b. vyumba vitatu.
    c. vyumba kumi.
    d. vyumba vitano.
    e. hakuna jibu sahihi.
    5. Kungawi ni chumba cha:
    a. kuwapasulia wajawazito.
    b. kuzalia wajawazito.
    c. kununulia dawa.
    d. kulalia wagonjwa.

    10.2. Matumizi ya msamiati kuhusu mazingira ya hospitali

    Kazi ya 3:

    Kwa kutumia Kamusi ya Kiswahili Sanifu au njia nyingine tofauti, toa 
    maana ya msamiati ufuatao na kuutungia sentensi sahihi.

    1. Kudunga                                 6. Kuhifadhi
    2. Matibabu                                7. Uchafu
    3. Mgonjwa                                8. Mjamzito
    4. Hali mahututi                      9. Kujifungua
    5. Kupenyeza                           10. Dharura

    Kazi ya 4:

    Oanisha maneno katika sehemu A na maana zake kutoka sehemu B.

    vv

    10.3. Sarufi: Matumizi ya kauli za vitenzi
    Kazi ya 5:
    Soma sentensi zifuatazo na kutofautisha viambishi vilivyokolea
    Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Maadili walikuwa wanapendana sana. 
    Waliandaa mpango wa kumwandikia Daktari Mkuu wa Hospitali kwa ajili 

    ya kuitembelea hospitali yake.

    Maelezo muhimu
    Viambishi vilivyokolea ni viambishi vya mnyambuliko wa vitenzi. 
    Mnyambuliko wa vitenzi ni jinsi vitenzi vinavyobadilika kulingana na kauli/

    hali mbalimbali.

    Hapo juu, kauli za vitenzi zilizotumiwa ni tatu kama ifuatavyo:
    i. Kauli ya kutenda.
    ii. Kauli ya kutendana.
    iii. Kauli ya kutendea.
    Yafuatayo ni maelezo kwa kila aina ya kauli: 
    1. Kauli ya Kutenda - kitendo katika hali yake ya kawaida (bila kunyambuliwa).
    2. Kauli ya Kutendana - unamfanya mtu kitendo, naye anakufanya vivyo hivyo.
    3. Kauli ya Kutendea - kufanya kitendo kwa niaba (au kwa ajili) ya mtu mwingine.

    Kazi ya 6:

    Onyesha mnyambuliko wa vitenzi ulivyochagua kisha uviweke katika 
    hali ya kutendea na kutendeana.

    Kazi ya 7:
    Tunga sentensi ambazo vitenzi vyake vinabeba kauli ya kutenda, 
    kutendea na kutendana 

    Kazi ya 8:
    Andika vitenzi vifuatavyo katika hali ya kutendea kwa kuzingatia 
    mabadiliko ya kimaana.
    1. Tumeandika barua kwa ajili ya rafiki zetu.
    2. Wazazi walifanya mema kwa niaba ya watoto wao
    3. Baba yake ameweka pesa kwenye akaunti kwa manufaa ya mtoto wake.

    10.4. Matumizi ya lugha: Sehemu muhimu za hospitali
    Maelezo muhimu kuhusu sehemu muhimu za hospitali
    Hospitali ni mahali pa kutibia wagonjwa. Kuna hospitali kubwa na nyingine 

    ndogo. Hospitali ndogo huitwa dispensali au zahanati.

    Hospitali ina sehemu muhimu zifuatazo:
    1. Pambajio: Sehemu ya kuwapokelea wagonjwa.
    2. Wodi: Sehemu ya kuwalaza wagonjwa wanapoendelea kupokea 
    matibabu.
    3. Kungawi: Chumba cha kujifungulia kwa waja wazito.
    4. Chumba cha upasuaji: Chumba cha kufanyiwa upasuaji wa wagonjwa.
    5. Wodi wa matibabu maalum: Chumba cha kushughulikia maradhi ambayo si ya kawaida k.m. maradhi ambayo yamezuka ghafla na bado hayaeleweki vizuri.
    6. Chumba cha matibabu ya dharura: Chumba cha kuwatibia wale wanaohitaji matibabu ya haraka sana k.m. waathiriwa wa ajali.
    7. Chumba cha matibabu ya kina: Chumba cha matibabu ya kiwango cha juu sana. Hususan hutumiwa kwa wale walio katika hali 
    mahututi. Chumba hiki huwa na mitambo na mashine za hali ya juu za kumsaidia mgonjwa.
    8. Maabara: Chumba cha kufanyia utafiti.
    9. Chumba cha dawa: Chumba cha kuhifadhia dawa zitolewazo kwa wagonjwa.
    10. Ufuoni/makafani: Mahali pa kuhifadhia maiti.

    10.5. Kusikiliza na Kuzungumza

    Kazi ya 10:
    Sikiliza taarifa ya habari moja kutoka redio au runinga juu ya mambo 
    ya afya. Isimulie mbele ya darasa.
    Kazi ya 11:
    Kwa ushirikiano na wenzako, igiza mazungumzo hapo juu
    Kazi ya 12:
    Fikiria zahanati au hospitali moja uliyoitembelea, kisha zungumzia 

    chumba kimoja ambamo uliingia na sababu za kuitembelea.

    10.6. Kuandika
    Kazi ya 13:

    Chora hospitali moja na kuonyesha sehemu zake angalau nne na 

    kueleza umuhimu wake

    bb

    Kazi ya 1:
    Tazama kwa makini mchoro hapa juu. Zungumzia vitu muhimu unavyoona 

    vyenye uhusiano na hospitali.

