• MADA YA 1: UANDISHI WA BARUA ZA KIRAFIKI, MWALIKO NA MATANGAZO

    Uwezo mahususi
    Kuandika barua za kirafiki, mwaliko na matangazo kwa watu mbalimbali

    Malengo ya ujifunzaji

    - Kutaja sehemu kuu za barua za kirafiki, mwaliko na matangazo 
    - Kuchunguza muundo wa barua za kirafiki, mwaliko na matangazo
    - Kutofautisha aina za barua za kirafiki, mwaliko na matangazo 
    - Kuelezea lugha inayofaa kutumiwa katika uandishi wa barua za kirafiki, 
    mwaliko na matangazo
    - Kutunga barua za kirafiki kwa watu mbalimbali, barua za mwaliko na 
    matangazo ya aina tofauti
    - Kuonyesha adabu na hehima kwa watu anaowaandikia

    - Kueleza matumizi ya aina za maneno

    KIDOKEZO
     Tazama kwa makini mchoro ufuatao kisha ujibu maswali  
    yaliyotolewa hapo chini:
    d

    Jibu maswali yafuatayo
    -- Ni nini unachoona kwenye mchoro?
    -- Ni mambo gani tunayotumia kwa kuwasiliana kimaandishi?
    SOMO LA 1: BARUA YA KIRAFIKI
    1.1. Kusoma na ufahamu: Wema Hauozi

    Soma barua ifuatayo kisha ujibu maswali ya ufahamu.


    Chuo cha Ualimu cha Amahoro
    S.L.P. 100,
    NGORORERO
    16/11/2019
    Mpendwa Amina,
    Salamu!
    Ninakuandikia waraka huu nikiwa nimejaa furaha ghaya kama mzazi aliyejifungua
    pacha salama salimini. Wewe u mzima? Wazazi wako hawajambo ? Nasi hapa
    nyumbani kwetu Ngororero mambo ni shwari.

    Nia yangu ya kukuandikia barua hii ni kukushukuru kwa dhati ya moyo wangu.

    Zaidi ya hayo ni kule kunialika kuja katika harusi ya dada yako huko kwenu. Harusi
    ile ilikuwa ya kukata na shoka kabisa. Ilinivutia sana, hasa nilivyoona kwamba
    harusi yenyewe ilionyesha utamaduni wetu wa Wanyarwanda bila kuchanganya
    mambo ya kizungu. Hilo ni jambo nadra sana siku hizi wakati ambapo watu wengi
    wamebobea uzunguni. Harusi ilionyesha mitindo ya asili na jadi. Bibi na bwana
    arusi walikuwa wakipendeza mno na wakachagua kufanana sana kama mboni za
    macho. Ninawaombea baraka za Bwana.

    Zaidi ya hayo, usafi uliokuwa nyumbani kwenu ulikuwa wa kuvutia. Ugani

    kulikuwa kunametameta na kupendeza kutokana na maua yaliyokuwa yakitoa
    harufu nzuri. Vyakula na vinywaji vilivyoandaliwa mezani vilikuwa safi kwenye
    kiwango kinachohitajiwa.

    Isitoshe, ninakushukuru tena kwa msaada ulionipatia ukanisaidia masomoni

    wakati tulipokuwa shuleni. Msaada wako ulinifaa zaidi kwa sababu niliweza
    kushinda vizuri. Jambo hili lilinionyesha kwamba u rafiki wa kweli. Unajua?
    Nilipofika nyumbani wazazi wangu walinichinjia jogoo! Nami wakati wowote ule
    utakapohitaji msaada kutoka kwangu niko tayari kukupatia kwa kuwa « wema
    hauozi ».

    Kisha nisalimie wazazi wako na ndugu zako, maana walinishughulikia kupita

    kiasi. Kwa hakika, ninashindwa niandike yapi hata waweze kuelewa upeo wa
    furaha yangu.
    Wako,
    gahamanjos

    GAHAMANYI Jonasi

    KAZI 1

    Maswali ya ufahamu :
    a) Ni nani aliyeandika barua hii?
    b) Taja jina la aliyeandikiwa barua.
    c) Mwandikaji wa barua anasomea katika shule gani?
    d) Mwandikajibarua anaishi wapi?

    e) Madhumuni ya barua hii ni yapi?

