Topic outline

  • MADA 1:MATUMIZI YA KISWAHILI KATIKA MAENEO YA UTAWALA

    • Uwezo mahususi:

    Kuzungumza na kuandika kwa ufasaha matini fupifupi kwa kutumia msamiati unaofaa katika mazingira ya utawala.

    • Malengo ya ujifunzaji:

    - Kutaja ngazi za utawala na viongozi wakuu wa serikali,

    - Kuonyesha msamiati unaofaa katika maeneo ya utawala,

    - Kuorodhesha sikukuu za kitaifa,

    - Kutaja aina mbalimbali za vitambulisho vinavyotumiwa,

    - Kutunga sentensi kwa kutumia majina ya viongozi na ngazi za utawala,

    - Kuchora kielelezo cha ngazi ya utawala nchini Rwanda, 

    - Kutunga matini fupi akitumia majina ya viongozi na aina mbalimbali za vitambulisho,

    - Kuheshimu viongozi na watu wengine wanaopatikana katika maeneo ya utawala,

    - Kueleza matumizi ya ngeli ya PA-M-KU.

    OK

    Kidokezo

    Zungumzia mchoro wa hapo juu

    SOMO LA 1: NCHI YETU RWANDA

    Kazi ya 1

    Angalia mchoro huu kisha ujibu maswali ya hapo chini.

    OK

    - Unaona nini kwenye mchoro huu?

     - Unafikiri kuwa watu hawa wanafanya nini?

    1.1. Kusoma na ufahamu: znchi yetu Rwanda

    Soma kifungu cha habari kifuatacho baadaye ujibu maswali ya ufahamu.

    Rwanda ni nchi ambayo inapatikana katika bara la Afrika, sehemu za Mashariki. Raia wake huitwa Wanyarwanda. Nchi ya Rwanda ni jamhuri inayotawaliwa na Rais.

    Utawala wa Rwanda unapatikana katika nyanja tatu. Nyanja hizo hushirikiana kama mafiga jikoni. Uwanja wa kwanza unahusiana na utungaji wa sheria. Kazi hii iko mikononi mwa bunge. Bunge la Rwanda lina vyumba viwili. Chumba cha wabunge wanaoongozwa na spika wa bunge na chumba cha seneti kinachoongozwa na spika wa seneti. Wabunge hutunga sheria na maseneta huchunguza sheria hizo na kuzithibitisha pamoja na kuchunga namna ambavyo serikali huweka sheria hizo matendoni.

    Uwanja wa pili ni wa kiutendaji. Uwanja huu unaongozwa na Rais akisaidiana na viongozi wengine kutoka ngazi za juu kufika ngazi za chini. Viongozi hao ni waziri mkuu na mawaziri wengine, wakuu wa mikoa, meya wa wilaya, makatibu watendaji wa tarafa na kata na wakuu wa vitongoji. Miongoni mwa viongozi hawa kuna wale wanaochaguliwa kwa upigaji kura, wanaoteuliwa na wengine wanaopitia katika mitihani.

    Uwanja wa tatu ni utawala wa kisheria unaohusiana na sheria, aina zake na jinsi sheria zinavyotumiwa. Sheria hizi hutumiwa wakati wa kuamua kesi mbalimbali zinazofikishwa mahakamani. Kuna mahakama za jadi, mahakama za ngazi ya chini, mahakama za ngazi za juu, mahakama za rufaa, mahakama maalum (za kibiashara, kijeshi) na mahakama kuu. Wanaosikiliza kesi na kutoa uamuzi huitwa majaji. Mashtaka hutayarishwa na waendeshamashtaka wakiongozwa na mwendeshamashtaka mkuu wa serikali.

    Rwanda ina majimbo/mikoa minne na Mji wa Kigali. Mikoa hiyo ni kama vile Mkoa wa Kusini, Mkoa wa Kaskazini, Mkoa wa Mashariki na Mkoa wa Magharibi. Kila mkoa unaongozwa na Mkuu wa mkoa au Gavana. Mikoa inagawanyika katika wilaya. Nchini Rwanda kuna wilaya thelathini. Kila wilaya inaongozwa na Mkuu wa wilaya au Meya akishirikiana na halmashauri ya wilaya. Wilaya inagawanyika katika Tarafa ambazo zinaongozwa na makatibu watendaji wakishirikiana na halmashauri ya tarafa. Tarafa nazo zinajengwa na kata/ mashina tofauti yaongozwayo na makatibu watendaji wa kata/mashina. Kila kata inajengwa na vijiji/vitongoji vinavyoongozwa na wakuu wa vitongoji.

    Taifa la Rwanda ni Jamhuri yenye nembo yake, bendera na Wimbo wa Taifa. Ina askari jeshi, askari polisi, askari kanzu na askari enyeji mbalimbali. Wanyarwanda ni watu wanaopenda kuchapa kazi ili kuendeleza nchi yao. Kila mwishoni mwa mwezi Wanyarwanda hufanya msaragambo kwa kufanya kazi za mikono (kujenga nyumba, kusafisha viwanja na barabara, kuzibua mifereji ya kupitisha maji na kadhalika). Baada ya kazi hizi Wanyarwanda huketi chini, viongozi wakawatangazia sera za serikali na kutatua mizozo mbalimbali.

    Katika maisha yao raia wa Rwanda na wengine wanaoishi au wanaoitembelea nchi ya Rwanda huwa na vitambulisho mbalimbali. Vitambulisho hivi ni kama vile kitambulisho cha utaifa, kadi ya upigaji kura, kadi ya huduma za afya, kadi ya ukimbizi (kwa wakimbizi), ruhusa ya kuendesha magari/pikipiki na pasipoti. Wafanyakazi hupewa kadi mbalimbali zinazotambulisha kazi zao na wanafunzi hupewa kadi zinazowatambulisha na kadhalika.

    Nchini Rwanda kuna sikukuu za kitaifa kama katika nchi nyingine. Sikukuu hizo ni kama Sikukuu ya Mwaka Mpya, Krisimasi, Idi (Idd-ul-fitr/Eid al-fitr), Pasaka na nyinginezo. Mara nyingi sikukuu hizi huambatana na shughuli za kidini. Sikukuu zinazohusiana na mambo ya kiutawala ni kama Sikukuu ya Mashujaa, Sikukuu ya Ukombozi, Sikukuu ya Wafanyakazi, Sikukuu ya Walimu pamoja na Sikukuu ya Uhuru. Wakati wa sikukuu zote hizi na nyinginezo ambazo hazikutajwa, Wanyarwanda hufurahi sana na kuchangia vyakula na vinywaji mbalimbali.

    Kazi ya 2 

    Maswali ya ufahamu

    1. Nchi ya Rwanda inapatikana kwenye bara gani? 

    2. Utawala wa Rwanda ni wa aina gani? 

    3. Kiongozi mkuu nchini Rwanda ni nani? 

    4. Taja nyanja tatu za uongozi wa Rwanda. 

    5. Kwa sababu gani Wanyarwanda husemekana kuwa wachapakazi? 

    6. Taja majina mawili ya:

    - viongozi wa kuchaguliwa 

    - viongozi wa kuteuliwa 

    - wanaopitia katika mitihani

    1.2. Msamiati kuhusu kifungu cha habari

    Kazi ya 3

    Toa maana za maneno yafuatayo:

    - Jamhuri 

    - Kura 

    - Kuteuliwa 

    - Majimbo 

    - Halmashauri

    Kazi ya 4

    Husisha sikukuu na tarehe

    OK

    1.3. Sarufi: Matumizi ya ngeli ya PA-M-KU

    Kazi ya 5

    Angalia sentensi zifuatazo ukichunguza majina na mofimu vilivyopigiwa mistari na kuzungumzia kwa ufupi matumizi yake katika sentensi hizo.

    a. Barabarani pamechafuka.

    b. Mezani kuna sahani mbili.

    c. Mfukoni mwangu mna fedha nyingi.

    d. Chumbani humu mna wanafunzi.

    e. Mahali hapa pamesafishwa.

    Maelezo muhimu 

    • Majina yaliyopigiwa mistrari yamo katika ngeli ya PA-M-KU

     • Majina ya ngeli hii si mengi sana. Kwa hiyo, Kiswahili kilichagua kupachika kiambishi -ni mwishoni mwa majina ya kawaida ili kupata majina ya ngeli hii.

    Mifano : 

    - Chumba+ni: chumbani

    - Kichwa+ ni: kichwani

    • Katika kitenzi, ngeli hii huwakilishwa na viambishi pa-, m- na ku-.

    Pa- : huonyesha mahali panapotambulika.

    M- : huonyesha ndani ndani mwa.

    Ku- : huonyesha juu ya na mahali pasipotambulika.

    • Wingi wa majina ya ngeli hii hutokana na wingi wa majina ya kawaida pamoja na kiambishi -ni. Majina haya hufuatwa na kitenzi chenye viambishi pa-, m- na ku-.

    PK

    OK

    Kazi ya 6

    Tumia viambishi mwafaka katika sentensi zifuatazo:

    a. Darasani –na wanafunzi. 

    b. Nyumbani kwetu –nanukia sana.

    c. Kichwani –na upara.

    d. Mahali hapa –tasafishwa. 

    e. Chumbani –mechafuka.

    ▫ Vivumishi vya ngeli ya PA-M-KU

    Kazi ya 7

    Chunguza maneno yenye wino uliokolea na kusema ni aina gani ya maneno.

    a. Nyumbani kupi kuna uchafu?

    b. Mnaenda mahali papi?

    c. Safisha mahali hapa.

    d. Chumbani mwa mtoto mna giza totoro.

    e. Mahali penyewe ni hapa

    f. Nyumbani humu mna usafi.

    g. Mezani kwetu kuna vitabu vingi.

    h. Safisha mahali hapa.

    i. Chumbani mwangu mna giza totoro.

    • Vivumishi vya kurejesha/ virejeshi

    a. Mfukoni mwenyewe

    b. Mezani kwenyewe

    c. Mahali penyewe


    • Vivumishi vya kuunganisha/ viunganishi/ vya A-unganifu

    a. Chumbani mwa mtoto.

    b. Nyumbani kwa Gapfizi

    c. Mahali pa kuchezea 

    • Vivumishi vya kuuliza

    a. Unaenda pahali papi ?

    b. Ni chumbani mpi ambamo hamna taa?

    c. Umeviweka vitambaa mezani kupi?

    • Vivumishi vya kumiliki/ vimilikishi

    OK


    • Vivumishi vya kuonyesha/ vionyeshi

    a. Chumbani humu/humo/mle

    b. Mezani huku/huko/kule

    c. Mahali hapa/hapo/pale


    • Vivumishi vya sifa

    a. Mahali pazuri

    b. Mezani kuzuri

    c. Chumbani mzuri


    Kazi ya 8

    Jaza nafasi kwa kutumia kivumishi mwafaka.

    a. Alitia maji mtungini…………..(pale, kule, mle, yule). 

    b. Nyumbani ……… kuna wanyama wengi wa mifugo (mwetu, petu, kwetu).

    c. Mezani……. hakuna uchafu (humu, huku, hapa, mle).

    d. Mezani huku ni…………….(mzuri, mazuri, kuzuri).

    e. Nimekutunza moyoni…… (kwangu, pangu, mwangu).

    f. Chumbani…………mlikuwa mchafu (kwenyewe, mwenyewe, penyewe).

    g. Nyoka ameingia chumbani…….Kamana (kwa, pa, cha, mwa).

    h. Unaishi mahali…….(ipi, hapi, papi, yapi)?

    i. Mahali ………pamejengwa nyumba nzuri (mwenyewe, kwenyewe, penyewe).

    j. Kichwani………mzee yule kuna mvi (mwa, cha, kwa, pa).

    1.4. Matumizi ya lugha: Maelezo muhimu kuhusu msamiati katika maeneo ya utawala

    Kazi ya 9

    Soma maelezo haya kuhusu msamiati katika maeneo ya utawala baadaye ujibu maswali ya hapo chini. 

    Katika maeneo ya utawala kuna misamiati mingi tofauti. Msamiati huo unahusiana na nyanja za utawala, ngazi za utawala, viongozi, vitambulisho vinavyotumiwa pamoja na sikukuu zinazoshehekewa katika nchi fulani. Hali hii inapatikana nchini Rwanda. Misamiati inayotumiwa ni kama hii ifuatayo:

    - Nchi: ni sehemu ya ardhi katika ulimwengu iliyogawanyika kisiasa kwa mipaka na kutambulikana kwa taifa yake.

    - Taifa: ni jamii ya watu wanaoishi katika nchi moja na wanaounganika kutokana na matukio ya kihistoria.

    - Taifa lisilokuwa jamhuri huitwa ufalme.

    - Nchi huru inaongozwa na katiba

    - Rwanda ni nchi, taifa na jamhuri. Uongozi wa Rwanda unaonyeshwa na Kielelezo kifuatacho:

    OK

    Maswali

    1. Ni nini tofauti iliyoko baina ya taifa na nchi?

    2. Ni nini tofauti iliyoko baina ya ufalme na jamhuri?

    3. Ni nini maana ya katiba?

    1.5. Kusikiliza na kuzungumza

    Kazi ya 10

    Sikiliza taarifa ya habari redioni baadaye ujadiliane na wenzako kuhusu msamiati katia maeneo ya utawala

    1.6. Kuandika

    Kazi ya 11

    Tunga mazungumzo ukibainisha msamiati kuhusu maeneo ya utawala, ukitilia mkazo kwenye matumizi ya majina ya ngeli ya PA-M-KU.


    Tathmini ya mada ya kwanza

    1. Taja nyanja tatu za uongozi wa Rwanda. 

    2. Taja aina tano za vitambulisho vinavyoweza kupatikana nchini Rwanda.

    3. Taja majina ya viongozi wanaochaguliwa na wale wanaoteuliwa pamoja na wale wanaopitia mitihani.

    4. Ni nini tofauti iliyoko baina ya ufalme na jamhuri?

    5. Kwa sababu gani Rwanda ni jamhuri?


  • MADA 2: KISWAHILI NA FASIHI SIMULIZI

    • Uwezo mahususi:

    Kusoma na kusimulia hadithi za masimulizi

    • Malengo ya kujifunza:

    - Kueleza maana ya fasihi,

    - Kutaja tanzu za fasihi,

    - Kuonyesha umuhimu wa Fasihi Simulizi,

    - Kutaja vipengele vya Fasihi Simulizi,

    - Kueleza maana ya hadithi,

    - Kusimulia hadithi,

    - Kukuza na kuhifadhi utamaduni, mila na desturi kupitia vipengele vya fasihi simulizi,

    - Kubaini na kuonyesha aina za maneno.

    Kidokezo

    Tazama kwa makini mchoro ufuatao kisha ujibu maswali yaliyotolewa hapo chini:

    OK

    Jibu maswali yafuatayo

    - Ni nini unachoona kwenye mchoro huu?

    - Unadhani kuwa watu hawa wanafanya nini?

    SOMO LA 2: DHANA YA FASIHI SIMULIZI

    Kazi ya 1

    Toa maelezo mafupi kuhusu mchoro huu.

    ok

    2.1. Kusoma na ufahamu: Dhana ya fasihi na umuhimu wake

    Soma kifungu cha habari kifuatacho kisha ujibu maswali ya ufahamu

    Ilikuwa Jumatatu moja wakati mwalimu wetu wa Kiswahili alipoingia darasani, mkoba begani na madaftari mkononi. Kama kawaida alitusalimia huku akitabasamu. Wanafunzi wote katika madarasa ya mchepuo wa ualimu tulimpenda sana kwani alikuwa mwerevu, mcheshi, mzuri tena mpole. Tena alijali watu wote na wote wakamheshimu. Wakati huo, nami nilikuwa nikisoma katika mwaka wa pili mchepuo wa ualimu.

    Mwalimu alianza somo ambalo liliwavutia wanafunzi wote darasani. Sote tulikuwa na vitabu vya Kiswahili vya mwanafunzi na kila mwanafunzi alikuwa amefungua kitabu chake. Mwalimu alituomba kuunda makundi ili tusome kifungu kuhusu dhana ya fasihi na umuhimu wake katika jamii. Aliomba makundi yote kujiandaa kwa kazi yao. Baadaye, kila kundi lilipewa dakika kumi na tano za kuwasilisha hadharani matokeo ya kazi. Makundi yote yalikuwa yamejitahidi kufanya kazi vizuri. Sote darasani tulielewa vizuri kwamba fasihi ni sanaa ya lugha ambayo hushughulikia masuala yanayomhusu binadamu. Yaani kazi ya Sanaa inayomulika hisi, mawazo na malengo ya jamii kwa kutumia lugha.

    Makundi yote yaligundua kwamba fasihi huzungumzia na kuonyesha maisha ya jamii, kwa kueleza mambo yote yaliyomo katika jamii hiyo: matatizo, mitazamo, migogoro, itikadi, na shughuli mbalimbali za kijamii zilizopo huwa ni mambo yanayobainishwa katika kazi ya fasihi; yaani sanaa ambayo hutumia lugha. Vile vile, wanafunzi wote walielewa kuwa kila mtu anayejishughulisha na utunzi wa kazi ya fasihi hulenga kudhihirisha hisia alizo nazo kulingana na mazingira anamoishi. Yeye huitazama jamii yake na kueleza yote yatendekayo katika jamii hiyo kwa njia ya lugha.

