• MADA YA HOTUBA 4 HOTUBA

    • Malengo ya ujifunzaji

    -- Kubainisha sehemu kuu za hotuba,

    -- Kueleza mwongozo wa kutunga hotuba nzuri,

    -- Kuonyesha tofauti iliyopo kati ya hotuba na aina mbalimbali za insha,

    -- Kueleza tofauti kati ya usemi wa asili na usemi wa taarifa.

    SOMO LA 8: MAANA YA HOTUBA

    8.1. Kusoma na Ufahamu: Hotuba ya Afisa wa Umoja na

    Maridhiano wilayani kwa Wananchi
    Soma hotuba ifuatayo kisha ujibu maswali uliyopewa hapo chini:
    Ndugu zangu wananchi, ndugu zangu wazalendo na ndugu zangu wazawa.
    Hamjambo!
    Ninasimama mbele zenu leo hii ili tuzungumzie kuhusu umoja wa Wanyarwanda.

    Hebu tujitazame leo tunaishi vipi? Je, tunaishi kwa umoja kama Wanyarwanda?
    Kabla sijasonga mbele, ningependa tukumbushane historia ya nchi yetu kuhusu
    umoja. Hapo zamani za kale, katika enzi za ufalme, Wanyarwanda walikuwa
    na umoja thabiti. Wote walikuwa wakimheshimu mfalme kwa pamoja bila ya
    ubaguzi wowote. Mizozo midogo midogo ilipokuwa ikitokota ilikuwa ikitatuliwa
    kidugu katika familia au katika vikao vya waungwana. Matatizo hayo yalikuwa
    yakihusiana na kama vile mifugo au mashamba. Matatizo magumu yalikuwa
    yakitatuliwa na viongozi na hata mfalme mwenyewe.

    Wakati huu, umoja wetu ulikuwa ukirutubishwa na sherehe au hafla mbalimbali.
    Mtu alipokuwa akitaka kujenga nyumba, majirani walikuwa wakimpa msaada
    “umuganda” kwa Kinyarwanda. Aliyekuwa na harusi, majirani walikuwa wakimpa
    msaada kama vile kazi za nyumbani zihusuzo matayarisho ya shughuli za harusi,
    pombe, n.k. Kwa kuonyesha urafiki wa hali ya juu, Wanyarwanda walikuwa
    wakichanganya damu na kuzawadiana mifugo hasa ng’ombe. Wakati wa vita,
    Wanyarwanda walikuwa wakipigania usalama wa nchi yao kwa pamoja bila
    ubaguzi wowote. Kwa upande wa malezi, mtoto alikuwa akikanywa na mtu
    mzima yeyote yule katika jamii.

    Ndugu zangu wananchi, wakati wa enzi za ukoloni, umoja wa Wanyarwanda
    ulivunjika. Kwanza, wakoloni hawa walidunisha ufalme na watu wengi wakaanza
    kugoma. Walivunja nguzo zote zilizokuwa zikishikilia umoja wa Wanyarwanda.
    Kitu kibaya mno walichotufanyia na ambacho hatuwezi kukisahau, walituletea
    makabila. Makabila haya yalipofika yalitenganisha watu: ndugu, mzazi na mtoto,

    mke na mume, walianza kuangaliana kwa kijicho na husuda.

    Baada ya uhuru, mambo yaligeuka balaa zaidi. Wanyarwanda wengi walianza
    kuuawa na Wanyarwanda wenzao. Hawa wa nyuma waligawana mashamba
    yao na mifugo yao, walichoma nyumba zao na kuwakimbiza hadi nchi jirani.
    Uvunjikaji huu wa umoja wetu ndio uliotufikisha kwenye mauwaji ya kimbari dhidi
    ya Watutsi yaliyotokea nchini mwetu mnano mwaka wa 1994.

    Afisa: Umoja oyee!
    Wasikilizaji: Oyee! Oyee!
    Afisa: Amani oyee!
    Wasikilizaji: Oyee! Oyee!
    Afisa: Utengano zuu!
    Wasikilizaji: Zuu!

    Ndugu wananchi wenzangu, wahenga walisema yaliyopita si ndwele, tugange
    yajayo. Yaliyopita yalipita lakini yalituachia kovu kubwa. Yawe somo kwetu. Siku
    hizi tunapaswa kusimama kidete na kuendelea na safari yetu ya kuendeleza
    nchi. Safari hii si ya mtu mmoja pekee bali ni safari ya sisi sote Wanyarwanda.