    11.1. Kusoma na ufahamu: Vifaa vya hospitalini

    vv

    Daktari: Kabla ya kutembelea vyumba vyote ambamo mmepatikana vifaa 
    mbalimbali, tazameni picha hizi za vifaa vipatikanavyo hospitalini. Picha hii ni ya 
    eksrei au uyoka ambayo ni mashine ya kutazamia viungo vya ndani ya mwili. 
    Muuguzi: Hii ni machela, yaani kigari au kitanda cha kubebea wagonjwa. 
    Aminata: Tafadhali Muuguzi. Je, naweza kuwasaidia? Picha inayofuata 
    ninajua jina lake.
    Muuguzi: Vizuri sana! Kushirikiana katika kazi zote ni jambo muhimu sana. 
    Fursa ni yako kiongozi wa darasa.
    Aminata: Ile ni mikroskopu au hadubini. Inatumiwa kuangalia vijidudu 
    vidogo sana ambavyo haviwezi kuonekana kwa macho tu. 
    Daktari: Hongera Aminata! Tuendelee. Hii ni dipfriza ambayo ni chombo 
    cha kuhifadhia dawa katika kipimo cha baridi kali sana. 
    Muuguzi: Jiko lile hutumiwa kuchemshia vyombo ili kuulia vijidudu na bakteria. 
    Kifaa hiki chenye umbo sawa na soksi kinaitwa glovu. Kinavaliwa mkononi 
    kumkinga muuguzi dhidi ya uchafu au kuambukizwa na maradhi. 
    Daktari: Vifaa hivi ninadhani vinafahamika kwa kila mtu. Vijana, nani ambaye anaweza kutuelezea?
    Bugingo: Hizi ni sindano. Zinatumiwa kupenyezea dawa mwilini. Pembeni 
    kuna makasi ambazo hutumiwa kwa kukatia vitu mbalimbali. 
    Muuguzi: Vijana, mpigieni makofi! Bendeji hii ni kitambaa cha kufungia 
    jeraha au kidonda kisichafuliwe. 
    Na hii ni plasta ambayo ni kitambaa kigumu sana cha kufungia sehemu ya 
    mwili iliyovunjika. 
    Daktari: Mwishoni, koleo hii husaidia kama kifaa cha kushikia vitu 
    vinavyotumiwa na daktari.

    Kazi ya 2:
    Maswali ya ufahamu
    a. Soma kifungu cha habari hapa juu na kujibu maswali ya 
    ufahamu yafuatayo:

    1. Mazungumzo haya yametokea wapi?
    2. Ni madhumuni gani ya wanafunzi kuitembelea sehemu hii?
    3. Ni wahusika gani waliowasiliana?
    4. Baadhi ya vifaa vilivyoonyeshwa, ni kifaa kipi ambacho kingeweza kuwatia hofu wanafunzi?
    5. Daktari ametumia mbinu gani ya kuonyesha na kuelezea vifaa? 
    b. Chagua jibu lililo sahihi kuliko mengine
    1. Kifungu hiki cha habari kinazungumzia:
    a. Vifaa vitumiwavyo hospitalini
    b. Daktari na wanafunzi
    c. Ziara ya wanafunzi hospitalini
    d. Hakuna jibu sahihi

    2. Katika maelezo yake, Daktari ameungwa mkono na

    a. muuguzi
    b. kiongozi wa darasa
    c. wanafunzi
    d. muuguzi pamoja na wanafunzi wawili.
    3. Dipfriza ni mojawapo ya:
    a. Wafanyakazi wa hospitalini
    b. Dawa za hospitalini
    c. Sehemu za hospitali
    d. Vifaa vya hospitalini.
    4. Machela inatumiwa kubeba
    a. Dawa za wagonjwa
    b. Walemavu
    c. Vifaa vya hospitalini
    d. Wagonjwa hospitalini.
    5. Daktari au Muuguzi anatumia bendeji
    a. Kumfunga kamba mgonjwa
    b. Kufungia kidonda
    c. Kufungia sehemu iliyovunjika
    d. Kumwezesha mgonjwa kutembeatembea.

    11.2. Matumizi ya msamiati

    Kazi ya 3:
    Kwa kutumia Kamusi ya Kiswahili Sanifu au njia nyingine tofauti, toa 
    maana ya msamiati ufuatao na kuutungia sentensi sahihi.
    i. Vidudu
    ii. Bakteria
    iii. Kuhifadhi 
    iv. Jeraha

    v. Kidonda

    Kazi ya 4:
    Jaza nafasi iliyoachwa wazi kwa kutafuta msamiati unaofaa kwenye 

    upande wa maneno na maana kwenye upande wa maelezo

    v

    Kazi ya 5:
    Kamilisha sentensi zifuatazo ili zilete maana kamili kwa kutumia 
    msamiati huu: eksirei, plasta, sindano, kuhifadhia baadhi ya dawa.
    1. Kitambaa kigumu sana cha kufungia sehemu iliyovunjika 
    huitwa.......................................................
    2. Dipfriza ni chombo...................................
    3. .......................ni kifaa cha kupenyezea dawa mwilini.
    4. ..................ni mashine ya kuonea viungo vya ndani ya mwili.

    11.3. Sarufi: Matumizi ya kauli za vitenzi
    Kazi ya 6:
    Soma sentensi zifuatazo na kutofautisha viambishi vilivyokolea
    Baada ya mpango kukamilika, walifikisha hoja zao kwa Mkuu wa shule 
    ambaye aliridhika na nia hiyo ya wanafunzi wake.
    Baadaye, walitumiwa barua na Daktari Mkuu wa hospitali ya kuwakubalia 
    ziara yao. 
    Maelezo muhimu
    Kauli za vitenzi zilizotumiwa katika sentensi hapo juu ni zifuatazo:
    i. Kauli ya kutendeka
    ii. Kauli ya kutendesha
    iii. Kauli ya kutendewa
    Yafuatayo ni maelezo kwa kila aina ya kauli: 
    1. Kauli ya Kutendeka - kitendo kukamilika au kuwa katika hali timilifu.
    2. Kauli ya Kutendewa - kitendo kufanywa kwa niaba yako au kwa ajili yako.