    Makundi yote yalipomaliza kuwasilisha, mwalimu wetu alisisitiza kwamba fasihi hutumia lugha kisanaa na kuwa malengo ya fasihi ni kuelimisha wanajamii, kuwaburudisha na kuwastarehesha. Yeye alieleza kwamba fasihi huwaonya wanaotenda maovu kuacha maovu yao, na kuwahimiza wanaotenda mema kuendeleza matendo yao mazuri. Vilevile, fasihi ni kioo cha jamii na mwavuli wake. Inalinda jamii kwa kuhifadhi na kueleza vitendo vyake ambapo vitendo vizuri huhimizwa na kuchochewa ilhali vitendo vibaya hukatazwa. Msanii ambaye ni mwanafasihi huitumia lugha fulani kwa kujulisha jamii mengi yaliyomo katika utamaduni wake.

    Zaidi ya hayo, tuliona kuwa fasihi hugawanyika katika tanzu kubwa mbili yaani fasihi simulizi na fasihi andishi. Fasihi simulizi hutegemea zaidi usemi ilhali fasihi andishi hutegemea zaidi maandishi kwa kiasi kikubwa. Katika fasihi simulizi kuna tanzu ndogo ambazo huitwa vipera. Vipera vya fasihi simulizi kama vile hadithi, maigizo, ushairi (wa kimapokeo), methali, vitendawili, nahau, na kadhalika. Katika fasihi andishi kuna tanzu tofauti k.v. hadithi fupi, hadithi ndefu (riwaya), tamthilia na mashairi (ya kisasa). Kwa upande mwingine tuligundua kwamba kuna fasihi ya Kiswahili na fasihi katika Kiswahi. Fasihi ya Kiswahili ni ile inayohusu Waswahili, utamaduni wao na mazingira yao. Lakini Fasihi katika Kiswahili ni fasihi inayohusu jamii isiyo ya Waswahili iliyotungwa kwa lugha ya Kiswahili.

    Somo hilo lilitupendeza sote kiasi kwamba tuliamua kujifunza vizuri lugha ya Kiswahili ili tuweze kuitumia kisanaa. Leo hii, wanafunzi wengi tuliosoma pamoja enzi hizo tunajishughulisha na kazi mbalimbali za kisanaa zinazotumia lugha ya Kiswahili. Baadhi yao ni waimbaji, watunzi wa mashairi na wandishi wa vitabu kama mimi. Kila mwaka tunakutania katika tamasha za kitamaduni na kupata tuzo nyingi.

    Kazi ya 2

    Maswali ya ufahamu

    1. Kwa kuegemea kifungu cha habari, nini maana ya fasihi? 

    2. Andika tanzu kubwa za fasihi. 

    3. Fasihi simulizi ina tanzu ndogo au vipera gani? Vitaje vipera vitano. 

    4. Kwa sababu gani fasihi huchukuliwa kama kioo cha jamii? 

    5. Taja aina nne za umuhimu wa fasihi katika jamii. 

    2.2. Msamiati kuhusu fasihi

    Kazi ya 3

    Toa maana za maneno yafuatayo:

    1. Mkoba 

    2. Akitabasamu 

    3. Mcheshi 

    4. Itikadi 

    5. Kujiandaa 

    Kazi ya 4

    Tumia maneno yafuatayo kwa kujaza mapengo: hulenga, tamasha, itikadi, enzi, ilhali.

    1. Si vizuri kuwa na …...kali katika jamii. 

    2. Wewe unasema kuwa fasihi ni ngumu ……wenzako wanaiona rahisi. 

    3. Katika…….za ukoloni fasihi ya Kiafrika ilidharauliwa. 

    4. Fasihi ………kuelimisha na kuonya jamii husika. 

    5. Kila mwaka wasanii huhudhuria ………za kitamaduni na kumulika kazi zao.

    2.3. Sarufi: Aina za maneno

    Kazi ya 5

    Angalia sentensi zifuatazo ukichunguza maneno yaliyopigiwa mistari kisha ujibu maswali ya hapo chini.

    a. Mtoto anacheza mpira wake.

    b. Yeye ni mrefu sana

    • Maneno yaliyopigiwa mistari ni : nomino, kitenzi, kivumishi, kiwakilishi.

    ▫ Nomino/ jina

    a. Maana ya nomino

    Nomino au jina ni neno linaloita kitu chenye uhai au kisicho na uhai kwa kukitofautisha na vingine.

    b. Aina za nomino

    - Nomino za pekee: haya ni maneno yanayotaja majina maalum ya watu, mahali, vitu na hata Mungu ( Mifano : Kamali, Kigali, Nyange, Mola, 

    Muhanga, Kagoyire, Akagera, Nyabarongo, Rwanda)

    - Nomino za kawaida: haya ni maneno yanayotaja vitu vya kawaida ambavyo si mahususi, yaani maneno haya hutaja vitu kwa jumla.

     (Mifano : mtu, mto, ndege, kanzu, kofia, …)

    - Nomino za dhana au za dhahania: ni maneno yanayotaja vitu vya kufikirika au vya hisi tu (Mifano : uchungu, usingizi, uchoyo, uwili, …)

    - Nomino za jamii/ za makundi: ni maneno yanayotumiwa kurejelea vitu au watu wanaotokea kwa makundi (Mifano : jeshi, kamati, kaumu, umati, umma, taifa, familia, …)

    - Nomino za wingi: ni maneno yanayorejelea vitu ambavyo huwa katika hali ya wingi (Mifano: maji, mafuta, mawaidha, maziwa, manukato, …)

    - Nomino za kitenzi-jina: haya ni maneno yanayotokea kwa vitenzi lakini yanapotumika huwa ni nomino (Mifano : kucheza kunapendeza. Kuimba ni kuzuri. Kutembea kwao kunachosha.)

    Kitenzi 

    a. Maana ya kitenzi

    Kitenzi ni neno linaloeleza jambo linalotendwa au kufanywa na nomino au kiwakilishi chake.

    b. Aina za vitenzi

    - Kitenzi halisi: ni kitenzi kimoja kinachotumiwa katika sentensi. Vitenzi halisi huchukua viambishi mbalimbali.

    Mifano: 

    - Mwanafunzi anasoma kitabu.

    - Mgeni wetu atawasili kesho.

    - Vitenzi vikuu: kitenzi kikuu hueleza kitendo chenyewe kwa wakati uliotajwa. Wakati mwingine vitenzi viwili hutumika pamoja kueleza kitendo kimoja. Kitenzi cha kwanza huitwa kisaidizi na cha pili ndicho kitenzi kikuu.

    Mifano: 

    - Mtoto alikuwa akisoma.

    - Yeye anataka kuondoka.

    - Vitenzi visaidizi: kama tulivyoeleza hapo juu, vitenzi visaidizi hutumika pamoja na vitenzi vikuu katika kueleza taarifa kamilifu.

    Mifano: 

    - Maandishi yangali yanasomeka.

    - Zamani watu walikuwa wanasaidiana kazini.

    • Vitenzi vishirikishi: haya ni maneno ambayo hutumiwa katika sentensi kuonyesha ushirikiano au uhusiano baina ya nomino na kiwakilishi, kivumishi na momino. Vitenzi vishirikishi vina dhana ya kitenzi kuwa au kuwa na.

    Vitenzi vishirikishi huwa vya aina mbili kuu :

     Vitenzi vishirikishi vikamilifu: hivi ni vitenzi vishirikishi vinavyoweza kuchukua viambishi vya wakati na viambishi nafsi.

    Mifano:

    - Wavuvi wangali baharini.

    - Wewe umekuwa mzembe.

    - Vitenzi vishirikishi vipungufu: hivi ni vitenzi vishirikishi ambavyo vinaweza huchukua viambishi nafsi lakini havichukui viambishi wakati.

    - Walimu si waongo.

    - Wewe u mrefu.

    - Mimi ni mwalimu.

    - Mimi ndimi mwalimu.

    Maswali

    a. Taja aina za nomino katika sentensi zifuatazo:

    - Mheshimiwa Rais atakuja.

    - Katika jamii ya Wanyarwanda watu husaidiana 

    b. Tunga sentensi ukitumia vitenzi vifuatavyo:

    - ni

    - mkisoma

    - palilia

    - sambaza

    - utakuwa

    2.4. Matumizi ya lugha: Dhana ya fasihi na umuhimu wake

    Maelezo muhimu kuhusu Fasihi 

    Maana ya fasihi

    Fasihi ni kazi ya sanaa inayomulika hisia, mawazo na malengo ya jamii kwa kutumia lugha. Fasihi ni sanaa ya lugha inayoshughulikia masuala mbalimbali yanayohusu binadamu. Ni kusema kuwa maneno hutumiwa kisanaa. Fasihi inaweza kuelezwa kwa mitazamo miwili. Mtazamo wa kwanza ni Fasihi ya Kiswahili ambayo ni ile inayohusu Waswahili, utamaduni wao na mazingira yao. Mtazano wa pili ni Fasihi katika Kiswahili ambayo ni fasihi inayohusu jamii isiyo ya Waswahili lakini iliyotungwa kwa lugha ya Kiswahili sanifu.

    i. Dhima ya fasihi

    Fasihi ina kazi muhimu katika jamii. Wanafasihi wengi huichukua kama kioo cha jamii, wengine wakaifananisha na mwamvuli/ mwavuli mkubwa kwa kuwa inalinda utamaduni wa jamii kutoingiliwa na mambo kutoka tamaduni nyingine.  Vilevile, fasihi huchukuliwa kama daraja linalounganisha vizazi na vizazi.

    Isitoshe, fasihi ina umuhimu wa kuelimisha na kuonya jamii; kuburudisha na kuelekeza na kuendeleza jamii pamoja na kuhifadhi utamaduni. Pia, fasihi huchukuliwa kama silaha ya ukombozi.

    ii. Aina za fasihi

    Katika lugha ya Kiswahili kuna aina mbili za fasihi: 

    Fasihi Andishi na Fasihi Simulizi. Fasihi Andishi ni aina ya fasihi inayohifadhiwa kimaandishi.

    Fasihi Simulizi ni masimulizi ya kale ambayo hayakuandikwa wala kunasiwa kwenye vinasasauti. Fasihi hii, ambayo ni asilia na kongwe zaidi duniani, ndiyo mzazi wa vipera vyote vya Fasihi Andishi. Kupitia kwenye fasihi hii,wanajamii husimuliana matukio, huelekezana kimaadili, huelimishana, hudumisha ushirikiano, huonyana na kupeana taarifa za malezi bora kwa njia ya kisanaa na ubunifu bila ya kutumia maandishi.

    iii. Vipera vya Fasihi Simulizi

    Fasihi Simulizi ina vipera vingi tofauti. Vipera hivyo ni kama ngano, hadithi, methali, nahau, misemo, methali, ushairi, n.k.

    a. Hadithi 

    Hadithi ni utungo wenye visa vya kubuni unaosimuliwa kwa lugha ya kinathari kwa kusudi la kuburudisha, kukuza maadili na kuunganisha jamii. Hadithi huwa na aina tofauti (hurafa/ kharafa, hekaya, ngano, miviga, mighani, visasili, n.k.).

    b. Methali/ mithali 

    Methali ni tungo fupi za sentensi moja ambazo hutoa funzo fulani kwa njia ya mafumbo. Ni tamko lenye kueleza wazo la busara la binadamu kwa ufupi sana.

    Mifano:

    - Mchumia juani hulia kivulini.

    - Mtegemea cha nduguye hufa maskini.

    - Bahati ya mwenzio usiilalie mlango wazi.

    - Masukuzi ya leo ndio msitu wa kesho.

    - Umoja ni nguvu, utengano ni udhaifu.

    - Mtenda kazi asishe ni kama asiyetenda.

    - Usione vyaelea, vimeundwa.

    - Tamaa mbele mauti nyuma.

    - Asiyesikia la mkuu huvunjika guu.

    c. Nahau

    Nahauni semi zinazotofautiana na maana yake ya nje. Huwa ni semi zenye mvuto na utamu wa lugha. Nahau huundwa kwa lugha ya kawaida, kwa kuashiria wazo la picha kutoka katika hali halisi ya maisha, ambazo aghalabu huwa ni misemo ambayo mtumiaji huitumia katika mazungumzo au maandishi hata bila kujua kuwa anaitumia. Baadhi ya nahau hudai kitenzi maalum ndani yake ili ziwe na maana kamili.

    Mifano:

    - Kujikaza kisabuni

    - Kufua dau

    - Kukata tamaa

    - Kukaa chonjo

    - Kula chumvi nyingi 

    d. Misemo

    Misemo ni semi fupi fupi zinazotumia maneno ya kawaida lakini maana yakehuwa fiche. Tofauti na nahau, misemo haihitaji kitenzi ndani yake ili ziwe na maana kamili.

    Mifano:

    - Pua na mdomo 

    - Lila na fila 

    - Domo kaya

    - Mkia wa mbuzi

    e. Vitendawili

    Kitendawili ni tungo fupi ambayo huwa ni swali wazi yaani swali linaloulizwa kwa kutumia lugha ya mafumbo ili kuchemsha bongo ya hadhira. Majibu hutolewa kwa makusudi ya kupima ufahamu wa hadhira kuhusu mazingira yake.

    Mifano: 

    - Mfalme katoa jicho jekundu: jua

    - Nanywa supu na kutupa nyama: mua

    - Mhuni wa ulimwengu: nyuki

    - Askari mlangoni: kufuli

    - Linakula lakini halimezi: shoka

    f. Ushairi simulizi 

    Ushairi ni mtungo wa kisanaa wenye mpangilio maalum wa lugha ya mkato katika usemi, maandishi au wimbo. Mtungo huo hufuata utaratibu wa urari na muwala maalum unaoheshimu na kuzingatia kanuni za utunzi wa shairi unaohusika. Ushairi simulizi ni ushairi unaoghanwa tu.

    Ushairi hujumuisha mashairi ya aina tofauti, tenzi, ngonjera, nyimbo, n.k.

    Kazi ya 6

    Maswali 

    1. Fasihi ni nini? 

    2. Taja aina tano za umuhimu wa fasihi katika jamii. 

    3. Ni nini tofauti kati ya fasihi ya Kiswahili na fasihi katika Kiswahili? 

    4. Taja vipera vitano vya Fasihi Simulizi. 

    2.5. Kusilikiza na kuzungumza

    Kazi ya 7

    Shirikiana na mwenzako mtegeane na kuteguliana vitendawili.

    2.6. Kuandika 

    Kazi ya 8

     “Fasihi ni kioo cha jamii.” Jadili.

    SOMO LA 3: HADITHI

    ok

    Kazi ya 1

    Zungumzia mchoro hapo juu na vitendo vinavyofanyika.

    3.1. Kusoma na ufahamu: Wafalme wawili

    Soma hadithi hii inayofuata kuhusu “Wafalme Wawili”, kisha jibu maswali ya ufahamu uliyotolewa hapo chini.

    Hapo zamani za kale, kulikuwa na wanyama waliokuwa wanaishi msituni. Kila mnyama alikuwa anaishi na mke wake na watoto wake tu, bila kujali wanyama wengine. Msituni huko hakukuwa na mfalme wala kiongozi yeyote wa wanyama hao. Walikuwa na uhuru wa kuishi na kutembea mahali huku na kule.

    Siku moja, walipotazama namna wanyama wa misitu mingine walivyoishi, walidhani kuwa wanyama hao walikuwa na furaha zaidi kuliko wao, kwa sababu wanyama wa misitu mingine walikuwa na mfalme. Walisema, “Jamani, acheni tujichagulie mfalme kama wanyama wa misitu mingine.” Siku ya kuchagua mfalme ilipofika, walikutania kwa Bwana Nungunungu. Wote walikuwa mahali huko: simba, tembo, chui, twiga, ngiri, sungura, nguchiro, fisi, nyoka, mbogo, ndege na samaki. Wagombeaji walikuwa watatu: tembo, simba na sungura. Kabla ya uchaguzi, kila mmoja alijaribu kuomba kura huku akijaribu kuwashawishi wanyama wengine kuhusu namna anavyofaa kuchaguliwa kuwa mfalme kuliko wagombea wengine. Kila mgombeaji alijinadi kuwa yeye ana tabia nzuri zaidi kuliko washindani wake.

    Simba na Sungura ndio waliotangulia kwa kujisifu. Ilipofika zamu ya Tembo kusema, alifungua domo lake na kusema: “Msituni hapa na misitu mingine yote hakuna mnyama aliyekuwa na nguvu kama mimi. Nikichaguliwa kuwa mfalme wenu, nitalinda usalama wenu, mabibi zenu na watoto wenu. Hakutakuwa na mnyama kutoka misitu mingine atakayewashambulia. Hata binadamu hataingia hapa tena.” Papo hapo akateuliwa kuwa mfalme wa wanyama wote msituni humo.

    Siku chache baadaye, Mfalme Tembo aliitisha mkutano wa wanyama wote. Wote waliitikia wito, wakafika mbele ya Mfalme. Hapo Mfalme Tembo alisema: “Tegeni masikio nyote kwa sababu jambo ninalotaka kuzungumzia ni zito na litaathiri kila mmoja wenu wakati wote...... Kazi ya kulinda usalama wenu ni kazi ngumu sana na inanilazimisha kula chakula kizuri kila siku. Mimi sitaendelea kula nyasi kuanzia leo. Hivyo inamaanisha kwamba kila siku ninahitaji wanyama watakaoniletea chakula ili nile vizuri!”