    Kwa hiyo, ninawaomba tuungane mikono. Serikali yetu ilipewa jina zuri “Serikali
    ya Umoja wa Wanyarwanda.” Umoja huu unapaswa kuwa uti wa mgongo wa
    maisha yetu kama Wanyarwanda. Tuishi kwa umoja, tusaidiane vilivyo kwa lolote
    lile. Haya yatakapotendeka, nchi yetu inakuwa paradiso ya Afrika na majirani zetu
    watatumezea mate.

    Ninawashukuru kwa kunitegea masikio na nina imani kuwa kuanzia leo
    mnakwenda kuimarisha umoja wetu zaidi ya sasa.

    Asanteni!

    Maelezo muhimu: Maana ya usemi wa asili na usemi wa taarifa

    • Usemi wa asili

    Ni yale maneno yanayotamkwa na mtu katika hali ya kwanza .

    • Usemi wa taarifa

    Iwapo mtu anataka kuwaambia wengine maneno ambayo yalizungumzwa

    na mtu mwingine bila kupotosha, kupunguza au kuongeza maana ya jambo

    analotaka kulitolea maelezo, basi maneno hayo anayoyasema ni ``usemi wa

    Taarifa.``

    Mambo muhimu katika usemi wa taarifa

    Wakati wa kuandika usemi wa taarifa kuna mambo muhimu ya kuzingatiwa ili

    usemi huo uwe wa taarifa sahihi.

    Maelezo muhimu: Maana ya usemi wa asili na usemi wa taarifa

    • Usemi wa asili

    Ni yale maneno yanayotamkwa na mtu katika hali ya kwanza .

    • Usemi wa taarifa

    Iwapo mtu anataka kuwaambia wengine maneno ambayo yalizungumzwa

    na mtu mwingine bila kupotosha, kupunguza au kuongeza maana ya jambo

    analotaka kulitolea maelezo, basi maneno hayo anayoyasema ni ``usemi wa

    Taarifa.``

    • Mambo muhimu katika usemi wa taarifa

    Wakati wa kuandika usemi wa taarifa kuna mambo muhimu ya kuzingatiwa ili

    usemi huo uwe wa taarifa sahihi.

    1. Nafsi ya kwanza hubadilika na kuwa nafsi ya tatu

    Mimi hugeuka kuwa yeye

    Sisi hugeuka kuwa wao

    Mfano:

    -- “Mimi ninasoma kwa bidi,” mtoto alisema.

    • Mtoto alisema kuwa yeye alisoma kwa bidi.

    -- “Sisi tulisoma kwa bidi,” watoto walisema.

    • Watoto walisema kuwa wao walisoma kwa bidi.

    2. Badala ya kutumia wakati uliopo, wakati uliopita –li- ndio hutumika.

    Mfano: Nina kazi nyingi ofisini.

    • Alisema kwamba alikuwa na kazi nyingi ofisini.

    3. Alama za kufunga na kufungua maneno hazitumiki kwenye usemi wa

    taarifa .

    4. Alama za kuuliza na kushangaa hazitumiki kwenye usemi wa taarifa

    5. Katika usemi wa taarifa mahali penye wakati ujao -ta- kwenye usemi

    wa asili hugeuka kuwa -nge-

    Mfano: “Nitaondoka kuelekea Kigali,” shangazi alisema.

    • Shangazi alisema kuwa angeondoka kuelekea Kigali.

    6. Baadhi ya maneno hubadilisha nyakati yanapotumika katika usemi wa

    taarifa .

    kama :

    Hapa huwa hapo

    leo huwa ---siku hiyo/ile

    wakati huu ------------wakati huo

    kwetu -------kwao

    kwangu ------kwake

    sasa -----wakati huo/ule

    Mfano:

    -- “Nitaondoka sasa,” mgeni alisema.

    • Mgeni alisema kuwa angeondoka wakati huo/ule.

    “Tutacheza leo uwanjani,” wanafunzi walisema.

    • Wanafunzi walisema kuwa wangecheza siku hiyo/ile uwanjani.