    3. Kauli ya Kutendesha - kumfanya mtu atende jambo fulani.

    Kazi ya 7:
    Onyesha mnyambuliko wa vitenzi vifuatavyo katika hali ya kutendeka 
    na kutendewa 
    Vitenzi ni kunywa, kuzaa, kupenda, kutaja na kujenga.
    Kazi ya 8:
    Tunga sentensi 3 ambazo vitenzi vyake vinabeba kauli ya kutendeka, 
    kutendesha na kutendewa

    Kazi ya 9:
    Soma kisa kifuatacho na kuweka vitenzi husika katika hali ya 
    kutendewa
    Baba alimpatia mtoto wake elimu kuhusu uhifadhi wa mazingira, 
    uzalishajimali pamoja na usawa wa kijinsia. Alimwelezea pia faida za 
    kupiga marufuku uvivu, ulevi pamoja na ukatili. Alimtungia hadithi za 
    kumwongoza na kumwelekeza katika njia nzuri za kimaisha. Baadaye, 
    alimpelekea wajibu wa kuzitetea haki za binadamu na kuishi kwa amani na 
    watu wote mahali popote atakapokuwepo. 
    11.4. Matumizi ya lugha: Vifaa vya hospitalini
    Kazi ya 10:

    Taja majina ya vifaa vifuatavyo na kueleza umuhimu wa kila kifaa.

    vvv

    Kazi ya 11:
    Tafuta vifaa vingine vinavyotumiwa hospitalini na kueleza umuhimu wake.
    Maelezo muhimu
    Hospitali hutumia vifaa mbalimbali wakati wa kuhudumia wagonjwa. Baadhi 
    ya vifaa hivyo ni hivi vifuatavyo:
    1. Eksrei/uyoka: mashine ya kuonea viungo vya ndani ya mwili.
    2. Machela: kigari au kitanda cha kubebea wagonjwa. 
    3. Mikroskopu/hadubini: kifaa kitumiwacho kuangalia vitu vidogo.
    4. Dipfriza: chombo cha kuhifadhia baadhi ya dawa zinazohitaji kuhifadhiwa katika kiwango cha baridi sana.
    5. Jiko: chombo cha kuchemshia vyombo ili kuulia viini na bakteria.
    6. Glovu: kitu kama soksi kitengenezwacho kwa mpira na huwekwa mkononi kukingia uchafu.
    7. Sindano: kifaa cha kupenyezea dawa mwilini.
    8. Sirinji: kifaa chenye umbo la bomba ambapo madaktari na wauguzi huchopeka sindano ili kumdunga mgonjwa au kufyonza sampuli ya damu.
    9. Makasi: kifaa ambacho hutumiwa kwa kukatia 
    10. Bendeji: kitambaa cha kufungia jeraha au kidonda
    11. Plasta: kitambaa kigumu sana cha kufungia sehemu iliyovunjika
    12. Koleo: kifaa cha kushikia vitu vinavyotumiwa na daktari.

    11.5. Kusikiliza na Kuzungumza

    Kazi ya 12:
    Kwa ushirikiano na wenzako, igiza mazungumzo yanayohusu vifaa 
    vya hospitalini.
    Kazi ya 13:
    Itembelee zahanati au hospitali moja, kisha uzungumzie vifaa 

    ulivyowahi kuviona.

    Kazi ya 14:
    Simulia hisia ulizokuwa nazo au ulizosikia kutoka mtu mwingine 
    kuhusu siku yako au yake ya kwanza kudungwa sindano hospitalini.
    11.6. Kuandika
    Kazi ya 15:
    Kamilisha sentensi zifuatazo kwa kuongozwa na muktadha wa vifaa vya hospitalini
    a. Nilipokuwa bado mtoto nilikuwa na woga wa kuenda hospitalini kwa sababu....................................
    b. Inasemekana leo kuwa Hospitali ya Roi Faisal ni maarufu sana kwa sababu....................................
    c. Hospitali au zahanati nyingi hushindwa kutoa huduma bora kwa sababu ya..................................
    d. Sindano hospitalini hutumiwa mara moja kwa mgonjwa kwa ajili ya.............................................

    SOMO LA 12: WAFANYAKAZI WA HOSPITALINI

    hh
    Kazi ya 1:
    Tazama kwa makini mchoro hapo juu kisha uzungumzie vitu muhimu 

    unavyoviona

    12.1. Kusoma na ufahamu: Kazi nzuri ya udaktari

    bb

    Wanafunzi wameendelea na matembezi yao hospitalini. Sasa ni wakati 
    wa kuongea na wafanyakazi.
    Muuguzi: Shukrani Daktari, ningependa tuelekee sehemu ambapo 
    tutawapata wafanyakazi mbalimbali ili niwaelezee kazi zao. Daktari au 
    tabibu mnayemwona hapa ndiye anayewatibu wagonjwa. Mimi ni Muuguzi 
    au nesi. Kazi yangu ni kumsaidia daktari katika kazi yake. 
    Mkunga: Jina langu ni Liberata. Mimi ni Mkunga. Kazi yangu ni kutoa 
    huduma kwa wajawazito wakati wa kujifungua. 
    Mhazigi: Ninaitwa Jean Paul. Mimi ni mhazigi. Wajibu wangu ni 
    kuwashughulikia waliovunjika viungo kama vile miguu au mikono. 
    Msaidizi: Ninaitwa Francoise, Msaidizi katika maabara. Mimi hutoa huduma 
    kwa wagonjwa. 
    Karani: Jina langu ni Shema, Karani wa hospitali. Jukumu langu ni kufanya 
    rekodi za wagonjwa. 
    Mfamasia: Mimi ni mfamasia na jina langu Pascasie. Kazi yangu ni kuziweka 
    dawa na kuzitoa kwa wagonjwa. 
    Daktari wa meno: Byiringiro Charles, daktari wa meno. Jukumu langu ni 
    kuwashughulikia wagonjwa walio na matatizo ya meno.