    1.2. Msamiati kuhusu barua

    KAZI 2

    Baada ya kusoma barua ya hapo juu eleza maneno yafuatayo
    -- Ghaya
    -- Shwari
    -- Nadra
    -- Wamebobea
    -- Dhati

    1.3. Sarufi : Aina za maneno ya Kiswahili

    KAZI 3
    Chunguza sentensi zifuatazo kisha utaje aina za maneno
    yaliyopigiwa mistari.
    -- Gahamanyi ni mwalimu wa chuo cha ualimu.
    -- Darasa linasafishwa na wanafunzi wale.

    -- Yeye atakuja kesho.

    Gahamanyi, ualimu : ni nomino/majina
    Ni, linasafishwa ni vitenzi
    Cha, wale ni vivumishi

    Yeye ni kiwakilishi

    Maelezo muhimu kuhusu aina za maneno
    Katika lugha ya Kiswahili kuna aina nane za maneno. Aina hizo ni kama vile
    nomino, kitenzi, kivumishi, kiwakilishi, kihusishi, kielezi, kiunganishi na kihisishi.
    Katika somo letu tutagusia kwenye aina nne yaani nomino, kivumushi, kiwakilishi
    na kitenzi.
    • Nomino (N)/ jina
    a) Maana ya nomino

    Nomino au jina ni neno linaloita kitu chenye uhai au kisicho hai kwa kukitoautisha
    na vingine.
    b) Aina za nonino
    -- Nomino za pekee : Butare, Nyanza, Ngororero , Gahamanyi, Ibilisi,
    Rukarara, Yesu, Akanyaru, …
    -- Nomino za kawaida : ndege, gari, nyumba, kiongozi, tarafa, gunia, kobe,
    miti …
    -- Nomino za dhana au za dhahania : unyama, uzalendo, ualimu, utu,
    ujinga, uroho…
    -- Nomino za jamii/ za makundi : umma, familia, jamii, bodi, baraza,
    genge, kikosi, jeshi, …
    -- Nomino za wingi : mate, maji, mafuta, amani, madaraka, …
    -- Nomino za kitenzi-jina : Kuishi kwingi kuona mengi. Kuimba kwake

    ni kuzuri.

    KAZI 4

    Baada ya kusoma maelezo ya hapo juu toa mifano mingine ya

    aina za nomino.

    KAZI 5

    Weka majina yafuatayo katika wingi

    s

    Vivumishi(V)
    a) Maan ya kivumishi
    Vivumishi au visifa ni maneno yanayotuelezea zaidi kuhusu nomino. Aghalabu
    vivumishi hutanguliwa na nomino.
    b) Aina za vivumishi
    • Vivumishi vya sifa

    Mifano:

    -- Mke mfupi yule ni mpole.
    -- Sauti nzuri humtoa nyoka mkali pangoni.
    • Vivumishi vimilikishi
    Vivumishi hivi hutumika kuonyesha nomino inayomiliki nyingine. Mizizi ya vivumishi
    hivi huundwa kulingana na nafsi mbalimbali. Mizizi hiyo ni: -angu, -ako, -ake,
    -etu, -enu, -ao.

    Mifano :

    -- Gari langu halina usukani.
    -- jamii yao inaishi vizuri.
    • Vivumishi vya idadi
    Hutueleza zaidi kuhusu kiasi, au idadi ya nomino. Kuna aina mbili za vivumishi
    vya idadi.

    a) Idadi kamili - hutumia nambari kuelezea idadi ya nomino.

    Mifano:
    -- Mmomonyoko wa ardhi ulibomoa nyumba tatu katika kijiji kimoja.
    -- Alipotaka kuoa wake wawili wanakijiji walimzuia.
    b) Idadi Isiyodhihirika - huelezea kiasi cha nomino kwa ujumla, bila kutaja
    idadi kamili.
    Mifano: Chache, nyingi, kadhaa, kidogo, wastani.

    Mifano
    :

    -- Watoto wengi waligeuka mayatima wakati wa mauaji ya kimbaridhidi ya
    Watusi yaliyotokea mnamo mwaka wa 1994.
    -- Mvua nyingi ilinyesha na kusababisha mmomonyoko wa ardhi.
    Vivumishi viulizi
    Vivumishi viulizi hutumika kuuliza swali.
    -ngapi?, -pi? wapi?, gani?
    Mifano:
    -- Mtu yule ana miguu mingapi?
    -- Ni mbuga ipi inayohifadhi simba nchini Rwanda?
    Vivumishi viashiria / vionyeshi
    Vivumishi viashiria hutumika kuonyesha au kuashiria nomino kulingana na mahali.
    Karibu: hapa, huyu, hiki, hili, huku, haya.
    Mbali kidogo: hapo, huyo, hiyo, hicho.
    Mbali zaidi: pale, lile, kile. ule, wale, pale.