    7. Mojawapo ya maneno yafuatayo hutumika katika usemi wa taarifa

    Kuwa----kama ----kwamba

    Mfano: -” Utanikuta mjini jioni hii, “Juma alimweleza rafiki yake.

    • Juma alimweleza rafiki yake kuwa angemkuta mjini jioni ile.

    Hotuba

    i) Maana ya hotuba

    Hotuba ni maelezo maalumu yanayotolewa na mtu mmoja mbele ya kundi la

    watu. Hotuba inaweza kutolewa kwa madhumuni ya kutaka kuhimiza kazi, kufanya

    kampeni fulani, kutoa taarifa fulani kwa watu.

    ii) Aina za hotuba

    a) Mahubiri: Ni hotuba za mafundisho ya kidini, zinazotolewa makanisani,

    misikitini, n.k.

    b) Hotuba za kisiasa: Ni hotuba zihusuzo taarifa ya serikali kama vile

    kuwahimiza watu na kuwaalika kutenda jambo fulani, n.k.

    c) Mihadhara: Ni hotuba au mafundisho ya mwalimu shuleni anapofundisha

    kundi la wanafunzi na hasa wanafunzi wa vyuo vikuu.

    iii) Sifa za hotuba

    -- Ukweli wa habari na taarifa

    -- Kujua vizuri aina ya watu unaowatolea hotuba, umri wao, kazi zao, n.k.

    -- Ufasaha wa lugha ili iweze kupendeza na kueleweka vizuri

    -- Nidhamu au adabu njema ya mzungumzaji mwenyewe asimamapo mbele

    ya watu

    -- Mantiki nzuri au mfuatano mzuri wa mawazo

    -- Sauti ya kusikika vizuri

    -- Kuvaa vizuri.

    iv) Tofauti kati ya hotuba na insha

    A) HOTUBA

    • Hotuba hutoa maneno halisi ya mzungumzaji/hatibu/kiongozi

    anapozungumzia hadhira kuhusu jambo fulani.

    • Mwandishi wa hotuba hatakiwi kuweka alama za kunukuu anapoanza

    hotuba yake

    • Mara nyingi hotuba huwa katika nafsi ya pili

    • Hotuba inaweza kutolewa na kiongozi wa kisiasa, utawala, kidini, kikundi,

    shirika fulani, daktari, n.k

    • Hotuba huanza kwa kutambua hadhira (waliohudhuria mkutano)

    • Waliohudhuria mkutano hutajwa kwa vyeo vyao kuanza kwa yule wa

    cheo cha juu hadi wa chini k.m: Waziri wa Elimu, Mkuu wa Wilaya,

    mabibi na mabwana,……..

    • Hatibu akiwa anawazungumzia hadhira isiyomjua, lazima ajitambulishe

    • Katika hotuba, hatibu hutoa mapendekezo

    • Mwisho wa hotuba humalizika kwa shukurani.

    B) INSHA

    • Mwandishi wa insha anaweza kunukuu yaliyosemwa na wengine

    • Insha inaweza kuwa na mada ambayo mwandishi anatakiwa kutetea au

    kupinga

    • Katika insha mwandishi hataji vyeo vya hadhira

    • Katika insha nyingi, mwandishi hatoi mapendekezo

    • Mwisho wa insha hupangwa katika aya na haumaliziki kwa shukurani

    Maswali

    1. Eleza maana ya hotuba

    2. Hotuba hutolewa kwa lengo gani?

    3. Taja aina za hotuba

    4. Eleza sifa muhimu za hotuba

    9.1. Kusoma na Ufahamu: Kazi ni Kazi

    Soma hotuba ya Katibu mtendaji wa wilaya katika harakati za uzinduzi
    wa elimu ya kujitegemea kwa vijana « Kazi ni Kazi » katika Tarafa ya

    Amani wilaya ya Tujitegemee

    Katibu: Kazi oyee !

    Vijana: oyee ! Oyee ! Oyee !

    Katibu: Uzembe zii !

    Vijana: Zii !

    Mheshimiwa Katibu Mtendaji wa Tarafa ya Amani,

    Waheshimiwa wakurugenzi wa shule na vyuo

    Waheshimiwa vijana,

    Mabwana na mabibi mliokusanyika hapa,

    Hamjambo?

