• MADA YA 6 UHAKIKI WA KAZI ZA FASIHI SIMULIZI

    Malengo ya Ujifunzaji:

    -- Kueleza maana ya uhakiki,
    -- Kubainisha taratibu au mbinu za uhakiki wa kazi za fasihi simulizi,
    -- Kuonyesha umuhimu wa kuhakiki kazi za fasihi,
    -- Kujadili maana ya uhakiki na mwongozo wake,
    -- Kuhakiki hadithi za masimulizi mbalimbali,
    -- Kutoa mapendekezo juu ya kazi za fasihi zilizohakikiwa,
    -- Kukuza falsafa tofauti zinazojidhihirisha kutoka ujumbe wa kazi za fasihi
    simulizi,

    -- Kuainisha aina za maneno katika Kiswahili.

    SOMO LA 12: MAANA YA UHAKIKI
    12.1. Kusoma na Ufahamu: Siku Njema Huonekana
    Asubuhi
    Soma kifungu kifuatacho, kisha ujibu maswali yaliyotolewa hapo
    chini.

    Ilikuwa Jumatatu asubuhi wakati mwalimu wetu wa Kiswahili Bibi Amina
    alipotuchekesha sana. Mwalimu huyu kwa kawaida yake alikuwa mcheshi
    na mwenye kupenda utani. Ilikuwa ni ajabu mno kumwona amekunja uso.

    Wanafunzi wote walikuwa wakimpenda na hata wagonjwa walikuwa wakijikaza
    kiume ili wawahi somo lake. Alikuwa mnene kiasi, macho mazuri kama gololi
    yaliyokuwa yakicheza katika vidimbwi vya machozi. Alipokuwa akicheka, vishimo
    vidogovidogo vilikuwa vikionekana kwenye mashavu yake. Sauti yake ilikuwa
    ikituvutia sana. Alikuwa akifundisha na wanafunzi sote tukatoka tukisema kuwa
    tumetosheka.

    Asubuhi hiyo, tulipofika shuleni tuliulizana habari mbalimbali. Kuna wale
    waliokuwa na habari za michezo na wengine walikuwa na habari zinazohusu
    maisha ya nchi yetu: uchumi, elimu, siasa, ufugaji, kilimo na kadhalika. Habari
    hizo zote tulikuwa tumezipata kutoka kwenye redio na nyingine kutoka kwenye
    runinga. Kwa kuwa nami nilikuwa sogora kwa kutia chumvi katika mazungumzo,
    kila siku wanafunzi walikuwa wakinizunguka kama nyuki wazengeavyo maua.

    Kengele ya kwanza ilipolia, sote tulikusanyika karibu na mlingoti wenye bendera
    ya taifa na kuanza kuimba wimbo wa taifa. Tulipomaliza, Joni, mwalimu wa somo
    la ujasiriamali, alipanda jukwaani na kuanza kutuhutubia kuhusu mada ya “Ndi
    Umunyarwanda.” Siku hiyo yeye alitilia mkazo kwenye umoja na maridhiano kati
    ya Wanyarwanda, uzalendo na mshikamano kama njia bora za kuendeleza nchi
    yetu. Alipomaliza, tuliingia madarasani na kuwasubiri walimu wetu.

    Kengele ya pili ilipolia mwalimu wetu wa Kiswahili alijtokeza na kutuamkia kama
    kawaida yake. Alikuwa na mkoba begani na vitabu pamoja na boksi la chaki
    mikononi. Sisi sote tulikuwa na hamu ya kusikia mchapo aliokuwa ametuletea
    asubuhi ile. Bila ya kusema neno lolote aliweka vifaa vyake mezani akaangaza
    macho kama aliyekuwa akishuku jambo baya fulani darasani. Sisi sote tulitulia
    tuli kama maji mtungini. Hayawi hayawi huwa. Alipomaliza ukaguzi wake
    alituuliza majina ya wale ambao hawakuhudhuria shule lakini sote tulikuwa hapo.
    Alitabasamu na kuanza somo lake.

    Kwanza alituuliza maswali kuhusu somo lililopita. Somo hilo lilikuwa vipengele
    vya fasihi simulizi. Tuliposonga mbele alituomba kumwonyesha kazi ya nyumbani
    aliyotupatia. Kazi hiyo ilikuwa uchambuzi wa hadithi. Sote tulikuwa tumejaribu
    kwa uwezo wetu. Alituuliza mbinu tulizotumia katika uchambuzi wetu, kila mtu
    akataja zake. Alitukagua kitambo kidogo, akatupongeza na kusema kuwa “Kweli
    siku njema huonekana asubuhi.” Mara hii alichukua chaki na kuandika neno
    “UHAKIKI” ubaoni. Nasi tukaanza kunong’onezana kwa kuwa ilikuwa mara ya
    kwanza kuona neno hilo. Tulishangaa sana kwa kuona kuwa hakuandika jaribio
    kama desturi yake ya kutuuliza kila alipokuwa akiingia darasani. Alipotangaza
    kuwa neno hilo lilikuwa somo la siku ile sote tulitega masikio.

    Pili, alitugawa katika makundi. Kila kundi lilikuwa limeundwa na wavulana na
    wasichana, na wanafunzi wenye matatizo maalum ya kielimu. Kila kundi lilipewa
    kitabu. Kabla hatujafungua vitabu, alituomba kukagua vema kama kila kundi
    lilipewa vitabu vya Kiswahili. Alituonya hivi huku akitwambia kuwa kulikuwa
    na mtu mmoja aliyeingia mgahawani bila kuuliza habari wala kusoma, akatia
    pilipili hoho nyingi kwenye chakula akidhani kwamba ni supu. Alipokula chakula
    hicho, aliwashwa na machozi yalimlemgalenga. Katika kujaribu kupoza koo lake,
    akashika na kunywa sabuni ya kunawia mikono akifikiri kwamba ni juisi. Sisi sote
    tulishika mbavu. Alituagiza kufungua vitabu na kuzungumzia kuhusu uhakiki wa
    kazi za fasihi simulizi. Tulipomaliza kuzungumza, kila kundi liliwasilisha.

    Tuliona kwamba uhakiki ni kazi ya kutathmini, kufasili na kuainisha kazi za fasihi.
    Ni kazi ya kusoma maandishi au kusikiliza mambo fulani kwa kuyachambua na
    kuyafafanua ili kupata ukweli wa mambo hayo.

    Zaidi ya hayo, tulisoma kuwa kwa kuhakiki maandishi au masimulizi,
    tunachunguza na kufafanua vipengele vya fani na maudhui. Katika fani kama sura
    ya nje ya maandishi au masimulizi, tunachunguza wahusika, muundo, mtindo
    na mengineyo. Kimaudhui, tunachunguza dhamira, ujumbe, migogoro, itikadi,
    falsafa na hata mtazamo. Wakati huu, mambo yaliyokuwa yakitushinda, mwalimu
    alikuwa akitusaidia ili tuyaelewe zaidi.