    Mifano :

    -- Kaeni mahali hapa.
    -- Kijana yule ni mchezaji.
    Vivumishi visisitizi

    Husisitiza nomino fulani kwa kurudia rudia kivumishi kiashiria.

    Mifano:
    -- Amekuja pahali papa hapa.

    -- Kiongozi yuyu huyu anatutawala vizuri.

    • Vivumishi virejeshi
    Hivi ni vivumishi ambavyo hurejelea nomino. Vivumishi hivi vinaweza kuwa
    vivumishi vya O-/-ye rejeshi au vivumishi viashiria vinapotumika kurejelea nomino.

    Mifano:

    -- Raia ambaye atakamatwa akiuza au akinunua magendo ataadhibiwa.
    -- Wanyama ambao ni wakali sana ni simba na chui.

    Vivumishi vya A-unganifu
    Vivumishi hivi hutuelezea zaidi kuhusu nomino kwa kuonyesha kitu kinachomiliki
    nomino hiyo. Huundwa kwa kuambatanisha kiambishi cha nafsi/ngeli pamoja na
    kiambishi -a cha a-unganifu, kisha nomino.
    Mfano: cha, la, kwa, za, ya, wa, …

    -- Uchungu wa mwana aujuaye mzazi.

    KAZI 6

    Pigia mstari vivumishi katika sentensi zifuatazo:
    a) Jua kali hili husababishwa na uharibifu wa mazingira yetu.
    b) Maneno matamu yalimtoa nyoka yule pangoni mle.
    c) Koti hilo refu limekugeuza mzee.
    d) Usafi utafanywa na sisi sote wenyewe.

    e) Ni walimu gani watakaofundisha somo la Kiswahili?


    Viwakilishi (w)

    a) Maana ya viwakilishi
    Viwakilishi vya nomino ni maneno yanayotumika badala ya nomino. Kiwakilishi

    hakiwezi kuambatanishwa na nomino inayorejelewa.

    b) Aina za viwakilishi
    Viwakilishi vya nafsi
    -- Viwakilishi nafsi huru: Mimi, wewe, yeye, sisi, nyinyi, wao.
    -- Viwakilishi nafsi viambata : Ni-, u-, a-, tu-, m-, wa-, mi-, li-, ya-, ki-, vi-,

    i-, zi-, ku-, pa-

    • Viwakilishi viashiria

    Viwakilishi viashiria (vionyeshi) hutumika badala ya nomino kwa kutumia
    kuonyesha nomino inayorejelewa bila kuitaja.
    -- Haya ni madhara ya uharibifu wa mazingira.

    -- Wale wanahitaji amani.

    • Viwakilishi visisitizi

    Hutumika kwa niaba ya nomino kwa kutumia kiashiria chake mara mbili mfululizo.
    Kwa mfano: yuyu huyu, wawa hawa, kiki hiki, papo hapo, mumu humu, zizi hizi,
    → Yuyu huyu ndiye rafiki yangu.

    • Viwakilishi vya sifa

    Husimama badala ya nomino kwa kurejelea sifa yake.
    Kwa mfano: -chungu, -eupe, -dogo, -zuri, -tamu, -embamba, -rembo, -gumu,
    -kali, ekundu.
    → Cheupe Kinapendeza.
    • Viwakilishi vya idadi
    Hutumika kusimama badala ya nomino kwa kurejelea idadi yake.
    a) Idadi Kamili - hutumia nambari kuelezea idadi ya nomino
    -- Ukikata mmoja panda miwili.
    -- Anafuga watatu tu.

    b
    ) Idadi isiyodhihirika - huelezea kiasi cha nomino kwa ujumla, bila kutaja
    idadi kamili.
    Mifano:
    -- Tutasikiliza maoni ya wengi baada ya kuuratibu mpango huu.
    -- Mengi yalisemwa kuhusu maradhi ya UKIMWI.

    • Viwakilishi viulizi

    Viwakilishi viulizi hutumika kwa niaba ya nomino katika kuulizia swali.
    Baadhi ya viwakilishi viulizi huchukua viambishi vya ngeli.
    Mifano:
    -- Uko wapi?
    -- Unahitaji vingapi?

    • Viwakilishi vimilikishi

    Viwakilishi hivi hurejelea nomino kwa kutumia vimilikishi.
    -- Kwetu kuna maji safi.
    -- Zao zilibomolewa na mvua kali.