    Aminata: Kwa mujibu wa wanafunzi wenzangu, tumenufaika zaidi kutokana 

    na safari hii. Kwa kweli, tungeliitembelea hospitali hii mwaka jana, tungelijua 
    haya yote tayari. Wahenga walisema kwamba asiyefika kwa mfalme 
    hudanganywa mengi. Tumebahatika kufika hapa na mengi tumeyaelewa. 
    Mireille: Sisi sote tumeridhika na maelezo tuliyopewa. Kwa upande wetu, 
    tunaahidi kuwaunga mkono kama iwezekanavyo kwa kuchagua mchepuo 
    wa udaktari ili kuwahudumia wagonjwa hospitalini.
    Daktari: Asanteni sana vijana. Kwa heri ya kuonana, tunawatakia kila la kheri!
    Aminata: Asante sana Daktari pamoja na Muuguzi, na sisi tunawatakia kazi 
    njema!
    Kazi ya 2:
    Soma kifungu cha habari hapo juu na kujibu maswali ya ufahamu 
    yafuatayo:

    1. Ni watu gani wanaozungumziwa katika mazungumzo haya?
    2. Matembezi haya yamekuwa na lengo lipi?
    3. Jadili faida pamoja na hasara kutoka ziara ya wanafunzi iliyozungumziwa.
    4. Wanafunzi wameridhika na ziara yao. Je, unakubaliana na ukweli huu? Eleza msimamo wako.

    12.2. Matumizi ya msamiati kuhusu mazingira ya hospitali
    Kazi ya 3:
    Kwa kutumia Kamusi ya Kiswahili Sanifu au njia nyingine tofauti, 
    toa maana ya msamiati ufuatao na kutungia sanifu sentensi sahihi.
    a. Kutibu
    b. Jukumu
    c. Mujibu
    d. Wahenga
    e. kuahidi
    Kazi ya 4:
    cc
    Kazi ya 5:

    Husisha wafanyakazi wafuatao na vifaa wanavyotumia

    vv

    12.3. Sarufi: Matumizi ya kauli za vitenzi
    Kazi ya 6:
    Soma sentensi zifuatazo na kutofautisha viambishi vilivyokolea
    Walipowasili hospitalini walikaribishwa na kupokelewa vizuri. Walielezewa
    mambo mengi sana na kuongezewa ujasiri wa kuchagua mchepuo wa 

    udaktari. Waliahidi kwamba kazi yao itafanywa kwa bidii.

    Maelezo muhimu
    Viambishi vilivyopigiwa mstari vinaonyesha kauli ya kutendwa ambayo 
    huathirika moja kwa moja na kitendo
    Kazi ya 7:
    Andika vitenzi vifuatavyo katika hali ya kutendewa kwa kuzingatia 
    mabadiliko ya kimaana.

    1. Wezi wameniiba pesa zangu.
    2. Tulimzaa mtoto wa kike miaka sita iliyopita.
    3. Dawa imewaua nzi wengi kutoka chooni.
    4. Kampuni ilimfikisha meneja wake mahakamani kwa sababu ya 
    uporaji mali.
    5. Tumekula chakula kitamu kwa wingi.
    6. Tulivua samaki wengi kutoka ziwa Kivu.
    7. Si vizuri kunywea pombe hospitalini.
    8. Wilaya itatengeneza barabara za lami nyingi.
    9. Dobi amefua nguo za aina mbalimbali.

    12.4. Matumizi ya lugha: Aina za kazi
    Kazi ya 8:
    Katika jozi, jadilini kuhusu kazi za watu mbalimbali mnazozijua.
    Maelezo muhimu
    Zipo kazi za aina nyingi duniani. Kazi hizi hutofautiana kulingana na ujuzi, 
    elimu na tajiriba ya kiwango cha juu. 
    Ifuatayo ni baadhi ya mifano mbalimbali ya kazi:
    Mhasibu: Mtaalamu wa kuweka hesabu ya fedha.
    Mhandisi/injinia: Mjuzi wa kutengeneza, kuhudumia na kuunda mitambo.
    Tarishi/Katikiro: Anayehudumu ofisini kwa kutumwa kupeleka habari au ujumbe.
    Bawabu: Alindaye mlangoni.
    Topasi/chura: Asafishaye choo.

