• MADA YA 8 UHAKIKI WA KAZI ZA FASIHI ANDISHI


    Malengo ya Ujifunzaji:
    -- Kueleza uhakiki wa kazi za fasihi na umuhimu wake,
    -- Kubainisha vipengele muhimu katika uhakiki wa kazi za fasihi andishi,
    -- Kutofautisha fani na maudhui,
    -- Kuhakiki kazi za tanzu mbalimbali za fasihi andishi,

    -- Kutumia kwa ufasaha viambishi rejeshi katika ngeli za majina mbalimbali.




    16.1. Kusoma na Ufahamu: Uhakiki kama Kazi ya
    Kitaalamu
    Jinsi binadamu alivyo, na anavyomudu maisha yake ya kila siku, hutokana na
    maarifa ya kielimu aliyoyapata darasani au katika tajiriba yake ya kimaisha. Aidha,
    watu hujishughulisha na kazi mbalimbali. Kutokana na tofauti za kazi, utawakuta
    mafundi katika kazi za ujenzi wa nyumba, mabingwa katika uwanja wa kiteknolojia,
    wabobezi katika uchumi na wataalamu katika mambo ya fasihi au lugha kwa
    ujumla. Hali kadhalika, jinsi dereva anavyojiamini katika uendeshaji wa gari,
    ndivyo mhakiki wa kazi za fasihi anavyotawala katika uchambuzi au uchanganuzi
    wa kazi za kifasihi zilizotungwa na wasanii.

    Jambo hili linatupeleka kwenye maswali yafuatayo: Je, uhakiki unamaanisha nini?

    Kwa nini uhakiki? Ni jukumu gani mhakiki wa kazi za kifasihi anastahili kutimiza?

    Kimsingi, kazi ya fasihi andishi ni aina ya sanaa ambayo hutumia maneno
    yaliyoandikwa kupitisha ujumbe, au ni sanaa inayowasilisha ujumbe kwa njia ya
    maandishi. Miongoni mwa kazi hizo ni pamoja na hadithi fupi, tamthiliya, riwaya
    pamoja na ushairi.

    Kwa hiyo, msanii hatungi kwa kutunga tu ila huongozwa na kutawaliwa na misingi
    ya kisanii katika ufundi wake. Katika mwelekeo huu, mhakiki hustahili kushiriki
    katika uchunguzi wa kazi ya msanii iliyotolewa ili kuichunguza au kuitathmini.

    Kwa hivyo, uhakiki ni kitendo cha kutathimini, kueleza, kuainisha na kutoa maoni
    juu ya kazi fulani ya fasihi kwa kuongozwa na kaida maalumu. Hali kadhalika,
    uhakiki wa kazi za fasihi ni kitendo cha kuchambua, kutathmini na kuainisha kazi
    ya fasihi ili kuona ubora na udhaifu wa kazi hiyo kwa kutumia kaida au vigezo
    husika vya fani na maudhui.

    Kutokana na maelezo haya, inaeleweka wazi kuwa mhakiki wa kazi za fasihi bila
    shaka huwa ni mtaalamu au mwerevu katika uwanja wa kifasihi ambaye huwa na
    uwezo au stadi za kuzisoma, kuzitafakari, na kuzitolea tathmini kazi za fasihi kwa
    kujiegemeza katika mwelekeo wa kaida maalum zinazotakiwa kuzingatiwa katika
    utunzi wa kazi hizo.
    Hivyo basi hatuna budi kukubali kuwa mhakiki wa kazi za fasihi huwa na jukumu
    au nafasi kubwa katika kazi za fasihi kama ifuatavyo:

    Kwanza, mhakaki ndiye anayefafanua kazi ya fasihi ili hadhira iweze kuelewa
    vizuri kazi hiyo. Vilevile mhakiki huwaonyesha watunzi au wasanii wa kifasihi
    ubora na udhaifu wa kazi zao. Kwa kufanya hayo mhakiki huwawezesha watunzi
    kutoa kazi bora zaidi.

    Pengine, inambidi mhakiki huyo awe na habari kamili juu ya mwandishi au msanii
    wa kazi inayohakikiwa. Maana yake, inambidi mhakiki kuelewa hali pamoja na
    mazingira aliyokuwemo msanii kama kielelezo cha hisia zake au hoja zake. Hivi
    mhakiki hufanikiwa kutambua sababu za hisia au dhamira zilizoendelezwa na
    msanii katika kazi yake.

    Hali kadhalika, mhakiki hutafakari kikamilifu kazi ya msanii na kuichambua
    kimawazo au kimalengo kwa kudhihirisha au kutambua maudhui pamoja na
    dhamira kuu au ndogondogo ambazo ni kiini cha kazi kamili ya msanii. Ili kulikabili
    jukumu hili, mhakiki hutoa majibu kwa maswali yafuatayo:

    Msanii anatufahamisha nini? Kazi ya msanii inamlenga nani? Anazungumzia nini
    na ni suluhisho gani analotutolea kwa shida alizozitaja? Mwandishi ametunga

    katika kipindi gani cha historia na katika mazingira gani?

    Mwisho, mhakiki huwa na jukumu la kurahisisha mawasiliano au kiungo kati
    ya hadhira na mtunzi. Jukumu hili hujidhihirisha kwa njia ya uchunguzi wa jinsi
    msanii alivyojenga sanaa yake ili ujumbe wake uwafikie walengwa husika, yaani
    uhakiki wa lugha iliyotumiwa na msanii pamoja na jinsi alivyowajenga wahusika
    katika kazi yake ya kifasihi. Kwa upande mwingine, uhakiki wa kazi mbalimbali
    za kifasihi humsaidia msomaji wa kazi husika ya kifasihi kuielewa au kupata

    mwangaza fulani juu ya kazi husika aisomayo.






    Maelezo muhimu ya kuzingatia
    Kiambishi rejeshi –ye- ni kiambishi kinachotumika katika tungo kwa kurejelea
    mawazo, nomino au mambo yaliyokwisha tajwa au yanayojulikana. Kiambishi hiki
    hujihusisha tu na majina ya ngeli ya A-WA- katika umoja, yaani majina ya watu,
    Mwenyezi Mungu, pamoja na wanyama. Matumizi ya kiambishi rejeshi – ye –
    hutumiwa kama ifuatavyo:

    • Katikati ya kiambishi nafsi cha kitenzi na mzizi wa kitenzi.
    Mfano: Aliyeshiriki
    • Kwenye mzizi wa amba- na ndi-
    Mfano: Mwanafunzi ambaye
    Binadamu ndiye
    • Mwishoni mwa kitenzi
    Mfano: Mnyama alindaye
    Tanbihi: Kiambishi rejeshi –ye- hugeuka – o - katika wingi.

    Mfano:
    i) Watu walioshiriki katika mauaji ya kimbari dhidi ya Watutsi nchini Rwanda
    wamekamatwa na kupelekwa mahakamani.
    ii) Wanafunzi ambao hufanya bidii hushinda mitihani bila tatitizo.

    iii) Mbwa ni wanyama walindao nyumba za watu.



    MAELEZO MUHIMU YA KUZINGATIA
    DHIMA ZA UHAKIKI WA KAZI ZA FASIHI ANDISHI

    Uhakiki ni kazi ambayo ina mchango mkubwa sana katika kazi za fasihi. Kwa
    msingi huo uhakiki una dhima zifuatazo:

    • Husaidia wasomaji kuilewa kazi ya fasihi kwa urahisi:
    Watunzi wa kazi za fasihi hutofautiana katika matumizi ya lugha na taswira, hivyo
    mhakiki anapofanya kazi ya uhakiki anamsaidia msomaji kuelewa vipengele hivi

    kwa kuvifafanua kwa lugha rahisi.