    Isitoshe, baada ya kuona maana ya uhakiki, mwalimu alituomba kueleza
    umuhimu wa uhakiki tukagundua kwamba uhakiki una umuhimu wa kumwezesha
    mhakiki kuchambua na kuelewa kazi ya fasihi au sanaa kwa ujumla, kuwezesha

    kulinganisha kazi tofauti na mengine mengi.

    Lakini katika uchambuzi wetu, tuligundua kuwa uhakiki una matatizo fulani kwa
    sababu ni sayansi ngumu inayoomba bidii, ukakamavu wa mhakiki, uwezo wake na
    mienendo ya jamii. Hili linatulazimisha tufanye mazoezi mengi ili tuweze kupevuka
    katika kazi hii. Tena tuliona kuwa, wakati mwingine, wahakiki hawakubaliani kwa
    kuwa kila mmoja ana namna yake ya kuona na kuelewa mambo.

    Somo lilipokaribia kutia nanga, sote tulikuwa tumeelewa kwamba uhakiki lilikuwa
    si somo geni kwa kuwa kila siku tunajaribu kuchambua yale tunayosoma au
    tunayoambiwa. Kutokana na weredi wa haraka tuliokuwa nao ndipo nilipokumbuka
    kuwa “Siku njema huonekana asubuhi.” Kabla ya kutuaga mwalimu alitupa kazi

    ya nyumbani ya kuhakiki hadithi.

    • Nomino/ jina

    a) Maana ya nomino

    Nomino au jina ni neno linaloita kitu chenye uhai au kisicho na uhai kwa

    kukitofautisha na vingine.

    b) Aina za nonino

    -- Nomino za pekee: Butare, Rusizi, Kamana, Ibilisi, Mukungwa, Akanyaru,

    -- Nomino za kawaida: barabara, gari, kuku, kiongozi, nchi, …

    -- Nomino za dhana au za dhahania: maridhiano, uzalendo, utoto, utu,

    upendo, …

    -- Nomino za jamii/ za makundi: jamii, jamaa, baraza, genge, kikosi, …

    -- Nomino za wingi: mawese, maji, mafuta, mamlaka, madaraka, …

    -- Nomino za kitenzi-jina: kuishi kwa amani kunapendeza. Kuimba ni

    kuzuri. Kufurahi kwako kunatutuliza. (kuishi, kuimba na kufurahi ni vitenzijina

    katika sentensi hizi)

    • Vivumishi

    a) Maana ya Kivumishi

    Vivumishi au visifa ni maneno yanayotuelezea zaidi kuhusu nomino. Aghalabu

    vivumishi hutanguliwa na nomino.

    b) Aina za vivumishi

    • Vivumishi vya sifa

    Mifano:

    -- Mke mrefu yule ni mtulivu.

    -- Tunapaswa kujenga jamii nzuri.

    -- Sauti nzuri humtoa nyoka mkali pangoni.

    • Vivumishi vimilikishi

    Vivumishi hivi hutumika kuonyesha umiliki wa nomino. Mizizi ya vivumishi hivi

    huundwa kulingana na nafsi mbalimbali. Mizizi hiyo ni : -angu, -ako, -ake, -etu,

    -enu, -ao.

    Mifano :

    -- Nyumba yangu haina mlango.

    -- Familia yake inaishi vizuri.

    • Vivumishi vya idadi

    Hutueleza zaidi kuhusu kiasi, au idadi ya nomino. Kuna aina mbili za vivumishi

    vya idadi.

    a) Idadi kamili - hutumia nambari kuelezea idadi ya nomino.

    Mifano:

    -- Mmomonyoko wa ardhi ulibomoa nyumba kumi katika vijiji viwili.

    -- Ili kupunguza uhasama unaotokana na ukewenza mume mmoja

    analazimishwa kuoa mke mmoja.

    b) Idadi Isiyodhihirika - huelezea kiasi cha nomino kwa ujumla, bila kutaja

    idadi kamili.

    Mifano: Chache, nyingi, kadhaa, kidogo, wastani.

    Mifano:

    -- Watoto kadhaa waligeuka mayatima wakati wa mauaji ya kimbari dhidi ya

    Watusi yaliyotokea mnamo mwaka wa 1994.

    -- Mvua nyingi ilinyesha na kusababisha mafuriko.

    • Vivumishi viulizi

    Vivumishi viulizi hutumika kuuliza swali.

    -ngapi?, -pi? wapi?, gani?

    Mifano:

    -- Mtu mzima ana meno mangapi?

    -- Ni mbuga gani inayohifadhi sokwe nchini Rwanda?

    • Vivumishi viashiria / vionyeshi

    Vivumishi viashiria hutumika kuonyesha au kuashiria nomino kulingana na mahali.

    Karibu: hapa, huyu, hiki, hili, huku, haya, ule, wale, pale.

    Mbali kidogo: hapo, huyo, hiyo, hicho.

    Mbali zaidi: pale, lile, kile.

    Mifano:

    -- Safisha mahali hapa.

    -- Mwanafunzi yule ni mchezaji kabumbu.

    • Vivumishi visisitizi

    Husisitiza nomino fulani kwa kurudia rudia kivumishi kiashiria

    Mifano:

    -- Anaishi pahali papa hapa.

    -- Mtu yuyu huyu anatuongoza vizuri.

    • Vivumishi virejeshi

    Hivi ni vivumishi ambavyo hurejelea nomino. Vivumishi hivi vinaweza kuwa

    vivumishi vya O-/-ye rejeshi au vivumishi viashiria vinapotumika kurejelea

    nomino.

    Mifano:

    -- Mwanafunzi ambaye ataenda nje ya shule bila ruhusa ataadhibiwa.

    -- Wanyama ambao wametoroka mbuga hawapaswi kuuawa.

    • Vivumishi vya A-unganifu

    Vivumishi hivi hutuelezea zaidi kuhusu nomino kwa kuonyesha kitu kinachomiliki

    nomino hiyo. Huundwa kwa kuambatanisha kiambishi cha nafsi/ngeli pamoja na

    kiambishi -a cha a-unganifu, kisha nomino.

    Mfano: cha, la, kwa, za, ya.

    -- Dawa ya moto si moto.

    • Viwakilishi

    a) Maana ya viwakilishi

    Viwakilishi vya nomino ni maneno yanayotumika badala ya nomino. Kiwakilishi

    hakiwezi kuambatanishwa na nomino inayorejelewa.

    b) Aina za viwakilishi

    • Viwakilishi vya nafsi

    -- Viwakilishi nafsi huru: Mimi, wewe, yeye, sisi, nyinyi, wao.

    -- Viwakilishi nafsi viambata : Ni-, u-, a-, tu-, m-, wa-, mi-, li-, ya-, ki-, vi-,

    i-, zi-, ku-, pa-

    • Viwakilishi viashiria

    Viwakilishi viashiria (vionyeshi) hutumika badala ya nomino kwa kuonyesha

    nomino inayorejelewa bila kuitaja.