    Tabibu/daktari/mganga: Mwenye ujuzi wa kutibu.
    Muuguzi/mualisaji: Ahudumiaye wagonjwa.
    Msarifu: Anayesimamia na kuidhinisha matumizi mazuri ya fedha katika 
    shirika.
    Dereva: Aendeshaye vyombo vya nchi kavu k.v. gari.
    Nahodha: Aendeshaye na kuongoza vyombo vya majini k.v. meli.
    Rubani/Mwanahewa: Aendeshaye na kuongoza vyombo vya angani 
    k.v.ndege.
    Utingo/taniboi: Mpakiaji na mpakuaji wa mizigo katika gari.
    Hamali/mpagazi/mchukuzi: Abebaye mizigo kwa malipo.
    Malenga: Mtunzi stadi wa mashairi na nyimbo.
    Manju: Stadi wa kutunga na kuimba nyimbo katika ngoma.
    Kuli: Apakiaye na kupakua shehena za forodhani.
    Dobi: Afuaye na kupiga nguo za watu pasi kwa malipo
    Sogora: Fundi wa kupiga ngoma
    Saisi: Atunzaye wanyama wanaopandwa k.v. punda na farasi.
    Msajili: Awekaye orodha ya kazi, vitu au viumbe.
    Mkalimani/mtarijumani: Afasiriaye lugha moja hadi nyingine.
    Sonara: Atengenezaye mapambo kwa kutumia madini.
    Kinyozi: Anyoaye nywele.
    Msusi/msosi: Asukaye watu nywele.
    Ngariba: Mtu anayefanya kazi ya kutahiri katika jando.
    Mkunga: Awasaidiaye wajawazito kujifungua.
    Kungwi: Afundishaye mwari wa kike au kiume.
    Mshenga: Atumwaye kupeleka habari za ndoa (posa).
    Refa: Mwamuzi katika mchezo k.v. soka
    Kasisi: Kiongozi wa kidini katika madhehebu fulani ya kikristo
    Imamu: Kiongozi wa kidini katika madhehebu fulani ya kiislamu.
    Hakimu: Aamuaye kesi katika mahakama.
    Kadhi: Hakimu wa kiislamu
    Mwekezaji: Anayeweka mali au pesa katika mradi au biashara.
    Meneja: Msimamizi au kiongozi katika kampuni au shirika.
    Karani: Afanyaye kazi ya kuandika k.m. barua na majarida.
    Kocha: Mwalimu wa mchezo k.v. soka, voliboli, n.k.
    Mkutubi: Ahifadhiye vitabu maktabani na kuviazima kwa wasomaji.
    Mnajimu: Mwenye elimu ya nyota. Hutabiri mambo.
    Mpigaramli: Abashiriaye kwa kupiga bao.
    Mwajiri: Aandikaye mtu kwa kazi ya malipo au mshahara.
    Mzegazega: Achotaye maji na kuyauza.
    Dalali: Auzaye bidhaa katika mnada (soko la kushindania bei)
    Manamba: Mfanyakazi wa muda katika shamba kubwa.
    Mnyapara: Msimamizi wa kazi.
    Mhazili: Sekretari - Atunzaye barua na majarida na kuandika kwa mashine ofisini.
    Mhadhiri: Mwalimu katika chuo kikuu.
    Mwashi: Fundi wa kujenga nyumba.
    Mhunzi: Afuaye vitu vya madini ya chuma au bati.
    Seremala : Atengenezaye samani za mbao au miti.
    Mfinyanzi: Atengenezaye vyombo vya udongo k.m. vyungu.
    Mvuvi: Afanyaye kazi ya kuvua samaki.
    Mwanaanga: Afanyaye utafiti wa hali ya anga.
    Mkabidhi: Mtu atunzaye mali kwa ajili ya mwingine
    Diwani: Anayewakilisha watu wake katika serikali za wilaya
    Mzoataka: Anayeokota takataka
    Kaimu: Anayeshikilia cheo au wadhifa fulani kwa muda.

    12.5. Kusikiliza na Kuzungumza
    Kazi ya 9:
    Kwa kushirikiana na wenzako,buni na uigize mazungumzo kuhusu 
    kazi za ufundi mbalimbali.
    Kazi ya 10:
    Itembelee zahanati au hospitali moja, kisha zungumzia wafanyakazi 
    uliowaona hapo.
    Kazi ya 11:
     “Daktari ni muhimu sana kuliko mwalimu”. Jadili na wenzako kauli hii.
    12.6. Kuandika
    Kazi ya 12:

    Kamilisha sentensi hizi kulingana na ujuzi wako
    a. Ili uwe na cheti cha udaktari, unapaswa kuwa na weledi katika 
    mchepuo wa...............................
    b. Baada ya kuhitimu masomo ya................................ mtu huweza 
    kupatiwa cheti cha urubani
    c. Hakimu ni mfanyakazi ambaye alihitimu masomo ya...................
    d. Kasisi huwa ameyazingatia masomo ya ........................
    e. Keshia huteuliwa baada ya masomo ya.....................................
    f. Katibu ni lazima awe na stadi katika elimu ya.........................
    cc
    Kazi ya 1:

    Tazama mchoro huu kwa makini na kuzungumzia unachoona.