    • Husaidia ukuaji wa kazi za fasihi:
    Mhakiki anapoonyesha ubora na udhaifu wa kazi ya mtunzi fulani, watunzi
    wengine pia watafunguka kifikra na kutunga kazi iliyobora zaidi.
    • Hukuza uelewa wa mhakiki:
    Kwa kuhakiki kazi mbalimbali za fasihi, mhakiki hujiongezea maarifa ya lugha
    pamoja na mambo yanayotokea katika jamii.

    NAFASI YA MHAKIKI WA KAZI ZA FASIHI ANDISHI
    Mhahiki kama mtaalamu wa kutathmini, kueleza, kuainisha na kutoa maoni
    juu ya kazi fulani ya fasihi kwa kuongozwa na kaida maalum, huwa na nafasi
    kubwa katika kazi za fasihi. Mhakiki ndiye anayefafanua kazi ya fasihi ili hadhira
    iweze kumwelewa vizuri mtunzi wa kazi hiyo. Kwa hiyo, hapa mhakiki anasaidia
    kurahisisha mawasiliano kati ya hadhira na mtunzi. Vilevile mtunzi huwaonyesha
    watunzi ubora na udhaifu wa kazi zao. Kwa kufanya hivyo, huwawezesha watunzi

    kufanya kazi bora zaidi.


    SOMO LA 17: TARATIBU ZA UHAKIKI WA KAZI ZA

    FASIHI ANDISHI



    17.1. Kusoma na Ufahamu: Uhakiki wa Fani na Maudhui
    Soma kifungu cha habari kifuatacho kisha ujibu maswali ya ufahamu
    hapo chini

    Wahenga walisema kuwa maneno huwa na utamu zaidi yanaporudiwa. Kwa hiyo,
    hatuna budi kukumbusha kuwa uhakiki ni kitendo cha kuchambua, kutathmini na
    kuainisha kazi ya fasihi ili kuona ubora na udhaifu wa kazi hiyo kwa kutumia kaida
    husika. Ili kazi yake itimizwe kwa hali mwafaka, mhakiki anastahili kupitia hatua

    tatu zifuatazo:

    Kwanza ni kuisoma kazi ya fasihi; hapa mhakiki anatakiwa kuisoma kazi husika ya
    fasihi kwa kina na kuielewa vizuri.

    Pili ni kuainisha na kuchambua mambo muhimu yanayojitokeza katika kazi hiyo
    kwa kuzingatia vipengele vya fani na maudhui.

    Tatu ni kutoa tathmini au kuelezea ubora na udhaifu wa kazi inayohusika. Je,
    tunapozungumzia vipengele vya fani na maudhui tunagusia nini?
    Tuchukue mfano wa barua pepe ambayo imeandikwa ovyo ovyo bila kuzingatia
    mitindo ya kisarufi, aya pamoja na alama za vituo. Mambo haya yote huchukuliwa
    kama umbo la barua pepe hii. Kama umbo hili halivutii basi msomaji hatakuwa na
    nia ya kuisoma barua pepe hii. Mfano wa pili ni wa nyumba inayong’aa kwa rangi
    na mapambo mbalimbali yaliyoko kwenye nyumba hiyo. Atakayeiona nyumba
    hii, atakuwa ameingiwa na udadisi wa kuingia ndani kwa sababu uzuri wake
    umemvutia mtazamaji. Umbo hilo ndilo linalolinganishwa na fani katika kazi za
    kifasihi.

    Hivyo, baada ya kuvutiwa na umbo la barua pepe, hamu au hiari ya kusoma
    ujumbe unaowasilishwa ndani yake itaongezeka. Ujumbe huo utatiliwa maanani
    na kupokewa kwa urahisi. Vilevile, mtazamaji aliyeridhika na umbo la nyumba
    hatasita kuingia ndani ili ashuhudie jinsi vifaa vya nyumbani vilivyo kama vile
    mpangilio wake, vyumba, milango, n.k. Atatafakari yeye mwenyewe ujumbe
    kuhusu uwezo mkubwa wa fundi aliyeijenga na kuipamba nyumba hiyo. Ujumbe
    huu au yaliyomo hufananishwa wazi na maudhui katika kazi za fasihi.

    Mifano ni wa msichana mrembo ambaye maumbile yake ni mithili ya malkia. Ah!
    Utapatwa na bumbwazi utakapomtathmini kimwenendo au kitabia. Mfano huu
    ungelikwenda sambamba na mtu ambaye unamkuta amevaa nguo za bei ghali
    iwapo mwili wake unatoa harufu mbaya; maana yake mwezi mzima umemalizika
    bila mtu huyo kuoga.

    Kwa hiyo, kazi ya msanii wa fasihi yoyote huwekwa mikononi mwa mhakiki ili
    kuitathmini na kutoa maoni yake kuhusu kufanikiwa au kutofanikiwa kwa msanii.
    Kwa upande mmoja, kufaulu au kutofaulu kwa msanii hutokana na jinsi umbo au
    fani ya kazi yake inavyowavutia walengwa wake.

    Kwa upande mwingine, kufaulu au kutofaulu kwa msanii huelezwa na jinsi ujumbe

    uliokusudiwa kuwasilishwa ulivyopangwa toka mwanzoni hadi mwishoni.


    17.2. Matumizi ya Msamiati



    Maelezo muhimu ya kuzingatia

    Kiambishi rejeshi husika ni – o - . Kirejeshi hiki hujihusisha na ngeli za majina

    kama ifuatavyo:

    • Katikati ya kiambishi nafsi cha kitenzi na mzizi wa kitenzi.

    • Kwenye mzizi wa amba- na ndi -

    • Mwishoni mwa kitenzi

    Mifano mbalimbali kuhusu ngeli za majina husika.

    Ngeli ya majina Matumizi ya kirejeshi – o –

    LI-YA- : Swali ambalo litaulizwa na wengi ndilo litakalojadiliwa.

    zaidi – Maswali ambayo yataulizwa na wengi ndiyo yatakayojadiliwa zaidi.

    KI-VI- : Kikulacho kinguoni mwako – Vikulavyo vingoni mwako.



    MWELEKEO WA MAELEZO

    i) UHAKIKI WA HADITHI FUPI NA RIWAYA

    Kwa kawaida, uhakiki wa kazi za fasihi andishi hutegemea FANI na MAUDHUI.

    A. MAMBO MUHIMU YA KUZINGATIA KATIKA UHAKIKI WA FANI

    Kama sura ya nje ya hadithi fupi au riwaya, fani hufanyiwa uhakiki kwa kuzingatia

    vipengele fifuatavyo:

    –– Wahusika

    –– Muundo

    –– Lugha

    –– Mtindo

    –– Mandhari

    a) WAHUSIKA: Ni watu au viumbe waliokusudiwa wawakilishe tabia za watu

    katika kazi za fasihi.

    Aina za wahusika: Wahusika wa hadithi fupi au riwaya hujigawa katika

    makundi makuu mawili:

    Wahusika wakuu: Mhusika mkuu ni mhusika mmoja au wawili ambao hujitokeza

    kutoka mwanzo hadi mwisho wa hadithi fupi.

    Wahusika wadogo: Ni aina ya wahusika muhimu sana ambao humsaidia

    mhusika mkuu kuipa hadithi au riwaya mwelekeo wa kisanaa na kimaudhui.

    Tabia za wahusika: Kutokana na majukumu yao, wahusika huonyesha tabia

    za aina tatu:

    Wahusika bapa: Ni aina ya wahusika ambao hawabadiliki kitabia kutoka

    mwanzoni mpaka mwishoni mwa hadithi fupi.