    Siku iliyofuata, Bwana Ngiri alitayarisha chakula. Siku nyingine, Nguciro akakiandaa chakula kizuri. Mambo yaliendelea namna hiyo mpaka wanyama wote majike kwa madume walipomaliza zamu yao. Ilipofika zamu ya Sungura, yeye alikimbia haraka kwa Mfalme Tembo kumuuliza swali moja. Alipofika hapo, Mfalme Tembo ndiye aliyekuwa wa kwanza kumuuliza Sungura: “Wewe raia mbaya unayedharau Mfalme, mbona hujaleta chakula? Unataka nife leo? Ama unataka wewe mwenyewe uwe chakula changu sasa hivi!”

    Sungura aliogopa sana na kuanza kutetemeka, lakini alijaribu na kumuuliza Mfalme swali moja lililobadilisha mambo msituni humo. “Kuna wafalme wangapi msituni humu? Sijui ni yupi atakayekuwa analetewa chakula kila siku kati yenu wawili” Sungura akasema. Mfalme Tembo kwa kusikia hayo, ghafla alifoka na kumuuliza Bwana Sungura, “Nani huyo mwendawazimu anayejidai kuwa Mfalme hapa? Twende ukanionyeshe haraka nikamfundishe somo moja ambalo hatalisahau maishani mwake!” Sungura alimwelekeza wakatembea kwa haraka sana kama kilomita tatu mpaka walipofika kwenye mto wenye kina kirefu.

    Sungura alimwonyesha Mfalme Tembo kwa kutumia kidole: “Tazama pale majini. Mfalme huyo anajificha ndani ya maji. Nenda kaongee naye. Lakini ujue kwamba yeye haogopi mnyama yeyote.” Sasa ndipo Mfalme Tembo alielekea kwenye mto kumtafuta mfalme huyo mwingine. Kwa kutazama ndani ya maji, aliona Tembo wa kiume mnono kama yeye na kumwambia, “Wewe raia mbaya sana, mjinga na shenzi! Toka hapo nikuonyeshe mfalme kati yetu!” Ghafla, Mfalme Tembo alijitupa ndani ya mto ili apigane na mfalme huyo. Lo! Alianza kupiga kelele kuomba msaada. “Mungu weee nisaidie..... nisaidie jameni ..... nisaidie .....!” Alilalama. Papo hapo, Sungura alishikwa na huruma sana na mara moja akaanza kupiga kelele kuomba wanyama wenzake kuja kumwokoa mfalme wao. Punde si punde wanyama wenye nguvu kama vile simba, vifaru, nyati na wengine wengi walikuja wakaogelea na kumwokoa mfalme wao.

    Baada ya tukio hilo, Tembo alihudumiwa kwa wiki tatu akapona. Siku tatu baadaye, Sungura alimsogelea mfalme wao na kuanza kumwelezea sababu iliyomfanya amdanganye mpaka ajitose majini. Mfalme Tembo alijuta kosa lake la kuwanyonya wenzake na kula mali zao mpaka akaamua kuwaita wanyama wote ili awaombe msamaha. Wanyama walipofika walifurahia kwamba mfalme wao ameweza kukiri kosa lake na kujiuzulu. Wao waliamua kumchagua Simba awe kiongozi wao naye akaahidi kwamba angekomesha tabia zote mbaya na mienendo mingine isiyofaa miongoni mwa wanajamii wote. Aliagiza sheria iwekwe na kila mwanajamii aheshimu wengine. Tangu siku hiyo, ndiye mfalme wa pori na wanyama wote huheshimu uamuzi wake.

    Huu ndio mwisho wa hadithi.

    Kazi ya 2

    Maswali ya ufahamu

    1. Ni sababu gani iliyowafanya wanyama msituni wajichagulie mfalme?

    2. Taja angalau majina matano ya wanyama waliohudhuria mkutano wa kuchagua mfalme.

    3. Kila mgombea kati ya wale watatu alipewa fursa ya kufanya nini?

    4. Ni juu ya kigezo kipi Bwana Tembo alichaguliwa kuwa mfalme wa wanyama?

    5. Alipoitisha mkutano wa wanyama wote baada ya kuchaguliwa, Mfalme Tembo aliwaambia nini?

    3.2. Msamiati kuhusu ‘‘Wafalme wawili’’

    Kazi ya 3

    Eleza maana ya maneno yaliyopigiwa mstari katika sentensi zifuatazo:

    1. Wanyama walimchagua Simba kuwa mfalme wao. 

    2. Walikuwa na uhuru wa kuishi kokote. 

    3. Kila mgombea uchaguzi alijaribu kuwashawishi wanyama wengine. 

    4. Tegeni masikio nyote nitakayowaelezea. 

    5. Meya yule aliposhindwa kutawala alijiuzulu. 

    3.3. Sarufi: aina za maneno ya Kiswahili

    Kazi ya 4

    Chunguza matumizi ya maneno yaliyopigiwa mistari ili uweze kubainisha aina zake

    1. Yeye ni mrefu.

    2. Nyumba nzuri imejengwa.

    3. Wewe ni nadhifu.

    • Maneno yaliyopigwa mistari ni vivumishi.

     ▫ Vivumishi

    a. Maana ya kivumishi

    Vivumishi ni maneno yanayotuelezea zaidi kuhusu nomino. Aghalabu vivumishi hutanguliwa na nomino.

    b. Aina za vivumishi

    • Vivumishi vya sifa

    Hivi ni vivumishi ambavyo hutoa sifa ya kitu, mtu, mahali, n.k

    Kwa mfano: kizuri, kali, safi, mrembo, …

    - Yule mama mpole hupika chakula kitamu.

    - Mvulana mkorofi aliadhibiwa na mwalimu kutokana na tabia zake mbaya.

    - Ghorofa hii ndefu ilijengwa na washi hodari.

    • Vivumishi vimilikishi/ vya kumiliki

    Vivumishi hivi hutumika kuonyesha kwamba nomino inaimiliki nyingine. Mizizi ya vivumishi hivi huundwa kulingana na nafsi mbalimbali : -angu, -ako, -ake, -etu, -enu, -ao

    Kwa mfano: changu, lako, yake, kwetu, vyenu, zao.

    - Baraka hutumia talanta zake kwa manufaa ya familia yetu.

    - Flora aliweka kitabu chako sebuleni mwako.

    - Dada yako amepata nguo yake katika sanduku lao.

    • Vivumishi vya idadi

    Hutueleza zaidi kuhusu kiasi, au idadi ya nomino. Kuna aina mbili za vivumishi vya idadi

    a. Idadi kamili au dhahiri - hutumia nambari kuelezea idadi ya nomino.

    Kwa mfano : tatu, mbili, kumi, ishirini na nne. 

    - Msichana mmoja amewaua panya wawili. 

    - Siku kumi zimepita tangu Bi Safina alipojifungua watoto watatu.

     b. Idadi isiyodhihirika au idadi isiyo dhahiri - hueleza kiasi cha nomino kwa jumla, bila kutaja idadi kamili au dhahiri

    Kwa mfano: chache, nyingi, kadhaa, kidogo, wastani. 

    - Watu wengi waliokuwa sokoni walinunua bidhaa kadhaa.

     - Baba yangu amekuwa tajiri kwa miaka isiyo michache. 

    - Baraka ana pesa kidogo mfukoni mwake.

     • Vivumishi viulizi/ vya kuuliza

    Vivumishi viulizi hutumika kuulizia swali. 

    Baadhi ya vivumishi viulizi huchukua viambishi vya ngeli.

    Kwa mfano: -ngapi?, -pi? 

    - Ni watumishi wangapi wamefukuzwa? - kuulizia idadi 

    - Je, ni dawati lipi lenye funguo zangu?

    Kunavyo vivumishi viulizi vingine ambavyo havichukui viambishi vyovyote.

    Kwa mfano: gani? 

    - Unazungumza kuhusu kipindi gani

    - Je, uliwahi kutembelea nchi gani?

    • Vivumishi viashiria / vionyeshi/ vya kuonyesha

    Vivumishi viashiria hutumika kuonyesha au kuashiria nomino kulingana na mahali.

    Kwa mfano: 

    Karibu - hapa, huyu, hiki, hili, huku, haya, huu, hawa.

     Mbali kidogo - hapo, huyo, hiyo, hicho, hizo. 

    Mbali zaidi - pale, lile, kile, zile, vile, wale. 

    - Msichana huyu ni mkubwa kuliko yule

    - Jani hili la mwembe limekauka. 

    - Tupa hapa mpira huo.

    • Vivumishi visisitizi

    Husisitiza nomino fulani kwa kurudia rudia kivumishi kiashiria

    Kwa mfano: huyu huyu, wawa hawa, kiki hiki, papo hapo, mumu humu, kuko huko.

    - Jahazi lili hili. 

    - Wembe ule ule.

     - Ng’ombe wawa hawa.

    Mfano: 

    Ng’ombe hawa hawa ni wanono. 

     Mtoto yule yule ni mweledi.

     • Vivumishi virejeshi.

    Hivi ni vivumishi ambavyo hurejelea nomino. Vivumishi hivi vinaweza kuwa vivumishi vya O-rejeshi vinavyotumika kurejelea nomino.

    Kwa mfano: ambaye, ambao, ambalo, ambacho.

     - Msichana ambaye alikuja ni Baraka Flora. 

    - Sauti ambayo uliisikia nje ya mlango ilikuwa ya Bi. Umutesi

     • Vivumishi vya KI-Mfanano

    Vivumishi vya KI- ya Mfanano hutumika kulinganisha sifa ya nomino na hali au tabia nyingine. Vivumishi hivi hutanguliwa na nomino, kiunganishi cha A-unganifu na huchukua kiungo KI.

    Kwa mfano: wa kifalme, za kijeshi, ya kitajiri, n.k. 

    - Chifu wa Vikwazoni anaishi maisha ya kimaskini.

     - Chali anapenda kusikiliza mziki wa kizungu. 

    - Bi. Naliza huvaa mavazi ya kifalme.

    • Vivumishi vya A-unganifu

    Vivumishi hivi hutuelezea zaidi kuhusu nomino kwa kuonyesha kitu kinachomiliki nomino hiyo. Huundwa kwa kuambatanisha kiambishi cha nafsi/ ngeli pamoja na kiambishi -a cha A-unganifu, kisha nomino.

    Kwa mfano: cha, la, kwa, za, ya.

     - Watoto wa mwalimu mkuu wana tabia nzuri. 

    - Chai ya daktari imemwagika.

    Kazi ya 5

    Pigia mstari vivumishi katika sentensi zifuatazo: 

    a. Kutokana na mvua kubwa iliyonyesha, hapatapatikana mazao bora. 

    b. Jambo zuri la kufanya ni kujitenga na mambo maovu duniani.

     c. Nguo ile imempendeza kijana yule. 

    d. Kiti hicho kimevunjika, niletee kile pale. 

    e. Ni mwanafunzi gani anaugua?

    • Viwakilishi 

    a. Maana ya viwakilishi

    Viwakilishi vya nomino ni maneno yanayotumika badala ya nomino. Kiwakilishi hakiwezi kuambatanishwa na nomino inayorejelewa, bali huiwakilisha nomino hiyo.

    b. Aina za viwakilishi

     • Viwakilishi vya nafsi

    Viwakilishi hivi hutumika kwa niaba ya nafsi kwa umoja na kwa wingi

    Kwa mfano: Mimi, wewe, yeye, sisi, nyinyi, wao ni viwakilishi nafsi huru.

     Ni, u, a, tu, m, wa ni viwakilishi nafsi viambata.

    OK

    - Sisi tuliwatangulia nyinyi kufika hapa. 

    - Mimi si mjinga kama vile yeye anavyofikiria

    Tnbh.: Viwakilishi mie na sie si sanifu. Vilivyo sanifu ni “mimi” na “sisi”.

    Viwakilishi viashiria

    Viwakilishi viashiria (vionyeshi) hutumika badala ya nomino kwa kuonyesha nomino inayorejelewa bila kuitaja.

    Kwa mfano: huyu, yule, hapa, huyo, hao, n.k. 

    - Hiki hakina maandishi yoyote.

    - Hao hawajui tofauti ya viwakilishi na vivumishi.

     - Tumekuja hapa ili kuwaburudisha kwa nyimbo tamu tamu.

    • Viwakilishi visisitizi

    Hutumika kwa niaba ya nomino kwa kutumia kiashiria chake mara mbili mfululizo.

    Kwa mfano yuyu huyu, wawa hawa, kiki hiki, papo hapo, mumu humu, kuko huko 

    - Zizi hizi ndizo zilizovunjika wiki jana. 

    - Yule yule aliyekamatwa juzi, ameiba tena.

    • Viwakilishi vya sifa

    Husimama badala ya nomino kwa kurejelea sifa yake.

    Kwa mfano: -eupe, -zuri, -tamu, -embamba, -rembo. 

    - Vyekundu vimehamishwa. 

    - Warembo wamewasili. 

    - Kitamu kitaliwa kwanza. 

    - Wema hutuzwa.

    • Viwakilishi vya idadi

    Hutumika kusimama badala ya nomino kwa kurejelea idadi yake. 

    a. Idadi kamili/ dhahiri - hutumia nambari kuelezea idadi ya nomino

    Kwa mfano: saba, mmoja, ishirini, wanne, hamsini na mbili. 

    - Wawili wamefukuzwa kazini leo jioni. 

    - Alimpatia mtoto wake elfu kununua chakula.

    b. Idadi isiyodhihirika/ idadi isiyo dhahiri- hueleza kiasi cha nomino kwa jumla, bila kutaja idadi kamili.

    Kwa mfano: chache, nyingi, kadhaa, kidogo, wastani. 

    - Tutazungumza na wachache kabla ya kuanzisha maonyesho yetu.

     - Wengi wamepita mwaka wa kwanza.

    • Viwakilishi viulizi

    Viwakilishi viulizi hutumika kwa niaba ya nomino kuulizia swali. 

    Baadhi ya viwakilishi viulizi huchukua viambishi vya ngeli.

    Kwa mfano: -ngapi?, -pi?

     - Vingapi vinahitajika? - kuulizia idadi.

    - Zipi zimepotea?

    Kuna viwakilishi viulizi vingine ambavyo havichukui viambishi vyovyote.

    Kwa mfano: nini?, nani, vipi? 

    - Yule mvulana alikupatia nini?

     - Uliongea naye vipi? 

    - kuulizia namna.

     - Nani amemwaga maji sakafuni? 

    - Nani anayeitwa?

    • Viwakilishi vimilikishi

    Viwakilishi hivi hurejelea nomino kwa kutumia vimilikishi.

    Kwa mfano: -angu, -ako, -ake, -etu, -enu, -ao.

     - Kwetu hakuna umeme. 

    - Lake limepigwa pasi. 

    - Zao zimeharibika tena.

    • Viwakilishi virejeshi

    Hutumia O-rejeshi kurejelea na kuwakilisha au kusimamia nomino

    Kwa mfano: ambaye, ambao, ambalo, ambacho, huyo, yule.

     - Ambalo lilipotea limepatikana. 

    - Ambaye hana mwana, aeleke jiwe.

    • Viwakilishi vya A-unganifu

    Huwakilisha nomino kwa kutaja kinachomiliki nomino hiyo. Huundwa kwa kuambatanisha kiambishi cha nafsi/ngeli pamoja na kiambishi -a cha a-unganifu, kisha nomino nyingine ikaandama.

    Kwa mfano: cha, la, kwa, za, ya 

    - Cha mlevi huliwa na mgema. 

    - Za watoto zitahifadhiwa.

    Kazi ya 6

    Pigia mistari viwakilishi katika sentensi zifuatazo kisha sema ni vya aina gani. 

    a. Kati ya haya mawili utachagua lipi? 

    b. Wengine wao walipomaliza masomo yao walirejea kule kule kuendelea na kazi. 

    c. Chochote afanyacho hufanikiwa. 

    d. Wengi wa wanafunzi ni wa kupita mtihani wowote.

     e. Miti ile iliyopandwa huko ni mingapi?

    3.4. Matumizi ya lugha: Maelezo muhimu kuhusu hadithi

    Kazi ya 7

    Soma maelezo muhimu yafuatayo kisha ujibu maswali ya hapo chini

    a. Maana ya hadithi

    Hadithi ni tungo za fasihi za masimulizi ambazo zinatumia lugha ya nathari (lugha ya mjazo, ya maongezi ya kila siku). Tena hadithi ni mambo ya kubuni huwa yanaeleza ukweli fulani katika jamii husika.

    b. Aina za hadithi 

    • Hekaya: Ni hadithi ambayo wahusika wake kwa kawaida ni binadamu tu. 

     • Hurafa: Ni aina ya hadithi ambayo wahusika wake huwa ni wanyama au vitu vingine ambavyo huwa vinapewa uhai. Wanyama hao husimamia aina ya tabia ya aina fulani ya binadamu. Katika hadithi za kiafrika na hasa za kibantu, wanyama kama sungura, tembo, fisi, kobe, simba, mbwa, nyoka, mjusi na wengineo husikika sana.