    -- Hiki ni chanzo cha maradhi.

    -- Hao wanataka maridhiano.

    • Viwakilishi visisitizi

    Hutumika kwa niaba ya nomino kwa kutumia kiashiria chake mara mbili mfululizo.

    Kwa mfano: yuyu huyu, wawa hawa, kiki hiki, papo hapo, mumu humu, zizi hizi,

    - Kiki hiki ndicho kinachonifurahisha,

    - Yuyu huyu alitueleza matumizi ya viwakilishi visisitizi

    • Viwakilishi vya sifa

    Husimama badala ya nomino kwa kurejelea sifa yake.

    Kwa mfano: -chungu, -eupe, -dogo, -zuri, -tamu, -embamba, -rembo, -gumu,

    -kali, ekundu.

    • Viwakilishi vya idadi

    Hutumika kusimama badala ya nomino kwa kurejelea idadi yake.

    a) Idadi Kamili - hutumia nambari kuelezea idadi ya nomino

    -- Wawili hugeuka mmoja.

    -- Alizaa watatu tu.

    b) Idadi isiyodhihirika - huelezea kiasi cha nomino kwa ujumla, bila kutaja

    idadi kamili.

    Mifano:

    -- Tutasikiliza maoni ya wengi kabla ya kuanzisha mradi huu.

    -- Vichache viliandikwa kuhusu maradhi ya UKIMWI.

    • Viwakilishi viulizi

    Viwakilishi viulizi hutumika kwa niaba ya nomino katika kuulizia swali.

    Baadhi ya viwakilishi viulizi huchukua viambishi vya ngeli.

    Mifano:

    -- Unaenda wapi?

    -- Ulinunua mangapi?

    • Viwakilishi vimilikishi

    Viwakilishi hivi hurejelea nomino kwa kutumia vimilikishi.

    -- Kwao hakuna maji safi.

    -- Yao yameharibika tena kutokana na mvua kali.

    • Viwakilishi virejeshi

    Hutumia O-rejeshi kurejelea na kusimamia nomino.

    Kwa mfano: ambaye, ambao, ambalo, ambacho, huyo, yule.

    -- Ambao walizaliwa mwaka huu watachanjwa.

    -- Ambacho kinahitajika kitatafutwa.

    • Viwakilishi vya A-unganifu

    Huwakilisha nomino kwa kutaja kinachomiliki nomino hiyo. Huundwa

    kwa kuambatanisha kiambishi cha nafsi/ngeli pamoja na kiambishi -a cha

    a-unganifu.

    Kwa mfano: cha, la, kwa, za, ya

    -- Cha mlevi huliwa na mgema.

    -- La kuvunja halina rubani.

    Kitenzi

    a) Maana ya kitenzi

    Kitenzi ni neno linaloeleza jambo linalotendwa au kufanywa na nomino au

    kiwakilishi chake.

    b) Aina za vitenzi

    • Kitenzi halisi: ni kitenzi kimoja kinachotumiwa katika sentensi.

    Mifano:

    -- Wanafunzi walipanda miti michache.

    -- Rais atafika kesho.

    • Vitenzi vikuu na vitenzi visaidizi: Wakati vitenzi viwili hutumika

    pamoja kueleza kitendo kimoja, kitenzi cha kwanza huitwa kisaidizi na

    cha pili ndicho kitenzi kikuu.

    Mifano:

    -- Yeye alikuwa akisoma.

    -- Wao wanahitaji kuishi vizuri.

    • Vitenzi vishirikishi: Vitenzi vishirikishi vina dhana ya kitenzi kuwa au

    kuwa na.

    Vitenzi vishirikishi huwa vya aina mbili kuu:

    • Vitenzi vishirikishi vikamilifu: hivi huchukua viambishi vya wakati na

    viambishi nafsi.

    Mifano:

    -- Watoto wangali kitandani.

    -- Wao wamekuwa na uzembe.

    • Vitenzi vishirikishi vipungufu: hivi huchukua viambishi nafsi lakini

    havichukui viambishi wakati.

    -- Wezi si wazuri.

    -- Yeye yu mkweli.

    -- Sisi ni walimu.

    Ukakiki wa Tanzu za Fasihi Simulizi
    • Maana ya Uhakiki

    Uhakiki ni utathmini, ufasili na uainishaji wa kazi ya fasihi. Ni uchambuzi wa ndani
    kabisa wa kitu au jambo ulioambatana na fikra za mchambuzi. Uhakiki ni kazi ya
    kusoma maandishi au kusikiliza mambo fulani kwa kuyachambua na kuyafafanua
    ili kupata ukweli wa mambo hayo.

    Uhakiki ni sayansi maalum ya kuchambua na kudadisi au kupima ubora au
    udhaifu wa kazi ya kisanaa hasa fasihi. Uhakiki wa tanzu za fasihi huzingatia
    mambo mawili muhimu yaani fani na maudhui. Fani na maudhui ni mambo mawili

    ambayo hayawezi kutengana kwa sababu moja hutegemea jingine.

    i) Fani
    Fani ni namna msanii anavyowasilisha maudhui yake kwa hadhira. Fani pia
    huweza kutazamwa kama umbo la nje la kazi ya sanaa yaani sura yake ya nje.
    Kuchunguza fani ni kuchunguza kiundani vipengele mbalimbali vya kifani na
    namna vilivyotumika ili kuwasilisha maudhui. Uchunguzi wa fani unazingatia
    vipengele vifuatavyo: wahusika, muundo, mtindo, mandhari, matumizi ya lugha.
    • Wahusika
    Wahusika ni watu, wanyama, vitu, hata viumbe vya kufikirika ambavyo msanii
    wa kazi ya fasihi hutumia ili kufanikisha ujumbe kwa jamii husika. Katika kazi
    za fasihi msanii huwagawa wahusika katika makundi mawili: wahusika wakuu
    na wahusika wadogo. Wahusika wakuu ni wale ambao wanajitokeza kuanzia
    mwanzo mpaka mwisho na ndio huwa msingi wa kazi ya fasihi hasa hadithi.

    Wahusika wadogo ni wale wote ambao wanajitokeza mara chache au sehemu
    mbalimbali katika kazi ya fasihi na huwasaidia wahusika wakuu katika kubeba
    maudhui. Wahusika wadogo hawa wanaweza kuwa watetezi (wakimsaidia
    mhusika mkuu) au wakawa wapinzani (wakimzuia mhusika mkuu).