    cc

    Daktari Mkuu pamoja na Muuguzi kutoka hospitali moja wilayani Gatsibo 
    wamepata fursa ya kuwatolea wagonjwa maonyo kuhusu umuhimu wa usafi 
    katika maeneo ya hospitali na mahali pengine.
    Daktari:                               Hamjambo wote!
    Wagonjwa:                         Hatujambo Daktari!
    Daktari:                              Haya! Kabla ya kuwatolea huduma mbalimbali, ningetaka tuongee 
    kidogo kuhusu usafi hapa hospitalini.
    Nani anayeweza kutuelezea kwa nini usafi hospitalini ni muhimu sana?
    Mgonjwa wa 1:          Usafi hospitalini ni lazima utiliwe maanani kwa sababu 
    pasipokuwa na usafi afya ya wagonjwa pamoja na 
    wafanyakazi wa hospitalini huwa katika hali mbaya sana.
    Daktari:                      Vizuri sana! Nani mwingine ambaye anaweza kutaja mahali ambapo 
    usafi unastahili kuliko pengine?
    Mgonjwa wa 2:            Mahali muhimu pakushughulikia mno ni kama vile vyooni, 
    vyumbani pamoja na nje ya hospitali.
    Muuguzi:                      Asante sana! Je, mnafikiri nini kwa mtu ambaye anakuja 
    hospitalini bila usafi wa mwili pamoja na mavazi yake?
    Mgonjwa wa 3:                           Kwa ukweli, watu kama hao wapo lakini tabia hiyo ni ya 
    kuepuka sana.
    Daktari:                  Ndiyo. Lakini ni lazima kujua kwamba usafi hospitalini 
    huchunguzwa kupitia vifaa vyote vinavyotumiwa, dawa 
    zinazotunzwa na kupewa wagonjwa, mahali pa kutolea 
    huduma tofauti bila kusahau usafi wa mwili na nguo kwa 
    wafanyakazi wa hospitalini.
    Muuguzi           :Sasa, nani ambaye anaweza kueleza hasara inayotokana 
    na ukosefu wa usafi kwa ujumla?
    Mgonjwa wa 4            : Si hospitalini tu, ukosefu wa usafi mahali popote huweza 
    kuambukiza magonjwa kadhaa kama vile ugonjwa wa 
    kipindupindu, kuhara, minyoo, n.k.
    Daktari                       : Asante sana! Basi, nani wa kueleza njia au jinsi magonjwa hayo yanavyosambazwa?
    Mgonjwa wa 5        :  Kwa mfano, kama vyoo havisafishwi vizuri, nzi huweza 
    kujitafutia makazi humo. Wadudu hawa wanapogusa
    kinyesi cha mgonjwa na kutua kwenye chakula cha watu 
    wazima vilelevile huwaambukiza ugonjwa wa kipindupindu 
    au kuhara. Lakini na matumizi ya maji machafu huweza 
    kuwa chanzo cha magonjwa haya.
    Muuguzi:                  Je, hakuna ugonjwa mwingine unaosababishwa na ukosefu 
    wa usafi kwenu nyumbani?
    Mgonjwa wa 6:                Taka zikitupwa mahali pasipofaa, madimbwi pamoja na 
    vichaka karibu na nyumba huwakaribisha mbu ambao 
    husababisha ugonjwa wa malaria.
    Daktari:                     Asante sana kwa mchango wenu. Kumbukeni kwamba 
    usafi ni ufunguo wa afya njema. Inatubidi kuushughulikia 
    mahali popote kwa ajili ya kuboresha maisha yetu mema.

    Kazi ya 2:

    Maswali ya Ufahamu
    Chagua jibu sahihi kuliko mengine 
    1. Tunatakiwa kuwa na usafi mahali popote kwa sababu
    a. usafi ni mzuri
    b. usafi wa mwili hulinda magonjwa
    c. penye ukosefu wa usafi maisha ya binadamu pamoja na ya 
    mazingira yake huathirika vibaya.
    d. Mbu huweza kujificha katika vichaka na kuambukiza ugonjwa wa 
    malaria. 
    2. Ugonjwa wa kipindupindu au kuhara husababishwa na 
    a. nzi
    b. uchafu kutoka kinyesi unaosambazwa na nzi pamoja na matumizi 
    ya maji machafu
    c. chakula kichafu na ambacho hakikuiva vizuri
    d. ukosefu wa vyoo safi na vya kutosha.

    3. Taka zote ni lazima

    a. zichomwe
    b. zitupwe shambani
    c. zitupwe jalalani baada ya kutofautisha zinazooza na zisizooza
    d. zihifadhiwe katika mashimo mbali na nyumba.
    4. Inastahili kuvaa glovu na bwelasuti wakati wa
    a. kula
    b. kupiga deki
    c. kuingia hospitalini
    d. kufanya usafi kwa ajili ya kujikinga na uchafu.
    5. Usafi hospitalini ni jukumu la 
    a. wagonjwa
    b. wagonjwa, wafanyakazi wa hospitali pamoja na yeyote anayekwenda hapo
    c. wafanyakazi wa hospitali

    d. hakuna jibu sahihi.

    13.2. Matumizi ya msamiati
    Kazi ya 3:

    Eleza maana ya maneno yafuatayo:
    1. Madimbwi 
    2. Kupiga deki 
    3. Huduma 
    4. Kuambukiza 
    5. Kipindupindu
    6. Kichaka
    7. Minyoo

    8. Bwelasuti

    Kazi ya 4:

    Kamilisha sentensi zifuatazo kwa kutumia choo, kuhara, deki, 
    kutiliwa maanani, taka.

    1. .....................ni kifaa chenye majimaji kinachotumiwa kuosha 
    sakafu ili kuondoa uchafu.
    2. Baada ya kujisaidia ni lazima umwage maji 
    katika........................................................................................
    3. Matumizi ya maji machafu yanaweza kuwa chanzo cha 
    kuambukizwa ugonjwa wa......................................
    4. Kila jamii inalazimishwa kuwa na jalala la 
    kutupia......................................................
    5. Usafi ni jambo la...........................mahali popote.
    13.3. Sarufi: Matumizi ya kauli ya kutendeshana
    Kazi ya 5:
    Soma sentensi zifuatazo na kueleza maana ya kitenzi baada ya 
    kuongezewa viambishi vilivyopigiwa mstari.