    Wahusika duara: Ni wahusika ambao wanabadilika kitabia kutokana na

    mabadiliko ya mazingira.

    Wahusika foili: Ni wahusika wenye tabia zinazobadilika kinusu. Wako kati ya

    wahusika bapa na wahusika duara.

    b) MUUNDO: Ni namna msanii anavyopanga visa vyake au fikra zake katika

    hadithi fupi, yaani mtiririko wa visa na matukio. Kinachozingatiwa hapa ni jinsi

    mwandishi alivyopanga kazi yake; mfano sura na sura, kisa na kisa au tukio

    na tukio.

    c) LUGHA: Kipengele cha lugha ni muhimu sana katika fasihi kwani ndicho

    hutenganisha fasihi na sanaa nyinginezo. Matumizi ya lugha katika fasihi yapo

    ya aina mbalimbali: kuna tamathaili za semi, misemo, nahau, methali, lahaja za

    wahusika, uchaguzi wa msamiati, miundo ya sentensi.

    Mifano ya tamathali za semi:

    • Tanakali za Sauti: Ni mbinu ya kutumia maneno yanayoiga sauti au

    hali fulani au namna kitendo kilivyofanyika.

    Mfano: anguka pa!

    • Tashbiha: Hii ni mbinu ya lugha inayolinganisha vitu au hali mbili tofauti

    kwa kutumia maneno ya kulinganisha; ‘kama’, ‘mithili ya’, ‘sawa na’.

    • Tashihisi: Hii ni mbinu ya kupatia kitu kisicho hai sifa za kiumbe mwenye

    uhai (sifa za kibinadamu).

    • Takriri: Ni mbinu ya kurudiarudia neno moja au kifungu cha maneno ili

    kusisitiza ujumbe fulani.

    • Ukinzani: Ukinzani ni mbinu ya kusisitiza ujumbe kwa kuambatanisha

    maneno ya kinyume au yanayokinzana.

    • Sitiari: Ni mbinu ya kulinganisha vitu viwili moja kwa moja kwa kutotumia

    viunganishi ambapo kitu kimoja hufanywa kuwa sawa kabisa na kitu

    kingine.

    • Taswira: Ni matumizi ya lugha/maneno yanayojenga picha ya hali au

    jambo fulani kwa msomaji.

    • Taashira: Ni matumizi ya lugha ya ishara kuwakilisha ujumbe fulani. Jina

    au kitu fulani kinatumika kumaanisha kitu kingine chenye uhusiano na

    kile kilichotumiwa.

    • Majazi: Majazi ni pale tabia za wahusika zinapoambatana na majina

    yao halisi.

    • Lakabu: Ni mbinu ya mhusika kupewa/kubandikwa jina na wahusika

    wengine ama yeye mwenyewe kujibandika jina linalooana na tabia/sifa

    zake.

    Chuku: Ni kutumia maneno yaliyotiliwa chumvi ili kusisitiza ujumbe

    fulani au kusifia kitu, kutilia chumvi.

    d) MTINDO: Mtindo ni namna ambavyo mwandishi huipa hadithi yake sura ya

    kifani na kimaudhui.

    Mtindo ndio unaotofautisha wasanii. Katika mtindo tunachunguza sana

    matumizi ya lugha.

    e) MANDHARI: Mandhari ni mazingira au mahali tukio la hadithi fupi lilipotokea.

    Kuna mandhari ya kubuni na mandhari ya kweli.

    B. MAMBO MUHIMU YA KUZINGATIA KATIKA MAUDHUI

    Maudhui ni jumla ya mawazo yote yanayozungumzwa katika kazi ya fasihi.

    Hujumuisha mawazo pamoja na mafunzo mbalimbali yaliyomsukuma msanii hadi

    akatunga na kusanii kazi fulani ya kifasihi. Mawazo na mafunzo haya hayazuki

    hivihivi tu. Kwa hiyo wakati wa kuyachambua na kuyajadili ni lazima yahusishwe

    na hali halisi ya kisiasa, kiutamaduni na kiuchumi zilizopo katika jamii, hali hizi

    ndizo zilimzaa, zilimlea na kumkuza msanii.

    Wakati wa kuchambua kazi za kifasihi mhakiki ni lazima ajiulize amaswali

    yafuatayo:

    -- Je, msanii anatueleza nini?

    -- Je, msanii kamtungia mtu wa tabaka gani?

    -- Anamtukuza nani?

    -- Anambeza nani?

    -- Msanii anataka tuchukue hatua gani katika utatuzi wa matatizo

    ayashughulikiayo katika kazi yake?

    Maudhui hujengwa na vipengele muhimu vifuatavyo: Dhamira, ujumbe,

    migogoro, msimamo wa msanii pamoja na falsafa yake.

    a) Dhamira: Ni mawazo yanayojitokeza sana katika kazi ya fasihi. Ni jumla
    ya maana anayoivumbua mwandishi aandikapo, na jumla ya maana
    anayoitambua msomaji katika usomaji wake.
    Kifasihi kuna aina mbili za dhamira yaani dhamira kuu na dhamira ndogondogo
    Dhamira kuu ni kiini cha kazi ya fasihi, ni wazo kuu.
    Dhamira ndogondogo ni mawazo madogomadogo ambayo hujenga dhamira
    kuu.
    b) Migogoro: Ni hali ya kutoelewana baina ya pande mbili yaani mtu na mtu,
    mtu na kikundi au mtu mwenyewe na nafsi yake. Migogoro ni mivutano na
    misuguano mbalimbali katika kazi za fasihi. Migogoro inaweza kuwa kati
    ya wahusika, familia zao au matabaka yao. Migogoro hii inaweza kuwa ya
    kiuchumi, kijamii, kisiasa, kiutamaduni, kifalsafa, n.k.
    c) Ujumbe: Ni funzo na maadili yaliyokusudiwa na mtunzi yaifikie jamii
    aliyoilenga kufikisha kazi yake ya fasihi.
    d) Falsafa: Ni imani na mwelekeo wa mwandishi kuhusu maisha katika jamii.
    e) Msimamo wa msanii: Msimamo wa msanii kuhusu masuala mbalilmbaili
    ya kijamii hubainishwa na mawazo, mafunzo, lengo na falsafa. Msimamo
    ndio uwezao kuwatofautisha wasanii wawili au zaidi wanaotunga kazi
    za fasihi zilizo na kiini na chimbuko moja. Kwa hiyo, msanii huweza
    kuchukua msimamo wa kimapinduzi au wa kiyakinifu kulingana na jinsi
    anavyoyazingatia maisha ya jamii inayozungumziwa.

    C. MAMBO MUHIMU YA KUZINGATIA KATIKA TAMTHILIA
    Tamthilia au mchezo wa kuigiza huweza kuhakikiwa jukwaani au kupitia maandishi.

    a) Uhakiki wa Kifani
    Wahusika: Wahusika katika tamthilia huwa wengi pamoja na tabia zao
    mbalimbali.Tamthilia huwa na wahusika halisi ambao wanajitetea jukwaani
    kimatendo na kitabia wakati.

    Muundo: Tamthilia huwa na sehemu tatu: Mwanzo, Katikati na Mwisho.
    Sehemu zake zinatazamiwa kuingiliana, kujengana na kukamilishana. Muundo
    katika tamthilia huangaliwa kwa kuzingatia idadi ya vitendo/ sehemu na idadi ya
    maonyesho.