    Wahusika wa kazi za fasihi wana tabia mbalimbali. Tabia ya kwanza ni ubapa
    yaani tabia ya kutobadilika kwa mhusika toka mwanzo hadi mwisho. Tabia ya pili
    ni uduara yaani tabia ya kubadilika kihulka, kimawazo na kisaikolojia kufuatana
    na mazingira mapya, wakati, hali, na kadhalika. Tabia ya tatu ni ufoili. Ni tabia
    inayojidhihirisha kati ya ubapa na uduara. Wahusika wenye tabia hii hawaonyeshi
    msimamo wao kama wanaweza kubadilika au kutobadilika.
    Mtindo
    Ni namna ambavyo msanii huipa kazi yake sura ya kifani na kimaudhui kwa njia
    ambayo msanii mwingine hawezi kuipa hivyo hata kama jambo lizungumziwalo
    na wasanii hawa wawili ni lile moja. Mtindo ndio unaomwezesha msomaji,
    msikilizaji au mtazamaji wa kazi ya fasihi amtambue msanii wa kazi hiyo bila
    kuelezwa au kusoma jina la msanii huyo. Kuchunguza mtindo wa kazi ya fasihi
    ni kuangalia matumizi ya lugha katika kazi hiyo. Wakati wa kufanya kazi hiyo

    tunajiuliza maswali yafuatayo:

    -- Msanii anatumia lugha namna gani? Je kuna tamathali za usemi, mafumbo,

    methali, nahau,…

    -- Picha alizochora msanii zinaeleweka au zimesaidia kurahisisha katika

    maelezo yake?

    -- Msanii anatumia mbinu zipi? Mazungumzo, mijadala, hadithi ndani ya

    hadithi,… ?

    • Muundo
    Ni mpangilio wa kiufundi anaoutumia msanii katika kupanga kazi yake. Pia ni
    mpangilio na mtiririko wa visa na matukio. Katika muundo tunaangalia vipengele
    kama ploti. Ploti ni mtiririko wa kiusababishi wa visa na matukio. Aidha, katika
    muundo tunajiuliza mtiririko huu wa visa na matukio ni wa moja kwa moja au ni
    wa kiurejeshi? Kama ni wa moja kwa moja ni muundo wa msago. Kama unaenda
    mbele na kurudi nyuma ni muundo rejeshi.

    • Mandhari
    Mandhari ni sura ya mahali popote palipotumiwa na msanii kwa kukisimika
    anachokisimulia katika kazi ya fasihi. Kuna Mandhari halisi yaani mahali
    panapoweza kuonekana, panapojulikana waziwazi, panapopatikana (nchi fulani,
    wilaya, mkoa, mlima,…) na Mandhari pakubuni yaani mahali pa kujiundia, pa
    kindoto pasipopatikana (mbinguni, jahanamu, ahera, ujinini, ...)

    • Muktadha
    Muktadha ni mazingira au hali ambamo tukio au jambo fulani hutendeka. Ni
    kusema kuwa msanii huishi katika jamii na jamii huzungukwa na mazingira
    mbalimbali. Mazingira haya yanaweza kuonekana katika kazi ya fasihi. Mazingira
    haya yanaweza kuonekana kulingana na lugha iliyotumiwa, msamiati uliotumiwa,
    mawazo fulani ya msanii yanayolingana na wakati fulani. Kwa mfano kazi za fasihi
    simulizi za enzi za ufalme ni tofauti na kazi zilizopatikana baada ya uhuru wa
    Rwanda.

    ii) Maudhui
    maudhui ni jumla ya mawazo yote yanayozungumziwa na masanii katika kazi ya
    kifasihi. Haya ndiyo huwa yamemsukuma msaniii kuisana kazi yake hii. Maudhui
    hujumuisha mawazo pamoja na mafunzo mbalimbali yaliyomsukuma msanii hadi
    akatunga na kusanii kazi yake ya kifasihi. Uchambuzi wa maudhui huzingatia
    vipengele kama vile dhamira, ujumbe, migogoro, falsafa na hata mtazamo.

    • Dhamira
    Dhamira ni wazo lililomo katika kazi za sanaa. Kwa kawaida, dhamira zinagawika
    katika makundi mawili, kuna dhamira kuu na dhamira ndogondogo.
    a) Dhamira kuu: ni kiini cha wazo kuu la msanii ambalo linaongoza
    ujumbe autakao msanii kufikisha kwa jamii. Dhamira kuu huweza kuhusu
    jamii, magonjwa ya zinaa, siasa, uzalendo, uchumi, ushirikiano, umoja na
    maridhiano, usawa wa jinsia, malezi bora, mapenzi, mazingira na maendeleo

    endelevu, n.k.

    b) Dhamira ndogondogo: ni dhamira zile mbalimbali zinazogusiwa na
    msanii ili kuendeleza dhamira kuu. Dhamira hizi husaidia dhamira kuu katika
    kujidhihirisha.

    • Ujumbe /Mafunzo
    Mafunzo ni masomo yanayopatikana katika kazi ya fasihi. Kila kazi ya sanaa huwa
    na ujumbe maalumu ambao msanii anataka uifikie jamii aliyoikusudia. Ujumbe
    katika kazi za kifasihi ni mafunzo mbalimbali ambayo hupatikana ndani ya kazi
    hiyo. Katika kazi ya fasihi dhamira kuu hubeba ujumbe wa msingi wakati ambapo
    dhamira ndogondogo hubeba ujumbe ambao husaidia kuujenga au kuupa uzito
    zaidi ujumbe wa msingi.

    • Migogoro
    Ni hali ya kutokubaliana kimawazo, kimatendo kati ya wahusika. Migogoro
    hii inaweza kuwa kati ya wahusika binafsi na kizazi kimoja au kati ya kizazi na
    kingine. Pia inaweza kuwa kati ya watawala na watawaliwa, jamii na misukosuko
    (misukumano) ya kijamii au kimazingira iliyomo katika eneo fulani.

    • Falsafa
    Kimsingi, falsafa ni elimu ya asili; busara au hekima. Falsafa ya msanii hugusiwa
    kutokana na jinsi anavyoelewa matatizo ya jamii na jinsi anavyoyatolea suluhisho
    kwa njia ya busara, amani na utulivu. Katika kazi za fasihi simulizi hususani hadithi
    zile za paukwa pakawa, falsafa inayojitokeza ni ile isemayo kuwa maisha ni
    mapambano ya wema dhidi ya ubaya na daima wema huushinda ubaya.

    TANBIHI
    Katika kuhakiki kazi za fasihi simulizi, kila kazi ina mbinu mahususi katika
    kuichambua. Kwa mfano uchambuzi wa nahau, methali na misemo unatofautiana
    sana na uchambuzi wa hadithi au mashairi.

