• MADA YA 7 TANZU ZA FASIHI ANDISHI

    Malengo ya Ujifunzaji
    -- Kueleza kwa ufasaha maana ya fasihi andishi,
    -- Kubainisha na kueleza tanzu za fasihi andishi,
    -- Kutetea dhima au umuhimu wa fasihi andishi katika jamii,
    -- Kutofautisha fasihi simulizi na fasihi andishi,

    -- Kutunga sentensi sahihi za Kiswahili kwa kuzingatia muundo wa sentensi.

    14.1. Kusoma na Ufahamu: Mwangaza wa Maisha

    Belinda na Didier ni wanafunzi wa Chuo cha Ualimu Malezi Bora. Katika
    mawasiliano yao wametetea umuhimu wa fasihi andishi katika kuimarisha
    ushirikiano, umoja na maridhiano katika kijiji chao.
    Belinda: Didy, hapa nimekufumbia fumbo aina ya chemshabongo. Tunu ya
    kupendeza kwako utakapolifumbua wazi.

    Didier: Tunu gani hiyo? Niambie Beli! Udadisi umeniingia mwilini kote! Maana
    yake nimesumbuka sana!
    Belinda: Didy umenaswa! Wewe hupenda kulipwa kabla ya kazi! Fumbua
    kwanza zawadi baadaye.
    Didier: Samahani dada! Sasa nimetega sikio. Lakini tafadhali usiniangushe

    mtegoni wa kushindwa.

    Belinda: Punguza wasiwasi kakangu! Fumbo ni hili: Ni kitu gani cha maajabu
    kilichochangia kuleta umoja na maridhiano katika kijiji chetu cha
    Ushujaa miaka miwili iliyopita?

    Didier: Fumbo kali sana! Jambo ninalokumbuka ni kwamba kabla ya miaka miwili
    iliyopita, hali ya umoja na maridhiano katika kijiji chetu ilikuwa imezorota
    mno. Iliboreshwa baadaye na mchango wa maigizo ya tamthilia kutoka
    Shirika la Burudani katika Jamii. Wachezaji waliigusia migogoro kadhaa
    inayoiangamiza jamii yetu na kuitolea suluhisho ambalo matokeo yake
    yalitufikisha kwenye ushirikiano, umoja na maridhiano.

    Belinda: Hongera Didy kwa fumbuo hili! Fumbo la pili sasa: Maigizo hayo ya
    tamthilia ni aina ya fasihi andishi. Kwa maoni yako, fasihi andishi ina
    lengo gani katika jamii kwa ujumla?

    Didier: Sitaki Beli, usininyang’anye! Kwanza kumbuka kuwa ahadi ni deni.
    Zawadi yangu vipi?

    Belinda: Hahaaaa! Bado fumbo halijafumbuliwa kikamilifu. Usikate tamaa,
    tunaelekea mwishoni mwake.

    Didier: Haidhuru! Fursa ninayo. Kwa maoni yangu, dhima ya fasihi yoyote ni
    kuielimisha na kuionya jamii kwa ajili ya kurekebisha mienendo ambayo
    si mizuri ndani ya wanajamii.

    Belinda: Vizuri sana Didy! Je, ni hayo tu? Hukumbuki jinsi raia walivyofurahia
    mdundo wa ngoma pamoja na sauti nyororo za wachezaji wa tamthilia
    hiyo?

    Didier: Kweli sana! Tamthilia ile ilikuwa na lengo jingine la kukuza lugha pamoja
    na kuiburudisha jamii.
    Belinda: Asante sana Didy kwa nia yako ya kuchunguza maendeleo ya jamii
    yetu.

    Didier: Inayofuata ni fursa ya kupewa zawadi yangu.
    Belinda: Umeishapewa! Kuelewa umuhimu wa fasihi andishi katika maendeleo
    ya jamii ni zawadi yenye thamani kubwa kuliko pesa au kitu kingine.

    Didier: Jambo hilo naliunga mkono. Matokeo ya fasihi ile yalikuwa mwangaza
    wa maisha katika jamii yetu.