    Mtindo: Tamthilia huwa na mgawiko wazi wa matendo na matukio kwa mujibu
    wa sehemu na sura mbalimbali. Majina ya wahusika huandikwa katika upande
    wa kushoto, kisha koloni, halafu hufuatiwa na maneno halisi yaliyotamkwa na
    mhusika huyo.

    Lugha: Tamthilia inatawaliwa na lugha ya mazungumzo katika majibizano au
    hata mazungumzo pweke. Ucheshi, porojo au mizaha, tamathali za usemi na
    onomatopia hutumiwa sana.
    D. UHAKIKI WA MASHAIRI
    Sawa na kazi nyingine za fasihi, uhakiki wa mashairi huzingatia fani na maudhui.

    a) Fani

    Uhakiki wa fani ya shairi huzingatia muundo wake, yaani jinsi shairi lilivyoundwa
    kwa kuangazia mizani, vina, mishororo n.k Aidha, ni muhimu kutaja aina na bahari
    za shairi zinazohusiana na kila sifa uliyoitaja.

    Idadi ya mishororo katika kila ubeti - Tumia idadi ya mishororo kubainisha
    aina ya shairi hilo.

    Kwa mfano: Shairi lina mishororo minne katika kila ubeti, kwa hivyo ni Tarbia.
    Idadi ya mizani katika kila mshororo na katika kila kipande cha
    mshororo.

    Kwa mfano: Kila mshororo una mizani kumi na sita: nane katika utao na nane
    katika ukwapi.
    Idadi ya vipande katika kila mshororo - Taja ikiwa shairi lina kipande
    kimoja, viwili, vitatu au vinne kisha utaje bahari yake.

    Kituo, kiishio au kibwagizo - Ikiwa mstari wa mwisho umerudiwa rudiwa,
    basi shairi lina kibwagizo au kiitikio, la sivyo lina kiishio.

    Vina - Zingatia vina vya kati na vya mwisho kutoka ubeti mmoja hadi mwingine.
    Kisha utaje ikiwa ni Mtiririko, Ukara au Ukaraguni.

    Matumizi ya lugha: Mtindo wa lugha hurejelea namna mbalimbali ambazo
    mshairi anatumia mbinu za lugha. Mshairi anaweza kutumia mbinu za lugha.
    kama vile: Tanakali za sauti, Tamathali za semi, n.k.

    Katika mtindo wa lugha mhakiki huchunguza uhuru wa msanii, yaani mshairi
    hafungwi na kanuni za kisarufi za lugha katika utunzi wa shairi. Anaweza kufanya
    makosa ya kisarufi kimakusudi ili shairi lizingatie umbo fulani.

    b) Maudhui
    Uhakiki wa maudhui ya shairi huzingatia vipengele vikuu ambavyo ni Dhamira

    (Dhamira kuu na dhamira ndogondogo) pamoja na Ujumbe.

    


    SOMO LA 18: MFANO WA UHAKIKI WA TAMTHILIA
    18.1. Kusoma na Ufahamu: Muhtasari wa Hawala ya Fedha

    Familia ya Mzee Ibrahim CHANDE imetumiwa hawala ya fedha na mpwaye
    anayesomea mjini London. Thamani ya hawala hiyo ni shilingi elfu mbili. Ibrahim
    CHANDE anapaswa kuchukua kiasi cha shilingi mia tatu, kiasi kingine cha
    shilingi miatano ampatie mama yake Abdul, mia tano zinazobakia amwekee
    mpwa wake.

    Hawala hii inaleta matumaini katika familia ya Ibrahim CHANDE. Familia
    nzima wanafikiri kwamba umaskini na njaa vimemalizika. Kwa kuwa wake zake
    CHANDE walitafuta mtu wa kuwasomea hawala ya fedha (kwa kuwa wao
    hawakujua kusoma wala kuandika), habari inazagaa mahali pote na majirani zote
    wanaarifiwa.

    Watu kadha wa kadha wanakuja kukopa fedha na chakula kwenye familia
    hiyo. Wengine wanamfuata Ibrahim CHANDE kila anapokwenda ili awasaidie
    kutokana na fedha hizo.

    Inambidi Ibrahim CHANDE aende kubadilisha hawala ya fedha posta. Anapofika
    anaombwa kuwa na kitambulisho lakini anakikosa. Hana kitambulisho chochote
    kile ila kadi ya chama isiyo na picha. Hivyo analazimika aende kwenye kituo cha

    polisi.

    Anapofika, anaelezwa kuwa hawezi kuwa na kitambulisho kama hana picha.
    Ibrahim CHANDE anamwendea AMBROZI ambaye ni mpigapicha. Anampiga
    picha na kumwambia kurudi kesho yake baada ya kulipa shilingi thelathini. Kwa
    bahati mbaya, anaporudi AMBROZI huyu anamnyang’anya picha pamoja na
    pesa zake.

    Siyo hayo tu, bali anamfanyia mabaya zaidi. MBAYE anajitolea kumsaidia
    CHANDE kutoa fedha kwenye posta. Kwa upande mwingine, dada yake
    CHANDE, yaani Mama Abdul, anakuja kudai pesa zake zilizoelezwa kwenye
    barua iliyokuja pamoja na hawala hiyo.

    Mzee huyo inambidi auze hereni za dhahabu za mkewe ili dada yake asiende
    mikono mitupu. Ibrahim CHANDE hapumziki hata kidogo. Mwishowe, MBAYE
    aliyejidai kumsaidia anamwambia kuwa fedha alizichukua kutoka posta lakini
    akanyang’anywa na wezi akiwa njiani.

    Matumaini yote ya Ibrahim CHANDE pamoja na wake zake yakafifia. Amne mke
    wake wa pili akaamua kwenda zake na Mama Dogo, mke wake wa kwanza

    akaenda kijijini kulima shamba.




    Maelezo muhimu ya kuzingatia
    Kiambishi rejeshi – o – kimehusishwa na majina ya ngeli za majina ya U-I na
    U-ZI. Kimetumiwa kama ifuatavyo:
    • Katikati ya kiambishi nafsi cha kitenzi na mzizi wa kitenzi.
    • Kwenye mzizi wa amba- na ndi-

    • Mwishoni wa kitenzi

    Mifano mbalimbali kuhusu ngeli za majina husika

    U-I- : Mti ulioanguka umefunga njia – Miti iliyonguka imefunga njia.

    Mti ulioanguka ndio uliofunga njia – Miti iliyoanguka ndiyo iliyofunga njia.

    U-ZI- : Tumenunua uzi unaoonekana vizuri - Tumenunua nyuzi zinazoonekana

    vizuri.


    MWELEKEO MUHIMU

    UHAKIKI WA FANI

    1. Wahusika na tabia zao

    a) Wahusika wakuu

    Ibrahim CHANDE ndiye mhusika mkuu katika tamthiliya “Hawala ya fedha”. Ana
    wake wawili: MAMA DOGO na AMNE. Habadiliki kitabia tangu mwanzo hadi
    mwisho wa mchezo, yeye ni mhusika bapa. Ubapa wake unadhihirishwa na
    ujinga wake anaokumbana nao katika habari yote. Mhusika huyu hajui kusoma
    wala kuandika. Isitoshe, hataki pia wake zake wawe na kisomo (uk. 4). Kwa kuwa
    inaruhusiwa katika dini ya Uislam, Ibrahim CHANDE ana wake wawili. Katika
    usemi wake wote kuna rejesta ya dini. Pengine anaonekana akitoa sadaka kwa

    maskini, wengine anakataa kuwapa.