    • Umuhimu wa Uhakiki
    Mara nyingi fasihi huwa ngumu kuielewa. Kuna wakati mtu anaweza kusoma au
    kusikiliza kazi ya fasihi akashindwa kuelewa alichojaribu kueleza msanii. Hapa
    ndipo uhakiki unahitajika ili kumwongoza katika kuelewa kazi hiyo.
    Kwa hiyo, uhakiki wa kazi za fasihi simulizi una umuhimu mkubwa. Baadhi ya
    umuhimu huo ni kama vile:

    a) Kuwezesha kuelewa kazi ya fasihi na kuchunguza kama inatimiza sifa zote.
    Kila kazi ya fasihi ina sifa zake. Kwa hiyo uhakiki unatusaidia kugundua
    kwamba kazi ya fasihi inajaza sifa zake zote.
    b) Kuwezesha kulinganisha kazi tofauti za fasihi. Hapa uhakiki unatuwezesha

    kupima uzito na ulegevu wa utunzi wa msanii.

    c) Kuwezesha kupanua lugha yetu kwa sababu katika kazi ya sanaa kunatumika
    msamiati, mifumo, semi na mambo mengine mengi yanayokuza lugha yetu.
    d) Kuwezesha kuchambua na kumulika mafunzo na maonyo yanayopatikana
    katika kazi za fasihi. Maonyo na mafunzo hayo yanaweza kutumiwa kwa

    kujirekebisha au kuirekebisha jamii.

    • Matatizo ya uhakiki
    Hakuna jambo lisilokuwa na ila. Matatizo ya uhakiki ni mengi sana. Kwanza ni
    vigumu kwa wahakiki kukubaliana kuwa hivi ndivyo ilivyo maana ya kazi ya sanaa
    husika. Kila mhakiki huweza kusoma na kuelewa kazi hiyo kwa namna yake.
    Pili, uhakiki wenyewe ni taaluma ngumu ambayo inahitaji kutumia bidii kubwa
    ya kuweza kuitawala. Wahakiki wengi wanafanya uchambuzi na uchambuzi huo
    ukichambuliwa ukaonekana bado una dosari. Jambo hili hutokana na mhakiki

    kuwa na changamoto mbalimbali. Changamoto hizo zinaweza kuwa :

    -- Kutokuwa na ujuzi wa kutosha kuhusu sifa za utanzu unaohakikiwa,

    -- Kutawaliwa kwa mhakiki na hisia zake zinazoweza kuleta upendeleo fulani,

    -- Kutofuata misingi inayozingatiwa katika uhakiki.

    Jibu maswali yafuatayo:

    1. Ni ipi maana ya uhakiki?

    2. Ni mambo gani tunayochunguza kwa kuhakiki kazi ya fasihi?

    3. Taja na ueleze tabia za wahusika.

    4. Ni tofauti gani iliyoko baina ya mandhali na muktadha?

    12.5. Kusikiliza na Kuzungumza



    13.1. Kusoma na Ufahamu: Kobe na Kijumbamshale
    Soma kifungu hiki kisha ujibu maswali uliyopewa hapo chini
    Hapo zamani za kale palikuwa na Kobe na Kijumbamshale. Kobe alikuwa
    mnyamavu, mshindani pamoja na mpole. Kila wakati alikuwa hafanyi jambo lolote
    ovyo ovyo wala kwa pupa. Kwake, kila jambo lilikuwa na mpango wake kabla ya
    kulishughulikia kimatendo.

    Kwa upande mwingine, Kijumbamshale alikuwa ndege mpinzani, mjuba, mpuuzi
    na mwenye majivuno. Mara nyingi alikuwa anafanya kazi bila mpango.

    Siku moja Kobe na Kijumbamshale walikutana njiani wote wakipunga upepo
    huku wakielekea kwa kasri ya Malkia Tembo. Walisalimiana na kukaa chini kabla
    hawajaendelea na safari. Kwa hiyo, walipata fursa ya kuongea sana. Maongezi yao
    yalipokuwa yakiendelea, Kobe alishangaa sana kumwona Fisi amekuja akikimbia
    mno. Alikuwa amechelewa kuhudhuria sherehe ya mtoto wa Malkia Tembo. Kobe
    hakuamini macho yake na kumwonyesha Kijumbamshale, “Angalia pale jinsi Fisi
    anavyokimbia kwa mwendo wa kasi. Anakimbia mbio kama umeme. Bila shaka
    hakuna mnyama hata ndege yeyote anayeweza kumshinda katika mashindano
    ya riadha.” Fisi aliwapitia bila kuwasalimia wakashangazwa na adabu yake.
    Kijumbamshale hakuridhishwa hata kamwe na maoni ya Kobe kuhusu Fisi. Mara
    moja alimgeukia na kumuuliza kwa dharau, “Je, una hakika kwa hayo yote ambayo
    umeyatamka? Nani aliyekuambia kuwa Fisi yule anaweza kuthubutu kunishinda
    mimi? Kama wewe ni mlemavu wa miguu na mabawa, usidhani kuwa sisi sote
    ni sawa nawe.”

    Kobe alijaribu kumsihi akisema, “Samahani rafiki yangu! Hii siyo sababu ya
    kukasirika kwa bure! Ukweli mtupu ni kwamba mimi ninaamini kwamba Fisi
    anaweza kunishinda katika zoezi la mashindano ya kukimbia. Lakini, wewe sahau
    hilo! Huwezi, huwezi na huwezi hata kamwe! Maishani mwangu wanyama wawili
    pamoja na ndege mmoja tu ndio niwaogopao katika mashindano ya namna hii.
    Hao ni Fisi, Sungura pamoja na Tai. Wengine hapana!”

    Kijumbamshale alikunja uso na kumwambia mwenzake, “Huna haya kuhakikisha
    hayo mbele yangu? Kobe hakutaka jambo hili lipambe moto. Hivyo, aliamua
    kutoa suluhu la kimatendo. “Acha tukubaliane kwenye mashindano ya kukimbia
    kilomita mbili wakati wa dakika sitini. Atakayeibuka mshindi ndiye atakayekuwa
    mheshimiwa kati yetu.” Kobe alipendekeza.

    Bila kusita, Kijumbamshale alikubaliana na Kobe hivi wakiamua siku, mahali
    pamoja, na wakati wa mashindano. Baada ya kutoka katika sherehe, Kobe
    hakupata tena utulivu. Alianza kufikiria juu ya mbinu angetumia kujinyakulia
    ushindi dhidi ya Kijumbamshale.

    Siku moja kabla ya mashindano kuwadia, Kobe alikaa peke yake na kufikiri.
    “Wazazi wangu kabla ya kuaga dunia, walinitolea maonyo ambayo sitayasahau
    hata siku moja. Wakati mmoja waliniambia ‘Chelewa chelewa utamkuta mtoto
    si wako’ na wakati mwingine ‘bandubandu humaliza gogo.” Kobe aliyakumbuka
    mashauri ya wazazi. Kutokana na haya, alijisemea kimoyomoyo, “Linalowezekana
    leo lisingoje kesho.” Papo hapo, aliamua kuandaa safari na kuelekea kwenye
    uwanja wa mashindano asubuhi na mapema. Aliahidiana na jogoo kwamba
    angemwamsha.