    Maswali ya ufahamu






    Maelezo muhimu
    Tungo ni neno au nomino inayotokana na kitenzi “tunga.” Kutunga ni kuweka/
    kushikamanisha vitu pamoja kwa kutumia kitu kama kamba au uzi kwa kupitishia
    ndani yake. Tunaposhikamanisha vitu pamoja tunapata kitu kinachoitwa utungo
    (katika umoja) au tungo (katika wingi). Kwa maana nyingine, utungo au sentensi
    ni kundi la neno moja au maneno zaidi yenye kiima na kiarifa na inayofuata kanuni
    za sarufi. Tungo ni neno au kikundi cha maneno ambacho hudokeza taarifa fulani
    ambayo huweza kuwa kamili au isiyo kamili.

    Muundo wa tungo
    Muundo wa sentensi kimapokeo/kikazi/kidhima huwa na vipengele vifuatavyo:
    • Kiima: Ni sehemu katika sentensi ambayo hujaza sehemu ya mtenda au
    mtendwa wa jambo linaloelezwa. Katika tungo kiima hutokea kushoto
    mwa kitenzi.

    • Kiarifa: Ni sehemu katika sentensi inayojazwa na maneno yanayoarifu
    tendo lililofanywa, linapofanywa au litakapofanywa. Kiarifa ndiyo
    sehemu muhimu zaidi katika sentensi ambayo wakati mwingine huweza
    kusimama pekee, kwani wakati mwingine huchukua viwakilishi vya kiima.
    Sentensi huwa na vifungu mbalimbali. Baadhi ya vifungu hivi ni vishazi na virai.

    i) Virai
    Kirai ni fungu la maneno lisilokuwa na kitenzi.
    Kuna aina nne za virai:
    • Kirai Nomino: ni fungu la maneno katika sentensi lenye nomino
    (Kikundi Nomino/Kiima)

    Mfano:
    Wanafunzi wanapaswa kushirikiana darasani na nje ya darasa.
    Walimu na wazazi wanaombwa kushughulikia pamoja maadili ya wanafunzi.
    Elimu kuhusu usawa wa jinsia inatakiwa kwa watu wa marika yote.
    • Kirai Kiwakilishi: ni fungu la maneno linalowakilisha nomino katika

    sentensi

    Mfano:
    Wenyewe watajenga nchi yao.
    Atakayetumia dawa za kulevya atahatarisha maisha yake.
    Wao walipanda miti mingi kwa ajili ya kuhifadhi mazingira.

    • Kirai Kivumishi: ni fungu la maneno katika sentensi linalotupa habari
    zaidi kuhusu nomino.

    Mfano:
    Matunda tuliyokuwa tunatarajia yatapatikana.
    Mahali penye kutupwa taka ovyo panaambukiza magonjwa.
    Mtu mkatili kuliko shetani hataleta mchango wowote katika jamii.
    • Kirai Kielezi: ni fungu la maneno linaloelezea zaidi kuhusu kitenzi au
    kivumishi.

    Mfano:
    Raia wanakatazwa kuponda mali yao ovyo ovyo.
    Wanawake na wanaume wakishirikiana wataishi kwa amani na furaha milele na
    milele

    b) Vishazi
    Kishazi ni sehemu ya sentensi yenye kitenzi. Kuna aina mbili za vishazi:
    1. Kishazi huru: huwa na maana kamili na kinaweza kujisimamia chenyewe
    kama sentensi.

    Mfano:
    Wanafunzi wote wa mwaka wa nne wamefanikiwa.
    Anayeingia katika mambo ya uzinifu anaweza kuambukizwa ugonjwa wa ukimwi.
    Tutafungua akaunti benkini kwa ajili ya kukuza kazi za kibiashara.

    2. Kishazi Tegemezi: huhitaji kuunganishwa na kishazi kingine ili kuleta
    maana iliyokusudiwa. Aghalabu huwa na kirejeshi k.v amba-, -enye, n.k

    Mfano:
    Kila mtu atapewa zawadi baada ya kuonyesha mwenendo mwema.

    Yeyote aliyehusika na vitendo vya mauaji ya kimbari dhidi ya Watutsi atahukumiwa.

    Maelezo muhimu
    Fasihi andishi ni sanaa itumiayo maandishi kufikisha ujumbe kwa hadhira
    iliyokusudiwa.
    Kwa maana nyingine, fasihi andishi ni aina ya sanaa ambayo hutumia maneno
    yaliyoandikwa kupitisha ujumbe.

    Ni sanaa inayopitishwa kwa njia ya maandishi.