    • Ngano: Hizi ni hadithi za kimapokeo ambazo zinatumia wahusika kama wanyama, wadudu, mizimu, miungu, miti, watu, na viumbe visivyo na uhai kama mawe, miamba, n.k. kueleza au kuonya jamii kuhusu maisha.

     • Visasili/ miviga: Ni hadithi ambazo husimulia mambo yanayohusiana na maumbile ya watu, wanyama, miti na vitu visivyo na uhai.

     • Soga: Hizi ni hadithi fupi za kuchekesha na kukejeli. Soga husema ukweli unaoumiza, lakini ukweli huo unajengewa kichekesho ili kupunguza ukali wa ukweli huo. Wahusika wa soga ni watu wa kubuni lakini wanapewa majina ya watu walio katika mazingira hayo.

    • Visakale/ Mighani: Ni hadithi zinazohusu watu waliotenda matendo ya kishujaa na wanaosifiwa katika jamii fulani.

    c. Umuhimu wa hadithi

    Hadithi hutoa sababu za hali mbalimbali katika dunia kama jamii inavyoiona. Husifu mema na kukashifu maovu. Hadithi hutoa maonyo, hurekebisha, huadhibu, huelimisha na kushauri. Hutoa mafunzo na maadili ya kufuatwa na jamii na kuiwezesha kubadili tabia. Hadithi huzingatia historia na utamaduni wa jamii inayohusika. Huendesha uhusiano wa jamii kwa kuiburudisha na kuboresha uwezo wa kukumbuka.

    • Hadithi husimuliwa na huwa na fomula yake katika utangulizi na mwisho wake

    Mifano ya mianzo ya hadithi za kimapokeo:

    1. Mtambaji: Paukwa!

    Hadhira: Pakawa!

    Mtambaji: Paukwa!

    Hadhira: Pakawa!

    Mtambaji: Kaondokea chanjagaa,

                          Kajenga nyumba kaka,

                         Mwanangu mwana siti;

                         Kijino kama chikichi,

                        Cha kujengea kikuta,

                         Na vilango vya kupitia,

                         Atokeani?

    Hadhira: Naam twaibu!

    Mtambaji: Hapo zamani za kale…………………

    2. Mtambaji: Paukwa!

    Hadhira: Pakawa!

    Mtambaji: Sahaniǃ

    Hadhira: Ya mcheleǃ

    Mtambaji: Giza

    Hadhira: La mwizi

    Mtambaji: Baiskeli

    Hadhira: Ya mwalimuǃ n.k.

    Mtambaji: Hadithi hadithi! 

    Hadhira: Hadithi njoo!

    Mtambaji: Hadithi hadithi!

    Hadhira: Hadithi njoo!

    Mtambaji: Hapo zamani za kale palikuwepo na …………………………

    • Hadithi huwa pia na miisho yake

    Tunasema: “Huu ndio mwisho wa hadithi” au “Hadithi inakomea hapa.”

    Maswali

    1. Hadithi ni nini? 

    2. Taja aina tano za hadithi. 

    3. Kwa sababu gani tunatumia wanyama katika hadithi? 

    4. Kuna tofauti gani kati ya hekaya na mighani? 

    5. Jaribu kuonyesha wanyama wanaotumiwa sana katika hadithi na uonyeshe tabia zao

    3.5. Kusikiliza na kuzungumza

    Kazi ya 8

    Mbele ya wanafunzi wenzako, simulia hadithi moja unaoyoifahamu kwa kuzingatia mianzo na miisho ya hadithi za kimapokeo kama zilivyoonyeshwa hapo juu.

    3.6. Kuandika

    Kazi ya 9

    Kwa kutumia Kiswahili fasaha, andika hadithi moja unayoifahamu kutoka katika jamii ya Rwanda, ukizingatia matumizi ya ngeli ya PA-M-KU.

    Tathmini ya mada ya pili

    1. Fasihi ni nini?

    2. Kwa sababu gani fasihi ina umuhimu katika jamii? (mambo matano)

    3. Je, inawezekana kutenganisha fasihi na jamii? Kwa nini? Eleza.

    4. Kwa sababu gani tunalinganisha fasihi na mwavuli/ mwamvuli mkubwa?

    5. Ni ipi maana ya hadithi?

    6. Taja aina tano za hadithi.

    7. Taja aina za maneno katika sentensi zifuatazo

    a. Yeye ana mkono mrefu, atafungwa.

    b. Nchi yetu ni nchi ya amani.

    c. Baba alikuwa akiendesha gari.

    d. Wengine warefu wamewasili.

    e. Dawa ya moto ni moto.


  • MADA YA 3:METHALI NA SEMI FUPIFUPI

    • Uwezo mahususi wa mada:

    Kutumia methali na semi fupi katika maisha ya kila siku.

    • Malengo ya ujifunzaji:

    - Kueleza maana ya methali, 

    - Kutoa maelezo ya nahau (semi fupi),

    - kueleza ujumbe unaopatikana katika methali na semi fupifupi,

    - Kuonyesha umuhimu wa methali na semi fupi katika jamii,

    - Kutaja na kueleza matumizi ya aina za maneno,

    - Kutumia methali na nahau katika mazungumzo,

    - Kutumia kwa usahihi aina za maneno,

    - Kuonyesha adabu na hehima kwa watu anaoongea nao.

    Kidokezo

    OK

    SOMO LA 4: LEO NI LEO

    4.1. Kusoma na ufahamu: Leo ni Leo

    Soma kifungu cha habari kifuatacho na baadaye ujibu maswali ya ufahamu yaliyotolewa hapo chini

    Hapo zamani za kale palikuwa na mzee mmoja aliyejulikana kama Gahigi. Gahigi alisifika sana kwa uwezo wake wa kutoa mawaidha kwa kutumia lugha ya mafumbo yenye hekima. Kila siku alikuwa akitumia methali/ mithali nyingi sana. Wengi walimsifu na kumwita maktaba ya jamii. Katika mahakama za jadi Mzee Gahigi alikuwa mpatanishi pamoja na wazee wengine. Kila alipozungumza na mkewe, watoto, marafiki na wengine alikuwa akitoa maneno makavu yenye busara.

    Siku moja mtoto wake Kagabo alichelewa kuamka asubuhi ili aende shuleni. Alimwamsha na kumwonya asizoee tabia mbaya ya kupenda kulala na kusahau kazi na majukumu muhimu kwa kumwambia, “Chelewa chelewa utamkuta mtoto si wako.” Gahigi alikuwa bingwa katika matumizi ya lugha iliyoweza kuwaonya na kuwarekebisha waliokutana naye. Alikuwa mzee mwenye huruma na alikuwa akimhurumia kila aliyesahau kutekeleza jambo linalomngoja. Kwa hivyo alimwambia mtoto wake aamke haraka ili aende shuleni. “Mtoto wangu, ndege aamkaye asubuhi hula wadudu watamu. Acha kushika blangeti na shuka yako ili uweze kuvuna matunda ya jasho lako la baadaye. Leo ni leo asemaye kesho ni mwongo. Mimi nimeanza kuzeeka lakini kama nisingetumika kazi vizuri msingeweza kusoma. Ukipoteza muda wako leo kesho hutaweza kuyarudia yaliyopaswa kutendeka leo.

    Basi mtoto aliamka, akanawa mwili wake huku Gahigi akimsihi afanye haraka ili afike shuleni mapema. Alimwelezea mengi kuhusu hasara zinazowapata wavivu na jinsi wanavyoponyokwa na bahati zinazojitokeza maishani mwao. Alizidi kumwambia maneno matamu yenye busara ambayo Kagabo aliyapenda na kuyazingatia. Siku nzima yeye alikuwa akikumbuka methali moja iliyomvutia sana, “Titi la nyati hukamuliwa kwa mashaka,’’ na nyingine iliyomwambia kuwa “Wakati una mabawa.” Tangu siku hiyo Kagabo aliamua kuzingatia mawaidha ya babake na kujizoeza kuwa na bidii katika shughuli zake za kila siku. Alipowasikia wanafunzi wenzake wakimwambia kwamba “Haraka haraka haina baraka” aliwaambia kuwa wangeweza kujutia hayo baadaye.

    Kila siku alikuwa wa kwanza kufika shuleni na kufuata vizuri maelezo ya mwalimu na mambo yote aliyofundishwa darasani. Alipopewa kazi, aliifanya haraka na kuimaliza kwa muda uliotarajiwa. Aliongozwa na maneno ya baba yake kwamba “Fanya kitu kinachofaa katika muda unaofaa.” Yeye alikuwa akishangaa kuona baadhi ya wanafunzi walikuwa wakiyapuuza maonyo yake kwa kuendeleza tabia za uvivu. Kila alipowaona wamechelewa alikumbuka maneno ya baba yake, ‘‘Chelewa chelewa utamkuta mtoto si wako. ’’ Kagabo 3636 alijitahidi kufanya kila liwezekanalo ili asonge mbele masomoni kwa kutarajia maisha mazuri ya baada ya masomo yake kama alivyopenda kumwambia baba yake

    Kagabo aliendelea kusoma kwa bidii akamaliza shule za msingi na kuingia katika shule za sekondari. Kazi zote alizoombwa kufanya alizifanya kwa makini akiongozwa na maneno ya baba, “Leo ni leo asemaye kesho ni mwongo.” Alipomaliza shule za sekondari alijiunga na chuo kikuu katika kitivo cha Lugha na Sanaa. Hapo bidii zake hazikupungua hata kidogo. Yeye alijua kwamba “Mchumia juani hulia kivulini.” Alipomaliza masomo yake alipewa kazi ya Mhariri Mkuu kwenye Televisheni ya Taifa. Hiyo ilikuwa kazi nzuri iliyoweza kumletea pato kubwa kila mwezi. Kazi yake ilimruhusu kutembelea mataifa mengi duniani ili kuonana na wahariri wengine katika makongamano na mikutano ya aina mbalimbali. Miaka miwili baadaye, alikuwa anajulikana kwa kila mtangazaji maarufu na kampuni nyingi za utangazaji zilianza kumwita kutoa mafunzo ya muda kwa watangazaji wao. Hapo alianza kufurahia uwezo wake na kukumbuka methali nyingi alizoambiwa na babake. Miongoni mwa maneno aliyoyakumbuka na ambayo alipenda kuwaambia watangazji wenzake yalikuwa yanaihusu methali tamu “Mchumia juani hulia kivulini.” Yeye alipenda kazi yake na kuifanya kwa usahihi na viongozi wake walimjua.

    Mwaka wa tatu baada ya masomo yake alikuwa amejijengea nyumba nzuri ya kisasa mjini na kujinunulia gari zuri la kisasa. Watu wengi waliomwona walishangaa kuona mtoto aliyetoka katika kijiji kisichojulikana amefikia kiwango kama hicho cha kutegemewa na wengi. Kwa kweli, utajiri wake ulikuwa umemwezesha kuwakumbuka wasiojiweza na kuwasaidia kwa moyo mkunjufu. Yeye hakuona taklifu au ugumu wowote kusaidia yeyote aliyemwendea. Yeye alishirikiana na viongozi wa kijiji chake katika mradi alioanzisha wa kusajili vijana wote waliokuwa wamesitisha masomo yao kwani alikuwa ameshajenga shule ya kiufundi huko kijijini. Kila wakati alipofika kijijini kwake, majirani wote walikuja na kukumbuka malezi aliyopewa na babake alipokuwa mtoto mchanga. Wote walifurahia matunda aliyoweza kuvuna babake Gahigi na kuambiana kati yao “Ivute ngozi ingali mbichi.” Wote walielewa kuwa watoto wao wangelizoezwa kutimiza wajibu wao mapema kama Kagabo wangeliweza kuwa na maisha mazuri kama yake.

    Mzee Gahigi alikuwa mtu wa ajabu aliyewaonya wanakijiji wote. Kila walipokutania katika shughuli mbalimbali za kijamii na za kimaendeleo ya kijamii alipenda kuwaambia, “Hakuna kitu cha bure katika dunia yetu, lazima tuchape kazi kwa bidii ili tufike tunapotaka kufika. Maisha mazuri ya watoto wetu yatatokana na malezi mema tutakayowapatia nasi tutafurahia jambo hili baadaye. Fuata nyuki ule asali kwa kuwa mtu huvuna kile alichokipanda.’’ Wazazi wenzake wote walimpongeza kwa maneno yake ya busara naye akakumbuka jinsi alivyochukuliwa na mtoto wake katika sherehe ya mwaka uliotangulia. 37 Kwa kweli, Kagabo alikuwa amemnunulia ng’ombe wa kisasa kama zawadi ya malezi mazuri aliyopewa. Baba yake alifurahi sana na kumshukuru mtoto wake.

    Kazi ya 1

    Maswali ya ufahamu:

    1. Taja majina ya wahusika muhimu wanaozungumziwa katika kifungu hiki?

    2. Kwa nini watu wengi waliyapenda maneno ya Mzee Gahigi?

    3. Mzee Gahigi alikuwa na kazi gani katika mahakama za jadi?

    4. Eleza jinsi tabia ya Kagabo ilivyobadilika.

    5. “Mchumia juani hulia kivulini.” Eleza jinsi usemi huu unavyohusiana na kifungu cha habari ulichosoma.

    6. Kuna funzo lolote unalolipata kutokana na kifungu hiki? Eleza

    4.2. Msamiati kuhusu methali

    Kazi ya 2

    Jaribu kutoa maana za maneno yafuatayo:

    Mafumbo

    Mawaidha

    Maktaba

    Shaka

    Baraka

    Kazi ya 3

    Eleza maana ya methali zifuatazo:

    1. Leo ni leo asemaye kesho ni mwongo.

    2. Chelewa chelewa utamkuta mtoto si wako.

    3. Ndege aamkaye asubuhi hula wadudu watamu.

    4. Wakati titi la nyati hukamuliwa kwa mashaka.

    5. Haraka haraka haina baraka.

    6. Ngoja ngoja huumiza matumbo. 

    7. Wakati una mabawa. 

    8. Mchumia juani hulia kivulini

    4.3. Sarufi: Sarufi kuhusu matumizi ya vielezi, viunganishi, vihusishi na vihisishi

    Kazi ya 4

    Taja aina za maneno ambayo yamepigiwa msitari katika sentensi hizi:

    1. Mtoto aliposoma sawasawa alipewa biskuti na wazazi.

    2. Nyimbo ziimbwazo kitoto huchekesha kwelikweli.

    3. Tulipanda ndizi kwa jembe lilelile.

    4. Vigelegele vililia lelelele lelelele juzi wakati wa harusi ya dada.

    5. Ukichokorachokora sikio lako utajitia mashakani polepole.

    Maelezo muhimu kuhusu vielezi

    Vielezi ni maneno yanayotoa habari zaidi kuhusu kitendo kilivyofanyika. Pia vielezi hutoa habari zaidi kuhusu hali, vivumishi na vielezi vingine. Tazama aina mbalimbali za vielezi katika jedwali na matumizi yake.

    OK

    OK

    Kazi ya 5

    Tumia viunganishi mwafaka kuunganisha sentensi zifuatazo:

    1. Hana nyuma. Hana mbele.

    2. Musabyimana alikula staftahi. Musabyimana alienda ofisini.

    3. Alimsogelea adui yake. Hakuwa na hofu.

    Kazi ya 6

    Tunga sentensi ukitumia viunganishi vinavyofuata:

    1. Mbali na

    2. Baada ya

    3. Lakini

    Maelezo muhimu kuhusu viunganishi

    Viunganishi ni maneno yanayofanya kazi ya kuunganisha. Huonyesha uhusiano baina ya neno na neno, fungu moja la maneno na fungu jingine au sentensi na sentensi.

    Mifano:

    1. au: Utanunua shati jekundu au jeupe?

    2. badala ya: Anatazama televisheni badala ya kucheza.

    3. bali: Kusema Kiswahili si vigumu, bali ni rahisi.

    4. basi: Nilitaka sana kula piza, basi nilienda mkahawani.

    5. bila: Basi lilifika bila mama.

    6. ijapo: Ijapo nitakufa, sitakubali uwongo.

    7. ila: Kila mtu amelala ila baba.

    8. ingawa: Anapenda familia yake ingawa yeye ni maskini.

    9. kama: Ninahitaji televisheni kama hii.

    10. kisha: soma mfano huu kisha usome sentensi ifuatayo.

    11. kwa sababu: Nilienda darasani kwa sababu nilitaka kusoma Kiswahili.

    12. kwamba; kuwa: Ninaona kwamba / kuwa mnyama huyu ni mkali.

    13. lakini: Uwera anacheka lakini Kabera analia.

    14. na: Nitanunua kalamu na daftari dukani.

    15. pamoja na: Nilienda dukani pamoja na mama yangu.

    16. tena: Sijui mtoto huyu, tena sijamwona.

    17. wala: Hakuna mchele wala unga.

    18. isipokuwa: Wanafunzi hawa ni wazuri isipokuwa Gakwaya.

    19. baada ya: Tulienda mkahawani baada ya darasa.

    20. kabla ya: Nilizungumza na mwalimu kabla ya kuingia hapa.

    21. ikiwa: Ikiwa nitapita mtihani, nitapata digrii yangu.