    Jogoo alipowika alfajiri, Kobe alikuwa ameishatoka nyumbani kwake kuelekea
    mahali pa mashindano. Njiani aliwakuta wanyama wengi waliokuwa wakisafisha
    mbuga yao na kuwasalimu. Walipomuuliza sababu ya safari yake, aliwaeleza
    kwamba alikuwa katika shindano la kukimbia. Isipokuwa nyani aliyempa motisha
    kwa kumpa ndizi, wanyama wengine walishika mbavu kwa vicheko kwa kuwa
    walikuwa wakijua uwezo wake wa kukimbia. Lakini yeye hakukata tamaa

    akaendelea na safari yake.

    Kobe alitembea, akatembea na kutembea. Saa nane mchana, Kobe alikuwa
    amesogelea mti mkubwa ambapo alikuwa amekubaliana na Kijumbamshale
    kuwa kikomo cha mashindano. Wakati huo ndipo Kijumbamshale alikumbuka
    kuwa siku hiyo ilistahili kuwa siku ya mashindano kati yake na Kobe. Alishtuka
    kwa ghafla na kuruka haraka kwa mwendo usio wa kawaida. Aliruka na kuruka!
    Lahaula! Alipokuwa umbali wa mita karibu mbili, Kobe alikuwa amejinyakulia
    ushindi, hivi akishangilia kwa furaha tele.

    Kijumbamshale alipomwona Kobe alipoteza nguvu za kuendelea kuruka na
    kuanguka chini. Kobe alisikia huruma moyoni na kumsogelea Kijumbamshale,
    “Pole sana ndugu yangu. Katika mashindano ni lazima kuwepo mshindi na
    anayeshindwa. Lakini siyo mwisho wa dunia. Somo kubwa kutokana na
    mashindano haya ni kwamba uwezo mkubwa wa kuruka pekee hautoshi, jambo
    muhimu zaidi ni maandalizi, akili na maarifa ya kufanikisha lengo lolote”.

    Kijumbamshale aliona haya na kufunga mdomo wake. Baada ya dakika chache,
    alizinduka na kumwambia Kobe, “Leo nimeona kuwa kila kitu kinawezekana
    maishani. Sina budi kukubali ushindi wako kwa sababu asiyekubali kushindwa
    si mshindani. Nimepiga saluti kwa heshima zako mheshimiwa.” Na huu ndio

    mwisho wa hadithi.

    Maelezo Muhimu kuhusu Aina za Maneno

    Katika lugha ya Kiswahili kuna aina nane za maneno. Aina hizo ni kama vile

    nomino, kitenzi, kivumishi, kiwakilishi, kihusishi, kielezi, kiunganishi na kihisishi.

    Katika somo letu tutagusia aina nne yaani kihusishi, kihisishi, kiunganishi na

    kielezi.

    Viunganishi

    Viunganishi ni maneno yanayofanya kazi ya kuunganisha. Huonyesha uhusiano

    baina ya neno na neno, fungu moja la maneno na fungu jingine au sentensi na

    sentensi.

    Mifano:

    -- Unataka maji au juisi?

    -- Anasoma kitabu badala ya kupiga ubwana.

    -- Kufanikiwa maishani si bahati bali ni kujishughulisha na kujitolea.

    -- Alishinda mtihani ijapokuwa alipatwa na ugonjwa mkali.

    -- Alienda shuleni bila kupata chakula.

    • Vihisishi

    Vihisishi ni maneno ambayo yanaonyesha hisia za mtu za ndani kwa mujibu wa

    hali na muktadha. Yanaonyesha hangaiko la moyo ama kudokeza mguso wa

    moyo ama hata wa akili. Mifano:

    -- Mtume! Umefika asubuhi hii!

    -- Lo! Mvua imenyesha!

    -- Salaa! Inawezekana mtu kunywa chupa ishirini za juisi!

    • Vielezi

    Vielezi ni maneno yanayotoa habari zaidi kuhusu kitendo kilivyofanyika. Pia vielezi

    hutoa habari zaidi kuhusu hali, vivumishi na vielezi vingine.

    Kuna vielezi vya namna, vielezi vya wakati, vielezi vya mahali na vielezi vya kiasi.

    Mifano:

    -- Mwanafunzi yule ameshinda mtihani vizuri.

    -- Mvua itanyesha kesho.

    -- Wanyama huishi misituni.

    -- Mvua ilinyesha mara mbili kwa mwezi.

    • Vihusishi

    Vihusishi ni maneno yanayoonyesha uhusiano baina ya watu au vitu viwili au

    zaidi. Kuna vihusishi vya mahali na vya wakati.

    Mifano:

    -- Nitakutembelea baada ya masomo .

    -- Alisafiri nje ya nchi.

    -- Ng’ombe hulala ndani ya zizi.

    -- Amefika hapa kabla ya mvua kunyesha.

    -- Wao wanaishi pamoja kwa amani.

    Uhakiki wa hadithi za masimulizi
    Uhakiki wa hadithi za masimulizi ni kazi au kitendo cha kuchambua na kufafanua
    vipenge vya fani na maudhui katika hadithi hizo. Vipengele vya fani na maudhui
    ni pamoja na wahusika, muundo, mtindo, dhamira, migogoro na ujumbe.

    Fani katika Hadithi za Masimulizi
    Ikumbukwe kuwa fani ni ufundi au mbinu anayoitumia msanii wa fasihi ili kutoa au
    kufikisha maudhui kwa watu aliowakusudia. Tunapohakiki hadithi ya masimulizi
    kifani, tunachunguza wahusika, mtindo, muundo, mandhari, na mengineyo.

    1. Wahusika
    Wahusika ni watu, wanyama, vitu, hata viumbe vya kufikirika ambavyo msanii
    wa hadithi hutumia ili kufanikisha ujumbe kwa jamii husika. Katika hadithi msanii
    huwagawa wahusika katika makundi mawili: wahusika wakuu na wahusika
    wadogo. Wahusika wadogo wanaweza kuwa watetezi au wakawa wapinzani.

    Wahusika katika hadithi za masimulizi hutegemea aina ya hadithi simulizi. Kwa
    mfano:
    • Ngano: Hadithi ambayo wahusika wake ni mchanganyiko wa wanyama,
    wadudu, mizimu, miungu, miti, watu, na viumbe visivyo na uhai kama
    mawe, miamba, n.k.
    • Hekaya: Hadithi ambayo wahusika wake kwa kawaida ni binadamu tu.
    • Hurafa: Hadithi ambazo wahusika wake huwa ni wanyama wanaopewa
    tabia na vitendo vya kibinadamu.
    • Visasili: Hadithi hizi zinazohusu asili ya mambo fulani.
    • Soga: Hizi ni hadithi fupi za kuchekesha na kukejeli. Wahusika wake ni
    watu wa kubuni lakini wanapewa majina ya watu walio katika mazingira
    hayo.
    • Visakale au Mighani: Ni hadithi ambazo wahusika wake ni watu

    waliotenda matendo ya kishujaa na wanaosifiwa katika jamii fulani.