    Maelezo ya kuzingatia
    • Kuburudisha jamii. Takribani vipera vyote vya fasihi huwa na kusudi la
    kufurahisha, kutumbuiza na kusisimua hadhira.
    • Kuelimisha. Fasihi hukusudia kuelimisha hadhira kuhusu jamii, mazingira,
    n.k
    • Kudumisha maadili katika jamii kwa kuelekeza, kuonya na kunasihi
    hadhira jinsi ya kufuata mwelekeo unaokubalika katika jamii.
    • Kuunganisha jamii. Fasihi huleta pamoja watu katika jamii. Kwa mfano,
    katika nyimbo, miviga, vichekesho.
    • Kukuza lugha. Aghalabu tungo zote za fasihi hutumia lugha. Isitoshe,
    fasihi hutumia mbinu nyingi za lugha. Wasimulizi na wandishi wa fasihi
    huhitaji kuwa na ukwasi wa lugha.
    • Kuhifadhi mila, tamaduni na itikadi za jamii. Aghalabu kazi za fasihi
    (hasahasa Fasihi Simulizi) huambatanishwa na desturi mbalimbali za
    jamii husika.
    • Kukuza uwezo wa kufikiri. Vipera vingi vya fasihi huwachochea hadhira

    kufikiri sana ili kupata suluhisho. k.m vitendawili, ngano za mtanziko, n.k

    15.1. Kusoma na Ufahamu: Akili ni Mali
    Dhana ya utajiri inaendelea kuwa mada tata kati ya matajiri na watu duni. Kuna
    wanaoshuku kuwa utajiri ni mali iliyorithiwa na vizazi vikongwe kwa vizazi vichanga.
    Watu wanaotetea msimamo huu hukubali kwamba unapozaliwa na kulelewa
    katika familia fukara hivyo utafariki katika hali ya wasiwasi na ya masumbuko.
    Wengine huamini kuwa utajiri hushughulikiwa na hufikiwa kwa njia tofauti. Hivyo
    utawasikia watu wakitoa madai kama ifuatavyo:

    “Utajiri wa jamaa yule ulipatikana kwa matumizi ya hila za hali ya juu.”
    “ Bwana yule hakuwa na nguo ya kujikinga dhidi ya upepo wala chumba cha
    kulala. Lakini leo ameishajenga ghorofa tele. Ametajirika hivi majuzi baada ya
    kutoka kuzimuni.”

    “ Unamuona bibi yule katika gari lenye thamani kubwa sana! Habari zilizosambaa
    zinasema kwamba alipandishwa vyeo miongoni mwa matajiri wanaojulikana
    kwa ngazi ya kimataifa baada ya kuwadhulumu urithi watoto yatima aliokuwa
    anawalea”.

    Licha ya madai haya yote, mimi nina ushahidi wangu nilioshuhudia mimi
    mwenyewe kwa macho yangu kuhusu familia moja ambayo ilipata utajiri
    kwa kutegemea akili za kielimu. Familia ya bwana Bahati na bibie Fifi ilikuwa
    haijulikani kamwe katika kijiji chao. Bahati alikuwa na kibarua katika kampuni
    moja ya utangazaji habari wakati ambapo mkewe Fifi alikuwa anaajiriwa katika
    duka la mavazi mjini. Ingawa wafanyakazi hawa walikuwa wanapata mshahara
    kila mwezi, mahitaji ya kimaisha yalikuwa yanaendelea kuwasumbua. Siku moja,
    bwana Bahati alijadiliana na mkewe juu ya njia mwafaka wangelipitia ili waridhike
    na masharti ya kimaisha. Makubaliano yao yaliichagua shughuli ya kutumia akili
    kama watu waliokuwa wasomi. Shughuli ya kuendeleza kazi za fasihi andishi
    ilipewa alama asilimia tisini na tano. Baada ya mpango kuiva, Bahati na mkewe
    waliunda kampuni yenye jina la Maisha ni Bora Ltd. Waliwaajiri wataalamu wa
    kutunga hadithi fupi, riwaya, tamthila pamoja na mashairi. Miezi minane baadaye,
    matunda ya kampuni yalikuwa yameanza kujitokeza. Matini za riwaya, hadithi fupi
    pamoja na mashairi yalichapwa na kununuliwa kwa wingi wakati ambapo kundi
    la wachezaji wa tamthilia lilikuwa likizunguka sehemu mbalimbali za nchi. Raia