    Kazi ya 7

    Tumia vihusishi vifuatavyo kukamilisha sentensi: Sawa na, karibu na, baada ya, hadi, moja kwa moja.

    1. Kitabu hiki ni ………………………………. kile.

    2. Alikimbizwa ………………………………. nyumba yake.

    3. ………………………………….. kula chakula tulinawa mikono.

    4. Walisoma ……………………………. usiku wa manane.

    5. Alienda ……………………………… kwa mwalimu mkuu.

    Maelezo muhimu kuhusu vihusishi

    Vihusishi ni maneno yanayoonyesha uhusiano baina ya watu au vitu viwili au zaidi. Kuna vihusishi vya kuonyesha mahali, wakati na hali.


    Mifano:

    1. kabla ya: Kabla ya kuimba nitakunywa chai.

    2. baada ya: Baada ya darasa nitasoma.

    3. nje ya: Niko nje ya nyumba.

    4. ndani ya: Nyoka ameingia ndani ya shimo.

    5. juu ya: Miti ilianguka juu ya nyumba.

    6. chini ya: Viatu vyangu viko chini ya meza.

    7. baina ya: Ninasoma kitabu baina ya Nimugire na Bariho.

    8. kati ya: Mimi hunywa pombe kati ya Ijumaa na Jumapili.

    9. mbele ya: Vitabu vipo mbele ya dirisha.

    10. nyuma ya: Paka analala nyuma ya kochi.

    11. karibu na: Ninaishi karibu na mji wa Huye.

    12. mbali na: Nyumba yako iko mbali na pwani.

    13. kando ya: Wilaya ya Nyamasheke iko kando ya ziwa Kivu.

    14. mpaka; hadi: Nitasoma kutoka saa nne hadi saa tano asubuhi. 

    Nilikimbia kutoka saa nane mpaka saa tisa mchana.

    15. kisha: Ninaenda sokoni kisha nitarudi nyumbani.

    16. tangu; toka: Nilisoma Kiswahili tangu saa mbili hadi saa tano asubuhi.

    Yeye atakaa hotelini toka Jumanne mpaka Ijumaa.

    17. katika: Tunazungumza katika Kiswahili.

    18. miongoni mwa: Mtoto anaimba miongoni mwa wazee.

    19. usoni pa: Anaishi usoni pa duka.

    20. pembeni mwa: Anakaa pembeni mwa darasa.

    21. ubavuni pa: Mtoto amekaa ubavuni pa mama.

    Kazi ya 8

    Soma sentensi zifuatazo kisha utaje aina za maneno yaliyopigiwa msitari.

    1. Haki ya Mungu! Mimi sikuiba.

    2. Rais wetu, oyee!

    3. Ala! Vipi mtu kujitia wazimu namna hii!

    4. Afanaalek! Nimesahau kabisa kuwa leo ni siku ya kuzaliwa kwangu.

    5. Huree! Tumemaliza kujenga nyumba.

    Maelezo muhimu kuhusu vihisishi

    Vihisishi ni maneno ambayo yanaonyesha hisia za mtu za ndani kwa mujibu wa hali na muktadha. Yanaonyesha hangaiko la moyo ama kudokeza mguso wa moyo ama hata wa akili. Kwa mfano: kuna kukosekana kwa matumaini, furaha, huruma, mshangao, hasira, wasiwasi na kadhalika. Ili kuonyesha baadhi ya mahangaiko haya, yapo maneno fulani yanayotumiwa.

    Mifano ya baadhi ya vihisishi ni hii ifuatayo: Aa!, hmmm!, Ebo!, eti!, alaa!, basi!, afanaalek!, ajabu!, pole!, sasa/tena!, haki ya Mungu!, ewe!, inshallah!, ohoo!, kumbe!, oyee!, hata!, salaale!, la hasha!, Alhamdulillah!, maskini! lo!, haya!, na kadhalika

    4.4. Matumizi ya lugha: Methali na nahau

    A. Methali

    Kazi ya 9

    Soma maelezo muhimu yanayofuata, kisha ujibu maswali hapo chini.

    Maelezo muhimu: Maana ya methali

    Methali ni tungo fupi za sentensi moja ambazo hutoa funzo fulani kwa njia ya mafumbo. Ni tamko lenye kueleza wazo la busara la binadamu kwa ufupi sana. Misemo hiyo huzingatia maneno yenye kuvutia masikio ya watu wanaozitumia na huelezea mambo mengi kwa kutumia maneno machache iwezekanavyo. Methali nyingi huwa na sehemu mbili: Sehemu ya kwanza hutoa hoja nayo sehemu ya pili hutoa suluhisho au matokeo.

    Mifano: Chelewa chelewa, utamkuta mtoto si wako.

     (Hoja)                       (Matokeo)

    Wakati titi la nyati, hukamuliwa kwa shaka.

     (Hoja)                     (Suluhisho)

    Mchumia juani, hulia kivulini.

    (Hoja)                     (Matokeo)

    Methali huhitaji hekima ili kujua maana yake. Inatumika kwa minajili ya kusema jambo fulani kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Kama tanzu nyingine za fasihi simulizi, methali huwa na maana ya nje (maana inayopatikana kutokana na maana za maneno yaliyotumika kuundia methali husika) na maana ya ndani (maana inayosemwa kwa ufiche/ maana fiche).

    Mifano: 

    1. Mpanda ngazi hushuka

    Maana ya nje: Mtu yeyote anayepanda juu ya ngazi ni lazima itafika muda wake kushuka kutoka juu ya ngazi hiyo.

    Maana ya ndani: Katika maisha mtu anayepata cheo au madaraka kuna siku anaweza kuyapoteza madaraka au cheo hicho.

    2. Leo ni leo asemaye kesho ni mwongo

    Maana ya nje: Siku hii ni siku hii, anayenena siku ifuatayo ni mdanganyifu.

    Maana ya ndani: Tendo linalowezekana kufanyika sasa lazima lifanyike, lisiahirishwe.

    Katika jamii methali zina umuhimu wa kuonya, kurekebisha, kutoa mafunzo, kutahadharisha na kuunganisha jamii.

    Maswali:

    1. Fafanua maana ya methali.

    2. Toa mifano miwili ya methali, kisha ubainishe sehemu zake mbili: hoja na matokeo au suluhisho.

    3. Toa methali mbili, kisha uonyeshe maana yake ya nje na maana yake ya ndani kwa kubainisha wakati wa kuitumia au namna inavyoweza kutumiwa katika mazungumzo ya watu

    Kazi ya 10

    Husisha methali kutoka safu A na methali yenye maana sawa na methali hiyo katika safu B.

    ok

    Kazi ya 11

    Linganisha methali toka safu A na maana mwafaka kutoka katika safu B.

    ok

    B. Nahau 

    Maelezo muhimu kuhusu nahau 

    Nahau ni semi zinazotofautiana na maana yake ya nje. Huwa ni semi zenye mvuto na utamu wa lugha. Nahau huundwa kwa lugha ya kawaida, kwa kuashiria wazo la picha kutoka katika hali halisi ya maisha, ambazo aghalabu huwa ni misemo ambayo mtumiaji huitumia katika maazungumzo au maandishi hata bila kujua kuwa anaitumia. Ni msemo wa picha ambao huwa na maana iliyofichika. Nahau huwa na undani wa kimaana kuliko baadhi ya misemo inayopatikana katika lugha fulani. Kutumia semi hizi kunaonyesha kuwa mtumiaji wa lugha amepevuka katika lugha kwani ufafanuzi wa picha zilizomo unahitaji ujuzi mkubwa wa lugha.

    Mifano ya nahau:

    1. Kuchukua sheria mkononi: kulipiza kisasi kwa jambo baya

    2. Kuenda aste aste: kuenda pole pole / taratibu.

    3. Kuenda chapu chapu: kuenda haraka

    4. Kuenda kasi: kuenda haraka haraka.

    5. Kufanya hila: kutenda jambo la udanganyifu

    6. Kufanya masihara / mizaha: kutenda mambo kwa mchezo

    7. Kufanya uchuro: hali ya kuwa na kisirani ; mkosi

    8. Kufanya utani: kufanya mzaha au mchezo

    9. Kufanya uzohali: kuwa na uvivu; kuzembea

    10. Kufuja mali: kuharibu mali, kutumia pesa vibaya

    Kazi ya 12

     Tumia mshale kwa kuhusisha nahau katika sehemu A na maana zake katika sehemu B.

    ok

    ok

    Kazi ya 13 

    Kwa ushirikiano na wenzako, husisha semi (nahau) zifuatazo katika safu A na maana zake katika safu B, kisha mtunge sentensi kwa kutumia nahau hizo.

    ok

    4.5. Kusikiliza na Kuzungumza: Majadiliano

    Kazi ya 14

    Shirikiana na wenzako katika utafutaji wa maana ya nahau zinazofuata:

    1. Kuchemsha bongo

    2. Kuchongea mtu

    3. Kubeza mtu

    4. Kuchungulia kaburi

    5. Kufafanua kinaga-ubaga

    6. Kupigwa kalamu

    7. Kumpa nyama ya ulimi


    4.6. Kuandika: Utungaji wa insha ya methali

    Kazi ya 15

    Tunga kifungu cha habari chenye mada ifuatayo: “Mchumia juani hulia kivulini.”

    Hakikisha kwamba unatumia vielezi, viunganishi, vihusishi, vihisishi na baadhi ya nahau ambazo zinafuata:

    Kufunga virago: kuondoka; kusafiri

    Kugaragara kitandani: kugeukageuka huku na huko kitandani

    Kujifungua mtoto: kuzaa kwa mwanamke

    Kukata kamba: kufariki, kutoroka

    Kukaza kamba: kujitahidi

    Kula chumvi nyingi: kuishi miaka mingi

    Kula kiapo: kuapa

    Kumpa mtu heko: kupongeza mtu

    Kumpa mtu mgongo / kisogo: kufanyia mtu mambo yaliyo kinyume na matarajio

    Kumpa mtu nyama ya ulimi: kumpa mtu maneno matamu

    Kuona cha mtemakuni: kujuta; kupata adhabu kali

    Kuona kilichomnyima nyoka miguu: kupata adhabu kali.

    Kuona kilichomnyima kanga manyoya: kupatwa na ubaya.

    Kupanda mbegu za chuki: kuwachochea watu wachukiane

    Kupiga marufuku: kukataza kitu kisheria

    Kuvunja mbavu: kuchekesha; kufanya au kusema maneno yanayochekesha.

    Kuvunja nyumba: kuharibu hali ya maisha baina ya mume na mke.

    Tathmini ya mada ya tatu

    1. Nini dhana ya methali?

    2. Maana ya nahau ni ipi?

    3. Taja umuhimu wa methali katika jamii.

    4. Taja aina za maneno ambayo yamepigiwa mistari katika sentensi zifuatazo:

    a. Nitakuonyesha kitabu changu kipya kesho.

    b. Mchungaji anahubiri mbele ya Wakristo.

    c. Angalia! Kalamu yako inaangukia chini ya meza.

    d. Timu ya Amavubi oyeee!

    e. Musaniwabo na Beneyo wanakwenda sokoni.

    5. “Mtoto umleavyo ndivyo akuavyo.” Jadili kwa kutozidi ukurasa mmoja.


  • MADA 4:MIJADALA

    Kidokezo

    ok

    SOMO LA 5: MAANA YA MJADALA

    5.1. Kusoma na ufahamu: Maana ya mjadala

    Soma kifungu kuhusu “Maana ya mjadala” ili ujibu maswali yaliyotolewa hapo chini

    Kuna mazungumzo ambayo hufanywa kuhusu suala fulani linalohitaji kujadiliwa na kutafutiwa ufumbuzi. Mazungumzo ya aina hii ndiyo hujulikana kwa jina la mijadala. Kwa kawaida, mjadala ni mazungumzo juu ya jambo maalum ambayo hufanywa na watu kwa kutoa hoja zao kwa jambo fulani linalotakiwa ufafanuzi au ufumbuzi wa suala lililopo.

    Mjadala ni aina ya majadiliano ambayo huhusisha watu wengi wanaotoa hoja kuhusu mada fulani. Miongoni mwa watu wanaohusika katika mjadala huwa kuna kiongozi ambaye jukumu lake ni kuongoza majadiliano kwa kupanga muda wa kuzungumza kwa kila msemaji anayeshiriki katika mazungumzo hayo. Katika mjadala, hakuna msemaji ambaye anaruhusiwa kutoa hoja bila kumuomba fursa kiongozi wa majadiliano.

    Mjadala huwa na mada ambayo humulika hoja zote zinazotolewa wakati wa mazungumzo. Kama kuna wasemaji ambao wanataka kukiuka mada katika hoja zao, kiongozi wa mjadala huwarekebisha kwa kuwakumbusha mada inayotolewa hoja.

    Mjadala huwa na malengo ya kukuza uwezo wa kitaaluma na hali ya udadisi kwa washiriki wa majadiliano. Mjadala hukuza uwezo wa kushawishi watu hadharani ili wakubaliane na mawazo ya msemaji kuhusu jambo fulani. Aidha humwezesha mtu kupanga mawazo yake kwa mfuatano mzuri wakati anapoandika insha au habari. Mjadala pia humsaidia mtu kutambua kipaji alicho nacho cha kuzungumza bila aibu mbele ya hadhira na kukuza stadi ya utumiaji wa lugha kwa kutumia msamiati na matamshi bora ya lugha. Humzoeza pia mtu kusikiliza maoni ya watu wengine, kupinga au kutetea maoni na hoja zao. Jambo muhimu ni kwamba majadiliano haya humpa fursa ya kuelewana na watu anaotofautina nao kimawazo.

    Wazungumzaji wanapofanya mjadala hukuza uwezo wao wa mazungumzo kuhusu suala fulani na hupanua kiwango chao cha msamiati na hupunguza woga wa kuongea hadharani. Isitoshe, mjadala hutumiwa kama nyenzo bora ya kutatua migogoro inayoweza kuzuka miongoni mwa wanajamii. Katika mjadala, watu wenye mawazo yaliyo kinyume na mada, hupata nafasi ya kujadiliana juu ya jambo fulani kwa madhumuni ya kutatua tatizo linalowakumba. Mjadala hutumiwa kwa kutatua tatizo na kuondoa migogoro miongoni mwa watu kwa njia ya amani.

    Katika mjadala, kama tulivyokwisha kusema, kunajitokeza wahusika ambao ni kiongozi wa mjadala na hadhira. Kiongozi ndiye ambaye ana jukumu la kuongoza mjadala. Kiongozi anaweza kuwa mtu mmoja au wawili kulingana na mada iliyochaguliwa au malengo ya majadiliano yenyewe. Ukichaguliwa kama kiongozi ni lazima uongoze mjadala ipasavyo na usikose kumpangia kila 51 msemaji muda atakaotumia ili waweze kuchangia mawazo yake.

    Kwa upande wa mjadala, kiongozi humruhusu yeyote atakaye kutoa mchango kwani hakuna makundi ya watetezi na wapinzani wa mjadala. Kiongozi huyu huwa na majukumu tofauti kwani ndiye anayetoa muhtasari wa mawazo yaliyotolewa.

    Katika mjadala, kuna hadhira pia ambayo hushiriki katika mazungumzo kwa kusikiliza na kutoa mchango wao kuhusu suala linalojadiliwa. Kila mtu aliye na hoja hunyosha mkono kuomba fursa ya kuzungumza. Lengo la kwanza la kila msemaji katika mjadala si kupata ushindi, kwani si mashindano bali lengo la kila msemaji ni kutoa mawazo kwa nia ya kutatua tatizo fulani linalofafanuliwa na kujadiliwa kwa pamoja. Hivyo, katika mjadala hakuna kushindania ushindi; kila mtu ambaye ana la kusema huruhusiwa na hutoa hoja kama apendavyo kuhusu mada ile inayohusika bila kukiuka taratibu zilizowekwa.

    Watu wanaoshiriki katika mijadala huhakikisha kuwa mjadala ni njia ya kukuza uwezo wa kufikiri na kutafuta masuluhisho kwa masuala yanayoikumba jamii fulani. Katika mazungumzo haya, kiongozi ndiye anayeongoza majadiliano ili wazungumzaji watoe mchango wao kuhusu suala lililopo. Kiongozi humpa fursa mzungumzaji kwa kusema, “Simama utoe mchango wako.” Mzungumzaji huweza kutoa hoja zake kulingana na anavyofikiria kuhusu suala husika. Mara nyingi, mjadala huweza kufanyika katika makundi madogo madogo au makubwa. Kiongozi hubainisha mada ya mjadala na kuhakikisha kuwa wakati wote wa mjadala kuna mwenendo mwema unaowaongoza washiriki wa mjadala husika.

    Mzungumzaji katika mjadala ni lazima awe na uwezo wa kupanga mawazo yake kwa mfuatano bora wenye mantiki. Mjadala hutumiwa kama nyenzo bora ya kutatua migogoro inayoweza kuzuka miongoni mwa wanajamii. Katika mjadala, watu wenye mawazo yaliyo kinyume na mada, hupata nafasi ya kujadiliana juu ya jambo fulani kwa madhumuni ya kutatua tatizo linalowakumba au kuikumba jamii nzima. Mjadala hutumiwa kwa kutatua tatizo na kuondoa migogoro miongoni mwa watu kwa njia ya amani.