    Tabia za wahusika katika hadithi za masimulizi

    Wahusika katika hadithi simulizi hupewa tabia za aina mbalimbali. Hawa
    wanaweza kuwa na tabia ya:
    • Ubapa: tabia ya kutobadilika
    • Uduara: tabia ya kubadilika
    • Ufoili: tabia ya kutoonyesha msimamo

    Kwa upande mwingine, katika hadithi za masimulizi tunatumia wanyana kwa
    mara nyingi. Wanyama hawa huwakilisha binadamu katika jamii waishimo. Hili
    ni kwa sababu utumiaji wa majina halisi ya watu unaweza kuzua ugomvi katika
    jamii. Wanyama wanaotumiwa sana katika hadithi za masimulizi ni kama:

    • Sungura: Mara nyingi Sungura hupewa tabia za ujanja, ndiyo sababu
    huonekana mahali pengi kama Sungura-mjanja. Kwa hiyo, Sungura
    huwakilisha watu wenye ujanja kwa madhumuni ya kula jasho la
    wengine, kuwaangamiza adui zao au kuwaangusha mtegoni pamoja na
    kuwategua wanyama wakubwa kama vile simba.

    • Simba: Mnyama huyu hutumika mara nyingi kama kiongozi au mfalme.
    Katika jamii ya wanadamu huwakilisha watu wenye ukali ambao
    wakiongea husikika na huogopewa sana.

    • Fisi: Mnyama huyu huonekana kama mhusika mwenye tamaa na ulafi
    ambaye fikra zake zimetawaliwa na tamaa yake. Pia fisi hupewa tabia ya
    uchoyo, woga pamoja na ujinga. Fisi hutumika kuwakilisha wanadamu
    waroho, woga, wazembe na wajinga, wasiopenda kufikiria sana kwani
    mawazo yao yametawaliwa na tamaa zao.

    • Nyani: Katika hadithi, nyani hudhihirisha hekima na uwezo wa kufanya
    uamuzi wa busara. Hutumika sana kama hakimu na huwakilisha viongozi
    wenye hekima katika jamii.

    • Nyoka: Mnyama huyu hupewa tabia ya hila na huwakilisha watu wenye
    hila/ udanganyifu katika jamii.

    • Kobe: Huwakilisha watu wanyamavu, ambao japo wanajua kufanya
    kitu, hawapendi kuchangia, lakini mwisho huibuka washindi; watu
    wasiokimbilia kufanya mambo.

    • Ndovu: Huwakilisha watu wenye kimbelembele, ambao hujisifu na
    kujitafutia umaarufu. Watu wa aina hii hupenda kuwa katika mstari wa
    mbele japo huenda hawana ujuzi wa kutosha katika jambo hilo.

    • Chui: Chui ni mnyama mkatili sana. Katika hadithi yeye huwakilisha
    tabia ya uharifu.

    • Kinyonga: Huyu huwakilisha tabia ya ugeugeu. Watu wenye tabia ya
    aina hii hawaonyeshi msimamo mmoja.

    • Kunguru: Huyu ni ndege mwoga sana. Katika hadithi yeye huwakilisha

    watu ambao ni waoga.

    2. Mtindo
    Mtindo ni mbinu ya kipekee kwa kila msanii katika ufundi wake wa kifasihi. Kwa
    mfano, namna msanii anavyotumia lugha (nahau, misemo, methali, tamathali
    za usemi) na anavyoteua msamiati wa msingi. Hii ni kwa sababu lugha ndiyo
    wenzo mkubwa wa msanii katika kazi za fasihi. Isitoshe kwa kuchunguza mtindo
    tunachunguza namna msanii anavyosimulia hadithi yake (anaweza kutumia nafsi
    ya kwanza, ya pili au ya tatu, anaweza kutumia nyimbo kwa ajili ya burudani, n.k.).
    Kwa kutunga hadithi ya masimulizi msanii anaweza kutumia majina ya watu au
    akatumia wanyama, wadudu, ndege, miungu na kadhalika.

    3. Muundo
    Ni mpangilio wa kiufundi anaoutumia msanii katika kupangilia zoezi lake, mpangilio
    na mtiririko wa hadithi, kwa upande wa visa na matukio. Msimuliaji anaweza
    kufuatanisha matukio moja kwa moja (Msago) au akasimulia kwa kurukaruka
    hatua, yaani msimuliaji anaweza kuanzia katikati, akaja mwisho na kumalizia na
    mwanzo (urejeshi).

    Isitoshe, hadithi za masimulizi au za paukwa pakawa huwa na mipangilio maalum.

    Hadithi hizi huwa na fomula yake katika utangulizi na mwisho wake.

    • Mianzo ya hadithi za kimapokeo

    i) Mtambaji: Paukwa!

    Hadhira: Pakawa!

    Mtambaji: Paukwa!

    Hadhira: Pakawa!

    Mtambaji: Kaondokea chanjagaa

    Kajenga nyumba kakaa

    Mwanangu mwana siti

    Vijino kama chikichi

    Cha kujengea kikuta

    Na vilango vya kupitia

    Atokeani!

    Hadhira: Naam twaibu!

    Mtambaji:Hapo zamani za kale………………….

    ii) Mtambaji: Paukwa!

    Hadhira: Pakawa!

    Mtambaji: Sahaniǃ

    Hadhira: Ya mcheleǃ

    Mtambaji: Giza!

    Hadhira: La mwizi!

    Mtambaji: Baiskeli!

    Hadhira: Ya mwalimuǃ n.k.

    Mtambaji: Hadithi hadithi!

    Hadhira: Hadithi njoo!

    Mtambaji: Hadithi hadithi!

    Hadhira: Hadithi njoo!

    Mtambaji: Hapo zamani za kale palikuwepo na …………………………

    iii) Msimulizi: Atokaeni!

    Hadhira: Naam Twaibu!

    Msimulizi: Kaondokea chanjagaa, n.k.

    • Hadithi huwa pia na miisho yake

    Hadithi ikimalizika tunasema: “Huu ndio mwisho wa hadithi” au “Hadithi

    inakomea hapa.”

    1. Mandhari
    Ni sehemu ambayo matukio ya hadithi au masimulizi hutokea. Mandhari huweza
    kuwa halisi kama vile nyumbani, baharini, njiani, msituni, kijijini, mjini lakini
    vyote vinavyojulikana au ya kufikirika kama vile kuzimuni, mbinguni, peponi na
    kadhalika. Katika hadithi nyingi za masimulizi wanatumia mandhali pa kubuni kwa

    sababu mandhari hayo huwa ni ya kujiundia.

    2. Muktadha
    Muktadha ni mazingira au hali ambamo tukio au jambo fulani hutendeka. Ni
    kusema kuwa msanii huishi katika jamii na jamii huzungukwa na mazingira
    mbalimbali. Mazingira haya yanaweza kuonekana katika hadithi. Ukichambua
    hadithi za masimulizi utagundua mazingira yaliyokuwa yakiwazunguka wasanii.
    Haya yote huonekana kulingana na msamiati na dhamira msanii alizotia ndani ya

    hadithi.