    walifurahia sana maadili kutoka tanzu hizo kwa sababu zilichangia sana kuijenga

    Baadhi ya mada zilizokuwa zimegusiwa mno katika kazi hizo za fasihi andishi
    ni kama vile umoja wa jamii, mapenzi, uhifadhi wa utamaduni, amani na utulivu
    katika jamii pamoja na vita dhidi ya umaskini. Mafanikio kutoka kazi hizi zote
    yaliiwezesha familia hii kununua magari ya kazi na ya ziara, kujenga nyumba ya
    kisasa, kuishi kwa raha na kuwalipia karo watoto wao katika shule siyo tu za humu
    Rwanda bali pia Marekani na Ulaya. Leo, familia ya bwana Bahati na mkewe Fifi

    imekuwa kielelezo kwa wasomi wote kuwa akili ni nywele, kila mtu ana zake.

    15.3. Sarufi: Aina za tungo katika Kiswahili
    Maelezo ya kuzingatia

    Kimuundo na kimaana, tungo hujigawa katika aina tatu kuu kama ifuatavyo:
    1. Tungo Sahili : Ni sentensi zenye kishazi kimoja na huwakilisha wazo
    moja tu.

    Mfano:
    Tumeelewa faida za fasihi andishi.
    Wanaume na wanawake huwa na haki sawa.

    2. Tungo ambatano: Ni sentensi zenye zaidi ya kishazi huru kimoja na
    huwakilisha mawazo mawili au zaidi. Aghalabu sentensi hizi hutumia
    viunganishi (U) au alama za uakifishaji kama vile kituo (.) na nukta-nusu (;)
    ili kubainisha wazo moja toka jingine.

    Mifano:
    Tulipanda miti kwa ajili ya kupigana dhidi ya mporomoko wa ardhi. Ardhi yetu
    iliporomoka.
    • Ingawa tulipanda miti kwa ajili ya kupigana dhidi ya mporomoko wa
    ardhi, ardhi yetu iliporomoka.

    Bwana Bahati na mkewe Fifi waliunda kampuni ya uandishi wa riwaya. Bwana
    Bahati na mkewe Fifi waliwaajiri wafanyakazi wengi.
    • Bwana Bahati na mkewe Fifi waliunda kampuni ya uandishi wa riwaya
    na kuwaajiri wafanyakazi wengi.

    Familia ya Bwana Bahati na mkewe Fifi ilijitafutia ajira. Familia ya Bwana Bahati
    na mkewe Fifi ilitajirika.

    • Familia ya Bwana Bahati na mkewe Fifi ilijitafutia ajira ikatajirika.
    3. Tungo Changamano: Ni sentensi zinazoundwa kwa kuunganisha
    kishazi huru pamoja na kishazi tegemezi au sentensi mbili kwa kutumia
    o-rejeshi ili kuleta zaidi ya wazo moja.

    Mifano:
    - Tumepata maelezo ya kutosha kuhusu elimu ya usanifishaji. Tulikuwa tunaomba
    maelezo hayo toka mwezi uliopita.
    • Tumepata maelezo ya kutosha kuhusu elimu ya usanifishaji ambayo
    tulikuwa tunayaomba toka mwezi uliopita.
    - Shirika jipya lilitunga tamthilia hii. Ni tamthilia inayovutia sana.

    • Shirika jipya ndilo lililotunga tamthilia hii inayovutia sana.

    Zingatia yafuatayo
    Kuna tanzu nne kuu za fasihi andishi ambazo ni zifuatazo:

    1. Hadithi fupi
    2. Riwaya
    3. Tamthilia
    4. Mashairi yaliyoandikwa
    A. HADITHI FUPI
    Hadithi Fupi ni aina ya kazi andishi ambayo huwa fupi; na huangazia wazo moja

    kwa kurejelea kisa kimoja.

    Hadithi fupi huwa na wahusika wachache na huchukua muda mfupi. Masuala

    mbalimbali huzingatiwa katika hadithi fupi kama vile masuala ya kijamii, kisiasa,

    kidini, kielimu, kiutamaduni, kiuchumi, n.k.