    Kwa upande wa mjadala, kiongozi humruhusu yeyote atakaye kutoa mchango kwani hakuna makundi ya watetezi na wapinzani wa mjadala. Kiongozi huyu huwa na majukumu tofauti kwani ndiye anayetoa muhtasari wa mawazo yaliyotolewa.

    Mzungumzaji katika mjadala ni lazima awe na uwezo wa kupanga mawazo yake kwa mfuatano mzuri. Yeye anakuza stadi ya utumiaji wa lugha kwa kuwa anaweza kuutumia msamiati na kujizoeza kutumia matamshi mazuri ya lugha.

    Jambo muhimu pia katika mijadala inayofanywa ni kwamba mazungumzo yanayofanywa huwazoeza wengi kusikiliza na kupima maoni na hoja za wenzao, kuelewana na wengine kutoka sehemu mbalimbali, kuheshimiana kulingana na mawazo tofauti yanayotolewa na kila mzungumzaji. Kwa hiyo, mjadala ni 5252 zoezi zuri kwa yeyote anayetaka kukuza uwezo wa mawasiliano, majadiliano, mahojiano, ujuzi wa kutoa maoni yake na kujitambua katika jamii yake.

    Mwisho, mjadala ni mazungumzo yanayoendeshwa na kushirikisha watu tofauti kwa kukidhi haja na malengo yanayotofautiana na kuingiliana kwa upande mwingine. Ni lazima kuelewa kuwa mjadala ni wenzo timamu wa kuimarisha stadi ya maongezi kuhusu mada fulani.

    Kazi ya 1

    Maswali ya ufahamu

    1. Eleza kwa ufupi maana ya mjadala.

    2. Ni zipi kazi za kiongozi wa mjadala ? 

    3. kwa sababu gani katika mjadala hakuna mshindi?

    5.2. Msamiati kuhusu Maana ya mjadala

    Kazi ya 2

    Tunga sentensi sahihi kwa kutumia maneno yafuatayo:

    1. Suala

    2. Hadhira 

    3. Kiongozi

    4. Majadilano

    5. Migogoro

    6. Jukumu

    Kazi ya 3

    Kamilisha sentensi zifuatazo kwa kutumia maneno yanayofaa kati ya haya yafuatayo: kuwashirikisha, mjadala, kupanga, mazungumzo, hoja, kiongozi, mada, kipaji, mahojiano, hadhira.

    1. Mjadala humsaidia mtu kutambua …………alicho nacho cha kuzungumza bila woga mbele ya wengine.

    2. Aliyechaguliwa kuongoza majadiliano kwa kupanga muda wa kuzungumza kwa kila msemaji huitwa ………………..

    3. …………… ni jumla ya wasikilizaji, watazamaji au wasomaji wa kazi maalumu ya kifasihi. 

    4. Katika mazungumzo lazima …………………mawazo kwa mfuatano mzuri.

    5. Uulizaji maswali ili kufahamu maarifa anayoyajua mtu hujulikana kama ………………..

    6. ………………… unahitajika kwa wanaohitaji ufafanuzi zaidi. 

    7. Mjadala huchukuliwa kama …………………………juu ya jambo maalumu.

    8. Watu wengi wanapojadiliana kuhusu mada fulani hutoa …………..ambazo husaidia wengine kuelewa ukweli fulani. 

    9. Mtu yeyote aliyehudhuria mkutano alipewa …………………ya kufanya jambo fulani.

    10. Mwalimu anaweza ……………………..wanafunzi katika uchaguzi wa mada.

    5.3. Sarufi: Matumizi ya viambishi rejeshi kulingana na ngeli za majina

    Soma na uchunguze sentensi zifuatazo: 

    Anavyokula ananitamanisha.

    Anamolala

    Anayecheka (umoja) wanaocheka (wingi)


    Maelezo muhimu

    Kiambishi ni kipande cha neno chenye maana ya kisarufi ambacho kinapachikwa kwa mfano kabla au baada ya mzizi wa neno katika vitenzi na kuwakilisha dhana fulani.

    -O- rejeshi hujitokeza katika shina amba-. Shina hili huongezewa viambihi vya 

    -o- rejeshi na kupata neno lionyeshalo urejeshi. Hapa tunapata maneno kama ambalo, ambaye, ambacho, ambazo, ambavyo, n.k. Haya ndiyo mazingira ya utokeaji wa -o- rejeshi. Zifuatazo ni dhima tano za -o- rejeshi:

    1. Huunganisha tungo mbili zenye dhana moja.

    Mfano:

    a. Mwalimu amefundisha.

    b. Mwalimu amehama.

    Jibu = Mwalimu ambaye amefundisha amehama.

    Kutokana na tungo hizi mbili tunaweza kupata tungo moja: Mwalimu ambaye amefundisha amehama

    2. Hudokeza idadi (umoja na wingi). Mfano: Anayecheka (umoja), wanaocheka (wingi).

    3. Kuonyesha mahali ambapo tendo hutendeka. Mfano: “Anamolala” (ndani)

    4. Huonyesha nafsi ya mtenda au mtendwa wa jambo. Mfano: Aliyeiba(umoja ) Walioiba (nafsi ya III wingi).

    Kazi ya 3

    Jaza nafasi. Tumia ‘o’ rejeshi iliyo mwafaka

    Kwa mfano :Wageni wasafirio wameondoka na mizigo yao. 

    1. Viatu viuzwa ------------- ni mitumba. 

    2. Safari ziandaliwa------------------zinatufurahisha. 

    3. Wateja wanunua-----------------wana pesa kama mchanga. 

    4. Mikate iokwa-------------itamalizwa yote.

    5. Watalii wafika------- hawatamani kuondoka. 

    6. Miche ipaliliwa-------- itanawiri vizuri.

    5.4. Matumizi ya lugha kuhusu ‘‘Maana ya mjadala ’’

    Kazi ya 4

    Soma maelezo yanayofuata ili kujibu maswali hapo chini

    • “Maana ya mjadala”

    ▫ Mjadala ni mazugumzo juu ya jambo fulani. Unaweza kufanyika katika makundi madogo madogo au makubwa. 

    ▫ Mjadala unaongozwa na mtu mmoja au watu wawili ambao wanazusha mawazo na kuhakikisha ikiwa kuna mwenendo mwema kati ya washiriki wa mjadala huo. 

    ▫ Kiongozi wa mjadala ndiye anayetoa muhtasari wa mawazo yaliyotolewa. Mada zinazojadiliwa katika mjadala ni zile ambazo zinahitaji ufafanuzi kutokana na mchango wa mawazo ya wengi. 

    ▫ Anayetoa hoja yake, anaweza kuunga mkono maoni ya mwenzake au kuyapinga kwa minajili ya kutoa mchango wake wa kutatua tatizo linalojadiliwa.

    ▫ Katika mjadala mada hutolewa mawazo na ndiyo inamulikia mjadala. Kiongozi wa mjadala hulazimika kuwasaidia wasemaji kutokiuka mada.

    ▫ Mjadala huwa na malengo yafuatayo:

    - Kukuza uwezo wa kitaaluma na hali ya udadisi kwa washiriki wa mjadala.

    - Kukuza uwezo wa kushawishi watu hadharani ili wakubaliane na mawazo ya msemaji kuhusu jambo fulani.

    - Kumwezesha mtu kupanga mawazo yake kwa mfuatano mzuri wakati anapoandika insha au habari.

    - Kumwezesha mtu kutambua kipaji alicho nacho cha kuzungumza bila aibu mbele ya hadhira.

    - Kukuza stadi ya utumiaji wa lugha kwa kutumia msamiati na matamshi bora ya lugha.

    - Kumzoeza mtu kusikiliza na kupinga au kutetea maoni na hoja za wengine.

    - Kuwapa watu wasaa wa kuelewana na wengine kutoka maeneo mbalimbali.

    ▫ Wahusika katika mjadala ni kiongozi na hadhira.

    ▫ Katika mjadala kila yeyote anayetaka kutoa hoja anaruhusiwa na kiongozi kutoa hoja yake apendavyo

    ▫ Katika mjadala hakuna washindi, kiongozi anatoa suluhisho kutokana na mawazo yaliyotolewa. Mjadala si mashindano wala malumbano.


    Maswali:

    1. Mjadala unaweza kuongozwa na watu watano. Ni kweli au si kweli? Eleza.

    2. Ni ipi kazi ya kiongozi katika mjadala?

    3. Jadili malengo matatu ya mjadala mzuri.

    4. Kwa sababu gani katika mjadala hakuna mshindi? 

    5. Jadili wahusika katika mjadala.

    5.5. Kusikiliza na Kuzungumza

    Kazi ya 5

    Jadili mada ifuatayo: “Maendeleo nchini huyafanya maisha ya Wanyarwanda yabadilike kwa kiwango cha juu.”


    5.6. Kuandika

    Kazi ya 6

    Andika mjadala kuhusu mada “Ubaya wa dawa za kulevya katika maisha ya binadamu.” Usizidi kurasa mbili.


    SOMO LA 6: MAANDALIZI NA UTEKELEZAJI WA MJADALA

    Kazi ya 1

    Jibu maswali yafuatayo:

    a. Mjadala ni nini?

    b. Taja watu wanaoshiriki katika mjadala.

    c. Unafikiri kuwa majukumu ya watu hao ni yapi?


    6.1. Kusoma na ufuhamu: “Mchango wa wazazi katika malezi ya watoto wao”

    Soma kifungu hiki kisha ujibu maswali ya ufahamu

    Kiongozi: Waheshimiwa mabibi na mabwana mliokusanyika hapa, kwanza ninataka niwakaribishe katika mjadala huu. Kama mnavyotuona hapa mbele yenu, mimi ninayewakaribisha ni kiongozi wa mjadala huu. Pembeni pangu mnayemwona ni kiongozi msaidizi. Mada ya mjadala wetu wa leo ni kama mnavyoisoma mbele yenu “MCHANGO WA WAZAZI KATIKA MALEZI YA WATOTO WAO.” Karibuni sana nyote na bila kupoteza muda, ningetaka kumkaribisha mshiriki aliye tayari atoe mchango wake.

    Mshiriki wa kwanza: Ninawashukuru sana viongozi na wasikilizaji washiriki wenzangu. Ni kweli kabisa wazazi ndio wenye jukumu la kwanza katika malezi ya watoto wao. Kama inavyojulikana malezi ya kwanza kwa mtoto huanzia nyumbani. Nyumbani ndipo mtoto anapopata malezi ya msingi ambayo humulikia maisha yake. Malezi haya ya kwanza yapatikanayo nyumbani humsaidia mtoto kufanikiwa katika maisha yake. Malezi haya yanatolewa na wazazi ambao ndio walezi muhimu wa watoto wao. Bila mchango wa wazazi, watoto hawawezi kupata elimu. Kwa hiyo, wazazi wana jukumu la kwanza katika malezi ya watoto wao. Ahsanteni kwa kunitega sikio.

    Kiongozi: Asante sana kwa hoja yako. Kama mlivyosikia, msemaji huyu ameeleza kwamba wazazi ndio wanaowapatia watoto wao malezi ya msingi ambayo yanawasaidia kufanikiwa maishani mwao. Tafadhalini, naomba mjaribu kutoa maoni mengine kuhusu suala hilo. Karibu bibi!

    Mshiriki wa pili: Asante sana kiongozi kwa fursa hii ya kuniruhusu kutoa mchango wangu. Kwa maoni yangu, ni kweli wazazi wana nafasi kubwa katika malezi ya watoto wao. Lakini, kuna matatizo makuu 57 ambayo wazazi hawatilii mkazo katika malezi hayo. Chunguza jinsi watoto na vijana wengine wanavyotumia dawa za kulevya. Siku hizi, idadi ya wanaokumbwa na matumizi ya dawa za kulevya huzidi kuongezeka. Wazazi wenzangu, mjue kwamba dawa za kulevya ni hatari sana kwa binadamu. Dawa hizi husababisha magonjwa mengi na huharibu ubongo wa watoto. Kwa upande wangu, kila mzazi lazima ashiriki katika malezi ya watoto wote anaokutana nao badala ya kuwafikiria watoto wake tu. Wazazi wote wakilitilia maana tatizo hili, lingemalizika haraka sana, watoto wetu wakaishi maisha mazuri.

    Kiongozi: Ninamshukuru sana mshiriki kwa maoni yake. Anaeleza kwamba wazazi hawazingatii wajibu wao kwa kutoa mchango wao kukomesha matumizi ya dawa za kulevya miongoni mwa vijana. Anaeleza pia kwamba malezi ya mtoto ni jukumu la kila mtu. Tunamshukuru sana. Hebu, tumsikilize pia mshiriki yule aliyenyosha mkono pale ili naye atoe hoja zake.

    Mshiriki wa tatu: Mheshimiwa kiongozi na wasikilizaji washiriki wenzangu. Watu ambao wako karibu sana na watoto ni wazazi wao ambao wana mchango wa kwanza katika malezi ya watoto hao. Wao huwatunza watoto wao, tangu wanapozaliwa na wakati wa kwenda shule unapofika, wao ndio wanaopiga hatua ya kwanza kuwapeleka shuleni. Wajibu wa kila mzazi ni kupeleka mtoto wake shuleni kwani anapata mwenendo mwema utakaomsaidia maishani mwake. Watoto wanapofika shuleni, ni vyema wazazi wao wawajibike kufuatilia malezi ya watoto wao kwa kuwashauri, kuwafundisha kuwa na mienendo mizuri, kuwanunulia vifaa vya shule na kuwalipia karo. Waheshimiwa wasikilizaji, kama mnavyoelewa, bila mchango wa wazazi, watoto hawawezi kupata elimu inayotolewa shuleni kwani wao ndio wanaorahisisha kila jambo linalotendewa mtoto, awe shuleni, nyumbani na mahali pengine. Asante sana kwa kunitega sikio, hayo ndiyo maoni yangu.

    Kiongozi: Waheshimiwa wasikilizaji washiriki, mawazo hayo ya mwenzetu mmeyasikia. Sasa ninataka kumkaribisha msemaji mwingine yeyote ambaye ana la kusema ili naye atoe mchango wake kwa ufumbuzi wa suala letu. Karibu sana bibi.

    Mshiriki wa nne: Asante sana kiongozi na wasikilizaji washiriki kwa kunipa fursa hii. Wapendwa wasikilizaji washiriki, taifa letu hufanya mengi ili iweze kukomesha matumizi ya dawa za kulevya miongoni mwa wananchi. Kwa nini wazazi tusiwasaidie viongozi wetu kupambana na janga hili ili tupige marufuku madawa ya kulevya ambayo huangamiza maisha ya watoto wetu? Serikali yetu imechukua uamuzi mzuri wa kuanzisha mradi wa elimu kwa wote ambapo kila mtoto anapelekwa shuleni akaendelea na masomo yake mpaka anapomaliza shule za sekondari. 5858 Kwa hivyo, ni lazima walimu na viongozi wa shule waelewe kwamba wanahitaji kushirikiana na wazazi ili waweze kutimiza wajibu wao mkubwa wa kubadilisha mienendo ya vijana wanaowalea hasa vijana wale wanaopatikana wakitumia madawa ya kulevya. Bila mchango wa wazazi kwa vijana hao, shule zetu haziwezi kufanikiwa kuwapatia watoto hao maadili yanayotakiwa. Kwa mfano, utamkuta kijana mmoja akikosekana shuleni kwa siku moja au mbili na akifika huwadanganya viongozi kwamba alikuwa ameenda nyumbani na viongozi hawa hukubali bila kuuliza wazazi wa mtoto huyo kuhusu ukweli wa yale aliyosingizia. Kwa kumaliza, ni vyema kila mtu anayehusika na malezi ya watoto awe mwalimu, kiongozi wa shule na hata majirani waelewe kwamba wazazi wana nafasi kubwa katika urekebishaji wa mienendo mibaya ya watoto wetu. Ahsanteni sana kwa kunitega sikio.

    Kiongozi: Ninamshukuru mshiriki mwenzetu kwa maelezo yake ambayo yamewagusa wengi. Yeye amesema kwamba ni lazima kuisaidia serikali katika kulinda watoto wetu dawa za kulevya. Ameeleza pia kwamba kila mtu anayehusika na malezi ya watoto aitambue kwanza nafasi ya wazazi kwa kujaribu kuwashirikisha kwa kila uamuzi kuhusu mienendo na tabia za watoto wao. Kwa hivyo, tunamshukuru sana kwa mawazo yake. Kama mnavyoona, mengi yamekwishaelezwa na muda unazidi kuyoyoma. Hebu nichukue fursa hii kuwakaribisha washiriki wengine wawili kabla ya kutamatisha mjadala wetu. Karibu sana.

    Mshiriki wa tano: Ahsante sana kiongozi kwa kunipa muda huu ili nami nitoe maoni yangu. Washiriki wenzangu, mawazo yaliyotolewa na waliotangulia ni mazuri sana na yanaeleweka waziwazi. Ni ukweli mtupu kwamba wazazi ndio wenye jukumu la kwanza katika malezi ya watoto wao na ndiyo maana wahenga walisema, “Mtoto hutazama kisogo cha mama yake”. Mzazi ni mfano unaoigwa na mtoto wake. Kama mzazi ana tabia nzuri mtoto naye bila shaka ataathiriwa vizuri na itakuwa kinyume kama mzazi ana tabia zisizopendeza. Kwa hivyo, mimi ningependa kuhimiza wazazi wote kukuza na kuendeleza tabia nzuri mbele ya watoto wao ili waweze kuigwa na kutumiwa kama mifano mizuri kwa malezi ya watoto wao kwani mtu hutoa kile alicho nacho na pia huvuna kile alichopanda. Ahsanteni.