    Isipokuwa ujinga wake wa kutojua kusoma na kuandika, mzee huyu anaonyesha
    moyo wa kusikiliza shida za watu wengine hasa hasa wale wanaotaka msaada
    kutoka kwake.

    b) Wahusika wadogowadogo au wasaidizi
    i) Mama Dogo: Huyu ni mke wa kwanza wa Ibrahim CHANDE. Yeye na Amne
    ni wake wenza. Hali yao ya uke wenza haiwatenganishi wala kuwafanya
    wachukiane. Wanaonyesha ushirikiano tangu mwanzo hadi mwisho wa
    mchezo. Mama Dogo anaonyesha busara katika maneno yake. Mfano
    bayana ni usemi wake (uk. 41), pale ambapo anasema:”Afugaye punda
    lazima ampendelee mlimaji nyasi. ” Katika usemi huu alitaka kuonyesha
    namna ambavyo hakuna mtu pekee anayeweza kujitosheleza. Kama mtu
    ana duka, anategemea wale ambao wanakuja kununua vitu katika duka hilo.

    Kwa sababu hiyo, mtu yeyote anapaswa kutodharau mwenzake. Kila wakati,
    Mama Dogo anaonekana akimtetea mumewe. Anaonekana akihangaishwa
    na usalama wa mumewe. Ili watu wasiendelee kumfuata Ibrahim CHANDE
    kwa ajili ya fedha, yeye alibuni kisingizio na kuwaambia watu kuwa mume
    amenyang’anywa fedha hizo (uk. 36-38). “Alipopata pesa watu wakamvamia
    (uk. 36).” “Majangili ndugu yakamvamia. Hata senti moja si yake. Mungu na
    Mtume, sasa pesa zimekwenda na heshima yetu pia imekwenda.” Pengine
    Mama Dogo anaonyesha imani katika Mungu. Anaamini kuwa Mwenyezi
    Mungu hasahau waamini wake (uk. 1). Yeye ndiye anaweza kunusuru maisha
    ya mtu aliye hatarini (uk. 37).

    ii) AMNE: Huyu ni mke wa pili wa Ibrahim CHANDE, yaani mke mwenza
    wa Mama Dogo. Tabia yake inaonyeshwa na ushirikiano anaokuwa nao
    kati yake na Mama Dogo mbele ya mume wao. Amne ana tamaa ya kuwa
    na kisomo. Anamwona mumewe kama mjinga wakati wowote anapomzuia
    kwenda kusoma. Mwishoni mwa mchezo, anaonyesha tabia ya kutoweza
    kuvumilia hali ya umaskini na njaa inayojitokeza katika familia yake. Alipokata
    tamaa ya kupata fedha zilizokuwa kwenye hawala iliyotumwa na Abdul,
    yeye aliamua kumtoroka mumewe.

    iii) Mbarka: Ni mwenye duka. Kutokana na mazingira au hali mbalimbali,
    yeye anabadilika kitabia. Wakati alipojua kuwa Ibrahim alikuwa na hawala
    ya fedha, alifurahi sana na kumkopa mchele bila wasiwasi. Lakini alipopata
    habari kuwa pesa za Ibrahim zimeibiwa, alikasirika na kuanza kumdai kwa
    fadhaa. Mbarka anaonyesha tabia za uduara.

    iv) Issa: Huyu ni rafiki yake Ibrahim CHANDE. Urafiki wao unatokana na
    kuwa Issa anataka sehemu ya fedha alizonazo Ibrahim. Yeye anaonyesha
    tabia ya unyonyaji. Kila alipoongozana na Ibrahim wakienda mjini, alitaka
    Ibrahim amlipie basi. Unyonyaji wake unaonyeshwa pia na kunyang’anya
    watu akitumia ujanja (uk. 16). Yeye alikuwa anaganda kwenye Ibrahim

    kama rubu ama kupe wagandavyo kwenye ng’ombe.


    v) Ambrozi: Ni mwenye studio. Yeye anaonyesha tabia ya kunyanyasa watu
    duni. Yeye ni mjangili: anachukua pesa za watu kwa bure na kuwadhulumu
    ili wasije wakamdai fedha zao. Lugha anayoitumia ni ya matusi. Amandina
    Lihamba alitumia katika mchezo wake wahusika wengine wa aina mbalimbali
    ili kuonyesha hali halisi ya maisha. Mojawapo wa wahusika hao ni bapa
    vielelezo. Majina yao yanaonyesha shughuli au tabia zao. Hao ni kama
    mchuuzi, polisi, karani, maskini na kadhalika. Mhusika Abdul anasimamia
    kundi la watu waliopata kisomo. Yeye anajua umuhimu wa kusoma, ndiyo
    sababu alienda Landon. Vilevile, anajua wazazi wanahitaji msaada kutoka
    kwa watoto wao wakati wakiwa na uwezo. Kwa sababu hiyo, alitumia
    mjomba wake pamoja na mama yake hawala ya fedha.

    2. Mtindo
    Mtindo ni kiwango cha lugha alichotumia mwandishi katika Hawala ya fedha.
    Lugha inayotumiwa ni ya mazungumzo kwani kitabu hiki ni cha mchezo wa
    kuigiza, yaani tamthiliya. Vipengele vya lugha vilivyotumiwa na msanii ni tamathali
    za usemi, nahau, methali, misemo na rejesta. Pengine alitumia lugha ya kawaida,

    lugha inayoeleweka kwa wazungumzaji wengi wa lugha hiyo.
    Tamathali za usemi

    a) Sitiari: mifano, - Umaskini bila nyumba ni kifo - Madeni yatushika mpaka
    pwani - Ndiye shetani mkubwa. b) Tashibiha - Kukusanyika kama sisimizi,
    (uk. 3) - Asiponilipa haraka nitamganda kama rubu, (uk. 16)

    ii) Methali - Kutoa ni moyo si utajiri, (uk. 13) - Ulimi hauna mfupa: ulimi
    husema yote, yaani mazuri na mabaya. - Dawa ya moto ni moto: kwa tatizo
    nzito lazima kauli nzito.

    iii) Nahau - Kutia chumvi, - Chungu nzima, - Kukata kauli, - Kuwa na mkono
    mrefu (kuwa na huruma kwa kila mtu), - Kuwa na mkono wa birika (kinyume
    na kuwa na mkono mrefu), - Kukata tamaa, - Kufariki dunia/kuaga dunia.

    3. Muundo
    Msanii alitumia muundo wa moja kwa moja, yaani hakufanya mazungumzo
    yanayoweza kutatanisha msomaji. Visa na matukio muhimu vya kuzingatia
    katika Hawala ya fedha ni hivi vifuatavyo: - Taarifa inayomfikia Ibrahim CHANDE
    yenye ujumbe wa kupelekewa hawala ya fedha na kuwa postani. - Tumaini la
    kuwa hawala ya fedha ingemwokoa toka hali yake ya umaskini, - Kupanda kwa
    madeni, - Harakati za kubadilisha hawala hiyo, - Kupanda kwa tumaini la Ibrahim,
    - Matumaini ya kupata vitambulisho, - Kupatikana kwa fedha na kuibiwa kwake
    (Upeo wa habari), - Kushuka chini kwa tumaini. Msanii amefaulu kujenga kiini

    kimoja kutokana na mchanganyiko wa matukio mbalimbali.

    4. Mandhari
    Mandhari inayozungumziwa mchezoni ni halisi. Kama tulivyoelezwa na mwandishi,
    habari hii inatokea katika mji mdogo pwani mwa Afrika Mashariki.

    U
    HAKIKI WA MAUDHUI
    Katika uchunguzi wa maudhui ya mchezo wa Hawala ya fedha tunachambua
    dhamira kuu pamoja na dhamira ndogo.