    Mfano: Hadithi fupi za Alley Yusufu Mugenzi

    Mifano mingine ya hadithi fupi za Kiswahili:

    -- Kachukua Hatua Nyingine

    -- Mayai Waziri wa Maradhi

    -- Siku ya Mganga

    -- Ngome ya Nafsi

    B. RIWAYA

    Riwaya ni kazi ya fasihi andishi ambayo huwa ndefu na aghalabu riwaya moja
    hujaza kitabu kizima. Riwaya huwa na wahusika wengi na huangazia mawazo
    kadhaa. Aidha, riwaya hufanyika katika mazingira mbalimbali na aghalabu
    huchukua muda mrefu ikilinganishwa na hadithi fupi. Kazi hii huhusisha
    binadamu,wanyama ama vitu vingine vinavyopewa uhai kama vile mizimu.

    Kunazo aina nyingi za Riwaya katika Fasihi Andishi. Ifuatayo ni baadhi ya mifano:
    Riwaya sahili: Ni aina ya riwaya ambayo visa vyake husimuliwa moja kwa moja
    na huwa rahisi kueleweka.

    Riwaya changamano: Hii ni riwaya ambayo huhitaji kusomwa kwa makini
    ili kueleweka. Aghalabu huwa na maudhui mengi na wahusika wengi ambao
    wanachangia katika tatizo kuu katika riwaya hiyo. Hujengwa kwa taharuki ili
    kuwavutia hadhira kutazamia jinsi tatizo kuu litakavyotatuliwa. Hutumia mbinu za
    taharuki na visengere nyuma/mbele.

    Riwaya ya kibarua: Ni riwaya ambayo hutumia muundo wa barua kuwasilisha

    ujumbe wake.

    Riwaya kiambo: Ni riwaya ambayo huhusisha masuala ya kawaida katika jamii.

    Mfano wa riwaya:
    Adili na Nduguze
    Utengano
    Siku Njema
    Mwisho wa Kosa

    Kiu

    C. TAMTHILIA
    Tamthilia ni sanaa ambayo huwasilisha mchezo wa kuigiza kwa njia ya
    maandishi. Majina ya wahusika huandikwa katika upande wa kushoto,
    kisha koloni, halafu hufuatiwa na maneno halisi yaliyotamkwa na mhusika
    huyo. Kwa maana nyingine,tamthilia ni mchezo wa kuigiza ulioandikwa
    ili uigizwe jukwaani kwa kuwasilisha ujumbe kwa jamii.

    Aina za jukwaa
    Kuna aina mbili za jukwaa:
    -- Jukwaa la akilini kama hali ya kujiundia akilini k.v. mchezo unaoigizwa
    redioni.
    -- Jukwaa la hadharani, yaani mahali ambapo maonyesho ya tamthilia
    yanaigiziwa mbele ya watazamaji au wasikilizaji.

    Aina za tamthilia
    Tamthilia au mchezo wa kuigiza huwa na aina mbalimbali kulingana na dhamira
    kuu inayoendelezwa. Utaipata tamthilia ya mapenzi, ya kihistoria, ya kisiasa, ya
    kidini, ya kiuchumi, n.k. Tamthilia hizi zote huangukia baadhi ya makundi makuu
    yafuatayo:

    Tanzia
    Ni aina ya tamthilia iliyojaa, huzuni ndani yake, mikasa, matokeo ya vifo na mateso
    makali. Mwisho wa tamthilia za aina hii huwa ni wa masikitiko, maanguko na
    hasara kubwa kwa mhusika mkuu au jamii inayoibushwa. Wengine huita aina hii

    tamthilia simanzi au trejedia.

    Ramsa
    Tamthilia zenye kuchekesha kutokana na utani, mzaha, kejeli, maneno
    yaonyeshayo ujinga, n.k. Iwapo tamthilia hizi huwa na dhana ya uchekeshaji,
    lengo lake ni kukosoa jamii, watawala na tabia mbaya na watu binafsi. Aina hii
    huitwa tena Tamthilia cheshi au komedia.