    Kiongozi: Ahsante sana mshiriki kwa mawazo yako mazuri. Naona kuna wengine wanaonyosha mikono yao ili kutoa michango yao kuhusu suala letu. Lakini, hebu tumsikilize mzazi yule ili tukamilishe mazungumzo yetu. Karibu sana.

    Mshiriki wa sita: Kiongozi na wasikilizaji washiriki wenzangu! Ni lazima tuelewekwamba mtoto hulelewa na watu wote wanaomzunguka 59 kwani hawa nao wana nafasi kubwa kwa kumwathiri vizuri au vibaya kulingana na mienendo na tabia zao. Mtoto afikapo shuleni, malezi yake huwa zaidi mikononi mwa walimu na viongozi wa shule ambao hufanya kazi kubwa ya kuwalea watoto na kuwaelimisha. Watoto humaliza muda mrefu mikononi mwa walimu na viongozi wa shule wanaomsaidia kurekebisha tabia mbaya na kuendeleza tabia nzuri huku wakimpa elimu itakayomfaa katika maisha yake. Mbali na hayo, mtoto akitembea barabarani, njiani na akienda kwingine anakotumwa na wazazi wake hukutana na watu ambao si wazazi wake, mtoto akipewa ruhusa ya kwenda kuangalia familia yake pana hukutana na watoto wengine katika familia hizo na hata watu wengine ambao si wazazi wake.

    Kwa hivyo, mimi naona kuwa watu wote wanamzunguka mtoto kuanzia wale wanaokaa naye nyumbani kama vile wazazi wake, ndugu zake na watumishi wa nyumbani, majirani na wengine ambao hukutana naye nao wanaweza kuathiri sana malezi ya mtoto na hata kuliko wazazi wake wanavyoweza kufanya. Ni mara ngapi tunasikia habari kwamba watoto wameathiriwa na watumishi wa nyumbani kwa kujiingiza katika vitendo na mienendo mibaya kama vile uzinzi, ulevi, matumizi ya maneno yasiyo na maadili, na kadhalika?

    Haya yote yanathibitisha kwamba malezi ya watato yanahusu watu wote wanaomzunguka mtoto huyo na kwamba wito unapaswa kutolewa kwao ili watambue wajibu wao kumlea mtoto. Wazazi humwelekeza mtoto wakati angali mchanga lakini aanzapo kwenda shuleni na kukutana na watu wengine, nafasi ya wazazi katika malezi yao huendelea lakini wanaomwathiri zaidi huwa ni watu wote anaokutana nao katika mazingira na shughuli zake mbalimbali. Asanteni sana kwa kunitega sikio; hayo ndiyo yalikuwa maoni yangu

    Kiongozi: Ninakushukuru sana kwa maelezo yako. Nasikia kwamba wewe unatilia mkazo kwamba watu wote wanapaswa kutoa mchango wao kwa kumlea mtoto badala ya kufikiria kwamba wazazi ndio wenye nafasi kubwa. Asante sana kwa mawazo hayo. Inaonekana kwamba watu wengi wangependa kutoa mchango wao lakini muda wetu hauturuhusu kuendelea kusikiliza hoja nyingine. Mjadala wetu unakaribia kufikia mwisho na ningependa kuwapongeza ninyi nyote kwa maoni na mawazo mazuri mliyoyatoa katika mjadala huu. Asante sana kwa wote mlioshiriki katika mjadala huu. Kichwa cha mjadala wa leo kilikuwa “MCHANGO WA WAZAZI KATIKA MALEZI YA WATOTO WAO.” Miongoni mwa hoja mlizozitoa ni wajibu wa wazazi kuwalinda watoto kutumia dawa za kulevya, kuwapeleka watoto shuleni na kufuatilia masomo na mienendo yao kokote wanakoenda, viongozi wa shule na walimu kushirikisha wazazi katika malezi ya watoto wao na watu wengine wanaokutana 6060 na mtoto kuelewa kwamba nao wanaweza kumwathiri mtoto huyo vizuri au vibaya. Waheshimiwa mabibi na mabwana hoja zote mlizozitoa zimezingatiwa na zimeeleweka vizuri. Ahsanteni sana kwa mchango wenu katika kupigania malezi bora kwa watoto wetu. Mjadala wa leo unaishia hapa. Njooni tena wakati mwingine kwa mada nyingine. Ahsanteni sana kwa kushiriki.

    Kazi ya 2

    Maswali ya ufahamu

    1. Malezi ya msingi mtoto huyapata wapi?

    2. Dawa za kulevya zina madhara gani kwa maisha ya vijana?

    3. Kwa nini mzazi ana wajibu wa kuwapeleka watoto shuleni?

    4. Eleza nafasi ya Serikali katika malezi ya watoto kama ilivyozungumziwa katika mjadala huu. 

    5. Viongozi na walimu hutakiwa kufanya nini kwa kuzingatia nafasi ya wazazi katika malezi ya watoto wao?

    6. Nini maana ya msemo ‘‘mtoto hutazama kisogo cha mama yake?’’

    7. Eleza msemo huu’’Mtu haulizwi kitu asichokuwa nacho’’

    8. Ni masomo gani uliyofaidika kutokana na mjadala huu huu baada ya kuusoma 


    6.2. Msamiati kuhusu «Andalio la mjadala»

    Kazi ya 3

    Tunga sentensi sahihi kwa kutumia maneno yafuatayo yanayotumika katika mjadala:

    1. Mchango

    2. Elimu 

    3. Dawa za kulevya

    4. Kisogo

    5. Kulea

    6. Kukaribisha

    7. Kiongozi 

    8. Ulevi

    9. Uzinzi

    10. Serikali

    Kazi ya 4 

    Husisha maneno yaliyoko katika sehemu A na maelezo yaliyopo katika sehemu B.

    ok

    6.3. Sarufi: Matumizi ya viambishi rejeshi kulingana na ngeli za majina

    Soma na uchunguze sentensi zifuatazo: 

    - Ng’ombe walionunuliwa walikuwa wanono.

    - Miti itakayopandwa itasaidia katika hali ya hewa.

    - Chakula tulichopata kilikuwa kitamu.

    - Mwizi aliyeiba mbuzi wangu ni yule.

    - Viti vilivyoletwa vilikuwa safi

    Maelezo Muhimu

     Kiambishini kipande chanenochenye maana yakisarufiambacho kinapachikwa kwa mfano kabla au baada ya mzizi wa neno katika vitenzi na kuwakilisha dhana fulani.

    -o- rejeshi hujitokeza katika shina amba-. Shina hili huongezewa viambihi vya 

    -o- rejeshi na kupata neno lionyeshalo urejeshi. Hapa tunapata maneno kama ambalo, ambaye, ambacho, n.k. haya ndiyo mazingira ya utokeaji wa -o- rejeshi.

    Kazi ya 5

    Kamilisha sentensi zifuatazo kwa kutumia ‘o ’rejeshi:

    1. Asiyekuwe ---- na lake halipo.

    2. Ngoma ivuma……………. ndiyo ya kupasuka. 

    3. Akufaa--- kwa dhiki ndiye rafiki yako.

    4. Zimwi likujua----- halikuli likakukumaliza.

    5. Wageni wafika ………. sasa ndio wetu. 

    6.4. Matumizi ya lugha: Maandalizi na utekelezaji wa mjadala

    Kazi ya 6

    Soma maelezo muhimu hapo chini kisha ujibu maswali yanayofuata:

    Maelezo muhimu kuhusu “Andalio la mjadala” 

    Mjadala ni mazugumzo juu ya jambo fulani. Unaweza kufanyika katika makundi madogo madogo au makubwa.

     • Mjadala unaongozwa na mtu mmoja au watu wawili ambao wanazusha mawazo na kuhakikisha ikiwa kuna mwenendo mwema kati ya washiriki wa mjadala huo. 

     • Kiongozi wa mjadala ndiye anayetoa muhtasari wa mawazo yaliyotolewa katika mjadala. 

     • Anayetoa hoja yake, anaweza kuunga mkono maoni ya mwenzake au kuyapinga kwa minajili ya kutoa mchango wake wa kutatua tatizo linalojadiliwa.

     • Mjadala unapomalizika, kiongozi huwapongeza waliohudhuria mjadala na kuwaalika katika mjadala mwingine.

    Mambo ya kuzingatia katika utekelezaji wa mjadala:

    • Kutumia vizuri muda uliopangwa,

    • Kuepukana na fujo na kelele,

    • Kupaza sauti unapotoa hoja kuhusu mada,

    • Kutoa maoni kwa madhumuni ya kutimiza lengo la mjadala,

    • Kutumia lugha ya adabu, isiyo ya matusi,

    • Kuwaheshimu wengine,

    • Kupanga mawazo yako kabla ya kupata fursa ya kuongea.

    Maswali 

    1. Eleza maana ya mjadala.

    2. Ni watu gani wanaoshiriki katika mjadala? Eleza. 

    3. Jadili mambo mawili ya kuzingatia katika uandalizi wa mjadala

    6.5. Kusikiliza na Kuzungumza

    Kazi ya 7

    Jadili na mwenzako kuhusu mada hii kisha muwasilishe maoni yenu kwa darasa.

    1. Faida na hasara za kuishi katika miji mikubwa. 

    6.6. Kuandika

    Kazi ya 8

    Andika mjadala kwenye ukurasa mmoja kuhusu “Malezi bora nchini Rwanda” huku ukitoa maoni yako kuhusu namna serikali na taifa zima linavyoweza kuwasaidia wanafunzi.

    Tathmini ya mada ya nne

    1. Eleza uhusiano na tofauti kati ya mjadala na mdahalo.

    2. Eleza mambo ya kuzingatia katika utekelezaji wa mjadala.

    3. Eleza mambo ya kujiepusha katika mjadala.

    4. Chagua na kujadili mada moja kati ya hizi zifuatazo:

    a. Wakoloni walileta mabaya mengi kuliko mazuri.

    b. Shule za bweni ni bora kuliko shule za kutwa.

    c. Uzuri wa mtu si urembo bali ni tabia.

    d. Kutoa si utajiri bali ni moyo.

  • MADA 5:UTUNGAJI WA INSHA ZA MASIMULIZI

    • Uwezo mahususi wa mada ndogo: 

    Kutunga insha fupifupi za masimulizi kwa kuzingatia kanuni za utungaji.

    • Malengo ya ujifunzaji:

    - Kutoa maana ya insha za masimulizi,

    - Kuonyesha sifa za aya njema,

    - Kutaja sehemu kuu za insha,

    - Kutoa na kueleza aina mbalimbali za insha,

    - Kutaja aina za alama za vituo,

    - Kukusanya hoja kuhusu mada husika na kuzipanga kwa mfuatano mzuri,

    - Kutunga insha za masimulizi kulingana na mada husika,

    - Kutumia kwa usahihi alama za vituo katika uandishi wa insha za masimulizi,

    - Kusimulia hadharani kiini cha insha iliyotungwa,

    Kidokezo

    ok

    SOMO LA 7: MAFANIKIO YA KUDUMU

    7.1. Kusoma na ufahamu: Mafanikio ya kudumu

    Soma kifungu hiki kisha ujibu maswali uliyopewa hapo chini

    Masengesho, kijana aliyezaliwa mwanapekee katika familia yake hakubahatika kulelewa na wazazi wake kwani walifariki angali mdogo akachukuliwa na kulelewa na shangazi yake ambapo alikuwa akisoma. Alipomaliza masomo yake katika shule za sekondari alipata cheti cha kuhitimu masomo hayo akiwa na alama nzuri. Jambo hili liliwafurahisha watu wengi wakiwemo walimu na majirani zake. Ndiyo maana ilikuwa tafrija ya kijiji kizima, tuliposherehekea siku ya kupata tuzo kwa kijana hodari ambaye aliyamudu maisha yake kiasi cha kuigwa na vijana wengine.

    Wengi waliompongeza siku hiyo walimletea zawadi nyingi. Alikuwa mwanafunzi mwenye bidii tangu shule za chekechea hadi kiwango alichofikia. Muda mfupi baadaye, alijiunga na vijana wenzake kufuata masomo ya muda mfupi yaliyokuwa yakitolewa kijijini mwake. Masomo hayo yaliwalenga vijana wote waliokuwa wamemaliza masomo yao ya shule za sekondari na yalilenga kuwawezesha kuandaa miradi midogo midogo ya kujikimu, kujiendeleza na jinsi ya kuifanikisha miradi hiyo. Masomo hayo yaliwafurahisha vijana wengi na Masengesho aliyafuata kwa makini, jambo lililokuwa desturi kwake.

    Masengesho alikuwa msichana mwenye mawazo na mtazamo imara wa maisha kiasi kwamba watu walishangaa kutokana na tabia na mienendo yake. Mafunzo yalifanyika kwa muda wa mwaka mzima akapewa cheti katika fani ya maandalizi na utekelezaji wa miradi ya kimaendeleo. Mwezi mmoja uliofuata Taasisi ya Maendeleo ya Rwanda ilihitaji kuajiri vijana waliokuwa wamemaliza masomo yao ili wasaidie katika kazi za ukalimani na upelekaji wa watalii kwenye vivutio vya utalii. Masengesho alipeleka ombi lake na baada ya muda mfupi akaitwa kwa mtihani na kuufaulu. Kazi ilipoanza aliifanya kwa bidii kiasi kwamba watalii wengi walifurahia huduma yake, wakampenda kwa uwezo wake wa kuzungumza lugha tofauti na bidii aliyoonesha kazini.

    Alifungua akaunti kwenye benki moja na kuanza kuhifadhi sehemu ya mshahara wake. Alipoona akaunti yake imekuwa na pesa za kutosha, aliamua kuomba mkopo ili aweze kuzalisha mali shamba lake kubwa ambalo mpaka wakati huo lilikuwa halijatumiwa vizuri. Aliandaa vizuri mradi wa kilimo na ufugaji, akajenga vibanda vya mifugo yake, akawaajiri baadhi ya vijana waliokuwa pamoja katika mafunzo ya muda ule mfupi, kila mmoja akapewa jukumu lake. Pamoja na kazi yake ya ukalimani, Masengesho alifuata vizuri mradi wake akanunua vifaa vilivyohitajika. Mwaka mmoja baadaye, alikuwa ameishapata mali nyingi na kuanza kujulikana kote nchini kwa uwezo wake wa kufanya mambo mengi kwa muda mfupi na kwa ukamilifu.

    Serikali ya Rwanda ilipotoa tuzo kwa watu waliochangia kubadilisha maisha ya watu wengine, Masengesho alikuwa miongoni mwa watu waliochangia kuyaboresha maisha ya majirani zao. Kila mtu katika kijiji chetu aliitikia mwaliko wake na wengi tulikuwa tunajivunia kuwa na kijana mwerevu kama yeye. Kwa sasa ameanza kuendeleza masomo yake katika Chuo Kikuu cha Rwanda ambapo anatarajia kupata Shahada yake ya kwanza katika uwanja wa Ukalimani. Masengesho amekuwa mfano mzuri kwa vijana wengine wengi ambao wanapoyakumbuka maisha yake, huyaamini yaliyosemwa na wahenga kwamba “Mchumia juani hulia kivulini” na kamba “Mvumilivu hula mbivu”. Wema kwa kila mtu, utulivu na upendo ni baadhi ya sifa zinazomtambulisha kijana huyu ambaye amewashangaza wengi wanaofahamu alipotoka.

    Kazi ya 1

    Maswali ya ufahamu

    1. Eleza hali ya maisha ya Masengesho alipokuwa mtoto mdogo.

    2. Kwa nini Masengesho alipewa zawadi nyingi baada ya kumaliza masomo yake ya shule za sekondari?

    3. Masomo ya muda mfupi aliyoyafuata yalihusu nini?

    4. Kwa nini Masengesho alipewa tuzo?

    5. Umepata funzo gani kutokana na kifungu hiki?

    6. Kulingana na kifungu hiki, eleza maana ya methali hizi: 

    a. Mvumilivu hula mbivu.

    b. Mchumia juani hulia kuvulini.

    7.2. Msamiati kuhusu kifungu cha habari

    Kazi ya 2

    Tunga sentensi sahihi kwa kutumia maneno yafuatayo. Chunguza matumizi yake katika kifungu cha habari hapo juu.