    • Viwakilishi virejeshi
    Hutumia O-/-ye-rejeshi kurejelea na kusimamia nomino.
    Kwa mfano: ambaye, ambao, ambalo, ambacho, huyo, yule.
    -- Ambao walizaliwa mwaka huu watapimwa.
    -- Ambaye anahitaji fedha za shule

    • Viwakilishi vya A-unganifu

    Huwakilishi nomino kwa kutaja kinachomilikiwa na nomino hiyo. Huundwa
    kwa kuambatanisha kiambishi cha nafsi/ngeli pamoja na kiambishi -a cha
    a-unganifu.

    Kwa mfano: cha, la, kwa, za, ya

    -- Cha mlevi huliwa na mgema.

    -- La kuvunda halina ubani.

    KAZI 7

    Taja aina za viwakilishi vinavyopatikana katika sentensi zifuatazo:
    -- Wao hawajafika kwangu.
    -- Yule mweusi aende nyumbani.
    -- La kuvunja halina rubani.

    -- Wengi walipanda miti kupambana na jangwa.

    1.4. Matumizi ya lugha

    KAZI 8

    Soma upya barua uliyopewa hapo awali kisha utoe maana ya

    barua ya kirafiki na uonyeshe sehemu zake kuu.

    Maelezo muhimu kuhusu barua ya kirafiki
    a) Maana ya barua
    Barua au waraka ni maandishi yaliyopangwa kwa utaratibu na mtiririko maalum
    kwa minajili ya kuwasilisha ujumbe fulani. Barua ni risala au mmjumbe mwepesi
    anayemwakilisha mtungaji wake kwa mtu mwingine na kuwasilisha taarifa yake

    kwa mtu huyo.

    Barua huandikwa kwa madhumuni mbalimbali kama kuarifu, kuomba kitu kama
    vile kazi, ruhusa; kuagiza bidhaa, n.k.

    Kuna aina nyingi za barua lakini katika kitabu hiki tutashuhulikia barua tatu tu

    ambazo ni:
    -- Barua za kikazi zenye madhumuni ya kazi.
    -- Barua za mwaliko zenye lengo la kualika mtu katika sherehe au sikukuu
    fulani
    -- Barua za kirafiki : ni zile ambazo huandikiwa na mtu au watu mbalimbali
    walio na uhusiano wa karibu na anayeandika; k.v rafiki, ndugu, n.k. Barua
    hizi zina uhuru mkubwa katika kuziandika. Hazidai utaratibu wa kipekee
    sana. Mtu huwa huru kuandika apendalo ilimradi halimvunjii mtu heshima
    yake.

    b) Sehemu za barua ya kirafiki

    c

    -- Anwani ya mwandikaji na tarehe: huandikwa kwenye pembe ya juu
    upande wa kulia wa karatasi. Mwandikaji anaandika mahali anapoandikia
    barua (au anapoishi). Anaweza kuongeza nambari za sanduku la posta
    (S.L.P.) na mji, nambari ya simu na akaunti ya barua pepe. Tarehe huandikwa
    chini ya anwani kwa kuacha nafasi ya mstari mmoja.
    -- Jina la mwandikiwa: huja chini ya tarehe lakini kwenye upande wa
    kushoto.
    -- Salamu: sehemu hii hutoa maamkizi kwa mwandikiwa na huandikwa
    chini ya jina la mwandikiwa.
    -- Utangulizi: hujitokeza katika aya ya kwanza. Mwandikaji humjulisha hali
    yake ilivyo,na kuuliza hali ya mwandikiwa na hata wenzake kwa jumla.
    -- Barua yeynyewe: huu ni ujumbe kamili wa barua. Mwandikaji anaweza
    kutumia aya moja au zaidi kulingana na urefu wa barua yake.
    -- Hitimisho la barua: ni sehemu ya mwisho ya barua. Sehemu hii
    huandikwa kwa aya moja na hujumlisha mambo ya kumuaga mwandikiwa.
    Kwenye sehemu hii unaongeza maneno ya kuvutia (Wako, Wako mpendwa,
    Mwanako, Wako mwaminifu, n.k.). Maneno haya huandikwa kwenye
    upande wa kulia kabla ya kutia sahihi.
    -- Sahihi ya mwandishi: huja chini ya hitimisho kwa upande wa kushoto.
    -- Jina la mwandikaji: huja chini ya sahihi ya mwandikaji.

    c) Aina za barua za kirafiki

    Barua za kirafiki zinaweza kuwa mwana kwa mzazi au mzazi kwa mwana, za
    mapenzi, za kindugu (kati ya ndugu), za kijamaa, n.k.