    1. Martha na Peter wanaelimishana mambo ya kujitegemea.
    2. Walikaribishana na kutoa hoja zao.

    3. Si vuzuri kugombanishana watu.

    Maelezo muhimu
    Kauli ya Kutendeshana - mtu anakufanya utende jambo fulani, nawe 
    unamfanya atende jambo hilo hilo.
    Kazi ya 6:
    Weka vitenzi vifuatavyo katika hali ya kutendeshana
    a. Wamepikiana chakula kitamu.
    b. Tumefanyana mambo mema ya kuieleza jamii yetu.
    c. Wamelimiana shamba la maharage.

    d. Mmechora michoro inayoeleza wazi usawa wa kijinsia

    13.4. Matumizi ya lugha: Msamiati kuhusu aina za magonjwa
    Kazi ya 7:
    Zungumzia aina mbalimbali za magonjwa yanayoweza kuhatarisha 
    maisha ya binadamu
    Maelezo ya kuzingatia
    a. Maana ya ugonjwa
    Ugonjwa ni hali au kitu kinachomfanya mtu, mnyama au mmea kuwa katika 
    afya duni. Pia ugunjwa huitwa maradhi, uele, ukongo. Kuna maradhi chungu 
    nzima yanayoweza kumwathiri mtu. Mengine yana tiba mengine hayana. 
    Mengine yanaambukizwa.
    Maradhi ya kuambukiza ni yale yanayoenea kutoka kwa mtu mmoja hadi 
    mwingine.
    b. Aina za maradhi
    Kuna aina mbalimbali za ugonjwa au maradhi. Ifuatayo ni miongoni mwa mifano.
    Saratani/kansa: ugonjwa usio na tiba kwa sasa. Ni ukuaji usio wa kawaida wa seli katika mwili.
    Malale: ugonjwa wa usingizi unaoambukizwa na mbung’o.
    Homa ya matumbo: taifodi
    Kwashakoo/ukosandisha: uele wa watoto unaosababishwa na uhaba wa chakula hususan protini.
    Surua/shurua/firangi/ukambi: ugonjwa wa watoto unaofanya ngozi kuwa na vipele. Hatua za kwanza huwa ni homa kali.
    Mafua/bombo: maradhi ya kuambukiza yanayosababisha mgonjwa kuumwa na koo na kichwa. Mgonjwa hutokwa na kamasi na kuwa na homa.
    Kaputula: uele wa kuhara. Tumbo la kuendesha.
    Baridi yabisi: maumivu ya mifupa au viungo yanayosababishwa na baridi 
    shadidi.
    Ukoma: uele wa kuambukiza wa mabatomabato ambao unaharibu mishipa 
    ya fahamu na kukata viungo vya mwili.
    Matumbwitumbwi / machibwichibwi: ugonjwa wa kuvimba mashavu hadi chini ya taya hususan kwa watoto
    Kisunzi/kizunguzungu / masua / gumbizi: uele wa kuhisi kichwa kikizunguka.
    Kipwepwe: ugonjwa wa ngozi unaosababisha madoa mekundu unaodaiwa kuletwa na chawa.
    Ndui: ugonjwa unaosababisha pele nyingi zenye majimaji na usaha.
    Kororo: uele wa kuvimba kooni.
    Ngiri: ugonjwa wa kukazana kwa mishipa iliyo sehemu za chini ya kitovu.
    Zongo: ugonjwa wa kuvimba tumbo kwa watoto wadogo.
    Vimbizi: hali ya kutoweza kupata pumzi kutokana na chakula kutosagika tumboni.
    Mbalanga / barasi: uele unaobadilisha rangi ya ngozi na kuwa na mabaka au matone.
    Rovu: ugonjwa wa kuvimba tezi kwenye shingo.
    Tetekuwanga / galagala / tetemaji: ugonjwa wa pele na homa kali wa kuambukizwa 

    13.5. Kusikiliza na kuzungumza

    Kazi ya 8:
    Igiza mazungumzo hapo juu kati ya Daktari na wagonjwa.
    Kazi ya 9:
    “Usafi ni ufunguo wa afya njema.” Jadili kauli hii.
    13.6. Kuandika
    Kazi ya 10:
    Tunga sentensi nne kwa kutumia vitenzi kama vile kuondoa, safisha, 
    kunawa, kuambukiza.

    SOMO LA 14: ADABU HOSPITALINI 
    Kazi ya 1:
    Eleza adabu inayotakiwa hospitalini na utoe sababu za adabu hiyo.
    14.1. Kusoma na ufahamu: Utaratibu hospitalini
    Yafuatayo ni mazungumzo mbele ya darasa ya wanafunzi walioitembelea 
    hospitali ya Girubuzima
    Mwalimu: Hamjambo vijana!
    Wanafunzi: Hatujambo mwalimu!
    Mwalimu: Kuna kundi la wanafunzi waliopewa kazi ya nyumbani kwenda 
    kuitembelea hospitali moja. 
    Nawaomba wafike mbele ya darasa na kutusimulia juu ya ziara 
    yao.
    Kiongozi wa kundi: Asante sana mwalimu kwa fursa hii. Kazi 
    tuliyoshughulikia ilikuwa inahusu mwenendo 
    hospitalini.
    Tuliitembelea hospitali moja inayoitwa Girubuzima. 
    Ningetaka niwashirikishe wenzangu katika 
    masimulizi haya.
    Mwanafunzi wa kwanza: Tulipoingia katika maeneo ya hospitali, tuliwakuta 
    watu wamekaa kimya mbele ya ofisi tofauti 
    kwa ajili ya kutaka kuhudumiwa.
    Mwanafunzi wa pili: Kwenye ukuta wa hospitali palikuwa pameandikwa 
    maonyo au maadili mbalimbali kuhusu utaratibu 
    unaofaa hospitalini kama ifuatavyo: 
    Mwanafunzi wa tatu: Hapa ni eneo la Hospitali. Inakatazwa kutenda 
    yafuatayo:Kuvuta sigara.
    Mwanafunzi wa nne: Kuchafua majengo ya hospitali na mazingira yake.
    Mwanafunzi wa tano: Kujisaidia pasipofaa.
    Mwanafunzi wa sita: Kutema mate hadharani.
    Mwanafunzi wa saba: Kupiga kelele.
    Mwanafunzi wa nane: Kuharibu vifaa vya hospitalini kama vile kuvunja vioo, viti, mlango, n.k.
    Mwanafunzi wa tisa: Kutumia pombe pamoja na dawa za kulevya.
    Mwanafunzi wa kumi: Kuonyesha tabia ya ukatili, ugomvi, chuki pamoja 
    na ubaguzi.
    Kiongozi wa kundi: Hii ndiyo miiko ya kupiga marufuku ndani ya hospitali tuliyoorodheshewa.
    Mwalimu: Asante sana kwa kazi hii! Darasa, pigieni makofi kundi hili.Maswali ya Ufahamu
    Kazi ya 2:
    Jibu maswali yafuatayo
    1. Habari hii imetokea wapi?
    2. Ni mbinu gani ya ufundishaji na ujifunzaji inayozungumziwa?
    3. Kwa nini maonyo yale yalitolewa hospitalini?
    4. Ni wahusika wangapi wanaojitokeza?