    Dhamira kuu
    a) Unyonyaji na kuharibika kwa urasimu
    Unyonyaji ni hali ya kutegemea wengine bila ya kufanya kazi; ni hali ya kuishi kwa
    jasho la mwingine. Katika tamthiliya Hawala ya fedha, unyonyaji unadhihirishwa
    na hasa hasa na majirani wa Ibrahim CHANDE wanaotaka awasaidie kwa kila
    hali baada ya kupata habari kuwa ametumiwa hawala ya fedha. Kuna wanaotaka
    awakopeshe mchele na wengine fedha kiasi kwamba angetimiza hoja zao angebaki
    mikono mitupu. Mhusika anayeonekana kuwa mnyonyaji kuliko wengine ni ISSA.

    Huyu anamsindikiza Ibrahim CHANDE katika harakati za kubadilisha hawala ya
    fedha ili apate fedha. Kila wanapoenda, ISSA anataka Ibrahim amlipie basi. Si
    hayo tu, anataka ampatie fedha za kutumia katika shughuli mbalimbali. Watu
    wengine wanaodhihirisha unyonyaji ni msichana aliyekutana na Ibrahim CHANDE
    akimuomba msaada kwa mara nyingi. Pengine ni Ambrozi, aliyemnyang’anya
    pesa zake alipoenda kujipigisha picha. Mhusika mwingine ni MBAYE aliyefaidi
    hawala isiyokuwa yake. Kwa upande mwingine kuna katika mchezo huu, hali ya
    kuharibika kwa urasimu. Ijulikane kuwa urasimu ni utaratibu wa kuendesha kazi
    za kiofisi kulingana na kanuni za kiutawala. Katika mchezo (tamthiliya) Hawala ya
    fedha kuharibika kwa urasimu kunatambulika kutokana na viongozi (makarani).

    Hawa hawafanyi kazi yao kama ilivyo. Hawakutaka kuendesha haraka mambo ya
    hawala ya fedha ya Ibrahim ili yeye awapatie rushwa.

    b) Ujinga
    Ujinga unatokana na tabia ya Ibrahim: kutojua kusoma, kukosa vitambulisho
    ambavyo ni mambo muhimu ya raia. Kwa ajili ya kutojua, ilimbidi Ibrahim
    kusomesha barua yake iliyohusu Hawala ya fedha. Habari hiyo ilipaswa kuwa

    siri lakini ilisambaa katika kijiji kizima kutokana na kuwa barua imesomeshwa.

    Dhamira ndogo
    -- Mvutano baina ya vizazi (vijana mbele ya wazazi)
    Mvutano huu unaelezwa na msichana mmoja aliyetukana Ibrahim baada ya
    kujionyesha mbele yake akitaka msaada na kunyimwa. Matusi yake yalienda
    pamoja na kumsingizia kuwa alitaka kumtongoza. Mvutano unaonekana pia

    kutokana na tabia ya Ambrozi aliyempiga Ibrahim badala ya kumpa picha zake.
    Alionyesha dharau kubwa mbele yake mzee.

    -- Nafasi ya mwanamke katika jamii
    Katika nchi nyingi za Afrika, mwanamke huonekana kama kiumbe duni. Mambo
    yanayokuwa vilevile katika Hawala ya fedha. Ibrahim anaonyesha dharau lakini
    wanawake hawa wanaonekana kuwa washauri wa nafasi ya kwanza wa mume
    wao.

    AMNE anaonekana kujikomboa kutoka dharau hiyo. Katika kitabu hiki, wanawake
    wengine huonekana wakitaka kusitisha mambo ya rushwa.

    -- Nafasi ya fedha katika maisha ya kila siku
    Dhamira hii inajidhihirisha katika matukio mengi ya habari hii. Kusomesha barua
    lazima fedha, kutafuta vitambulisho ni fedha, picha, chakula, safari katika basi ni
    mambo hayo hayo. Inadhihirika kuwa watu wote wametekwa na tamaa ya fedha
    ili waweze kufanya shughuli zao mbalimbali. Mfano wa watu wanaotamani fedha
    kuliko wengine ni ISSA. Huyu anatumia hila ili aweze kuzipata.

    Migogoro
    Tamathiliya hii ina migogoro kadhaa ambayo inajitokeza katika jamii.
    Mgogoro wa kiuchumi ni wa kwanza kuonyeshwa. Mgogoro huu unaiathiri jamii
    kwa kiwango kikubwa. Wenye nacho wameonyeshwa kuwa ndio wanyanyasaji
    wakubwa wa watu wa chini. Mwandishi anaelekea kueleza kwamba si sawa
    kuwa na matabaka ya wafanyakazi na wafanyiwa kazi, yaani, mabwana na
    watwana (uk.38).

    Mgogoro mwingine unatokana na hali ya mazingira kati ya ukale na
    usasa. Mwandishi anaelezea athari za kutojua kusoma na kuandika katika jamii.

    Kwa upande mmoja kuna watu wangependa kusoma, wengine hawataki.

    Ujumbe
    Tamthiliya ya Hawala ya Fedha ina ujumbe ufuatao:
    -- Ni vema kuwa na busara katika utekelezaji wa mambo.
    -- Elimu ni ufunguo wa maisha. Ni vema kuwa na tahadhari wakati wa
    matumizi ya fedha.
    -- Uvivu ni kikwazo kikubwa kwa maendeleo ya jamii.
    Falsafa
    Hawala ya Fedha ni tamthiliya inayoonyesha falsafa ya mapambano dhidi ya
    unyonge. Msimamo wa mwandishi na falsafa yake juu ya maisha ni kuwa watu
    wasikate tamaa wanapokutana na matatizo. Utatuzi wa matatizo si wa siku moja,

    unachukua muda na hatimaye ushindi lazima upatikane.

    19.1. Kusoma na Ufahamu: Kila Mtoto na Koja Lake
    Rubyogo lilikuwa jina la kupanga la bwana Ndizihiwe. Wengine walikuwa
    wanamwita Nyangufi. Majina haya aliyapewa utotoni mwake alipokuwa na umri
    wa miaka mitatu. Asili ya jina hili ilielezwa na kimo chake: Ndizihiwe alikuwa
    mfupi sana na mwembamba. Aliyekuwa amemwona hakuwa anaamini kwamba
    siku moja mtoto huyu atafikia kuwa mtu mzima. Wazazi wake walikuwa wakiishi
    kwa mnung’uniko na fedheha katika kijiji cha Shengerero, Jimbo la Kusini nchini
    Rwanda.

    Ntawiheba (kifupi cha Ntawihebagihumeka) na mkewe Bazubagira walikuwa
    wazazi wa Rubyogo. Huyu alikuwa mtoto wa pekee. Familia ya Rubyogo
    ilikuwa inaishi kwa kutegemea kilimo tu. Wakati mmoja wazazi wake walikuwa
    wakifurahia mavuno ya kilimo chao na wakati mwingine kulalamikia hali ya hewa.
    Mathalan, hali hii ya malalamiko ilikuwa ikijitokeza hususan wakati wa maafa.

    Ntawiheba na mkewe walifanya bidii kwa kumlea ipasavyo mtoto wao. Walimpatia
    maadili toka utotoni hadi alipoanza elimu ya msingi. Ntawiheba na Bazubagira
    walikuwa wanapendana sana na kushirikiana katika kazi zote za kijamii. Majirani
    zao walikuwa wakiitamani familia yao. Aidha, Ntawiheba na mkewe walikuwa

    kielelezo cha familia yenye kuishi kwa amani na masikilizano.