    Vijana ni nani ambaye hapendi kuishi? Sote tunapenda kuishi tena bila shaka
    kwa raha. Licha ya hivyo, ili tuishi maisha ya raha mstarehe tunahitaji kufanya kazi.
    Kazi ndio msingi wa uhai wa binadamu. Mtu asipofanya kazi hawezi kuyapata
    mahitaji yake ya kila siku.

    Kazi siyo adhabu kwani binadamu ameumbwa ili afanye kazi; ndiyo maana ana
    akili, mikono, miguu, na viungo, vingine vya mwili. Viungo vyote hivi lazima vifanye
    kazi ili maisha yawe mazuri. Mtu anahitaji kula, kuvaa na kuishi mahali pazuri. Lakini
    ili kuyapata mahitaji yote, ni lazima afanye kazi. Hivyo basi, tunalazimika kufanya
    kazi kwa kuwa kazi ni kitendo cha maendeleo. Maendeleo ya mtu huletwa na
    kazi. Binadamu hupiga hatua za kwenda mbele kimaendeleo akifanya kazi kwa
    bidii. Bila kufanya kazi, maendeleo ya nchi husimama ama hurudi nyuma.

    Kazi ni za aina nyingi. Kuna kazi zinazotolewa na serikali au makampuni fulani na
    kazi za kujitegemea. Kazi zote hizo ni kama vile kilimo, ufugaji, ujenzi, uchukuzi,
    ulindaji wa usalama, ufanyabiasha na kadhalika. Kazi hizi zote zipo ili kujenga
    nchi yetu. Hii ni kwa sababu nchi yetu itajengwa na mikono ya wananchi wake.
    Siku hizi kuna wale wanaochagua kazi na kupuuza nyingine ati si kazi za heshima.
    Msemo wa Kinyarwanda unasema « Hakuna kazi mbaya isipokuwa kuiba na
    kuroga. » na Waswahili husema « Kazi mbi si mchezo mwema.»

    Siku hizi kuna ongezeko la wasomi. Ongezeko hili halilingani na kazi zinazotolewa
    na serikali yetu au makampuni na mashirika ya kibinafsi. Ndiyo maana tunahimizwa
    sisi wenyewe kujitengenezea kazi za kibinafsi (kujiajiri). Sote hatuwezi kukaa
    ofisini. Tuna mikono na akili, tengeneza kazi na usitegemee wengine kwani
    « Mtegemea cha nduguye hufa maskini. »

    Kazi ni wajibu wa kila mtu. Kila mtu analazimika kufanya kazi ili atoe mchango
    wake katika maendeleo ya jamii. Mtu ni sehemu ya jamii. Kama mtu hafanyi kazi
    hulegeza maendeleo ya jamii na matokeo yake ni kwamba jamii hukumbwa na
    umaskini. Vijana, mnataka nchi yetu iendelee kuitwa maskini? Hapana! Nchi yetu
    inapaswa kusonga mbele kama nchi nyingine zilizoendelea. « Mkiona vyaelea
    vimeundwa. » Nchi zile zilizoendelea zilifikia kwenye kiwango kile kutokana
    na juhudi, uzalendo na bidii ya raia wao. Kwa hiyo fukuzeni uvivu, ugoigoi na

    uzembe. Saidieni serikali yetu katika kazi za « umuganda.»

    Vijana kumbukeni kuwa kazi ni bakora ya kuondosha umasikini maishani. Ili kuwa
    na maisha bora, ni lazima kufanya kazi. Kumbuka kuwa hakuna mtu mwingine
    atakayekufanyia kazi. Aidha, kumbuka kuwa jamii isiyofanya kazi ni jamii yenye
    watu waliokufa. Kwa hiyo, kila mmoja akumbuke kutimiza wajibu wake. Msemo
    wa Kinyarwanda unasema « Asiyefanya kazi hapaswi kula. »

    Leo ningependa nitie nanga hapa. Ninawashukuru kwa kunitegea masikio.
    Kuanzia leo tuzidi kuchapa kazi ipasavyo. Hii ni kwa kuwa “Kazi ni kazi, la muhimu
    mtu amudu maisha.”

    Asanteni!

    Maelezo Muhimu
    Usemi wa asili ni yale maneno yanayotamkwa na mtu katika hali ya kwanza lakini
    usemi wa taarifa ni kurudia maneno yaliyosemwa na mtu kwa njia nyingi bila
    kupotosha maana ya kwanza. Usemi wa asili hutumia alama za mtajo, kuuliza
    na kushangaa lakini usemi wa taarifa huishia kwa nukta. Katika usemi wa taarifa

    nyakati na nafsi za vitenzi vilivyotumiwa katika usemi wa asili hubadilika.