    5. Unadhani maonyo yale yalitolewa na nani?

    14.2. Matumizi ya msamiati
    Kazi ya 3:

    Oanisha msamiati kutoka sehemu A na maana yake katika sehemu B

    dd

    cc

    14.3. Sarufi: Matumizi ya kauli za vitenzi
    Kazi ya 4:
    Soma sentensi zifuatazo na kueleza maana ya kitenzi baada ya 
    kuongezewa viambishi

    1. Mama na shangazi wamepikiana chakula kitamu sana.
    2. Kagina na Amina waliimbiana nyimbo za kuvutia.
    3. Mimi na binamu yangu tulitembeleana mwishoni mwa mwaka uliopita.
    Maelezo muhimu
    Viambishi vilivyopigiwa mstari vinaonyesha kauli ya kutendeana yaani 
    unafanya kitendo kwa niaba ya mtu, naye anafanya kitendo hicho kwa niaba yako.
    14.4. Matumizi ya lugha: Muhtasari kuhusu kauli za vitenzi
    Kazi ya 5:
    Unganisha kauli za vitenzi vifuatavyo: fanya, lima, piga, cheza, lipa, 
    penda, omba, dunga katika jedwali moja na kutoa mifano husika kwa 
    kila kauli.

    1. Kauli ya Kutenda: Kitendo katika hali yake ya kawaida (bila 
    kunyambuliwa)
    2. Kauli ya Kutendea: Kufanya kitendo kwa niaba(au kwa ajili) ya 
    mtu mwingine
    3. Kauli ya Kutendana: Unamfanya mtu kitendo, naye anakufanya 
    vivyo hivyo
    4. Kauli ya Kutendeana: Unafanya kitendo kwa niaba ya mtu, naye 
    anafanya kitendo hicho kwa niaba yako.
    5. Kauli ya Kutendwa: Kuathirika moja kwa moja na kitendo
    6. Kauli ya Kutendewa : Kitendo kufanywa kwa niaba yako au kwa 
    ajili yako.
    7. Kauli ya Kutendeka: Kitendo kukamilika au kuwa katika hali timilifu
    8. Kauli ya Kutendesha : Kumfanya mtu atende jambo fulani
    9. Kauli ya Kutendeshana: Mtu anakufanya utende jambo fulani, 
    nawe unamfanya atende jambo lilo hilo

                  vv
    f

    14.5. Kusikiliza na kuzungumza
    Kazi ya 6:
    Simulia mbele ya darasa muhtasari wa mazungumzo hapo juu baina 
    ya mwalimu na wanafunzi
    Kazi ya 7:
    Kwa ushirikiano na wenzako, igiza mazungumzo hayo.
    14.6. Kuandika
    Kazi ya 8:

    Buni mazungumzo mafupimafupi baina ya mwanafunzi na mzazi wake 
    kuhusu umuhimu wa usafi na uandike maneno yasiyopungua 100.Tathmini ya mada
    1. Taja vifaa angalau vinne vya hospitalini na kueleza umuhimu wake
    2. Baadhi ya sehemu muhimu za hospitali, chagua tatu na kueleza umuhimu wake.
    3. Kamilisha sentensi zifuatazo:
    i. Kazi ya muuguzi ni..................................................................
    ii. Karani hospitalini hushughulikia...............................................
    iii. Tabibu ni mfanyakazi wa hospitalini anaye..................................
    iv. Mfanyakazi wa hospitalini anayeshughulikia waliovunjika viungo vya mwili huitwa................ 
    v. Anayetoa huduma kwa wajawazito wakati wa kujifungua huitwa..............................................
    4. Jadili hasara zinazoweza kujitokeza kwa sababu ya ukosefu wa usafi.
    5. Zungumzia kasoro angalau tano ambazo zinachukuliwa kama mwiko hospitalini.
    6. Weka vitenzi vinavyopatikana katika sentensi zifuatazo katika hali ya kutendwa.
    a. Tumesafisha vyumba, vyoo pamoja na jikoni kwa ajili ya kujilinda uchafu.
    b. Jana wageni walikula chakula kwa wingi.
    c. Si vizuri kupiga kelele hospitalini.
    d. Tunakunywa maji baada ya kuchemka.
    e. Sisi huvaa tai shingoni.



    MADA YA 2 MSAMIATI KUHUSU MAZINGIRA YA NYUMBANIMADA YA 4 MSAMIATI KUHUSU MAENEO YA UTAWALA