    Siku moja alipokuwa katika kazi ya kupalilia migomba, Ntawiheba alipata fursa
    ya kuwaza juu ya maisha ya familia yake kwa siku za baadaye. “Je, ni jambo
    la busara kweli kumzaa mtoto mmoja tu na tena mwenye ulemavu wa kimo?”
    Alijinung’unikia. Wazo la ukewenza lilimtawala sana na kumsumbua kupita
    kipimo.
    Alipofika nyumbani jioni, mkewe alimkaribisha kwa chakula cha mchana lakini
    yeye alikipokea kwa shingo upande. Mkewe alipomtupia maneno ya utani,
    mumewe hakumwonyesha jino. Aliendelea kuonyesha hali ya kukasirika na
    kukosa furaha moyoni mwake. Hali hii ilimkera mkewe na kumsogelea, “Mume
    wangu mpendwa, mbona hali yako leo imenitisha? Ni balaa ipi iliyokufikia siku ya
    leo?”, mkewe alimbembeleza.

    Ntawiheba alishindwa kuficha sababu za huzuni yake. “Mke wangu, miaka kumi na
    miwili imemalizika tangu siku yetu ya kufunga ndoa. Maisha tuliyo nayo leo unajua
    wazi haturidhiki nayo. Zaidi ya hayo, unaona jinsi mtoto wetu alivyo kimaumbile:

    mfupi mithili ya kinu! Unadhani kuwa Rubyogo atatufuta machozi kweli? Mimi
    ningependekeza nimwoe....” Anguka pa! Kabla hajakamilisha sentensi hii, mkewe
    alipatwa na mshituko na kuanguka chini kama mtu aliyepoteza fahamu. Mumewe
    huruma ilimwingia na kumhudumia kwa haraka. Alimwimbia wimbo mzuri sana
    wa kimapenzi, ule ule ulioimbwa siku ya ndoa yao. Punde si punde, Bazubagira
    alizinduka na kumwangalia mumewe machoni. Alimkumbatia na kuweka kichwa
    chake kifuani pa mumewe. “Mume wangu, ni shetani yupi aliyekutembelea leo?
    Kwa nini unataka nijitoe uhai kweli? Ni kosa gani nililokutendea kusudi uchukue
    uamuzi huo wa kuniletea mkemwenza wa kunitesa? Kwa nini hukubali kwamba
    mtoto ni sawa na mwingine hata akiwa na kasoro fulani? Mume wangu, kila
    mtoto na koja lake!”, Bazubagira aliongea kwa huzuni mno machozi yakimtoka
    machoni.

    Ntawiheba alipigwa na bumbuwazi kisha akaangua kilio. Hali hii ilirudisha
    kumbukumbu ya ahadi aliyoitoa siku ya ndoa yao mbele ya mkuu wa wilaya
    pamoja na mbele ya kasisi kanisani. Hivyo, alimwomba mkewe msamaha na
    kumwahidi kutofikiria tena hata siku moja mpango mbaya ule.

    Ndizihiwe alipoingia shule za sekondari alionyesha maarifa yasiyo ya kawaida.
    Toka mwaka wa kwanza hadi wa mwisho alikuwa akishika nafasi ya kwanza.

    Vilevile, alichaguliwa kuendelea na elimu katika chuo kikuuu huko Huye. Hapo
    alifanya maajabu zaidi! Mwishoni mwa masomo yake ilitangazwa nchini kote
    kuwa ndiye aliyejinyakulia shahada yenye alama za juu katika Kitivo cha Uhasibu.

    Miaka michache baadaye aliajiriwa kama meneja mkuu katika kampuni moja
    ya kuagiza bidhaa kutoka nje za nchi. Ndizihiwe alionyesha ubingwa sana
    katika kazi yake na kuongezewa mshahara wa kuridhisha. Aliwajengea wazazi

    wake nyumba ya kisasa na akawanunulia gari zuri la kutembelea. Leo wazazi

    wake Ndizihiwe wanaishi kwa kheri na fanaka wakifurahia kuwasimulia hadithi
    wajukuu wao wanne: Fany, Fils, Fiyette pamoja na Fisto. Katika masimulizi yao
    hawakusahau kusisitiza kuwa “Akiba haiozi” pamoja na “Mtoto umleavyo ndivyo
    akuavyo”.

    Maelezo muhimu ya kuzingatia
    Kiambishi rejeshi – o – kimehusishwa na majina ya ngeli za majina ya U- na PAM-
    KU. Kimetumiwa kama ifuatavyo:
    • Katikati ya kiambishi nafsi cha kitenzi na mzizi wa kitenzi.
    • Kwenye mzizi wa amba- na ndi-
    • Mwishoni mwa kitenzi

    a) Uzalendo ambao una maana ni ule kutoka nchi asili.
    b) Ushirikiano unaotakiwa kati ya mume na mke ndio utakaoimarisha uchumi
    wa nchi yetu.
    c) Mahali paliposafishwa ndipo pazuri.
    d) Chumbani mnamoingia ndimo mnamolala.
    e) Nchini tunamoishi ndimo tutakamofanikiwa.

    f) Mezani ambako kumewekwa vitabu kumesafishwa.

    MWELEKEO MUHIMU
    UHAKIKI WA FANI
    1. Wahusika na tabia zao
    a) Wahusika wakuu

    Ntawiheba pamoja na Bazubagira ndio wahusika wakuu katika hadithi fupi
    “Kila Mtoto na Koja Lake.” Ntawiheba ni mume wa Bazubagira. Ametawaliwa na
    tabia ya ufoili: mwanzoni alikuwa amevumilia hali ya familia yake hivi akisikilizana
    na mkewe. Baadaye amebadilisha mawazo na kutaka kumwoa mwanamke wa
    pili. Mwishoni amekubali kushawishiwa na mkewe na kutulia. Ni mwanamume
    mwenye huruma, mapenzi na msanii pia. Ameonyesha sanaa yake wakati
    alipomwiimbia mkewe wimbo wa mapenzi ili asiendelee kupoteza akili.

    Bazubagira ni mkewe. Yeye ameongozwa na tabia ya ubapa: habadiliki kimawazo
    na msimamo wake ni kumlea mtoto wao Ndizihiwe ingawa kimo chake kilikuwa
    kinaonekana kama kasoro. Ni mwanamke mwenye huruma na mapenzi: anatimiza
    ahadi la ndoa yake na mumewe.

    b) Wahusika wadogowadogo au wasaidizi
    Ndizihiwe ndiye mhusika msaidizi. Mtoto wa pekee wa bwana Ntawiheba na
    mkewe Bazubagira, Ndizihiwe ametumiwa na mwandishi kuendeleza mtiririko
    wa visa au matokeo. Iwapo kimo chake kinazusha dukuduku au fedheha katika
    familia yake, Ndizihiwe ni mtoto mwenye akili. Amemudu masomo yake na
    kupewa vyeo. Ni mtoto mwenye mawazo ya kimaendeleo na ya kijamii.
    2. Mtindo
    Mwandishi ametumia mtindo wa nathari, yaani aya. Lugha iliyotumiwa ni ya
    kawaida, rahisi kueleweka. Baadhi ya vipengele vya lugha vilivyotumiwa na
    msanii kuna tanakali za sauti tamathali za usemi, nahau, methali.
    Tanakali za sauti
    Mfano: Anguka pa !
    Konsonansi (mbinu ya kusawazisha konsonanti mwanzoni mwa neno) - Fils,

    Fiyette pamoja na Fisto.