    1. Mafanikio 

    2. Akaunti 

    3. Tafrija

    4. Mradi

    5. Kukata tamaa

    Kazi ya 3 

    Husisha maneno kutoka sehemu A na maana yake katika sehemu B

    ok

    7.3. Sarufi kuhusu matumizi ya alama za vituo 

    Kazi ya 4

    Angalia sentensi ambazo zinafuata na kujadili na mwenzako unavyoziona:

    1. Ehee! Kumbe yeye ni mwizi!

    2. Mwalimu wa mitaala wa shule yetu ni mtu mpole kabisa.

    3. Ninaenda sokoni kununua vitu vingi: kuku, maembe, mapapai, machungwa, madaftari, na kalamu.

    4. Nyinyi mnaona vipi siku za leo?

    5. Masomo haya si ya kukuangamiza; masomo haya ni ya kuboresha hali ya maisha yako.

    Ndani ya sentenzi hizi kuna matumizi ya alama za vituo mbalimbali kulingana na maumbile ya kila sentensi. Kuna alama ya kushangaa, alama ya nukta au kituo, alama ya nuktambili au koloni, alama ya mkato wa chini au koma, alama ya kuuliza au kiulizi au ulizo pamoja na alama ya nukta na mkato au semikoloni

    Maelezo muhimu 

     ALAMA ZA UANDISHI (ALAMA ZA UAKIFISHAJI) NA MATUMIZI YAKE

     Kuandika ni tofauti na kuzungumza, katika maandishi ili yaweze kusomeka na kueleweka vizuri ni muhimu sana kuzingatia uakifishaji (matumizi ya alama za vituo). Sasa kabla hatujashika kalamu na kuanza kuandika insha zetu, ni vyema tukazijua alama hizi na jinsi zinavyotumika.

    1. Matumizi ya nukta (.): Nukta au kituo kikuu hutumika kama ifuatavyo:

    Kuonyesha mwisho wa sentensi.

    Kwa mfano: 

    - Mtoto amelala.

    - Jua limechomoza mapema.

    - Aliniponya kwa kuwa alipendezwa nami.

    Katika kufupisha maneno.

    Kwa mfano: 

    - S.L.P.

    - Dkt. Mukeshimana

    - n.k.

    Kuonyesha saa.

    Kwa mfano: Sasa nii saa 8.00

    Katika hesabu kuonyesha desimali.

    Kwa mfano: Nimepata alama 40.5

    2. Matumizi ya mkato au koma (,): Mkato au koma hutumika kama ifuatavyo:

    Kuonyesha orodha ya vitu.

    Kwa mfano: Usisahau kununua mkate, soda, kitumbua na chapati.

    Kugawanya mawazo katika sentensi.

    Kwa mfano: Baada ya kusikiliza kesi yake, hakimu alimhukumu kifungo chamiaka 10 jela.

    3. Matumizi ya alama za mtajo (vinukuu) (‘) na (“): Alama za mtajo hutumika kwa:Kunukuu usemi halisi.

    Kwa mfano: “Ukiniletea zawadi nitakupenda sana,” Mugenga alimwambia Ndayizigiye.

    Kuonyesha maneno yasiyo ya Kiswahili unapochanganya ndimi katika sentensi.

    Kwa mfano: Huyu ndiye mchezaji “number one.”

    4. Alama ya kuuliza (kiulizi/ ulizo) (?): Kiulizi hutumika:Kuulizia swali.

    Kwa mfano: Ulikuwa wapi muda wote huo?

    5. Alama ya hisi (mshangao) (!): Matumizi ya alama ya hisi ni:

    Kuonyesha hisia k.v mshangao, hasira, furaha, n.k.

    Kwa mfano: Hoyeeeee!

                              Haiwezekani!

    Kuigiza tanakali za sauti.

    Kwa mfano: Maji yalimwagika mwaaaa!

    6. Matumizi ya nukta-mkato/ semi-koloni (;): Nukta-mkato hutumika:

    Kuorodhesha vitu au mawazo hasa ikiwa yana maneno zaidi ya moja.

    Kwa mfano: Maria alinituma nimpelekee kitabu cha kufundishia Kiswahili kwa 

    Wageni; madaftari mawili makubwa; baiskeli ndogo za watoto na vikombe vinne.

    Kuunganishia vishazi huru viwili.

    Kwa mfano: Tuliandamana kwa moyo wa kizalendo; tukapata haki yetu.

    7. Matumizi ya nuktambili (nukta pacha/ koloni) (smile: Nuktambili hutumika:

    Kuonyesha mwanzo wa orodha.

    Kwa mfano: Ukifika sokoni nunua vitu vifuatavyo: maembe 2, sukari kilo 1, unga wa ngano kilo 6, vitunguu kilo 1, mafuta ya kupikia lita 10 na unga wa mahindi mfuko mmoja.

    Kunukuu ukurasa wa Bibilia.

    Kwa mfano: Yohana kutoka 20:4 Biblia inasema….

    Kuonyesha msemaji katika tamthilia au mchezo wa kuigiza.

    Kwa mfano: Mkulima: Nyinyi walanguzi mnatukandamiza sana.

    Mlanguzi: Viwanda hakuna, sasa unadhani sisi tutauza kwa faranga ngapi? 

    Hatuwakandamizi, serikali yenu ndiyo inayowakandamiza.

    8. Matumizi ya kistari kifupi (-): Kistari kifupi hutumika:

    Kuunganisha maneno mawili.

    Kwa mfano: Mfa-maji

                             Mwana-harakati

    Kuonyesha hadi, au mpaka.

    Kwa mfano: Umeme umepanda kutoka elfu 20 – 60 kwa mwezi.

    9. Alama za mabano ya mduara/ parandesi egg: Mabano hutumika:

    Kutoa maelezo zaidi.

    Kwa mfano: Wanafunzi wote (wasichana na wavulana) wanaweza kujua Kiswahili.

    Kufungia herufi za kuorodheshwa.

    Kwa mfano: 

    a. huelimisha 

    b. huburudisha 

    c. huonya

    10. Mkwaju (/): Hutumiwa kuonyesha kuwa kitu mojawapo ya vitu vilivyotajwa chaweza kutumiwa badala ya vingine.

    Kwa mfano: Uwayo alikaa kimya/ alitulia.

    7.4. Matumizi ya lugha

    Kazi ya 5

    Weka alama za vituo katika dondoo la insha ambayo inafuata ili iwe na maana

    Hmm Unataka nikuambie sifa za mtu ninayempenda Bila shaka ninampenda sana baba Baba yangu anaitwa John Mugabo Yeye ni mrefu na mweupe Baba ana macho mazuri na nywele nyingi nyeusi kichwani Yeye hupenda kuvaa mavazi tofauti suti kanzu mashati meupe na suruali nyeusi kila wakati isipokuwa Jumamosi tunapoenda kucheza kandanda naye Baba ni mchezaji hodari sana katika kandanda na yeye hufurahia sana mchezo huu Baba yangu ni mwalimu mkuu katika shule ya sekondari ya Kigali Anaheshimiwa sana na walimu wote wanafunzi na hata wazazi Sifa zake nzuri ndizo zimfanyazo baba apendwe na kila mtu.

    Kazi ya 6

    Soma kuhusu sehemu za insha ya masimulizi kisha ujibu maswali:

    Insha ya masimulizi huwa na kichwa cha habari cha insha ambacho ni maneno machache, takribani matano, ambayo ndiyo jina la insha. Kichwa cha habari huandikwa juu, katikati kwenye ukurasa wa kwanza wa insha. Mara nyingi, huandikwa kwa herufi kubwa na hubeba wazo kuu la insha. Insha ya masimulizi huwa na utangulizi ambao ni sehemu ya mwanzo yenye urefu usiozidi aya moja. Utangulizi hudondoa kwa ufupi kabisa kile kinachoelezwa kwenye insha.

    Kiini cha insha ya masimulizi ni sehemu tunayoweza kusema kwamba ni insha yenyewe. Kwenye kiini ndipo ufafanuzi wote hutolewa. Ufafanuzi huu hupangwa katika aya moja au zaidi. Hapa ndipo mwandishi hubainisha mawazo yake, huthibitisha, hushawishi, huhimiza na hufafanua. Baada ya kiini huja hitimisho, yaani sehemu ya mwisho wa insha ya masimulizi ambayo haizidi aya moja. Katika sehemu hii, mwandishi anaweza kurejelea kwa ufupi sana yale aliyoyazungumzia katika insha yake. Anaweza kuonyesha msimamo wake, anaweza kutoa mapendekezo, au kuwahimiza walengwa wake kuchukua hatua fulani.

    Katika kuandika insha ya masimulizi, mwandishi atazingatia mambo haya: atabaini ni mada gani ya kuandikia na kuielewa vema; atapanga mawazo katika mtiririko wenye mantiki, atatumia mtindo unaoendana na kusudi la insha ya masimulizi. Kwa mfano, mtindo wa masimulizi unafaa kwa hadithi au insha nyingine za kisanaa. Atatumia lugha fasaha na inayoeleweka, atafuata kanuni za uandishi, kwa mfano matumizi ya alama za uandishi, aya, herufi kubwa na herufi ndogo. Mwandishi atapanga insha katika msuko au muundo wake, yaani kichwa, utangulizi, kiini na hitimisho

    Maswali:

    1. Kwa sababu gani utangulizi mzuri ni muhimu katika insha?

    2. Jadili sehemu kuu za insha.

    3. Jadili mambo ya kuzingatia katika uandishi wa insha.

    7.5. Kusikiliza na kuzungumza

    Kazi ya 7

    Sikiliza mkufunzi anavyosoma maelezo kuhusu aina za insha, soma maelezo kwa kumwiga mkufunzi na kujibu maswali yanayofuata.

    Insha ni za aina nyingi kulingana na namna zilivyoandikwa au kusudi lake. Katika utungaji wa insha kuna insha za masimulizi, insha za wasifu, insha za picha, insha za mdokezo, insha za methali, insha za hoja na insha za kubuni. Insha za masimulizi ni aina ya insha ambazo ndani yake mwandishi anasimulia au anaeleza tukio fulani maalum la kweli kwa njia ya kisanaa, ambapo insha za wasifu ni aina za insha ambazo hueleza sifa za mtu, kitu au jambo fulani. Insha za aina hii husimulia sifa, maisha au maelezo mengine muhimu kuhusu mtu fulani, kitu fulani au jambo fulani. Ni kusema kuwa katika aina hizi za insha mwandishi anaandika kuhusu uzuri au ubaya wa mtu, kitu au jambo fulani.

    Insha za picha hueleza picha iliyotolewa. Ni kusema kwamba mwandishi hueleza mambo anayoyaona kwenye picha au mchoro. Analazimika kufanya andiko lenye mfuatano wa mawazo kulingana na mfuatano wa picha au michoro aliyopewa. Insha za mdokezo ni zile ambazo mwandishi hupewa mwongozo wa kufuatilia katika utunzi wake. Kwa mfano, mwandishi anaweza kupewa orodha ya hoja kadhaa kutokana na kichwa kilichotolewa akajenga insha. Vilevile anaweza kupewa utangulizi au kimalizio cha insha na kuagizwa aendelee na insha au aanze insha aliyopewa.

    Insha ya methali ni insha ambayo mada yake huwa ni methali ambayo mwandishi anapaswa kujadilia. Katika uandishi wa insha ya aina hii, mwandishi ni lazima atoe hoja kwa kukubaliana na methali iliyotolewa. Insha za hoja ni insha ambazo mwandishi analazimishwa kutoa hoja zinazotetea mada na nyingine zinazopinga mada. Mwishoni mwa insha hii, mwandishi anaonesha msimamo wake kulingana na mada iliyotolewa. Kwa kumaliza, insha za kubuni ni zile ambazo hutungwa kuhusu mawazo yanayozuliwa na ambayo si matukio ya kawaida. Ni kusema kwamba mwandishi hubuni mandhari, wahusika, matukio, na kadhalika.

    Maswali

    1. Taja aina za insha.

    2. Kifungu ulichokisoma ni aina gani ya insha? Kwa sababu gani?

    3. Ni nini tofauti iliyoko baina ya insha ya wasifu na insha ya masimulizi.

    4. Kwa sababu gani mara zote mwandishi wa insha ya methali hulazimishwa kutetea methali aliyopewa?


    7.6. Kuandika kuhusu utungaji wa insha ya masimulizi 

    Kazi ya 8

    Soma maelezo muhimu hapo chini kisha uandike insha ya masimulizi kuhusu mada ifuatayo kwa kufuata uandishi mzuri wa aya na hata wa insha yenyewe.

    Mada: Rafiki yako anayesoma katika kidato cha tano amefukuzwa shuleni kwa sababu anatumia dawa za kulevya na kushiriki ulevi. Simulia kilichoendelea.

    Maelezo muhimu

    Aya katika uandishi wa insha: Aya ni fungu au mkusanyiko wa sentensi ambazo zinazungumzia wazo moja kuu. Zifuatazo ni namna za kuandika aya nzuri, sifa za aya nzuri na mbinu za kuelekeza uandishi na upangaji wa aya.

    1. Ujongezaji wa maandishi: Hii ndiyo sifa ya kwanza inayobainisha kuwepo kwa aya katika maandishi. Ni nafasi ya msitari mmoja au miwili inayoachwa kati ya aya moja na aya nyingine. Neno la kwanza la aya linaweza pia kusukumwa mbele kidogo kabla ya kuanza aya kama ishara ya aya mpya katika maandishi.

    2. Matumizi ya sentensi-mada: Hii ni sentensi kuu inayomwelekeza msomaji juu ya kile kitakachozungumziwa katika aya husika. Mara nyingi sentensi hii huwa ya kwanza katika aya na maneno yanayofuata yakiwa yanazunguka au yanaeleza yale yaliyotangulizwa katika sentensi mada hiyo.

    3. Aya huhusika kuwa na dhamira kuu: Kila aya huwa na wazo kuu moja inalozungumzia. Hairuhusiwi kuzungumzia dhamira mbili tofauti katika aya moja

    4. Muundo wa kimantiki: Aya inapaswa kuwa na mantiki; yaani hoja zilizomo katika aya moja zinapaswa kuwa na mantiki kiasi kwamba hakuna jambo lililomo katika aya lisiloendana na kile kilichokusudiwa na mwandishi wa aya. 

    5. Aya kuwa na sifa ya ubayana: Ni lazima kila aya iweze kuwa inajieleza kwa msomaji, maana yake haipaswi kuwa tatanishi. 

    6. Muwala na ushikamanifu: Aya inapaswa kuwa na ushikamanifu au upatanifu wa kimuundo. Kila hoja inapaswa kuwa kiendelezo na mjazo wa ile iliyoitangulia.

    7. Maneno ya mpishano: Haya ni maneno yanayosukuma aya ya chini na kuihusisha na aya ya juu ili kuleta umoja katika hoja za aya zinazokaribiana. Maneno haya ni kama viunganishi ama maneno mengine ya upatanishi wa kisarufi.


    Tathmini ya mada ya tano

    1. Nini maana ya insha za masimulizi?

    2. Sehemu za insha ya masimulizi ni zipi?

    3. Taja aina za insha.

    4. Weka alama za vituo kwenye sentensi zifuatazo:

    a. Afanalek Kumbe nimesahau kuwa leo ni siku yangu ya kuzaliwa

    b. Wanafunzi wa kidato cha tano wanakosa miaka mingapi kumalizia shule za upili

    c. Nipelekee kwenye ofisi yangu vyombo vifuatavyo kalamu karatasi meza viti deski na makabati

    d. Mwalimu alisema Fanyeni kazi hii katika dakika arobaini tu

    e. Watu wote wanaume na wanawake watashiriki katika mkutano wa kijiji chetu

    5. Tunga insha ya masimulizi yenye matumizi ya alama za vituo sahihi kuhusu shule yako. Usizidi ukurasa mmoja.


    Marejeo

    1. Bakhressa, S.K na Wenzake (2008). Kiswahili Fasaha. Kitabu cha Mwanafunzi. Kidato cha Tatu. Oxford University Press, East Africa Ltd, Nairobi, Kenya.

    2. TUKI (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Toleo la Pili. Oxford University Press.

    3. Bakhressa, S.K na Wenzake (2008). Kiswahili Sanifu. Kitabu cha Mwanafunzi. Darasa la Saba. Oxford University Press, East Africa Ltd, Elgon Road, Upper Hill, Nairobi, Kenya.

    4. Nkwera, F.M.V. (1978). Sarufi na Fasihi Sekondari na Vyuo. Tanzania Publishing House, Dar Es Salaam.

    5. HARERIMANA, F. (2017). Tujivunie Lugha Yetu. Kitabu cha Mwanafunzi, Kidato cha 5. MK Publishers (R) Ltd. Kigali, Rwanda.

    6. Ndalu, A. E. (2016). Masomo ya Kiswahili Sanifu. Kitabu cha Mwanafunzi. Kidato cha 2. Moran (E.A) Publishers Limited.

    7. Ntawiyanga, S. (2017). Kiswahili kwa Shule za Rwanda. Mchepuo wa Lugha, Kidato cha 5. Longhorn Publishers (Rwanda) Limited. Kigali, Rwanda.

    8. Kenya Literature Bureau (2006). Kiswahili kwa Darasa la Nane. Kitabu cha Wanafunzi. Kenya Literature Bureau, Nairobi, Kenya. 

    9. Ntawiyanga, S. na Wenzake (2017). Kiswahili kwa Shule za Rwanda. Mchepuo wa Lugha, Kidato cha 6. Longhorn Publishers (Rwanda) Limited. Kigali, Rwanda.

    10. Niyirora, E. & Ndayambaje, L. (2012). Kiswahili Sanifu kwa Shule za Sekondari. Kitabu cha Mwanafunzi Kidato cha Tano. Tan Prints (India) Pvt. Ltd.

    11. http://learn.e-limu.org/topic/view/?c=207&t=1579