    Mbali na vipengele vilivyotajwa hapo juu, tunapochambua hadithi
    tunaanzia kwa kutaja kichwa na mtunzi kama anajulikana. Lakini mara nyingi
    watunzi wa kazi za masimulizi hawajulikani. Kazi za masimulizi ni mali ya jamii.

    • Maudhui katika hadithi za masimulizi
    Maana ya maudhui

    Katika somo la kwanza katika mada hii tuliona kuwa, katika kazi ya fasihi, maudhui
    ni jumla ya mambo yote yanayozungumzwa au yaliyomsukuma msanii kuisana
    kazi yake.

    Katika uhakiki wa hadithi za masimulizi kimaudhui, vipengele vifuatavyo ni lazima
    vizingatiwe: dhamira, migogoro, mitazamo falsafa, ujumbe pamoja na msimamo
    wa msanii.

    1. Dhamira
    Dhamira huelezwa kama wazo kuu au mawazo mbalimbali yanayojitokeza katika
    kazi ya fasihi. Kwa kawaida, dhamira zinagawika katika makundi mawili, kuna
    dhamira kuu na dhamira ndogondogo. Dhamira zinazozungumziwa sana katika
    hadithi za masimulizi ni uongozi, amani na maendeleo, mauaji, uroho, ujanja, hila,
    uchoyo, upendo, uzalendo, ushirikiano, ujinga, uhaini, usaliti, wivu na kadhalika.

    2. Migogoro
    Migogoro ni mivutano na misuguano mbalimbali katika kazi za fasihi. Migogoro
    inaweza kuwa kati ya wahusika, familia zao, matabaka yao, au hata katika nyadhifa
    mbalimbali.Vilevile, migogoro yaweza kuwa ya kiuchumi, kijamii, migogoro ya
    nafsi, migogoro ya kisiasa, n.k. Katika hadithi za masimulizi nyingi tunakuta
    migogoro kati ya wahusika wenye nguvu na wale wasio na nguvu na kwa mara
    zote wenye nguvu huishia kwa kuanguka.

    3. Falsafa
    Kimsingi, falsafa ni elimu ya asili; busara au hekima. Falsafa ya msanii hugusiwa
    kutokana na jinsi anavyoelewa matatizo ya jamii na jinsi anavyoyatolea suluhisho
    kwa njia ya busara, amani na utulivu. Falsafa ya msanii wa hadithi za masimulizi
    hugundulika unaposoma hadithi zake nyingi. Hapo ndipo utagundua mawazo au
    saikolojia yake.

    4. Ujumbe
    Kila kazi ya sanaa huwa na ujumbe maalumu ambao msanii anataka uifikie jamii
    aliyoikusudia. Ujumbe katika hadithi za masimulizi ni mafunzo mbalimbali ambayo
    hupatikana ndani yake. Kwa kuwa hadithi zina umuhimu wa kuelimisha jamii
    ndiyo maana kila unapomaliza kusoma au kusikiliza hadithi unaombwa kueleza

    somo ambalo umepata.

    Jibu maswali yafuatayo
    1. Katika uhakiki wa fani ya hadithi tunachunguza nini ?
    2. Taja na ueleze aina tano za hadithi.
    3. Falsafa ya masanii ni nini?
    4. Kwa sababu gani kuelewa usuli ni jambo muhimu?

    • Mfano wa uhakiki wa hadithi ya masimulizi
    1. Fani

    • Kichwa cha hadithi: Kobe na Kijumbamshale
    • Mtunzi: hajulikani.
    • Wahusika
    • Wahusika wakuu: Kijumbamshale, Kobe
    • Wahusika wadogo: Jogoo, Fisi na Nyani na wanyama waliokuwa
    wakisafisha mbuga.
    • Watetezi: Jogoo (Alimwamsha Kobe) na Nyani (alimpatia ndizi)
    • Wapinzani: Wanyama waliokuwa wakisafisha mbuga (walimcheka
    Kobe).
    • Tabia za wahusika: Kobe ni mhusika bapa kwa sababu hakubadilika
    na Kijumbamshale ni mhusika duara kwa sababu alibadilika kimawazo
    (alianzia kwa kupinga uwezo wa Kobe lakini mwishowe alikubali).
    • Aina ya hadithi: Hurafa (wahusika ni wanyama na ndege).
    • Mtindo: Katika hadithi hii masanii alitumia lugha ya kawaida. Hadithi
    imeandikwa kwa lugha ya nathari (katika aya). Msanii alitia mazungumzo
    katikati. Msanii alitumia:

    -- Nahau: kunyakua ushindi (kushinda), kupunga hewa (kupumuzika), kukunja
    uso (kukasirika)
    -- Methali: Chelewachelewa utamkuta mtoto si wako, bandubandu huisha
    gogo, linalowezekana leo lisingoje kesho.
    -- Tamathali za usemi: kukimbia mbio kama umeme (tashbiha), takriri
    (chelewachelewa, bandubandu).

    • Muundo
    -- Mwanzo wa hadithi ni “Hapo zamani za kale”. Na mwisho wake ni “Na huu
    ndio mwisho wa hadithi.”
    -- Msanii alitumia msago kwa sababu alisimulia moja kwa moja bila
    kuchanganya matukio.
    -- Msanii alitumia nafsi ya tatu kwa kusimulia hadithi yake. Lakini pia alitumia
    nafsi ya kwanza na ya pili alipotumia mazungumzo kati ya Kijumbamshale

    na Kobe.

    • Mandhari
    Mahali panaposimuliwa hadithini ni njiani, kasri ya Malkia Tembo, Mbuga ya
    wanyama: mandhari haya ni halisi kwa sababu ni mahali panapoweza kuonekana.
    • Muktadha
    Mtunzi alikuwa akiishi katika mazingira yenye dharau, bezo na upinzani kati ya
    watu.
    2. Maudhui
    • Dhamira
    • Dhamira kuu: kupingana kati ya kobe na Kijumbamshale
    • Dhamira ndogo: usafi, harusi, michezo, dharau
    • Migogoro
    Migogoro inayopatikana katika hadithi hii ni migogoro kati ya wahusika
    Kijumbamshale na Kobe (kutokubaliana kwa yule anayeweza kushinda mwingine
    katika mbio).

    • Falsafa
    Falsafa ya mtunzi inatazamwa kwa kuangalia ni kipi ambacho mtunzi anaangalia
    kuwa huo ndio ukweli katika maisha. Katika hadithi hii, inaonekana mtunzi
    anaamini kwamba mafanikio katika maisha yanaletwa na uthubutu na maandalizi
    ya kina.

    • Ujumbe/ funzo
    -- Kutodharauliana
    -- Kukubali matokeo ya shindano

    -- Kuwa na adabu njema (Fisi alipitia wenzake bila kuwasalimu)

    MADA YA 5 UANDISHI WA RIPOTIMADA YA 7 TANZU ZA FASIHI ANDISHI