    1.5. Kusikiliza na kuzungumza
    KAZI 9
    Tunga barua kisha uisomee wenzako hadharani kwa kuonyesha vitabia
    1.6. Kuandika

    KAZI 10
    Mwandikie rafiki yako barua ukimwomba muende pamoja

    kutembelea Mbuga ya Wanyama ya Akagera.

    SOMO LA 2: BARUA YA MWALIKO
    2.1. Kusoma na ufahamu: Ndoa ya dadangu
    Soma kifungu cha habari kifuatacho kisha ujibu maswali ya ufahamu.

    NDOA YA DADANGU

    v

    Ilikuwa Jumamosi tarehe 15 mwezi wa Novemba wakati nilipohudhuria harusi ya
    dada yangu Mukashema Maria aliyefungana pingu za maisha na Mutabazi Joni.
    Harusi yenyewe ilikuwa ya kukata na shoka.

    Kabla ya wiki mbili za arusi kufanyika familia mbili zilikuwa katika pilikapilika za

    hapa na pale ili kuandaa sherehe hii ya harusi. Kwa upande wa familia yangu sisi
    watoto tulikuwa tukitumwa huku na kule kwa kuwaalika watu watakaohudhulia
    harusi hii. Wazazi wangu waliwaalika wazee majirani na dada yangu akawaalika
    wenzake hasa wa rika lake. Wote walikuwa wakipelekewa barua za mialiko.

    Siku moja kabla, nyumbani kwetu tulifanya usafi na majirani walikuwa wakimsaidia

    baba kutayarisha pombe ya mtama, ya ndizi na juisi. Wengine walikuwa
    wakipamba uga na kujenga nyumba za mahema.

    Siku hiyo ilipowadia watu walimiminika kuelekea nyumbani kwetu. Asubuhi

    majira ya saa nne hivi, familia ya bwana harusi ilifika kwetu na kukaribishwa kwa
    taadhima. Walikuwa wamekuja kuposa na kutoa mahari. Waliandaliwa vyakula
    na vinywaji mezani wakafurahi sana. Furaha yao ilipandishwa na nyimbo pamoja

    na ngoma za wachezaji waliokuwa hapo.

    Baada ya hapo bi harusi alivishwa veli. Bwana harusi alirudi kumchukua akiwa
    na gari la kifahari wakaenda kanisani ili kuvishana pete mbele ya Bwana. Nasi
    tuliandamana nao tukiwa katika magari kadhaa. Watu walipoona mlolongo wa
    magari hayo waliduwaa wakidhani kuwa kulikuwa na kongamano la kimataifa
    katika kijiji chetu.

    Tulipotoka kanisani, tulifurika bustanini kama ilivyoelezwa kwenye barua za

    mwaliko walizopewa watu. Watu walikuwa wengi sana na sherehe ilifana sana.
    Tuliandaliwa vinywaji na vyakula tele tele. Watu wote walifurahi sana na kucheza

    ngoma na nyimbo za utanaduni

    KAZI 1

    Maswali ya ufahamu
    a) Harusi inayosimuliwa ilifanyika lini ?
    b) Harusi hiyo ilikuwa ya kina nani ?
    c) Ni vinywaji gani vilivyotayarishwa siku moja kabla ya sherehe?
    d) Watu waliokuja harusini walipataje habari hizo?

    e) Kwa sababu gani watu walioona magari walishangaa?

    2.2. Msamiati

    KAZI 2

    Eleza maneno yafuatayo
    a) Aliyefungana pingu za maisha
    b) Pilikapilika
    c) Kifahari
    d) Mahema

    e) Veli

    2.3. Sarufi: Aina za maneno

    KAZI 3

    Tazama sentensi zifuatazo kisha ueleze maneno yaliyopigiwa
    mistari
    a) Nyumbani humu mna usafi.
    b) Tia taka nje.

    c) Simba anaishi ndani ya msitu ule.