    Tanzia – ramsa
    Tanzia – ramsa au simanzi – cheshi ni mchezo wenye sifa za ramsa, lakini ndani
    ya uchekeshaji wake na tanzia kama vile kifo cha mhusika mkuu au kuanguka
    kwa jamii. Pengine huitwa Trejikomedia.
    Mfano wa tamthilia
    Hawala ya Fedha
    Kifo Kisimani
    Shamba la Wanyama
    Mstahiki Meya

    D. MASHAIRI YALIYOANDIKWA
    Ushairi ni utungo wa kisanaa unaotumia maneno ya mkato na lugha yenye
    kuvutia (lugha teule na mpangilio fulani wa maneno badala ya kutumia lugha
    natharia) na ambayo yamepangwa kwa urari wa mizani na vina maalum. Ushairi
    unaweza kuwa kipera cha fasihi simulizi (nyimbo) na pia katika fasihi andishi kwa
    sababu mashairi yanaweza kuwasilishwa kwa njia ya kukariri na pia kwa njia ya
    maandishi. Mashairi yanayoghaniwa badala ya kusomwa huitwa maghani.
    Kuna aina kuu tatu za ushairi: Mashairi, Ngonjera, Tendi au Tenzi.

    Mashairi:
    Shairi ni mtungo wa kisanaa wenye mpangilio maalum na kutumia lugha ya
    mkato na mnato kwa kuelezea hisi na mawazo ya jamii husika na kuwasilisha
    ujumbe fulani. Mashairi hugawika katika makundi mawili: mashairi ya kimapokeo
    au mashairi arudhi na mashairi huru. Mashairi arudhi hutungwa kwa kufuata au
    kuzingatia sheria na kanuni au kaida za utunzi kama vile kuzingatia vina, idadi
    fulani ya mizani, mishororo na vipande vya mishororo. Kulingana na idadi ya
    mishororo katika kila ubeti, mashairi huweza kugawika tena katika aina mbalimbali

    kama ifuatavyo:

    1. Tamonitha ni shairi lenye mshororo mmoja kwa kila ubeti.
    2. Tathnia ni shairi lenye mishororo miwili kwa kila ubeti.
    3. Tathlitha ni shairi lenye mishororo mitatu kwa kila ubeti.
    4. Tarbia ni shairi lenye mishoro minne kwa kila ubeti.
    5. Takhmisa ni shairi lenye mishororo mitano kwa kila ubeti.
    6. Tasdisa shairi lenye mishororo sita.

    Ngonjera:
    Ngonjera ni shairi lenye malumbano na majibizano kati ya watu wawili au zaidi.

    Tenzi
    Tenzi ni aina ya shairi ambayo ni mtungo mrefu wa kishairi unaoelezea habari au
    masuala mbalimbali kishairi. Utenzi huwa hauna vina vya kati katika mistari yake
    bali kila ubeti una vina vya namna moja katika mistari yake isipokuwa mstari wa
    mwisho wa ubeti.

    Kuna mambo mengine muhimu kuhusu shairi. Mishororo ya shairi huwa na
    majina maalum.

    Mwanzo huwa ni mshororo wa kwanza wa ubeti.
    Mloto huwa ni mshororo wa pili wa ubeti.
    Mlea huwa ni mshororo wa tatu wa ubeti
    Kituo huwa ni mshororo wa mwisho wa ubeti.

    Kuna aina mbili za vituo ambazo ni kituo kimalizio na kituo kibwagizo. Kituo
    kimalizio ni kituo ambacho hakirudiwi mwishoni mwa kila ubeti katika shairi. Kituo
    kibwagizo ni kituo kinachorudiwarudiwa mwishoni mwa kila ubeti.
    Vipande au sehemu za mishororo ni zifuatazo:
    Ukwapi: Ni kipande cha kwanza cha mshororo.
    Utao: Ni kipande cha pili cha mshororo.

    Mwandamizi: Ni kipande cha tatu cha mshororo.

    Dhima ya ushairi
    Kama mtungaji wa kazi nyingine za fasihi, mshairi huwa na madhumuni yafuatayo

    kwa jamii:

    -- Kuburudisha

    -- Kuhamasisha jamii

    -- Kukuza sanaa na ukwasi wa lugha

    -- Kuliwaza

    -- Kuelimisha

    -- Kuonya, kutahadharisha, kunasihi na kuelekeza

    -- Kupitisha ujumbe fulani

    -- Kusifia mtu au kitu

    -- Kukejeli au kukemea mambo yanayoenda kinyume na maadili ya jamii.

    MADA YA 6 UHAKIKI WA KAZI ZA FASIHI SIMULIZIMADA YA 8 UHAKIKI WA KAZI ZA FASIHI ANDISHI