    Tamathali za usemi
    a) Tashihisi (mbinu ya kupatia kitu kisicho hai sifa za kiumbe mwenye uhai
    (sifa za kibinadamu) - ni shetani yupi aliyekutembelea leo?
    b) Tashibiha (mbinu ya lugha inayolinganisha vitu au hali mbili tofauti kwa
    kutumia maneno ya kulinganisha; ‘kama’, ‘mithili ya’, ‘sawa na’) - mfupi
    mithili ya kinu.
    i) Methali – Kila mtoto na koja lake; Akiba haiozi; Mtoto umleavyo ndivyo
    akuavyo.
    ii) Nahau – kufanya bidii, kupokea kwa shingo upande, kuonyesha jino,
    kufunga ndoa, kufuta machozi, kujitoa mhanga, kupatwa na bumbwazi.
    3. Muundo
    Msanii ametumia muundo wa moja kwa moja, yaani hakufanya mazungumzo
    yanayoweza kutatanisha msomaji. Mtiririko wa visa na matukio muhimu
    umejitokeza kama ifuatavyo :

    -- Asili ya jina la Rubyogo
    -- Maisha ya familia ya Ntawiheba na mkewe Bazubagira
    -- Elimu na mafanikio ya Ndizihiwe
    -- Upeo: Hali ya kheri na furaha katika familia ya Ndizihiwe na wazazi wake.
    4. Mandhari
    Hadithi fupi imetokea katika kijiji cha Shengerero, jimbo la kusini nchini Rwanda.
    UHAKIKI WA MAUDHUI
    Dhamira kuu
    a) Haki za Watoto
    Mtoto yeyote anastahili kupewa haki zake zote za kimaisha hata akiwa na ulemavu.
    Ingawa Ndizihiwe alikuwa na ulemavu wa kimo alijiamini katika masomo yake
    pamoja na kazi zake na kufurahia baadaye matokeo mazuri.
    b) Maadili Mema
    Malezi bora kwa watoto huchangia kukuza akili na mienendo mizuri. Ndizihiwe

    alipata manufaa kutokana na maadili aliyopewa na wazazi wake.

    Dhamira Ndogo
    -- Mapenzi ya ndoa
    Ntawigira na mkewe wasingelikuwa na mapenzi ya ndoa hawangelisikilizana
    baada ya Ntawigira kubadilisha mawazo yake ya kutaka kumwoa mke wa pili.
    Wimbo wa mapenzi aliomwimbia Bazubagira na kumfanya apate nafuu.

    -- Uwazi
    Mume na mke wanapaswa kuwa wazi katika mawasiliano yao ya kila siku. Jambo
    la Ntawiheba kutoboa siri la mpango wake kwa mkewe lilichangia kupata suluhu
    la mzozo uliokuwa umezuka.

    -- Ukewenza
    Dai la Ntawiheba kwamba kumwoa mke wa pili kutakuwa suluhisho la matatizo
    katika jamii yake lilibanwa na pingamizi ya sheria. Hivyo sheria katika Jamhuri ya
    Rwanda haikubali utamaduni wa ukewenza.

    -- Umuhimu wa elimu
    Baadaya ya kuhitimu masomo ya uhasibu katika chuo kikuu, Ndizihwe alipata
    kazi katika kampuni ya kuagiza bidhaa kutoka nje ya nchi. Alipewa mshahara wa
    kuridhisha akawajengea wazazi wake nyumba ya kisasa na akawanunulia gari la
    kutembelea

    Migogoro
    Hadithi fupi imeizingatia migogoro mbalimbali:
    Mgogoro wa kijamii: Kimo cha Ndizihiwe kilileta hali ya manung’uniko na
    fedheha katika jamii yake;

    Hali ya maisha ilimfanya Ntawiheba akimbilie kwenye suluhu ya ukewenza.
    Mgogoro wa kisheria na kidini : Ahadi ya ndoa serikalini na kanisani ilikuwa
    kizuizi kwa uamuzi wa Ntawiheba kumwoa mke wa pili.
    Mgogoro wa kielimu : Mafanikio katika familia nyingi hutokana na kiwango
    cha elimu wanajamii walicho nacho. Mathalan, Ndizihiwe alifaidika katika maisha

    yake kutokana na elimu yake.

    Ujumbe

    -- Watoto wote wanapaswa kuwa na haki sawa hata walemavu

    -- Wazazi wana jukumu la kuwapatia watoto wao maadili

    -- Elimu ni msingi wa maendeleo ya jamii.

    -- Mvumilivu hula mbivu.

    Falsafa

    Msimamo wa mwandishi na falsafa yake ni kwamba mtu yeyote, apende asipende,
    huwa na nguvu kama sifa pamoja na udhaifu kama kasoro. Kwa hiyo, litakuwa
    jambo la aibu kumnyima au kumnyanyasa mtu haki zake kwa kupitia vigezo vya
    kimaumbile, kiafya, kikabila, kidini, kijamii, n.k. Hakuna mtu anayeweza kuthubutu
    kudai kuwa huyu au yule atakuwa nini wakati ujao au atafaulu hiki na kushindwa
    kile. Pengine, si vizuri kuzubaika mno kwa maisha uliyonayo leo kwa sababu

    hujui kitakochotokea kesho au kesho kutwa.

    MAREJEO
    Bakhressa,S.K. na Wenzake (2008). Kiswahili Sanifu. Kitabu cha Mwanafunzi.
    Darasa la Saba. Oxford University Press, East Africa Ltd, Elgon Road, Upper
    Hill, Nairobi, Kenya.

    Bakhressa, S.K. na Wenzake (2008). Kiswahili Sanifu. Kitabu cha Mwanafunzi.
    Darasa la 8. Oxford University Press, East Africa Ltd, Elgon Road, Upper Hill,
    Nairobi, Kenya.

    Hererimana, F. (2017). Tujivunie Lugha Yetu. Kitabu cha Mwanafunzi, Kidato
    cha 5. MK Publishers (R) Ltd. Kigali, Rwanda.

    Kenya Literature Bureau (2006). Kiswahili kwa Darasa la nane. Kitabu cha
    Wanafunzi. Kenya Literature Bureau, Nairobi, Kenya.
    Kihore, Y.M. na Wenzake (2012). Sarufi Maumbo ya Kiswahili Sanifu, Sekondari
    na Vyuo. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,
    Tanzania.

    Massamba, D.P.B. na Wenzake (2009). Sarufi Miundo ya Kiswahili Sanifu,
    Sekondari na Vyuo. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dar es
    Salaam, Tanzania.

    Ndalu, A.E. (2016). Masomo ya Kiswahili Sanifu. Kitabu cha mwanafunzi.
    Kidato cha 2. Moran (E.A) Publishers Limited.

    Niyirora, E. & Ndayambaje, L. (2012). Kiswahili Sanifu kwa Shule za Sekondari.
    Kitabu cha Mwanafunzi kidato cha tano, Tan Prints (India) Pvt. Ltd.

    Nkwera, F.M.V (1979). Sarufi na Fasihi, Sekondari na Vyuo.Tanzania Publishing
    House, Dar es Salaam,Tanzania.

    Ntawiyanga, S. na Wenzake (2017). Kiswahili kwa Shule za Rwanda. Mchepuo
    wa Lugha, Kidato cha 5. Longhorn Publishers (Rwanda) Limited. Kigali, Rwanda.


    Ntawiyanga, S. na Wenzake (2017). Kiswahili kwa Shule za Rwanda. Mchepuo
    wa Lugha, Kidato cha 6. Longhorn Publishers (Rwanda) Limited. Kigali, Rwanda.
    Waititu, F. na Wenzake (2008). Kiswahili Fasaha. Kitabu cha Mwanafunzi.

    Kidato cha tatu. Oxford University Press, East Africa Ltd, Nairobi, Kenya.

    TUKI (2004): Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Toleo la pili. Oxford University Press.

    MADA YA 7 TANZU ZA FASIHI ANDISHITopic 9