    Maelezo muhimu kuhusu aina za maneno
    Katika lugha ya Kiswahili kuna aina nane za maneno. Aina hizo ni kama vile
    nomino, kitenzi, kivumishi, kiwakilishi, kihusishi, kielezi, kiunganishi na kihisishi.
    Katika somo letu tutagusia kwenye aina tatu yaani kitenzi, kielezi na kihusishi.
    • Kitenzi
    a) Maana ya kitenzi

    Kitenzi ni neno linaloeleza jambo linalotendwa au kufanywa na nomino au
    kiwakilishi chake.
    b) Aina za vitenzi
    -- Kitenzi halisi: Ni kitenzi kimoja kinachotumiwa katika sentensi.
    Mifano :
    -- Raia walifanya msaragambo.
    -- Meya amekuja hapa.
    -- Vitenzi vikuu na vitenzi visaidizi: Wakati vitenzi viwili hutumika pamoja
    kueleza kitendo kimoja, kitenzi cha kwanza huitwa kisaidizi na cha pili
    ndicho kitenzi kikuu.
    Mifano :
    -- Yeye alikuwa akicheza.
    -- Wao wanahitaji kula vizuri.
    Vitenzi vishirikishi: Vitenzi vishirikishi vina dhana ya kitenzi kuwa au
    kuwa na.
    Vitenzi vishirikishi huwa vya aina mbili kuu :
    Vitenzi vishirikishi vikamilifu: Hivi huchukua viambishi vya wakati
    na viambishi nafsi.
    Mifano :
    -- Wanafunzi wangali usingizini
    -- Yeye atakuwa mzembe.
    Vitenzi vishirikishi vipungufu : Hivi huchukua viambishi nafsi lakini
    havichukui viambishi wakati.
    -- Walozi si wazuri.
    -- Yeye yu mkweli.

    -- Nyinyi ni walimu wa kesho.

    KAZI 4

    Tunga sentensi ukitumia vitenzi vifuatavyo :
    • - yu
    • - kimuona
    • - u
    • - kaa

    • - ni

    • Vielezi
    Vielezi ni maneno yanayotoa habari zaidi kuhusu kitendo kilivyofanyika. Pia vielezi
    hutoa habari zaidi kuhusu hali, vivumishi na vielezi vingine.

    Kuna vielezi vya namna, vielezi vya wakati, vielezi vya mahali na vielezi vya kiasi.


    Mifano :

    -- Mwanafunzi-mwalimu yule ameshinda mtihani vizuri (Kielezi cha
    namna).

    -- Mvua ilinyesha jana (kielezi cha wakati).
    -- Samaki huishi baharini (kielezi cha mahali).

    -- Anamtembelea mara kwa mara (kielezi cha kiasi).

    KAZI 5

    Onyesha na utaje aina za vielezi vinavyopatikana katika sentensi
    zifuatazo:
    -- Simba huenda kimya anapowinda.
    -- Vijana wa siku hizi huvaa kizungu, kichina na kihindi mara chache.
    -- Wewe uliitwa mara kadhaa na hujaitika leo.
    -- Gunia hili limejaa sana inafaa lipakuliwe.

    -- Imenyesha mchana kutwa

    • Vihusishi (H)
    Vihusishi ni maneno yanayoonyesha uhusiano baina ya watu au vitu viwili au

    zaidi. Kuna vihusishi vya mahali na vya wakati.

    Mifano:
    -- Tutaonana baada ya wiki moja .
    -- Si vizuri kuishi kando ya mto.
    -- Ng’ombe hulala ndani ya zizi.
    -- Ameondoka hapa kabla ya mvua kunyesha.

    -- Wao wanaishi pamoja kwa amani.

    KAZI 6

    Tumia vihusishi vifuatavyo kwa kujaza mapengo: katika, kabla ya,
    mbele ya, baada ya, pembeni mwa.
    a) Miti ilipandwa................nyumba.
    b) .................mvua kunyesha unaona dalili zake.
    c) Watu wengi waliangamia ..............ajali ya ndege iliyotokea nchini
    Kongo.
    d) ...............kuondoka tulimfuata huko.

    e) Hakuna mtu anayeishi...............shimo siku hizi nchini Rwanda.

    2.4. Matumizi ya lugha

    KAZI 7

    Jibu maswali yafuatayo
    a) Mtu anapowakaribisha wengine karamuni anatumia nini?
    b) Mtu anaweza kuwaalika wengine kwa madhumuni gani?
    KAZI 7
    Maelezo muhimu kuhusu barua za mwaliko
    Maana ya barua za mwaliko
    Barua ya mwaliko ni ujumbe unaotolewa kwa kumkaribisha mtu kuhudhuria
    shughuli au hafla fulani. Barua za mwaliko zinaweza kuwa na madhumuni
    yafuatayo:
    Sherehe
    Karamu
    Harusi

    Ubatizo

    Sikukuu ya kufunga mwaka
    Sikukuu ya kupata cheti au digrii
    Kuadhimisha miaka fulani, n.k

    Mambo ya kuzingatiwa katika uandishi wa barua ya mwaliko

    Jina la mwalikwa
    Sababu ya mwaliko
    Mahali ukaribisho utakapofanyika, terehe na saa
    Jina na anwani ya mkaribishaji

    a) Mifano ya barua za mwaliko

    • Barua ya mwaliko kwenye harusi

    d

    Karibu sana!