    9.4. Matumizi ya Lugha: Maelezo muhimu Kuhusu Muundo

    wa Hotuba

    Soma maelezo yafuatayo kisha ujibu maswali hapo chini.

    • Muundo wa hotuba

    Hotuba ina sehemu zifuatazo:

    1. Anwani: Anwani, mada au kichwa cha hotuba huchukua mada ya hotuba.

    Hiki ndicho kichwa chake hotuba.

    Mfano: Hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Rwanda katika Sikukuu ya Mashujaa.

    2. Utangulizi: Mazungumzo katika utangulizi yanatoa mwangaza ama

    picha ya habari inayokusudiwa kuzungumzwa. Anza hotuba yako kwa

    kuwatambua waliohudhuria mkutano. Wataje kwa majina au vyeo vyao

    kuanzia kwa yule wa cheo cha juu hadi wa chini, mabibi na mabwana.

    Kumbuka kwamba huhitaji kuwasalimia. Kuwatambua kwa vyeo vyao vya

    pekee kunatosha.

    Mfano: Waziri wa Elimu, Gavana wa Jimbo la Kusini, Mkuu wa Wilaya ya Nyanza,

    Wanachama wa kikundi hiki cha Elimu Bora, mabibi na mabwana. Ni matumaini

    yangu kwamba nyote mna afya nzuri.

    3. Mwili/Kiini: Hakikisha kuwa kuna mtiririko wa hoja kuanzia mwanzo hadi

    mwisho. Ujumbe wako wote unapaswa kuwa katika usemi halisi wala si

    wa taarifa. Panga mawazo kufuatana na uzito ama umuhimu wake. Wazo

    muhimu lazima lianze kuzungumziwa kwa ukamilifu halafu lifuatiwe na

    mawazo mengine, nayo kwa kikamilifu.

    4. Mwisho: Hapa mazungumzo yajumlishe mawazo yote yaliyozungumziwa

    kwa maelezo fasaha. Ni vizuri kwa hotuba kufungwa kwa picha inayofanana

    na ile ya utangulizi ili kumbukumbu ya habari ibaki katika mawazo ya

    wasikilizaji.

    • Sifa za hotuba

    Hotuba safi huzingatia mambo haya:

    • Ukweli wa habari na taarifa: Ni lazima mhutubi ahakikishe kuwa yale

    anayozungumzia yana uhusiano na ukweli.

    • Ufasaha wa lugha: lazima mhutubi kutumia lugha fasaha, nzuri, safi

    na yenye kusikika vizuri kwa kila msikilizaji. Si vizuri kutumia lugha ya

    mafumbo.

    • Mantiki nzuri: Ni lazima kuweka kwa mfuatano mzuri wa mawazo au

    fikra.

    • Nidhamu: Yaani adabu njema ya mzungumzaji mwenyewe asimamapo

    mbele ya watu.

    • Sauti ya kusikia wazi pamoja na ishara zinazoeleweka na zinazohusiana

    na yasemwayo. -Ishara hizo si za lazima iwapo hotuba inatolewa kwa

    njia ya redio.

    • Umuhimu wa hotuba

    Hotuba huwa na umuhimu kwa mhutubu na kwa wanaohutubiwa.

    Umuhimu huo ni kama vile:

    • Kujenga ushirikiano

    • Kuheshimiana

    • Huondoaa ubaguzi wa kijinsia

    • Huhamasisha watu kuwa viongozi walio bora

    • Huwahamasisha watu kukuza vipawa na kushiriki katika kuonyesha

    vipaji mbalimbali kama michezo ya kuigiza n,k kwa kusikiliza hotuba

    zitolewazo.

    Maswali

    1. Hotuba inatarajiwa kuwa na sehemu zipi?

    2. Katika kuanza hotuba yake, mhutubi hufanya nini?

    3. Habari yenyewe hutolewa katika sehemu gani? Kwa nini?

    4. Mwisho wa hotuba una maumbile gani?

    MADA YA 3 UTUNGAJI WA INSHAMADA YA 5 UANDISHI WA RIPOTI