                                                                                                                    RWEMA Eric

    2.5. Kusikiliza na Kuzungumza
    KAZI 8
    Shirikiana na wenzako mzungumzie kuhusu uandishi wa barua za mwaliko.

    2.6. Kuandika
    KAZI 9

    Mkaribishe mwenzako kwenye sikukuu yako ya kuzaliwa

    SOMO LA 3: MATANGAZO
    KAZI 1
    Tazama kwa makini mchoro ufuatao kisha ujibu maswali

    yaliyotolewa hapo chini:

    v

    Jibu maswali yafuatayo:
    –– Ni nini unachoona kwenye mchoro huu?

    –– Unafikiri kuwa mtu huyo mwenye kipazasauti anafanya nini?

    3.1. Kusoma na ufahamu: Tangazo la ajira
    Soma tangazo lifuatalo kisha ujibu maswali ya ufahamu.
    TANGAZO LA AJIRA
    Wilaya ya CHAPAKAZI inayo furaha ghaya ya kuwatangazia watu wote wenye
    uwezo kwamba ina nafasi za ajira za ufundishaji katika shule za chekechea na
    msingi. Nafasi hizo ni kama zifuatazo:
    1. Walimu wa Kiswahili katika shule za msingi (nafasi kumi)
    2. Walimu wa Kinyarwanda katika shule za msingi (nafasi tatu)
    3. Walimu wa Hisabati katika shule za msingi (nafasi tano)
    4. Walimu wa Kifaransa katika shule za msingi (nafasi tano)
    5. Walimu wa Kiingereza katika shule za msingi (nafasi tano)
    6. Walimu wa Mafunzo ya kijamii katika shule za msingi (nafasi tano)
    7. Walimu wa Sayansi katika shule za msingi (nafasi mbili)
    8. Walimu katika shule za chekechea (nafasi ishirini)

    Anayehitaji kazi hizo anapaswa kuwa na sifa zifuatazo:

    1. Kuwa Mnyarwanda,
    2. Kuwa na astashahada ya ukufunzi (A2),
    3. Kuwa na uwezo wa kutumia tarakilishi na vifaa vingine vya TEHAMA,
    4. Kuwa na uwezo wa kutumia Kinyarwanda na Kiingereza kwa ujumla.
    Kwa wakufunzi wa Kiswahili wanapaswa kuwa na uwezo wa kutumia
    kinyarwanda, Kiingereza na Kiswahili. Wakufunzi wa Kifaransa wanapaswa
    kuwa na uwezo wa kutumia Kinyarwanda, Kiingereza na Kifaransa.
    5. Kuwa na afya bora,
    6. Kuwa na umri usiozidi miaka thelathini,
    7. Kuwa na uwezo wa kufanyia kazi katika eneo na mazingira yoyote.

    Barua zenye maombi ya kazi pamoja na viambatisho vingine kama vile wasifu kazi,

    kitambulisho cha uraia na astashahada, vitapokelewa hadi tarehe 20/12/2019

    katika ofisi ya katibu wa wilaya. Tarehe ya kusailiwa mtaijuzwa baadaye.

    Tangazo limetolewa tarehe 1/12/2019.

    Meya wa Wilaya ya Chapakazi
    (Saini + mhuri)

    GAHIZI Musa

    KAZI 2
    Jibu maswali yafuatayo
    Tangazo hili ni la aina gani?
    Tangazo hili linalenga nani ?
    Tangazo hili linatangaza nini ?
    Neno TEKNOHAMA ni ufupisho wa nini ?

    Kwa sababu gani Meya wa wilaya alitia saini yake kwenye tangazo?

    KAZI 3
    3.2. Msamiati kuhusu tangazo
    Eleza maneno yafuatayo :
    -- Ajira
    -- Shule za chekechea
    -- Viambatisho
    -- Astashahada

    -- Mhuri

    3.3. Sarufi: Aina za maneno ya kiswahili
    KAZI 4
    Chunguza sentensi zifuatazo kisha utaje aina za maneno
    yaliyopigiwa mistari.

    -- Kobe na Kijumbamshale walikaa chini ya mti ili kuzungumza.
    -- Lo! Umemwona mshamba yule!

    -- Fisi wala Simba hawakucheza mchezo wa riadha.

    Maelezo muhimu kuhusu aina za maneno
    KAZI 5
    Soma maelezo yafuatayo kisha ujadili kuhusu matumizi ya maneno
    yanayounganisha sentensi:
    Katika lugha ya Kiswahili kuna aina nane za maneno. Aina hizo ni kama
    vile nomino, kitenzi, kivumishi, kiwakilishi, kihusishi, kielezi, kiunganishi na

    kihisishi. Katika somo letu tutaona aina mbili yaani kiunganishi na kihisishi.

    • Viunganishi (U)
    Viunganishi ni maneno yanayofanya kazi ya kuunganisha. Huonyesha uhusiano
    baina ya neno na neno, fungu moja la maneno na fungu jingine au sentensi na
    sentensi.

    Mifano:

    a) Unataka maji au juisi?
    b) Anasoma kitabu badala ya kupiga ubwana.
    c) Kufanikiwa maishani si bahati bali ni kujishughulisha na kujitolea.
    d) Alishinda mtihani ijapokuwa alipatwa na ugonjwa mkali.
    e) Alienda shuleni bila kupata chakula.

    KAZI 6

    Tunga sentensi sahihi kwa kutumia viunganishi vifuatavyo:

    a) Halafu
    b) Kisha
    c) Ili
    d) Ingawa

    e) Kama

    • Vihisishi (I)
    Vihisishi ni maneno ambayo yanaonyesha hisia za mtu za ndani kwa mujibu wa
    hali na muktadha. Yanaonyesha hangaiko la moyo ama kudokeza mguso wa

    moyo ama hata wa akili.

    Mifano:
    Mtume! Umefika asubuhi hii!
    Lo! Mvua imenyesha!

    Salaa! Inawezekana mtu kunywa chupa ishirini za juisi!

    KAZI 7
    Tunga sentensi sahihi kwa kutumia vihishi vifuatavyo:
    a) Mungu wangu!
    b) Mama wee!
    c) Ng’o!
    d) Barabara!

    e) Masalale

    3.4. Matumizi ya lugha
    KAZI 8
    Soma upya tangazo la hapo juu kisha ujadiliane na wenzako kuhusu muundo

    wa matanganzo.

    Maelezo muhimu kuhusu matangazo
    Maana ya tangazo
    Tangazo au ilani ni mpangilio wa maandishi kwa mtindo maalumu kwa lengo la
    kupasha habari ama kupokeza ujumbe fulani wa kidhalura au muhimu. Taarifa
    inayosambazwa kwa tangazo inaweza kuwa kifo, mkutano, taratibu za kutumia
    barabara vizuri, kazi na mengineyo.

    Aina za matangazo

    Zipo aina nyingi za matangazo
    Matangazo ya kibiashara
    Matangazo ya kifo
    Matangazo ya serikali, n.k.
    Mambo ya kuzingatiwa katika uandishi wa matangazo
    Kwa kuandika tangazo ni lazima kuzingatia mambo yafuatayo :
    Kichwa cha tangazo
    Kutaja anayetoa tangazo
    Kutaja walengwa wa tangazo
    Ujumbe wa tangazo

    Sahihi na jina la anayetoa tangazo (tangazo lisilokuwa na sehemu hii huitwa
    tetesi, fununu au uvumi)

    Mfano wa tangazo

    m

    3.5. Kusikiliza na Kuzungumza
    KAZI 9
    Sikiliza matangazo redioni kisha ujadiliane na wenzako kwa

    kuzingatia maudhui, aina ya matangazo na lugha iliyotumiwa.

    3.6. Kuandika
    KAZI 10

    Tunga tangazo la kibiashara

    Tathmini ya mada
    1. Eleza maana ya barua.
    2. Taja aina za barua tulizoona.
    3. Zitaje sehemu kuu za barua ya kirafiki.
    4. Ni mambo gani muhimu yanayopaswa kuonekana kwenye barua ya
    mwaliko?
    5. Tunga tangazo la kazi.
    6. Taja aina za meneno yanayojenga sentensi zifuatzo.
    -- Eeh! Unataka kitu gani?
    -- Wao walikufa hapa na kuondoka haraka.
    -- Mama alikuwa akipalilia maharagwe yake katika bonde lile.
    -- Ingawa mvua ilinyesha vizuri, mavuno yanaendelea kudidimia.

    -- Chukua hicho kizuri ila hakitoshi.

    MADA YA 2: UTUNGAJI WA BARUA RASMI